Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Michezo ya Kompyuta Nina umri wa miaka 15, na nataka kuwashukuru sana kwa makala “Vijana Huuliza . . . Je, Nicheze Michezo ya Kompyuta au ya Vidio?” (Agosti 22, 1996) Hiyo ilionyesha kwelikweli ubaya wa michezo hiyo, nayo itasaidia Wakristo wachanganue mazuri na mabaya ya kuicheza.
F. R., Indonesia
Nina umri wa miaka 17, na nilikuwa napenda michezo yenye jeuri ya kompyuta. Nilifikiri kwamba michezo hiyo haikuniathiri, lakini nikawa mraibu kwelikweli wa michezo hiyo—hasa aina yenye jeuri mliyotaja. Sasa nimeharibu diski zangu zote za kompyuta ambazo zinahusika na ujeuri na damu. Tokeo limekuwa nini? Nahisi vizuri zaidi, na nina wakati mwingi zaidi wa kusoma, kujifunza, na kuzungumza juu ya Yehova Mungu.
S. A., Ugiriki
Ubikira Asanteni kwa makala yenu fupi lakini nzuri ajabu yenye kichwa “Ubikira—Kwa Nini?” (Agosti 22, 1996) Katika siku hizi za kisasa watu wafikiriapo ni lazima uwe na sura mbaya ukichagua kuwa bikira, nilitiwa moyo sana kuona watu wachanga warembo wanaotegemeza viwango vya Yehova. Asanteni tena!
R. D., Marekani
Wahindi wa Amerika Nataka kuonyesha uthamini wangu kwa mfululizo “Wahindi wa Amerika—Wakati Wao Ujao Una Nini?” (Septemba 8, 1996) Nilizisoma makala hizo sana na nitazisoma tena. Sehemu ya ufufuo hasa ilinigusa moyo sana.
S. B., Italia
Makala hizo zilinigusa moyo kuliko makala nyinginezo zote. Zilinisaidia kutambua kwamba nilikuwa nawabagua Wahindi na hilo halipatani na kanuni za kimungu. Tangu siku zangu za shule, nilikuwa na maoni kwamba Wahindi walikuwa tu wakatili wabaya. Vitabu vya historia havikutupa kamwe maoni sahihi juu ya ulimwengu unaotuzingira. Makala zenu zilinisaidia kuona hali mbaya ya Wenyeji wa Amerika—kikiwa kielelezo kingine cha ‘mtu kuwa na uwezo juu ya mwenzake kwa kumwumiza.’—Mhubiri 8:9, ZSB.
M. M., Marekani
Nikiwa mzao wa Wenyeji wa Amerika, nilisoma makala zenu kwa msisimko mwingi. Nililia machozi niliposoma juu ya mateseko yaliyovumiliwa na watu ambao walikuwa wamependa sana uumbaji. Jinsi ninavyotamani siku ambayo Mungu atabadilisha ukosefu wote wa haki ambao wanadamu wote wamefanyiwa na sisi sote kuweza kushiriki pamoja dunia hiyo iliyo paradiso.
N. S., Marekani
Pompeii Majuzi nilisoma kwa makini makala yenu “Pompeii—Mahali Palipobaki Vilevile.” (Septemba 8, 1996) Ilikuwa ni kana kwamba nilikuwa huko! Lakini ningependa jambo fulani lieleweshwe wazi. Makala hiyo yasema kwamba mtu yeyote azuruye Pompeii “bado aweza kuona vinu vya kusagia mahindi.” Labda mnisahihishe, lakini je, mahindi si nafaka ambayo ilipatikana katika bara la Amerika pekee ambayo haikujulikana kwa Wazungu hadi siku za Christopher Columbus?
R. D., Marekani
Pole kama tulitokeza utatanishi kwa jambo hilo. Ingekuwa afadhali kama tungesema kwamba vinu vya kusagia “nafaka” vyaweza kuonekana huko. Kwa kupendeza neno la Kiingereza “corn” laweza kumaanisha tu “mbegu za nafaka za nyasi,” kama vile ngano au oti.—Mhariri.
Tangu utotoni nimevutiwa na historia ya kale. Historia ya Pompeii hasa imenivutia siku zote. Niliposoma makala hiyo, nilihisi kana kwamba nilikuwa nasafiri kupitia jiji hilo. Ajabu! Nilijifunza mambo mengi madogo-madogo ambayo sikuyafahamu. Pia nilipenda ulinganifu uliofanywa na wakati wa mwisho katika siku zetu. Asanteni kwa kunisaidia kujua sehemu ambazo siwezi kuzuru.
J. S. A., Brazili