“Ebu Fumbua Tu Macho Yako Uone”
WATOTO wako huona nini? Vita? Uhalifu? Uchafuzi? Umaskini? Ugonjwa? Ni kweli kwamba haya ni mambo halisi ambayo yapo sikuzote. Lakini je, umewafundisha kutazama zaidi ya mambo hayo na kuona wakati ujao mzuri ajabu ambao umeahidiwa katika Biblia? Wazazi wa Joel Pierson mwenye umri wa miaka tisa wamemfundisha hivyo. Kukiwa na matokeo gani?
Fikiria yale aliyoandika Joel kwa habari yenye kichwa “Ebu Fumbua Tu Macho Yako Uone.” Kichwa hicho kilikuwa mgawo wa kuandika insha uliopewa vijana katika shule za umma za wilaya fulani katika Virginia, Marekani. Ona jinsi insha ya Joel, iliyochapishwa katika gazeti la habari The Central Virginian, la Agosti 22, 1996, inavyofunua kwamba tumaini lake linategemea yale aliyojifunza kutokana na Neno la Mungu. Yeye aliandika:
“Ebu fumbua tu macho yako uone, umaridadi wote uliokusudiwa uwepo.
“Je, haingekuwa ajabu kuamka asubuhi moja na kusikia kwamba hakuna uchafuzi tena? Badala ya kusikia habari za mauaji na uhalifu, watu wanaishi kwa amani na kwa furaha.
“Majirani wanafanya kazi pamoja na kusaidia rafiki kujenga nyumba yake. Karibu na hapo, twaona wengine wakipanda bustani. Na si hiyo tu, wana makusudi mazuri. Kila mtu anajiunga na wengine ili kusaidiana. Hakutakuwa tena na maskini, na kutakuwapo wingi wa chakula. Kutakuwa na muungano na amani duniani kote. Hakuna mtu atakayekuwa na njaa au ugonjwa tena. Kuna mazingira yenye kuvutia ya kutazama na tazama, mtoto amepanda simbamarara! Na si simbamarara pekee bali wanyama wote wanaishi kwa amani na wanadamu.
“Ningependa kuishi mahali kama hapo. Je, ungependa kuishi hapo pamoja nami?”
Je, kweli Mungu aahidi baraka kama zile ambazo Joel mchanga afafanua hapa? Kwa hakika, ndiyo! Tafadhali fungua Biblia yako na usome ahadi hizo zinazopatikana katika Zaburi 46:8, 9; 67:6; 72:16; Isaya 2:3, 4; 11:6-9; 33:24; 65:17-25; Mathayo 6:9, 10; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.