Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Utunzaji—Kukabili Huo Ugumu Mfululizo huu bora sana wa makala (Februari 8, 1997) ulinitia moyo sana. Nina miaka 17, na ninamtunza babu yangu ambaye alishikwa na mshtuko wa akili na mama yangu ambaye amekuwa na tatizo la akili. Nilipata faraja kusoma kwamba ni kawaida kukasirikia wagonjwa nyakati fulani na kujiuliza, ‘Kwa nini ni mimi niliyepatwa na jambo hili?’ Pia nilithamini ile makala kuhusu msaada wenye kutumika ambao waweza kupatiwa mtunzaji.
P. T., Italia
Ufafanuzi wenu juu ya hisia za watunzaji wa wapendwa walio wagonjwa ulikuwa sahihi na wenye ufahamu sana. Namshukuru Yehova kwa kuwachochea mwandike makala nzuri hizi. Nina hakika kuwa zitasaidia sisi sote tulio katika hali hii kukubali hali na kuendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe na bidii.
B. V., Jamhuri ya Cheki
Nikiwa nimetaliki hivi karibuni, mimi ni mama ya matineja wawili, na mwana wangu amesumbuliwa sana na Tatizo la Upungufu wa Makini Kutokana na Utendaji wa Kupita Kiasi (ADHD). Ule mkazo unaohusika na mzigo huu ni mkubwa sana. Kupitia makala za juzijuzi juu ya utunzaji, niliweza kuelewa hisi zangu za aibu, hasira, mshuko-moyo na kutoweza kusaidia. Kutaja jambo lenye kutia moyo, ndugu wenye umri mkubwa katika kutaniko wamesaidia sana kumtunza mwana wangu. Ni shangwe kama nini kuona upendo ukionyeshwa kwa matendo!
C. C., Marekani
Mume wangu amerukwa akili naye hutegemea utunzaji wangu. Niliogopa ya kwamba singalifaulu. Jeanny, anayetajwa katika makala, alinipa ushujaa wakati aliposhauri: “Hofu ya kile kiwezacho kutukia mara nyingi ni mbaya kuliko kile kitakachotukia kihalisi.”
A. P., Slovakia
Wakati mmoja nilikuwa mtunzaji na nilikuwa na hisia nyingi zinazotajwa katika hizo makala. Mara nyingi sikuweza kuwaambia wengine juu ya mfadhaiko wangu na hatia yangu. Makala hizi zimeniwezesha kuzungumzia hisia zangu.
F. F., Nigeria
Sikufikiria kamwe kwamba makala hizo za pekee zingaliweza kuchapishwa. Mama yangu amekuwa mgonjwa kitandani tangu mwaka wa 1989. Nikiwa mwana wake wa pekee, bila ndugu wala baba, nilihitaji kutwaa daraka la utunzaji. Nakubaliana na fungu la mwisho katika huo mfululizo—kwamba Yehova na mwana wake Yesu Kristo, ndio watunzaji wenye huruma zaidi. Katika pindi nyingi wakati hali ilipokuwa yenye kutamausha na nikafikiri singeweza kukabiliana nayo, nilimgeukia Yehova kwa sala na kumwomba anisaidie. Kwa kujua tu ya kwamba alinisikiliza, ningehisi nguvu zikinirudia.
M. A. M., Peru
Mume wangu ni mgonjwa, na nimeshuhudia karibu kila jambo lililotajwa na gazeti hilo. Nakumbuka pindi nyingi wakati ndugu na dada walipouliza kuhusu mume wangu. Nyakati nyingine niliudhika, nikijiuliza, ‘Kwa nini wao huuliza kumhusu wakati wote? Namna gani mimi?’ Sasa naelewa kuwa hisia kama hizi ni za kawaida tu.
M. A. I. I., Uhispania
Kasoro za Kujifunza Mimi ni mzazi wa mvulana mwenye umri wa miaka kumi mwenye kuathiriwa vibaya na Tatizo la Upungufu wa Makini Kutokana na Utendaji wa Kupita Kiasi (ADHD). Ninafurahi sana kuwaeleza ya kwamba tangu ule mfululizo wa “Msaada kwa Watoto Wenye Kasoro za Kujifunza” (Februari 22, 1997) ulipochapishwa, marafiki kadhaa wamenieleza kwamba ijapokuwa wamejaribu kuelewa ile kasoro na kunisaidia, hawakupata kamwe kuelewa kabisa jinsi mwana wangu nami tulivyohisi. Wengi wao walieleza kwamba wangekuwa tayari hata zaidi ili kusaidia. Dada mmoja katika kutaniko alitumia wakati fulani kurudia makala hiyo pamoja na mwana wangu na kumtia moyo. Mwana wangu alinijia baadaye na kuomba kusoma gazeti tena.
L. A. D., Marekani