Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Vifo vya Vitoto Asanteni kwa sehemu iliyokuwa katika “Kuutazama Ulimwengu” yenye kichwa “Kuvuta Sigareti Kwahusianishwa na Vifo vya Vitoto.” (Januari 22, 1997) Natumaini kwamba kila mama ataichukua kwa uzito sehemu hii. Karibu mvulana wangu mchanga afe kwa Ugonjwa wa Kifo cha Ghafula cha Vitoto (SIDS) kwa sababu niliendelea kuvuta sigareti wakati wa ujauzito. Kwa mwaka mmoja baada ya tukio hili alihitaji kutumia kifaa cha kusaidia moyo wakati wote alipokuwa amelala kidogo ili iwapo moyo wake ungesimama, kifaa hiki kingetoa onyo. Laiti ningalimjua Yehova wakati huo. Ningaliacha kuvuta sigareti, na pengine mimi pamoja na mwana wangu tungaliepuka ogofyo hili.
A. C. A., Marekani
Mwenye Kuteseka kwa Yabisi-Kavu Ningependa kueleza shukrani zangu kwa mambo yaliyompata Luretta Maass, yenye kichwa “Niwapo Dhaifu, Ndipo Niwapo Mwenye Nguvu.” (Januari 22, 1997) Nina umri wa miaka 27 nami pia nimekuwa nikisumbuliwa na baridi yabisi. Ijapokuwa matibabu hupunguza maumivu, nyakati nyingine mimi huhisi nimekatishwa tamaa kidogo na kuvunjika moyo kwa sababu ugonjwa wangu umenilazimu kuacha kutumikia nikiwa mhubiri wa wakati wote. Azimio la Luretta Maass la kumtumikia Yehova licha ya ugonjwa wake, ni lenye kuchochea sana. Sitakubali nivunjike moyo; nataka kufanya zaidi katika kazi ya kuhubiri.
A. B., Italia
Mama yangu amesumbuliwa na baridi yabisi kwa zaidi ya miaka 30. Inasikitisha kwamba maumivu hayo hayawezi kutulizwa hata kidogo. Najivunia mama yangu, kwa kuwa anafaulu kuhudhuria karibu mikutano yote ya kutaniko. Akiwa amekalia kiti chake chenye magurudumu, hushiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na hata aweza bado kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Na licha ya maradhi yake, yeye halalamiki kamwe.
S. M., Ujerumani
Furiko la Noa Makala “Maoni ya Biblia: Furiko—Kweli au Hekaya?” (Februari 8, 1997) kwa kweli ilinisaidia kuchukua kwa uzito tukio hili la kihistoria. Mimi, kama wengine wengi, nilifunzwa juu ya Furiko nilipokuwa na umri mchanga. Hata hivyo, sikutambua kuwa simulizi la Furiko huonwa na wengi kuwa hadithi ya wakati wa kulala tu. Uhakika wa kwamba Yesu alinganisha siku za mwisho na siku za Noa waonyesha kuwa lile Furiko lilikuwa halisi kikweli.
S. M., Marekani
Kukabiliana na Msiba Hivi karibuni nimekabiliana na majaribu mengi, moja baada ya jingine. Niliandikia rafiki mmoja barua nikieleza baadhi ya majaribu haya na kunukuu Zaburi 126:5: “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.” Wazia jinsi nilivyohisi, mara tu baada ya kumalizia barua hiyo, nilipopokea toleo la Februari 8, 1997, lenye makala “Kupanda kwa Machozi, Kuvuna kwa Shangwe,” ambayo msingi wake ulikuwa andiko hilo. Mambo aliyojionea Raymond Kirkup yalikuwa yenye kutia imani nguvu kwelikweli.
P. B., Jamaika
Utunzaji Ule mfululizo “Utunzaji—Kukabili Huo Ugumu” (Februari 8, 1997) umekuwa faraja kubwa kwangu katika wakati ambao umekuwa mgumu zaidi. Mama yangu mpendwa, ambaye amekuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova kwa miaka mingi, ameshindwa na ugonjwa wa akili ambao umemdhoofisha. Pia ana ugonjwa wa kutetemeka na ugonjwa wa yabisi-kavu kali. Nilihuzunishwa na kushtushwa na kudhoofika kwake haraka. Nikiwa mwana wake wa pekee, nimehisi ule uzito wa kumtunza. Lakini makala hiyo ya ajabu ilikuwa yenye kuelewa hali sana! Ilikuja ikiwa zawadi halisi kutoka kwa Yehova. Asanteni sana kwa msaada huu wenye upendo.
R. H., Uingereza