Vijana Huuliza . . .
Kwa Nini Ndugu Yangu Anapata Uangalifu Wote?
“Kinachonisumbua ni kwamba wakati ndugu na dada zangu wanapokosa adabu, wao hupata uangalifu mwingi sana—chanya na hasi. Lakini kwa vile naelekea kuwa mtiifu, napuuzwa.”—Kay mwenye umri wa miaka 18.a
“Ndugu zangu na dada zangu hupewa uangalifu zaidi na wanatendewa vizuri zaidi. Uangalifu wowote ninaopata kwa kawaida ni namna fulani ya shauri. Ningehisi afadhali ikiwa ningejua kuwa wao hushauriwa pia.”—Ruth mwenye umri wa miaka 15.
“Naona ni kama ndugu na dada zangu wakubwa hupata mapendeleo na uangalifu zaidi.”—Bill mwenye umri wa miaka 13.
KUANZIA siku tunapozaliwa, sisi sote twahitaji uangalifu kutoka kwa wazazi wetu. Na ikiwa wahisi kuwa hupati sehemu yako unayostahili ya uangalifu huo, kwa kueleweka waweza kuhisi kuumizwa na kuwa na hasira. Hasa ikiwa yaonekana kama ndugu yako—mkubwa zaidi, mdogo zaidi, aliye na adabu nzuri zaidi, au hata asiyetii kupita wote—ndiye aonekanaye kila wakati. Waweza hata kuhisi kama Daudi alivyohisi alipoandika: “Nimesahauliwa kama mfu asiyekumbukwa; nimekuwa kama chombo kilichovunjika.”—Zaburi 31:12.
Kumtazama ndugu akipata uangalifu ambao ungependa kuupata kwaweza kuumiza. Lakini hilo ni lazima lamaanisha kuwa hupendwi? La hasha. Wakati mwingine vijana hupata uangalifu zaidi kwa sababu wana uwezo usio wa kawaida au utu wenye urafiki. Kenneth mwenye umri wa miaka 11 asema: “Hata ingawa ndugu yangu mdogo Arthur yuko katika darasa la tatu, anacheza katika bendi ya darasa la tano. Pia anafanya vizuri katika michezo na hesabu. Kwa kweli, yeye hupata alama A katika masomo yake yote shuleni. Nyakati nyingine nafikiri watu humpenda yeye kuliko mimi, lakini simwonei wivu. Labda kidogo tu.”
Kisha kuna vijana wengine wanaoelekea kupata sehemu kubwa zaidi ya wakati wa wazazi wao kwa sababu tu wao ni wakubwa zaidi—au ni wachanga zaidi. Biblia husema kumhusu kijana Yusufu: “Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake.” (Mwanzo 37:3, 4) Kwa upande ule mwingine, Todd mwenye umri wa miaka 18 alihisi kuwa ndugu yake alipendelewa kwa vile alikuwa mkubwa zaidi. Yeye akumbuka: “Wakati mmoja tuliambiwa tulete picha ya utotoni tuliyoipenda zaidi kwa ajili ya mradi fulani shuleni. Ningeweza tu kupata picha chache zangu mwenyewe nami nikaona picha nyingi zaidi za ndugu yangu mkubwa. Ilinifanya nijiulize kwa nini.”
Hata hivyo, mara nyingi ndugu yako hupewa uangalifu zaidi kwa sababu ana tatizo—labda matatizo ambayo wewe huyajui. “Nilipokuwa na umri wa karibu miaka 16, ndugu yangu mkubwa alikuwa na wakati mgumu,” aeleza Cassandra, mwenye umri wa miaka 22 sasa. “Hakuwa na uhakika ikiwa alitaka kweli kumtumikia Yehova, na wazazi wangu wakaelekeza uangalifu wao mwingi zaidi kwake. Wakati huo sikuelewa sababu ya hilo. Nilihisi kuwa hawakunijali hata kidogo. Ilinifanya nihisi huzuni na kujiona nimepuuzwa—kukasirika pia.”
Sababu Inayowafanya Waonyeshe Upendeleo
Hata hivyo, nyakati nyingine, wazazi ni wenye hatia ya kuonyesha upendeleo wa wazi. Mama mmoja alikiri: “Najua kijana wangu, Paul, anajua kwa uchungu tunavyomwonea fahari binti yetu. Yeye ametuambia waziwazi, ‘Wewe na baba huangaliana kila wakati Liz anaposema jambo.’ Mwanzoni hatukujua alikuwa akizungumza juu ya nini. Kisha tukatambua kuwa kila wakati tuliangaliana kwa sababu tulipendezwa na aliyosema binti yetu. Kwa vile ametutahadharisha, tumefanya jitihada kubwa ya kutofanya hivyo tena.”
Kwanza kabisa, kwa nini wazazi huonyesha upendeleo? Sababu yaweza kuwa jinsi wao wenyewe walivyolelewa. Kwa kielelezo, ikiwa mama yako alilelewa akiwa mtoto mchanga zaidi, aweza kuwa karibu zaidi na mtoto wake mchanga zaidi. Bila kutambua hilo, aweza kuwa akikubaliana na huyo mtoto kukiwa na bishano. Ama mzazi aweza kuwa na upendezi kwa mtoto ambaye ana mwelekeo kama wake au mapendezi sawa. Fikiria yale Biblia husema juu ya Isaka na Rebeka kuhusu wana wao mapacha, Yakobo na Esau: “Watoto wakakua, Esau alikuwa mtu ajuaye kuwinda wanyama, mtu wa nyikani, na Yakobo alikuwa mtu mtulivu, mwenye kukaa hemani. Basi Isaka akampenda Esau, kwa sababu alikula mawindo yake, na Rebeka akampenda Yakobo.”—Mwanzo 25:27, 28.
Ufanyeje ikiwa wazazi wako waonekana kuonyesha upendeleo kwa mmoja wa ndugu zako?b Waweza kujaribu kuongea na wazazi wako kwa njia tulivu, isiyo ya kulaumu. (Mithali 15:22) Kwa kuwasikiliza kwa staha, waweza kuona mambo jinsi wayaonavyo. Hii yaweza kutuliza kukatishwa kwako tamaa. (Mithali 19:11) Tineja mmoja husema: “Ilinisumbua sana kuona kwamba mama alivutiwa zaidi na ndugu yangu kuliko mimi. Nilipomwuliza kuhusu hilo, alieleza kuwa ni kwa vile yeye afanana sana na baba, hivyo avutiwa zaidi naye. Na kwa vile mimi nafanana sana naye, baba avutiwa zaidi nami. Hivyohivyo kwa vile mimi na yeye twafanana zaidi, twasumbuana zaidi. Na kwa vile baba na ndugu yangu wafanana sana, wao hukasirishana sana. Alipoeleza hivyo—hata ingawa sikufurahia sana jambo hilo—ningeweza kulikubali.”
Kutendewa kwa Upendeleo—Ni Ukosefu wa Haki?
Hata hivyo, kwa nini wazazi hawawezi kumtendea kila mmoja sawa na mwingine. Beth, ambaye sasa ana umri wa miaka 18, asema: “Nilipokuwa na umri wa karibu miaka 13, nilihisi kuwa ndugu yangu nami tulistahili kutendewa kwa njia sawa—kwa njia ileile. Lakini ni mimi niliyekuwa nikikemewa kila wakati, hali yeye hakuwa akipewa nidhamu yoyote. Na alitumia muda mwingi akiwa na baba wakitengeneza gari. Ilionekana kuwa ukosefu mkubwa wa haki.”
Lakini kupendelea si lazima kuwe ukosefu wa haki. Fikiria jinsi Yesu Kristo alivyowatendea mitume wake. Bila shaka aliwapenda wote 12, hali aliwaalika 3 tu kati yao kushuhudia matukio fulani ya maana, kutia ndani ufufuo wa binti Yairo na mgeuko-umbo. (Mathayo 17:1; Marko 5:37) Zaidi ya hilo, Yesu alikuwa na urafiki wa karibu hasa na mtume Yohana. (Yohana 13:23; 19:26; 20:2; 21:7, 20) Je, ilikuwa ni kupendelea? Bila shaka. Je, ilikuwa ukosefu wa haki? La hasha. Kwani ingawa Yesu alivutiwa na mitume fulani hasa, hakupuuza mahitaji ya mitume wake wengine.—Marko 6:31-34.
Kwa njia sawa na hiyo, yaweza kuwa kwamba mmoja wa ndugu zako apata uangalifu wa pekee kwa sababu ya vipawa, utu, au mahitaji. Kwa kawaida, kuchunguza hili kwaweza kuleta uchungu mwingi. Lakini swali ni, Je, mahitaji yako kwa kweli yanapuuzwa? Unapohitaji shauri la wazazi wako, msaada wao, au tegemezo lao, je, wako tayari kukusaidia? Ikiwa ndivyo, waweza kusema kwa kweli kuwa umetendewa isivyo haki? Biblia hututia moyo kushughulika na wengine “kulingana na mahitaji yao.” (Waroma 12:13) Kwa kuwa wewe na ndugu zako ni watu mmoja-mmoja wenye mahitaji mbalimbali, haitawezekana kwa wazazi wenu kuwatendea sawasawa kila wakati.
Hivyo, Beth, aliyetajwa hapo awali, aling’amua kwamba kutendewa bila upendeleo si haki sikuzote na kwamba kutendewa kwa haki si upendeleo sikuzote. Yeye asema: “Nilikuja kutambua kuwa ndugu yangu nami tu watu wawili tofauti na twahitaji kutendewa kwa njia tofauti. Nikifikiria yaliyopita, siwezi kuamini sikuweza kuona hilo nilipokuwa mchanga zaidi. Nafikiri sikuweza kutambua hilo kwa sababu ya vile nilivyoyaona mambo wakati huo.”
Kujifunza Kuwa Mwenye Ufahamu
Ndiyo, jinsi unavyotenda katika hali yako itategemea sana “jinsi unavyoangalia mambo.” Kama kuangalia kupitia kioo chenye rangi, hisia zako zaweza kuathiri jinsi unavyoyaona mambo. Na uhitaji wa kihisia-moyo wa uangalifu wa wazazi na kukubaliwa nao ni wenye nguvu. Watafiti Stephen Bank na Michael Kahn waonelea: “Hata ikiwa wazazi wangeweza kutimiza ile ndoto isiyowezekana ya kuwatendea watoto wao walio tofauti kabisa kwa usawa kabisa, kila mtoto atawafikiria wazazi wake kuwa wawapendelea watoto wengine.”
Kwa kielelezo, angalia tena vile walivyosema wale vijana watatu mwanzoni. Hali yao yaweza kuonekana kuwa isiyo na matumaini ila tu jambo moja: Wao ni ndugu! Ndiyo, kila mmoja huwazia kuwa hao wengine wanapewa uangalifu zaidi na kwamba yeye ndiye anayepuuzwa! Kisha, mara nyingi, njia yetu ya kuona mambo hupotoshwa. “Mwenye roho ya utulivu ana busara [“ufahamu,” NW],” yasema Mithali 17:27. Kuwa mwenye ufahamu ni kuona mambo kihalisi na kwa njia ifaayo si kihisia. Ufahamu waweza kukusaidia kutambua ya kwamba hata ingawa wazazi wako huenda wasiwatendee kwa usawa, wana masilahi bora zaidi ya nyinyi nyote! Kutambua hili kwaweza kukusaidia kuepuka kukasirika na kuwa mwenye uchungu.
Lakini, namna gani ikiwa yaonekana kwako kwamba kwa kweli hupati uangalifu unaostahili? Waweza kufanya nini? Hili litashughulikiwa katika makala ya Amkeni! ya wakati ujao.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Makala ya baadaye itaendeleza kikamili habari kuhusu jinsi ya kushughulika na upendeleo.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Utendaji wenye upendeleo waweza kuonekana kuwa si wenye haki