Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 11/22 kur. 18-20
  • Naweza Kushughulikiaje Upendeleo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kushughulikiaje Upendeleo?
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Zuia Ulimi Wako!
  • Ukosefu wa Utii Wenye Hila
  • Hatari ya Kujitenga
  • Ile Hatari ya Husuda
  • Kwa Nini Ndugu Yangu Anapata Uangalifu Wote?
    Amkeni!—1997
  • Wangewezaje Kunitendea Hivyo?
    Amkeni!—1990
  • Nawezaje Kujijengea Jina Bila Kuwategemea Ndugu Zangu?
    Amkeni!—2003
  • Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 11/22 kur. 18-20

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kushughulikiaje Upendeleo?

“Dada yangu ni mdogo wangu kwa miaka miwili naye hupokea uangalifu wote. . . . Haionekani kuwa haki.”—Rebecca.a

KADIRI ndugu au dada yako apatavyo uangalifu zaidi, ndivyo uelekeavyo kuhisi umepuuzwa. Na ikiwa una ndugu aliye na vipawa vyenye kutokeza, anayekabili matatizo mazito, au aliye na mapendezi ama utu unaofanana na wa wazazi wako, yaelekea utapigana vita vikali sana ili upokee uangalifu wowote! Kadiri ufikirivyo juu ya hilo, ndivyo uwezavyo kuumia na kukasirika zaidi.b

Hata hivyo, Biblia inatahadharisha: “Mwe na hofu wala msitende dhambi, tafakarini vitandani mwenu na kutulia.” (Zaburi 4:4) Wakati unapokuwa umeudhika na mwenye hasira, unaelekea zaidi kusema au kufanya jambo ambalo huenda ukajutia baadaye. Kumbuka jinsi Kaini alivyofadhaikia, hali yenye upendeleo ambayo ndugu yake, Abeli, alifurahia pamoja na Mungu. Mungu alimwonya: “Dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde.” (Mwanzo 4:3-16) Kaini alishindwa kudhibiti hisia zake, na matokeo yakawa yenye msiba!

Ni kweli, hukaribii kuwa muua-binadamu kama Kaini. Hata hivyo, upendeleo waweza kuamsha hisia na hisia-moyo zisizofaa. Kwa hiyo huenda ikawa hatari zinakuotea mlangoni pako! Ni zipi baadhi ya hizo? Na waweza kudhibitije hali hii?

Zuia Ulimi Wako!

Wakati Beth alipokuwa na miaka 13, alihisi kwamba wazazi wake walipendelea ndugu yake na kumtendea yeye isivyo haki. Akumbuka: “Tulipigiana makelele sana na mama, lakini hili halikutimiza jambo lolote. Sikuwa nikisikiliza aliyosema, naye hakunisikiliza, kwa hiyo hakuna lililotimizwa.” Labda wewe pia umegundua ya kwamba kupiga makelele hufanya tu hali iwe mbaya zaidi. Waefeso 4:31 lasema: “Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.”

Huhitaji kupiga kelele ili ueleze maoni yako. Kwa vyovyote vile, kwa kawaida mfikio wenye utulivu huwa na matokeo zaidi. Mithali 25:15 lasema: “Kwa uvumilivu mwingi mkuu husadikishwa; na ulimi laini huvunja mfupa.” Kwa hiyo ikiwa wazazi wako waelekea kuwa na hatia ya upendeleo, usipige kelele na kuwashtaki. Ngoja hadi wakati unaofaa, kisha zungumza nao kwa njia ya upole na yenye staha.—Linganisha Mithali 15:23.

Ukilenga kasoro za wazazi wako au kuwashutumu kwa sababu ya jinsi “wasivyo wenye haki,” utakuwa tu ukiwatenganisha nawe au kuwafanya wawe katika hali ya kujitetea. Badala yake waonyeshe waziwazi jinsi matendo yao yanavyokuathiri. (‘Kwa kweli mimi huumia sana mnaponipuuza.’) Huenda wakasukumwa kufikiria kwa uzito hisia zako. Pia ‘uwe mwepesi sana juu ya kusikia.’ (Yakobo 1:19) Huenda hata ikawa kwamba kumbe wazazi wako wana sababu halali za kumpatia ndugu yako uangalifu zaidi. Labda ana matatizo usiyoyafahamu.

Namna gani ikiwa wewe hufoka kwa hasira na kusema bila subira wakati unapokasirika? Mithali 25:28 humlinganisha mtu “asiyetawala roho yake” na mji “usio na kuta”; yaelekea atashindwa na hisia zake zisizokamilika. Kwa upande mwingine, uwezo wa kudhibiti hisia zako ni ishara ya nguvu halisi! (Mithali 16:32) Kwa nini usingoje basi, mpaka utakapotulia kabla ya kueleza jinsi unavyohisi, pengine hata kungojea mpaka siku itakayofuata? Huenda ukaliona kuwa jambo lenye msaada kutoka kwenye hali hiyo, labda kufanya matembezi au mazoezi fulani. (Mithali 17:14) Kwa kuzuia midomo yako, unaweza kuepuka kusema jambo lenye kuumiza au la upumbavu.—Mithali 10:19; 13:3; 17:27.

Ukosefu wa Utii Wenye Hila

Mtego mwingine wa kuepukwa ni kutotii. Marie mwenye umri wa miaka 16 alitambua kwamba ndugu yake mdogo hakuadhibiwa kamwe alipovuruga funzo la Biblia la familia. Akiwa amevunjwa moyo na ule ulioonekana kuwa upendeleo, “alisusia” funzo hilo. Je, umepata kukaa kimya au kudhihirisha roho ya kutoshirikiana wakati ulipohisi hukutendewa kwa njia ya haki?

Ikiwa ndivyo, matendo hayo ya hila yapingana na amri ya Biblia ya kuheshimu na kutii wazazi wako. (Waefeso 6:1, 2) Zaidi ya hilo, ukosefu wa utii huharibu uhusiano wako pamoja na wazazi wako. Ni afadhali kuzungumzia matatizo yako pamoja na wazazi wako. Mithali 24:26 huonyesha kwamba “atoaye jawabu la haki” hustahiwa na wengine. Wakati Marie alipozungumzia jambo hili na mama yake, waliafikiana, na mambo yakaanza kuwa bora.

Hatari ya Kujitenga

Njia nyingine isiyofaa ya kushughulikia upendeleo ni kujitenga na familia au kutafuta uangalifu kutoka kwa wasioamini. Ndilo lililompata Cassandra: “Nilijitenga na familia yangu na kugeukia marafiki walimwengu niliowapata shuleni. Hata nikawa na marafiki wa kiume, na wazazi wangu hawakujua. Kisha nilihuzunika sana nikawa na dhamiri yenye hatia kwa sababu nilijua sikuwa ninafanya jambo jema. Nilitaka kutoka katika hali hii, lakini sikuona namna ya kuwaeleza wazazi wangu.”

Ni hatari kujitenga na familia yako na waamini wenzako—na hasa unapokuwa umeudhika na hufikiri waziwazi. Mithali 18:1 laonya: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.” Ikiwa waliona kuwa jambo gumu kuwafikia wazazi wako wakati huu, tafuta rafiki Mkristo kama yule anayesimuliwa katika Mithali 17:17: “Rafiki [“Mwandamani wa kweli,” NW] hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Kwa kawaida “mwandamani wa kweli” hupatikana kwa urahisi miongoni mwa washiriki waliokomaa wa kutaniko.

Cassandra alipata “mwandamani wa kweli” wakati alipokuwa na uhitaji: “Wakati mwangalizi wa mzunguko [mhudumu asafiriye] alipozuru kutaniko letu, wazazi wangu walinitia moyo nihubiri pamoja naye. Yeye na mke wake walikuwa ni watu wenye msaada sana, na walinionyesha upendezi wa kweli. Ningeweza kuzungumza nao. Sikuhisi kama wangenilaumu. Walitambua ya kwamba kulelewa tu ukiwa Mkristo hakumaanishi umekamilika.” Kitia-moyo chao na mashauri yakawa tu ndiyo Cassandra aliyohitaji!—Mithali 13:20.

Ile Hatari ya Husuda

Mithali 27:4 laonya: “Ghadhabu ni kali, na hasira ni gharika; lakini ni nani awezaye kusimama mbele ya wivu.” Husuda na wivu juu ya ndugu anayependelewa umechochea vijana wengine watende bila subira. Mwanamke mmoja alikiri: “Nilipokuwa mchanga, nilikuwa na tita nyembamba la nywele ya rangi ya hudhurungi na dada yangu alikuwa na nywele za singa zenye kuvutia ambazo ziliteremka hadi kiunoni mwake. Baba yangu alizisifu nywele zake sikuzote. Alimwita ‘Rapunzel’ wake. Usiku mmoja alipokuwa amelala, nilichukua makasi ya mama ya kushonea nikatembea kimya-kimya hadi kitandani mwake na kunyoa nywele nyingi kwa kadiri nilivyoweza.”—Siblings Without Rivalry, cha Adele Faber na Elaine Mazlish.

Si ajabu basi, kwamba katika Biblia husuda huelezwa kuwa mojawapo ya “kazi [mbovu] za mwili.” (Wagalatia 5:19-21; Waroma 1:28-32) Hata hivyo, “mwelekeo wa kuhusudu” hukaa ndani yetu sote. (Yakobo 4:5) Hivyo ukijipata unapanga njama ili ndugu yako aingie taabani, kumfanya aonekane vibaya, au katika njia nyingine kujaribu kumtendea vibaya, husuda yaweza kuwa “inakuotea mlangoni,” ikijaribu kukushinda!

Waweza kufanya nini ukipata ya kwamba unafungia hisia hizo zenye kudhuru? Kwanza, jaribu kusali kwa Mungu ili upate roho yake. Wagalatia 5:16 yasema: “Fulizeni kutembea kwa roho na hamtatekeleza tamaa ya kimwili hata kidogo.” (Linganisha Tito 3:3-5.) Pia inaweza kusaidia kutafakari juu ya hisia zako za kweli kuelekea ndugu yako. Waweza kusema kwa kweli huna upendo wowote kumwelekea—licha ya kinyongo chako? Ndiyo, Maandiko yatuambia kwamba “upendo hauna wivu.” (1  Wakorintho 13:4) Basi kataa kudumu katika mawazo hasi yenye kuamsha husuda. Jaribu kufurahi pamoja na ndugu yako ikiwa anapata uangalifu wa pekee kutoka kwa wazazi wako.—Linganisha Waroma 12:15.

Maongezi yako pamoja na wazazi wako yaweza kuthibitika kuwa yenye mafaa kwa habari hii. Wakisadiki kuwa wanahitaji kukupa uangalifu zaidi, hili litakusaidia sana katika kushinda hisia za husuda kuelekea ndugu zako. Namna gani ikiwa hakuna maendeleo nyumbani na upendeleo wadumu? Usikasirike, usipige makelele, au kuwaasi wazazi wako. Jaribu kudumisha mwelekeo wenye kusaidia na wenye utii. Ikiwa ni lazima, tafuta tegemezo la wale katika kutaniko la Kikristo waliokomaa. Zaidi ya yote, mkaribie Yehova Mungu. Kumbuka maneno ya mtunga-zaburi: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.”—Zaburi 27:10.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Ona makala “Kwa Nini Ndugu Yangu Anapata Uangalifu Wote?” katika toleo la Amkeni! la Oktoba 22, 1997.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kueleza kwamba unahisi umedharauliwa kwaweza kusuluhisha hilo tatizo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki