Vijana Huuliza . . .
Kuna Ubaya Gani Kuchuma Pesa?
“KWA kweli pesa ndicho kitu muhimu zaidi ulimwenguni.” Akadai mwandishi wa michezo ya kuigiza Mwingereza George Bernard Shaw. Je, wakubaliana naye? Labda wahisi zaidi kama Tanya mwenye umri wa miaka 17, asemaye: “Sitaki kuwa tajiri, ila tu niwe salama kifedha.” Avian mchanga vilevile huona pesa, si kama kitu cha maana zaidi katika ulimwengu, bali kama kitu muhimu cha kumsaidia kufikia miradi fulani. Yeye asema: “Pesa ni muhimu kwa mahitaji yangu, kama vile nguo na usafiri.”
Je, ulijua kuwa Biblia pia hutoa hoja kama hiyo? Kwenye Mhubiri 7:12, Biblia husema kuwa ‘Fedha ni ulinzi.’ Umaskini umeelezwa kuwa “adui mkubwa kwa furaha ya binadamu.” Na kuwa na pesa za kutosha kwaweza kukulinda—angalau kwa kiasi fulani—kutokana na matatizo ambayo kwa kawaida huletwa na umaskini. Pesa zaweza pia kukulinda kutokana na misiba isiyotarajiwa. “Biblia husema kwamba ‘wakati na tukio lisilotazamiwa hutupata sote,’” asema Phyllis mchanga. “Hatuwezi kamwe kujua magumu yatakapotupata, kwa hiyo twahitaji kuwa na pesa akibani.” (Mhubiri 9:11, NW) Na ingawa pesa zaweza kuonekana kuwa za maana kwako sasa, zaweza kuwa na fungu la maana hata zaidi katika wakati wako ujao.
Lile “Wimbi la Ufuatiaji Vitu vya Kimwili”
Ijapokuwa hangaiko la kiasi fulani la kuwa na pesa za kutosha ni jambo la kawaida na linalofaa, kwa vijana fulani pesa zimekuwa tamaa isiyozuilika. Vijana 160,000 walipoulizwa, “Ni nini ambacho wataka zaidi maishani?,” asilimia 22 walisema, “Kuwa tajiri.”
Hakuna shaka kuwa hamu hii ya pesa inachochewa na kile gazeti Newsweek lilikiita “wimbi la ufuatiaji vitu vya kimwili” ambalo limeukumba ulimwengu. “Mimi ni mtu mwenye kufuatia vitu vya kimwili sana na hukazia uangalifu vibandiko vya vitu,” asema Martin mwenye umri wa miaka 18. “Naamini kwa uthabiti kuwa wapata kile ulicholipia. Hivyo, natumia pesa nyingi kwa vitu nitakavyo.” Martin si kijana pekee ‘atumiaye pesa nyingi.’ Gazeti U.S.News & World Report laripoti: “Mwaka jana vijana wenye umri wa kati ya miaka 12 hadi 19 [katika Marekani] walifanya ununuzi mkubwa zaidi usiozuilika, wakitumia kufikia dola bilioni 109 katika ununuzi, ongezeko la asilimia 38 zaidi ya 1990.”
Hata hivyo, vijana hutoa wapi pesa za kununua nguo mpya, diski songamano, na vifaa vya kompyuta? Kulingana na U.S.News & World Report: “Karibu nusu ya vijana wote wenye umri wa miaka 16 hadi 19 wana kazi za nusu wakati.” Ikifanywa kwa usawaziko, kazi ya baada ya shule yaweza kuwa na manufaa, kama vile kumfunza kijana kuchukua madaraka. Hata hivyo, kwa wazi vijana wengine hupita mipaka katika jambo hili. Gazeti Newsweek laonelea: “Wanasaikolojia na walimu huona mkazo katika wanafunzi [wanaofanya kazi]. Wana wakati mchache wa kufanya mgawo wa masomo ya nyumbani, na walimu ambao kwa kawaida huwatazama wanafunzi wachovu wakijaribu kukaza fikira kwa kawaida huitikia kwa kushusha viwango vya maksi.”
Ijapokuwa hivyo, vijana wachache wanaofanya kazi wanakubali kuacha vyanzo vyao vya kupata pesa. “Shule ni ya muhimu,” asema Vanessa mchanga, “na ndivyo na pesa. Mgawo wa masomo ya nyumbani hauna mshahara.” Kuchuma pesa kuna umaana gani kwako? Je, kuchuma pesa nyingi ndilo lengo lako kuu maishani?
“Waazimiao Kuwa Matajiri”
Biblia hushughulika na maswali aya haya. Mtume Paulo aliandika: “Wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo. Kwa maana kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10.
Paulo kwa hakika alijua alichokuwa akizungumzia. Kabla ya kuwa Mkristo, alikuwa mmoja wa wale viongozi wa kidini wajulikanao kuwa “Mafarisayo,” ambao Biblia huwaelezea kuwa “wapenda-fedha.” (Luka 16:14) Ijapokuwa hivyo, mtume hakuhukumu kuchuma pesa kwenyewe. Badala ya hivyo, alitoa onyo kwa wale “waazimiao kuwa matajiri” au, kama tafsiri nyingine isemavyo, kwa watu “wawekao mioyo yao katika kuwa wenye mali.” (Phillips) Lakini ni nini kilicho kibaya sana katika kufanya hivyo?
Kama vile Paulo alivyoeleza, hao “huanguka ndani ya kishawishi na mtego.” Andiko la Mithali 28:20 hutoa hoja kama hiyo isemapo: “Afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa.” Wakifikiri kuwa hawana ya kutosha, vijana wengine wamegeukia kuiba.
Kweli, vijana wengi hawangefikiria kuiba. Lakini wengine wanaweza kujihusisha katika tabia zenye kuhatarisha vilevile. Gazeti Christianity Today laripoti: “Wataalamu fulani huamini kuwa kucheza kamari kupita kiasi kumekuwa uraibu wenye kukua haraka zaidi wa matineja.” Katika eneo moja katika Marekani, “karibu asilimia 90 ya matineja walikuwa wamekata tikiti za bahati nasibu isivyo halali kufikia mwaka wao wa mwisho shuleni.” Vijana wengine hugeukia hatua zenye kukata tumaini hata zaidi. “Ni vigumu kupata kazi nadhifu,” asema Matthew mwenye umri wa miaka 16. “Kwa hiyo mimi hupata nyingi za pesa zangu kwa kuuza na kubadilisha vitu. . . . Mara kwa mara [nilikuwa] nikilangua [dawa za kulevya].”
‘Hutumbukiza Ndani ya Uharibifu’
Kweli, kuwa na pesa kwaweza kumpa mtu hisi ya uhuru. Lakini kama Paulo aelezavyo, mwishowe, ufuatiaji wa pesa waweza kumfanya mtu awe mtumwa wa “tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo.” Ndiyo, mara tu uanzapo kuongozwa na kupenda pesa, tamaa, wivu wa uuaji kimakusudi, na tamaa nyinginezo zenye kuumiza zaweza kukutawala. (Linganisha Wakolosai 3:5.) Makala fulani katika gazeti ’Teen ilionelea kuwa matineja wengine wanaweza kuwa na husuda kuelekea magari au mavazi ya vijana wengine “hivi kwamba wanashindwa kabisa.” Husuda kama hiyo wakati mwingine “huzidi kuwa chuki ya kibinafsi,” makala hiyo yaongezea, “na tineja anakuwa hawezi kufikiria jambo lolote isipokuwa kile ambacho hana.”
Kisha, jua ya kwamba tamaa hiyo ya kutaka mali haitakufanya ‘uanguke tu ndani ya kishawishi’ bali pia yaweza kukufanya ‘utumbukie ndani ya uharibifu na uangamizo.’ Mfafanuzi mmoja wa Biblia Albert Barnes aonelea hivi: “Mfano ni ule wa mvunjiko, ambapo meli na vyote vilivyoko ndani, hutumbukia pamoja. Uharibifu ni kamili. Kuna uangamizo kamili wa furaha, wa wema wa adili, wa sifa, na wa nafsi.”—Linganisha 1 Timotheo 1:19.
Kwa usahihi, basi, Paulo asema kuwa “kupenda fedha [kunakochukua wakati mwingi mno] ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote.” Likiwa tokeo, wengi “wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma kotekote kwa maumivu mengi.” Chukua kwa kielelezo, kijana tutakayemwita Rory. Kufikia umri wa miaka 12 alianza kucheza kamari. “Ilikuwa njia ya kupata pesa bila kufanya chochote,” akumbuka. Punde si punde, alikuwa na deni la mamia ya dola na akiwapuuza marafiki, familia na kazi ya shule. “Nilijaribu kuacha,” akiri, lakini alishindwa mara nyingi. Aliendelea ‘kujichoma mwenyewe kotekote kwa maumivu mengi’ hadi alipotafuta msaada akiwa na umri wa miaka 19. Mwandikaji Douglas Kennedy hatii chumvi wakati ambapo, katika kitabu chake Chasing Mammon, anaita ufuatiaji wa pesa “ono lenye kuvuruga.”
Kupata Usawaziko
Hivyo, shauri la Solomoni lafaa sasa kama lilivyofaa karne zilizopita: “Usijitaabishe ili kupata utajiri; acha kuzitegemea akili zako mwenyewe. Je! utavikazia macho vile ambavyo si kitu? Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa, kama tai arukaye mbinguni.” (Mithali 23:4, 5) Mali za kimwili ni za muda tu, kwa hiyo ni upumbavu kufanya ufuatiaji wa mali kuwa lengo lako kuu maishani. “Sitaki kujifunga katika miradi ambayo ni ya kufuatia vitu vya kimwili kabisa,” asema kijana Mkristo aitwaye Maureen. “Najua tu,” yeye asema, “kwamba hali yangu ya kiroho ndiyo gharama nitakayolipa ikiwa nitajiingiza katika kuchuma pesa tu.”
Kweli, pesa ni za lazima. Na kuwa na mapato ya kutosha kutakuwezesha kuyajali mahitaji yako—na labda hata kuwasaidia wengine kimwili mara kwa mara. (Waefeso 4:28) Jifunze kufanya kazi kwa bidii ili kuchuma pesa kwa kufuata haki. Pia, jifunze kuweka akiba, kupanga bajeti na kutumia pesa zako kwa busara. Lakini usifanye kamwe pesa kuwa jambo la maana zaidi maishani mwako. Jaribu kuwa na maoni yaliyosawazika yaliyoonyeshwa na mwandikaji wa Mithali 30:8, aliyesali hivi: Usinipe umaskini wala utajiri.” Kwa kutanguliza masilahi ya kiroho, utaweza kupata utajiri ulio bora zaidi. Kama vile Mithali 10:22 husema, “baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”
[Picha katika ukurasa wa 13]
Vijana wengi hutaka pesa ili waweze kufikia kiwango sawa na marika zao