Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kutenga na Ushirika Nilithamini ile makala “Maoni ya Biblia: Sababu Inayofanya Kutenga na Ushirika Kuwe Mpango Wenye Upendo.” (Septemba 8, 1996) Mimi mwenyewe nilitengwa na ushirika katika 1987 na kurudishwa 1988, baada ya kujifunza somo. Mpango huu wenye upendo ulinisaidia kufanya marekebisho katika mtindo-maisha na washiriki wangu. Tumebarikiwa kama nini kuwa na tengenezo ambalo hutambua viwango vya Biblia!
R. R., Marekani
Mimi pia nilitengwa na ushirika wa kutaniko. Wakati huo nilihisi kwamba ilikuwa adhabu kali na kwamba lilikuwa jambo baya sana ambalo mtu angeweza kufanyiwa. Nilikosea! Kabla ya kutengwa na ushirika, wazee wa kutaniko walifanya jitihada nyingi sana kunisaidia kutubu. Sikuthamini msaada huo wakati huo. Kutengwa na ushirika kulininyenyekeza sana. Kulinisukuma kuona jinsi uhusiano wetu pamoja na Yehova ulivyo wa maana.
B. T., Marekani
Wenyeji wa Amerika Asanteni kwa mfululizo “Wahindi wa Amerika—Wakati Wao Ujao Una Nini?” (Septemba 8, 1996) Sikuzote nimekuwa nikipendezwa na historia ya Wenyeji wa Amerika. Kwa mara nyingine tena, nilipendezwa na hali ya kusema kweli, kutopendelea, na usahihi wa kihistoria wa magazeti yenu.
A. M., Italia
Mtu hawezi kuona kamwe mwalimu au wakili Mwenyeji wa Amerika akionyeshwa kwenye ukurasa wa mbele wa gazeti. Michoro ya kikale, kama ule uliokuwa kwenye ukurasa wa juu wa toleo lenu, ndiyo huonyeshwa. Utumizi wenye kuendelea wa michoro hii huzuia jitihada zetu dhidi ya maoni yanayoshikiliwa na wengi.
K. M. T., Marekani
Kwa hakika haikuwa nia yetu kuendeleza maoni yoyote yenye kudhuru yanayoshikiliwa na wengi. Mchoro wa jalada ulinuiwa kutokeza Wenyeji wa Amerika katika njia chanya na yenye heshima. Vazi la kitamaduni lilitumiwa kwa sababu lilifaa kwa habari hiyo na lingeweza kutambulishwa kwa urahisi na wasomaji wetu duniani pote. Kwa kupendeza, wasomaji wengi walio Wenyeji wa Amerika walionyesha uthamini kwa makala na vilevile mchoro. Wengine wanatamani kudumisha njia zao za kale na bado watavaa mavazi yao ya kitamaduni katika pindi fulani.—Mhariri.
Kwa kuwa nafanya kazi katika jumba la makumbusho nikiwa mtaalamu wa sayansi ya makabila ya binadamu hasa za Amerika Kaskazini, napendezwa sana na kichwa hicho. Je, ingewezekana mnipelekee nakala kumi za toleo hilo, nitakazozisambaza kwa wengine wanaopendezwa na Wahindi wa Amerika?
P. B., Ujerumani
Tulifurahi kukubali ombi hilo.—Mhariri.
Machache niliyojua kuhusu Wahindi yalitoka sinemani. Naweza kuona kutokana na makala hizi kwamba sinema za Marekani hazikuonyesha ukweli halisi. Maoni yangu kuhusu Wahindi yamebadilika.
T. M., Marekani
Nusu ya ukoo wangu ni ya Wenyeji wa Amerika, kwa hiyo nilisisimuka kusoma toleo hilo. Hata hivyo, kinyume na maoni ya wengi, Fahali Aketiye hakuwa kiongozi kwenye pigano la Little Bighorn.
P. H., Marekani
Yaonekana kwamba ni jambo la kubishaniwa miongoni mwa wanahistoria kama Fahali Aketiye alishiriki mwenyewe katika pigano hilo. Maoni yaonekanayo kuwa yenye kukubaliwa zaidi miongoni mwa wasomi hupatikana katika gazeti lenye kuheshimiwa “Natural History,” ambalo husema: “Kulingana na masimulizi ya Wahindi, Fahali Aketiye, ambaye nyakati fulani alifikiriwa kuwa mshindani wa Custer katika pigano, hakushiriki katika pigano hilo lakini alijishughulisha na kutengeneza dawa za kuwaimarisha mashujaa wa kivita Wahindi.” Kama habari yenye kurekebisha itafunuliwa ni jambo linalobaki kuonwa.—Mhariri.