Kudhibiti Hali ya Kuogopa Watu
“Jambo kuu zaidi ambalo wenye kuogopa watu wapaswa kukumbuka ni kwamba magonjwa ya woga huweza kutibiwa vizuri. Si jambo ambalo ni lazima liwasumbue maishani.”—Dakt. Chris Sletten.
KWA furaha, wengi wenye kuogopa watu wamesaidiwa kupunguza wasiwasi wao na hata kukabili hali zenye watu ambazo waliogopa kwa miaka mingi. Ikiwa unashikwa na woga wa watu, uwe na hakika ya kwamba wewe pia unaweza kujifunza njia nzuri za kukabiliana na ugonjwa huo. Ili kufanya hivyo, utahitaji kushughulikia (1) dalili za woga wako, (2) mambo unayoamini kuhusu hali unazoogopa, na (3) tabia ambayo hutokezwa na hofu zako.
Kanuni za Biblia zaweza kusaidia. Ni kweli kwamba Neno la Mungu si kitabu cha kitiba, wala halitaji ugonjwa wa “kuogopa watu.” Lakini, Biblia inaweza kukusaidia ‘kushika hekima kamili na busara’ unaposhughulikia hofu zako.—Mithali 3:21; Isaya 48:17.
Kudhibiti Dalili za Woga Wako
Dalili zinazoonyesha kuogopa watu hutofautiana kwa kila mtu. Mwili wako hutendaje unapokaribia hali unayoihofu? Je, mikono yako hutetemeka? Je, moyo wako hupiga haraka-haraka? Je, wewe hupata maumivu ya tumbo? Je, wewe hutoka jasho au hubadilika uso, au mdomo wako hukauka?
Ni kweli kwamba haipendezi kufikiri juu ya kutoka jasho, kugugumiza, au kutetemeka mbele ya wengine. Lakini kuwa na wasiwasi juu ya litakalotokea hakutasaidia. Yesu aliuliza kwa kufaa hivi: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika aweza kuongeza dhiraa moja kwenye muda wake wa uhai?” (Mathayo 6:27; linganisha Mithali 12:25.) Kwa kweli, kukazia tu akili juu ya dalili unazoonyesha unapokuwa na woga na vile huenda wengine wakafikiri kunaweza tu kuharibu mambo zaidi. “Wakifikiri kuwa watu wengine wanatambua kwamba wana wasiwasi, wenye kuogopa watu huhangaika hata zaidi,” lasema The Harvard Mental Health Letter. “Wao hutarajia kwamba wataharibu mambo—tazamio ambalo hutokeza mahangaiko zaidi wanapokaribia hali wanazoogopa.”
Unaweza kupunguza ukali wa dalili za woga wako kwa kupumua polepole kutoka kwenye kiwambo. (Ona sanduku “Chunga Jinsi Unavyopumua!”) Mazoezi ya kawaida yenye kutuliza misuli ni muhimu pia. (1 Timotheo 4:8) Huenda pia ukahitaji kufanya mabadiliko fulani katika njia yako ya maisha. Kwa mfano, Biblia hushauri hivi: “Heri konzi moja pamoja na utulivu, kuliko konzi mbili pamoja na taabu; na kujilisha upepo.” (Mhubiri 4:6) Basi hakikisha kwamba unapumzika vya kutosha. Kwa kuongezea, chunga ulaji wako. Usiwe unakosa kula nyakati nyingine na unapaswa kula saa zilezile ambazo wewe hula. Huenda ikawa lazima kupunguza kafeini, ambayo yaweza kuchangia sana kutokeza wasiwasi.
Zaidi ya yote, uwe mwenye subira. (Mhubiri 7:8) Kikundi kimoja cha madaktari charipoti hivi: “Baada ya muda, utaona kwamba, ingawa bado unahisi wasiwasi fulani katika hali fulani zenye watu, dalili zako za woga zitapunguka sana. Jambo muhimu zaidi ni kwamba kwa kufanya mazoezi, utakuwa mwenye uhakika zaidi, nawe utakuwa katika hali njema zaidi ya kuingia katika hali zenye watu ambazo wewe huhofu.”
Kuzikabili Fikira Zako Zinazotokeza Woga
Imesemwa kwamba huwezi kupatwa na hisia fulani bila ya wewe kuifikiria kwanza. Ndivyo ilivyo na kuogopa watu. Kwa hiyo, ili kupunguza dalili zinazoonyesha woga wako, huenda ukahitaji kuchunguza “mawazo ya moyoni” ambayo huzichochea.—Zaburi 94:19.
Wataalamu fulani husema kwamba kuogopa watu hasa ni hofu ya kukataliwa na watu. Kwa mfano, katika kikusanyiko cha kirafiki, mtu anayeogopa watu aweza kujiambia hivi, ‘Naonekana mjinga. Ni lazima watu wanaona kwamba sifai hapa. Nina hakika kila mtu ananicheka.’ Tracy, ambaye aliogopa watu alikuwa na hisia kama hizo. Lakini, baadaye alifikiria hisia hizo. Akatambua kwamba watu hawana wakati wa kumchunguza na kumhukumu. “Hata nikisema jambo ambalo halichekeshi,” Tracy akata kauli, “je, inafaa kwa mtu mwingine kunikataa kwa sababu ya jambo hilo?”
Kama Tracy, huenda ukahitaji kukabili mawazo mapotovu kama hayo ya uwezekano wa kukataliwa na wengine na kadiri ya kukataliwa na wengine katika vikusanyiko vya kirafiki. Je, kweli kuna sababu nzuri za kuamini kwamba watu wataudhika nawe ikiwa kweli utafanya vile unavyohofu? Hata kama wengine wataudhika, je, kuna sababu ya kukata kauli kwamba masaibu hayo hayatapita? Je, kweli maoni ya mtu mwingine yaweza kubadili jinsi wewe ulivyo? Biblia yashauri hivi kwa hekima: “Usitie moyoni mwako maneno yote yaliyosemwa.”—Mhubiri 7:21.
Kikiandika juu ya woga wa watu, kikundi fulani cha madaktari kilisema: “Matatizo hutokea wakati watu wanapofikiria kupita kiasi matokeo ya kukataliwa na wengine. Kukataliwa na wengine kwaweza kuvunja moyo sana. Kwaweza kuumiza sana. Lakini si lazima kukuvunje moyo. Si msiba ila tu wewe ukuone kuwa msiba.”
Biblia yatusaidia tujione kihalisi. Inakiri hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2) Ndiyo, hakuna mtu ambaye amekamilika na asiyepatwa na hali zake ambazo nyakati nyingine huaibisha. Kujua jambo hili hutusaidia kukubali udhaifu wa wengine, na kutia moyo wengine watuelewe pia. Na hata hivyo, Wakristo wajua kwamba yule ambaye kibali chake ni muhimu kabisa ni Yehova Mungu—naye hazingatii makosa yetu.—Zaburi 103:13, 14; 130:3.
Kukabili Hofu Zako
Ili kushinda vita vyako dhidi ya woga wa watu, upesi au baadaye utahitaji kukabili hofu zako. Mwanzoni, huenda ukatishwa na wazo hilo. Mpaka sasa, labda umeepuka vikao vya kirafiki ambavyo huenda vikachochea hofu zako. Lakini, yaelekea kwamba hali hiyo iliondoa uhakika wako na kuzidisha hata zaidi hofu zako. Kwa sababu nzuri, Biblia yataarifu hivi: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.”—Mithali 18:1.
Kwa kutofautisha, kukabili hofu zako huenda kukapunguza wasiwasi wako.a Dakt. John R. Marshall asema: “Mara nyingi sisi huwatia moyo wenye kuogopa watu—hasa wale ambao wanahofu hali fulani hususa, kama kuogopa kusema mbele ya watu—wajilazimishe kutenda katika hali na mashirika yanayohitaji wachangamane na watu.”
Kukabili hali ambazo umehofu kutakusadikisha (1) kwamba kasoro zenye aibu mara nyingi hazitafanya ukataliwe na wengine na (2) kwamba hata zikifanya ukataliwe kwa kadiri fulani, huo si msiba. Lakini, kumbuka uwe mwenye saburi na maendeleo yako. Huwezi kufanikiwa mara moja, wala si jambo halisi kutarajia woga wote upotee. Kulingana na Dakt. Sally Winston, lengo la tiba, si kuondoa dalili zinazoonyesha woga wako, bali ni kuzifanya zisiwe jambo kuu. Ikiwa dalili hizo za woga si jambo kuu, basi hizo hupotea au angalau hupungua.
Wakristo wana kichocheo chenye nguvu cha kushinda hofu zao za watu. Kwa kweli, wao huambiwa “tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe.” (Waebrania 10:24, 25) Kwa kuwa utendaji wa Kikristo mara nyingi huhusisha kuchangamana na wengine, kufanya bidii kudhibiti hofu zako za watu kwaweza kusaidia sana maendeleo yako ya kiroho. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 2:42; 1 Wathesalonike 5:14) Mtajie Yehova Mungu jambo hilo katika sala, kwa kuwa yeye aweza kukupa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.” (2 Wakorintho 4:7; 1 Yohana 5:14) Omba Yehova akusaidie kupata usawaziko juu ya kibali cha wengine na kusitawisha stadi za kufanya kile anachotaka.
Ni kweli kwamba matatizo ya kila mtu mwenye woga wa watu ni ya kipekee, na kila mmoja atakuwa na mambo tofauti ya kukabili na nguvu tofauti za kukabiliana. Wengine wamefanya maendeleo makubwa sana kwa kutumia madokezo ambayo yamezungumziwa. Kuna visa ambavyo huenda msaada zaidi ukahitajika. Kwa mfano, wengine wametibiwa.b Wengine wametafuta msaada wa wataalamu wa akili. Amkeni! halipendekezi wala kudhamini tiba aina fulani hususa. Ni uamuzi wa kibinafsi kwa Mkristo kufuatia tiba hiyo. Lakini apaswa kuwa mwangalifu ili tiba yoyote anayopokea isihitilafiane na kanuni za Biblia.
Watu ‘Wenye Hisia Kama Zetu’
Biblia yaweza kuwa kitia-moyo kikubwa, kwa kuwa ina mifano halisi ya watu ambao walishinda magumu yao ili wafanye matakwa ya Mungu. Fikiria Eliya. Akiwa mmoja wa manabii mashuhuri zaidi katika Israeli, yeye alionyesha ujasiri uwezao kuonekana kuzidi ule wa kibinadamu. Lakini, Biblia inatuhakikishia kwamba “Eliya alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu.” (Yakobo 5:17) Yeye aliweza kupatwa na pindi za hofu kuu na wasiwasi.—1 Wafalme 19:1-4.
Mtume Mkristo Paulo alienda Korintho “katika udhaifu na katika hofu na kwa kutetemeka sana,” yaonekana kwa sababu alitilia shaka sana uwezo wake mwenyewe. Na kwa kweli yeye alikataliwa kwa kiasi fulani. Kwa kweli, wapinzani fulani wa Paulo walisema hivi: “Kuwapo kwake mwenyewe binafsi ni dhaifu na usemi wake wa kudharaulika.” Lakini, hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba Paulo aliruhusu maoni ya wengine yaliyopotoka kuathiri jinsi alivyojiona mwenyewe au alivyoona uwezo wake.—1 Wakorintho 2:3-5; 2 Wakorintho 10:10.
Musa alikosa uhakika katika uwezo wake wa kumfikia Farao, akidai kuwa yeye ‘si mwepesi wa kusema na ulimi wake ni mzito.’ (Kutoka 4:10) Hata Yehova Mungu alipoahidi kumsaidia, Musa aliomba: “Hasha, Bwana, tafadhali tuma mtu mwingine.” (Kutoka 4:13, Today’s English Version) Musa hakutambua uwezo wake, lakini Yehova alitambua uwezo wake mbalimbali. Alimwona Musa kuwa mtu mwenye uwezo wa kiakili na kimwili wa kutimiza mgawo huo. Na bado, kwa upendo Yehova alimwandalia Musa msaidizi. Yeye hakumlazimisha Musa amkabili Farao akiwa peke yake.—Kutoka 4:14, 15.
Yeremia vilevile alikuwa kielelezo chenye kutokeza kwa habari hii. Alipopewa utume wa kuwa nabii wa Mungu, kijana huyo alijibu: “Aa, Bwana MUNGU! tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” Yeremia hakuwa na uwezo wa kutekeleza mgawo wake. Lakini, Yehova alikuwa naye. Alimsaidia Yeremia awe “mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote.”—Yeremia 1:6, 18, 19.
Basi, ikiwa hofu na wasiwasi zakufanya uteseke, usikate kauli ya kwamba huna imani au kwamba Yehova amekukataa. Tofauti na hiyo, “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.”—Zaburi 34:18.
Kwa kweli, vielelezo vya Biblia vinavyotajwa juu vyaonyesha kwamba hata wanaume thabiti wenye imani walipambana na hisia za kupungukiwa. Ingawa Yehova hahitaji zaidi ya jinsi kila mmoja awezavyo kutoa, aliwasaidia Eliya, Paulo, Musa, na Yeremia watimize mengi zaidi kuliko walivyotazamia. Kwa kuwa Yehova “anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi,” uwe na hakika ya kwamba anaweza kukusaidia pia.—Zaburi 103:14.
[Maelezo ya Chini]
a Madaktari fulani hupendekeza kwamba hatua hii ikionekana kuwa ngumu sana, fanya mazoezi kwa kujiwazia tu mwenyewe kwamba upo katika hali unazoogopa. Wazia matukio yote katika hali hiyo kadiri iwezekanavyo. Huenda ukawa na wasiwasi zaidi; lakini endelea kujikumbusha kwamba haielekei utakataliwa na wengine au kukataliwa hakuwezi kuwa kubaya jinsi ufikirivyo, na uwazie mwisho wa hali hiyo unaounga mkono maoni yako.
b Wale wanaofikiria kutibiwa wapaswa kupima hatari na manufaa za tiba hiyo. Wao pia wapaswa kufikiria ikiwa woga wao ni mbaya sana hivi kwamba wanahitaji dawa. Wataalamu wengi huhisi kwamba dawa hufanya kazi vizuri zaidi ikiwa inaambatana na mashauri yanayoshughulikia hofu na tabia za mtu huyo mwenye woga.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
Chunga Jinsi Unavyopumua!
WATU wengine wanaoogopa watu huweza kupunguza dalili zinazoonyesha woga wao kwa kuzingatia jinsi wanavyopumua. Kwanza, hiyo huenda ikaonekana kuwa ajabu. Kwani, kila mtu anajua kupumua! Lakini watalaamu wasema kwamba watu wengi wenye matatizo ya mahangaiko hawapumui vizuri. Mara nyingi, wanapumua kidogo-kidogo, haraka-haraka, au wanapumua sana kutoka kifuani.
Fanya mazoezi ya kupumua ndani na nje polepole. Kupumua kupitia pua badala ya mdomo hufanya iwe rahisi sana kupumua polepole. Pia, jifunze kupumua kutoka kwenye kiwambo cha kifua, kwa kuwa kupumua kutoka sehemu ya juu ya kifua huongeza uwezekano wa kupumua haraka-haraka. Ili ujipime kwa habari hii, unapokuwa umesimama, weka mkono wako mmoja juu kidogo tu ya nyonga na mwingine katikati ya kifua chako. Unapopumua, tazama ni mkono upi unaosonga zaidi. Ikiwa ni mkono ulio kwenye kifua chako, unahitaji kufanya mazoezi ya kupumua kutoka kwenye kiwambo cha kifua.
Bila shaka, si lazima kila pumzi itoke kwenye kiwambo cha kifua. (Uwiano wa kawaida wa pumzi ya kiwambo cha kifua na pumzi ya kifua ni karibu mara 4 kwa 1, lakini hiyo hutofautiana nyakati nyingine.) Na yafaa kutahadhari: Wale ambao wana matatizo ya kudumu ya kupumua—kama ugonjwa wa kuvimba mapafu au pumu—wapaswa kumwona daktari kabla ya kuanza kutumia mbinu hizo za kupumua.
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Woga Utokezapo Hofu ya Ghafula
WATU fulani wenye kuogopa watu huwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba wanashikwa na hofu ya ghafula. Hofu hiyo ya ghafula na yenye nguvu sana hufanya mtu apumue haraka-haraka sana, ahisi anataka kuzimia, na ahisi kama anapatwa na mshiko wa moyo.
Watafiti wanasema kwamba njia bora ni kutong’ang’ana na hofu hiyo. Badala yake, wao humshauri mwenye hofu ‘avumilie’ mpaka iishe. “Huwezi kuikomesha mara ianzapo,” asema Jerilyn Ross. “Ni lazima itulie yenyewe. Endelea tu kujiambia kwamba inahofisha, lakini si hatari. Itaisha.”
Melvin Green, ambaye ni mkurugenzi wa shirika linalotibu watu wanaoogopa sehemu za peupe, hulinganisha hofu hiyo na wimbi dogo liwezalo kuonekana likielekea kwenye ufuo. “Hilo lalingana na hofu yako ya kwanza,” yeye asema. “Wimbi hilo likaribiapo bara hilo huzidi kuwa kubwa na kubwa. Hilo lafanana na hofu yako inayozidi kuongezeka. Punde si punde wimbi hilo ni kubwa sana na limefikia upeo. Kisha linaisha na kuwa dogo tena na kutokomea kwenye ufuo. Mfano huo waonyesha mwanzo na mwisho wa hofu yako.” Green asema kwamba wenye hofu hawapaswi kung’ang’ana na hofu zao, lakini waziache zitulie zenyewe.
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Ili kusaidia kupunguza wasiwasi wako, chunga ulaji wako, fanya mazoezi kwa ukawaida, na upumzike vizuri
[Picha katika ukurasa wa 10]
Yehova aliwasaidia wanaume kama Musa watimize mengi zaidi katika utumishi wao kuliko walivyotazamia