Kuukabili Huo Ugumu
MASHAMBULIO dhidi ya maadili ya kingono huanza mapema maishani kwa sababu ya kupatikana kwa televisheni, vitabu, magazeti, sinema, na muziki ambao huonyesha ngono. Vijana huhimizwa kuwa na tabia za kingono za watu wazima ingawa wao si imara kihisia-moyo. Wazazi wengine hata huongezea msongo wa kingono kwa kuruhusu miadi ya kijinsia katika umri mchanga. Msongo wa marika hutia moyo kufanya miadi ya kijinsia, na vijana wengi ambao wana marafiki wa jinsia tofauti wenye kutegemeka hujiachilia na kuanza kufanya ngono. “Ni kawaida kama nini . . . kwa msichana tineja ambaye anahisi hapendwi na wazazi wake . . . kuanza kukumbatiana kimapenzi na rafiki yake mvulana kwa kudhani kimakosa kwamba kufanya hivyo kutamfanya apendwe na awe na rafiki wa karibu sana,” asema Luther Baker, profesa wa chunguzi za familia.
Vijana huelekea kuishi miaka ya ubalehe kana kwamba huo ndio mwisho wa maisha zao badala ya kuishi kana kwamba ndiyo matayarisho ya maisha. “Wakiwa wamewaka kwa uwezo wao mpya wa kingono na kusadikishwa na marika kwamba uwezo wa kingono ndio uanamume, vijana wengi wamekuwa waoteaji wa kingono” katika ubalehe wao, asema Profesa Baker. Miaka ipatayo 30 iliyopita, mwanahistoria Arnold Toynbee aliomboleza juu ya hila inayofanyiwa vijana wetu, kwa kuwa aliamini kwamba historia imeonyesha kwamba sababu moja inayofanya nchi za Magharibi ziwe na akili ni ule uwezo wa kuahirisha ‘utendaji wa kingono’ wa wabalehe ili wazingatie kupata ujuzi.
Wazazi Ambao Wana Uvutano Mzuri
Wazazi ambao hawaruhusu wabalehe kufanya miadi ya kijinsia ya kujifurahisha huonyesha hangaiko zuri kwa afya na furaha ya wakati ujao wa watoto wao. Kwa kuwa na viwango vya juu vya maadili na kudumisha uwasiliano mzuri, wao waweza kuwa na uvutano katika maisha za watoto wao. Utafiti unaochunguza tabia za kingono za vijana waonyesha kwamba “uvutano huo waweza kufanya watoto waahirishe utendaji wa kingono,” kulingana na Journal of Marriage and the Family.
Wazazi ambao huwatia watoto nidhamu na kuwafanya kuwa wenye madaraka hupata matokeo bora zaidi. “Wabalehe na wazazi wao wakiwa na maadili yenye kukazia kuwajibika, uwezekano wa wabalehe kushika mimba kabla ya ndoa hupunguka sana,” uchunguzi mmoja wathibitisha. Jambo hilo hutaka wazazi wafahamu utendaji wa watoto wao—wakichunguza mgawo wao wa masomo ya nyumbani; wakijua mahali walipo na pia washiriki wao; wakiwawekea miradi iwezayo kutimizwa; na kuwafundisha mambo ya kiroho. Watoto wanaokua wakiwa na uwasiliano wa karibu na wazazi wao watajihisi vizuri zaidi na hawatahangaikia mwenendo wao wa kingono.
Shauri bora zaidi kwa wazazi na watoto ni hekima ipatikanayo katika Biblia. Wazazi katika Israeli waliamriwa wafundishe watoto wao maadili. Yehova aliwauliza: “Tena liko taifa gani kubwa, lililo na amri na hukumu zenye haki kama torati hii yote, ninayoiweka mbele yenu leo”? Ni hizi ‘amri zenye haki’ ambazo walipaswa kufundisha watoto wao katika hali changamfu na ya upendo ya kifamilia. “Uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” Watoto walihimizwa: “Shika maagizo ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” Uwasiliano mchangamfu wenye ukaribu kama huo na mafundisho ya baba na mama ndiyo yanayojenga katika watoto wao mtazamo wenye usawaziko kuelekea maisha na mwenendo wa kingono, ambao ‘utamlinda’ kijana maishani mwake mwote.—Kumbukumbu la Torati 4:8; 6:7; Mithali 6:20, 22.
Vijana, kwa nini mharibu wakati wenu ujao kwa kushindwa na tamaa za kingono? Miaka ya utineja ni karibu saba. Miaka hiyo inapasa kutumiwa kukua kiakili, kihisia-moyo, na kiroho na kusitawisha mtazamo wenye usawaziko kuhusu mwenendo wa kingono, katika matayarisho ya miaka ijayo 50 au 60 ya maisha. Wazazi, chukueni madaraka yenu mliyopewa na Mungu kwa uzito, na mlinde watoto wenu wasipatwe na majonzi moyoni yanayoletwa na maradhi yanayopitishwa kingono na mimba zisizotakiwa. (Mhubiri 11:10) Acheni watoto wenu waone katika maisha zenu za kila siku jinsi upendo na ufikirio kwa wengine hujenga mahusiano yenye kudumu.
Kuukabili kwa Mafanikio Huo Ugumu
Usiruhusu ashiki ya kingono ambayo imeenea iharibu maoni yako juu ya maisha na kuharibu fursa yako ya kuwa na wakati ujao wenye kuridhisha na wenye furaha. Tafakari juu ya vielelezo vingi vya mahusiano ya kibinadamu katika Biblia. Uwe na hakika kwamba maisha na upendo hudumisha uchangamfu muda mrefu baada ya miaka ya utineja. Uhalisi huu unapofikiriwa kwa uzito kwa kupatana na mapenzi ya kimungu kwa wanaume na wanawake Wakristo, basi msingi unawekwa kwa ajili ya muungano wenye upendo na wenye kudumu kati ya watu wawili ambao wamependana.
Uchunguzapo wenzi wanaotajwa katika Biblia kama vile Yakobo na Raheli, Boazi na Ruthu, pamoja na yule kijana mchungaji na msichana Mshulami, utaona kwamba walikuwa na uvutano fulani wa kingono katika mahusiano yao. Lakini, usomapo kwa uangalifu Mwanzo sura ya 28 na ya 29, kitabu cha Ruthu, na Wimbo Ulio Bora, utaona kwamba kulikuwa na mambo mengine muhimu zaidi ambayo huboresha mahusiano hayo.a
Kubali Maandalizi ya Yehova kwa Ajili ya Uhai
Yehova, Muumba wa jamii ya wanadamu, huelewa mwenendo wa kingono wa wanadamu na tamaa zihusikazo. Kwa upendo, ametuumba katika sura yake, si tukiwa na “urithi unaotufanya tufanye ngono ovyoovyo,” lakini tukiwa na uwezo wa kudhibiti hisia zetu kwa kupatana na mapenzi ya kimungu. “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu, . . . kwamba mjiepushe na uasherati; kwamba kila mmoja wenu apaswe kujua jinsi ya kupata umiliki wa chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono kama ile waliyo nayo pia mataifa wale wasiomjua Mungu; kwamba yeyote asifikie hatua ya kudhuru na kuziingilia haki za ndugu yake katika jambo hilo.”—1 Wathesalonike 4:3-6.
Jambo hilo ladhihirishwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Wao hustahi viwango vya juu vya Mungu kwa wanaume na wanawake Wakristo. Wanaume wazee wanaonwa kama baba, “wanaume vijana zaidi kama ndugu, wanawake wazee zaidi kama mama, wanawake vijana zaidi kama dada kwa usafi wote wa kiadili.” (1 Timotheo 5:1, 2) Hayo ni mazingira yafaayo kama nini kwa wanaume na wanawake wachanga kufurahia wafikiapo uwezo wao kamili, bila misongo ya kufanya miadi ya kijinsia na kufunga ndoa kabla ya wakati ufaao au bila maradhi yanayopitishwa kingono! Familia ya Kikristo yenye utendaji, ikiwa imeimarishwa na kutaniko la Kikristo, ni mahali salama katika ulimwengu wenye kichaa cha ngono.
Kwa kutumia kanuni za Biblia maishani mwao, vijana Wakristo hawana ashiki ya kingono nao hupata shangwe katika kutii himizo hilo linalotolewa na Neno la Mungu: “Wewe kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako, ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako, lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote Mungu atakuleta hukumuni. Kwa hiyo ondoa majonzi moyoni mwako, nawe uuondoe ubaya mwilini mwako; kwa maana ujana ni ubatili, na utu uzima pia.”—Mhubiri 11:9, 10.
[Maelezo ya Chini]
a Ona ukurasa wa 247 wa kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Blabu katika ukurasa wa 10]
Usiruhusu ashiki ya kingono iharibu fursa yako ya kuwa na wakati ujao wenye kuridhisha na wenye furaha
[Picha katika ukurasa wa 9]
Vijana wanaojihusisha na utendaji wa familia hawaelekei kutafuta mahusiano ya kingono