Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 8/8 kur. 3-5
  • Kusamehe na Kusahau Je, Kwawezekana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kusamehe na Kusahau Je, Kwawezekana?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Athari za Kiakili na za Kihisia-Moyo
  • Tufanye Nini?
  • Je, Tuyakumbuke Yaliyopita?
    Amkeni!—1998
  • Ukatili—Mungu Ana Suluhisho Gani?
    Amkeni!—1998
  • Ulimwengu Ulikuwaje Miaka 50 Iliyopita?
    Amkeni!—1995
  • Ulimwengu wa Leo Wenye Ukatili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 8/8 kur. 3-5

Kusamehe na Kusahau Je, Kwawezekana?

ZAIDI ya nusu-karne imepita tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, mwaka wa 1945. Vita hiyo ya duniani pote ilikuwa yenye ukatili zaidi na yenye hasara zaidi kuliko vita vyote katika historia ya wanadamu.

Vita ya Ulimwengu ya Pili ilidumu kwa miaka sita na kusababisha vifo vya watu wapatao milioni 50, kutia ndani raia. Wengine wengi walilemazwa kimwili, na kuvurugika kiakili na kihisia-moyo. Wengi ambao walipitia miaka hiyo ya vita yenye msiba, wangali wanakumbuka kwa uchungu ukatili uliofanywa na kuwakumbuka wapendwa wao waliokufa.

Kuna kumbukumbu za ukatili uliofanywa na Wanazi wakati wa yale Maangamizi Makubwa, wakati ambapo mamilioni ya watu wasio na hatia waliuawa kinyama. Katika Ulaya na Asia, ukatili mwingi ulifanywa na majeshi yenye kushambulia, ambayo yaliua, yalibaka, yalipora, na kuhofisha raia. Vilevile, watu wengi waliathiriwa na mashambulizi ya ndege za kijeshi ambazo zilisababisha uharibifu mkubwa, majeruhi, na vifo vya wanaume, wanawake, na watoto wengi wasio na hatia. Mamilioni ya wanajeshi pia walipata magumu katika vita mbalimbali duniani.

Athari za Kiakili na za Kihisia-Moyo

Athari nyingi za kiakili na za kihisia-moyo zilizosababishwa na matukio yenye kuogofya sana ya wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili zingali dhahiri shahiri katika akili za watu wengi walioishi wakati huo ambao bado wangali hai. Wangependa kuzisahau kumbukumbu hizo mbaya na zenye uchungu. Lakini wameshindwa. Wengine hurudiwa na picha za ukatili huo ambao huwatesa kama ndoto za kutisha zenye kujirudia-rudia.

Hata hivyo, wengine hawataki kusahau ama kwa sababu wanataka kulipiza kisasi ama kwa sababu wanataka kuwakumbuka wenzao waliouawa. Na pia kuna maoni yaliyoenea kwamba ukatili uliofanywa zamani wapaswa kukumbukwa na wanadamu kwa ujumla kwa matumaini ya kwamba hautarudiwa kamwe.

Miaka michache iliyopita, katika kipindi cha 1994-1995, hisia zilizoenea wakati wa maadhimisho ya miaka 50 ya Siku Kubwa (siku ambayo mataifa yenye Muungano yalipoanza mashambulizi katika Normandy Juni 1944) na mwisho wa vita ya ulimwengu ya pili katika Ulaya (mnamo Mei 1945) yalidhihirisha kwamba ilikuwa vigumu sana kwa wengi waliojionea mambo hayo kusamehe na kusahau. Mara nyingi, pendekezo lolote la kutaka mapatano kati ya wale ambao zamani walikuwa maadui hukataliwa. Kwa hiyo, mashujaa wa vita wa Uingereza walikataa kualika wawakilishi wa Ujerumani katika maadhimisho ya kuingia kwa majeshi ya Muungano katika Normandy.

Kuhusu ukatili uliofanywa na Wanazi katika Vita ya Ulimwengu ya Pili na ugumu wa kusamehe na kusahau, mwandikaji Vladimir Jankélévitch alijieleza hivi: “Kuhusu uhalifu wenye kuchukiza sana hivyo, elekeo la kawaida . . . ni kughadhabika na kukataa katakata kusahau na kuwasaka wahalifu hao—kama walivyoahidi mahakimu wa Mahakama ya Mataifa yenye Muungano ya Nuremberg—hadi mwisho wa dunia.” Mwandikaji uyo huyo aliendelea kusema: “Tungefurahi kusema, tukifuata kinyume cha ile sala ambayo Yesu alimtolea Mungu katika Gospeli kulingana na Mtakatifu Luka: Bwana, usiwasamehe, kwa kuwa wanajua wanachofanya.”—Linganisha Luka 23:34.

Kwa kuhuzunisha, tangu 1945 na kuendelea, hadi wakati wetu, ukatili mwingine mwingi umeendelea kumwaga damu duniani—nchini Kambodia, Rwanda, Bosnia, tukitaja kifupi tu. Ukatili huo umesababisha vifo vya mamilioni ya watu, na vilevile kuacha idadi kubwa sana ya wajane na mayatima, maisha yaliyoharibiwa, na kuacha wengi wakiwa na kumbukumbu zenye kusikitisha sana.

Bila shaka, karne hii ya 20 imekuwa wakati wa ukatili mbaya zaidi. Ni kama tu Biblia ilivyotabiri kwa usahihi muda mrefu kabla ya wakati huu—watu wamekuwa “wakali” na “wasio na upendo wa wema.”—2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 6:4-8.

Tufanye Nini?

Watu wakikabili ukatili kama huo, wao hutenda kwa njia tofauti-tofauti. Lakini vipi sisi? Je, tuukumbuke? Au tuusahau? Je, kukumbuka kwamaanisha kuwafungia kinyongo cha ndani maadui wa zamani, tukikataa kusamehe? Kwa upande mwingine, je kusamehe kwamaanisha kwamba mtu aweza kusahau kabisa kumbukumbu zote zenye uchungu?

Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu, anafikiri nini juu ya uhalifu wenye ukatili ambao umefanywa katika wakati wetu na katika nyakati zilizopita? Je, atawasamehe waliofanya ukatili? Na je, haijachelewa mno kwa Mungu kuwapa ridhaa watu waliokufa katika ukatili huo? Je, kuna tumaini lolote thabiti kwamba ukatili utapata kwisha, kwa kuwa umekuwa ukiendelea kwa maelfu ya miaka? Mungu Mweza-Yote atasuluhishaje mambo hayo yenye kutatanisha?

[Picha katika ukurasa wa 4]

Watoto ambao wazazi wao waliuawa kikatili wakutana katika kambi ya wakimbizi

[Hisani]

UN PHOTO 186797/J. Isaac

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

U.S. Navy photo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki