Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 8/8 kur. 8-11
  • Ukatili—Mungu Ana Suluhisho Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukatili—Mungu Ana Suluhisho Gani?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Unafiki
  • Masomo Tunayopata Katika Biblia
  • Mambo Anayoyakumbuka Mungu na Anayoyasahau
  • Hakimu wa Mwisho
  • Ulimwengu Mpya U Karibu!
  • Kusamehe na Kusahau Je, Kwawezekana?
    Amkeni!—1998
  • Je, Tuyakumbuke Yaliyopita?
    Amkeni!—1998
  • Mungu wa Kweli na Wakati Ujao Wako
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
  • Utawala wa Haki Wafanya Dunia kuwa Paradiso
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 8/8 kur. 8-11

Ukatili—Mungu Ana Suluhisho Gani?

UKATILI unaweza kuzuiwaje? Kuna suluhisho gani? Tunapojifunza historia, inakuwa wazi kwamba masuluhisho ya wanadamu yameshindwa. Kwa hakika, kuna kujipinga kwingi, au hata unafiki wa wazi, katika njia ambayo viongozi wa kibinadamu wameshughulikia jambo hili.

Kwa mfano, fikiria mwaka wa 1995. Huo ulikuwa uadhimisho wa mwaka wa 50 wa mwisho wa Maangamizi Makubwa ya Nazi, wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, na kulipuliwa kwa bomu la atomu. Mwaka huo, sherehe za ukumbusho zilizohudhuriwa na viongozi wa ulimwengu zilifanywa katika sehemu nyingi za ulimwengu. Kwa nini? Ili kuonyesha jinsi wanavyokirihi ukatili uliofanywa ili usipate kurudiwa tena. Lakini, wachunguzi fulani waliona tu kujipinga kubaya katika sherehe hizo.

Unafiki

Katika sherehe hizo zilizotangazwa sana, wawakilishi wote wa kidini na wa kiserikali walitaka waonwe kuwa wafadhili au angalau wasionwe kuwa waovu. Lakini, mataifa yaliyoshutumu ukatili uliofanywa wakati uliopita yamejirundikia silaha, yakipanga bajeti ya pesa nyingi sana kwa sababu ya vita. Wakati uo huo, hayajasuluhisha matatizo mazito kama vile umaskini, kupotoka kwa maadili, na uchafuzi, mara nyingi yakisema kwamba hayana pesa za kutosha.

Dini ya kilimwengu inataka kuandika upya historia ambayo inafunika ukimya wake wa muda mrefu juu ya ukatili wa utawala wa kimabavu na kuficha ushirikiano wake na watawala hao wa kimabavu. Dini hizo hazikuzuia kamwe watu wa dini moja wasiuane. Kwa mfano, katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, Mkatoliki alimwua Mkatoliki na Mprotestanti alimwua Mprotestanti eti kwa sababu walikuwa watu wa mataifa tofauti na kwenye pande zinazopigana. Pande zote mbili zilidai kuwa za Kikristo lakini zikafanya mambo yaliyokuwa tofauti kabisa na mafundisho ya Yesu. (Mathayo 26:52; Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:10-12; 4:20, 21) Dini nyinginezo zimefanya vivyo hivyo. Leo, katika sehemu nyingi za ulimwengu, ukatili ungali unafanywa na watu wa dini hizo.

Wakati wa Yesu, viongozi wa kidini walikuwa wanafiki. Yesu aliwashutumu, akisema: “Ole wenu nyinyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa sababu nyinyi mwajenga makaburi ya manabii na kuyarembesha makaburi ya ukumbusho ya waadilifu, nanyi mwasema, ‘Kama tungekuwa katika siku za baba zetu wa zamani, hatungekuwa washiriki pamoja nao katika damu ya manabii.’ Kwa hiyo mnatoa ushahidi dhidi yenu wenyewe kwamba nyinyi ni wana wa wale waliowaua manabii kimakusudi.” (Mathayo 23:29-31) Viongozi hao wa kidini walidai kuwa wenye kumcha Mungu lakini walikuwa wanafiki ambao walimnyanyasa Yesu na wanafunzi wake.

Masomo Tunayopata Katika Biblia

Masomo yaweza kupatikana katika historia ya kilimwengu, lakini Biblia ndiyo chanzo cha masomo yenye kunufaisha zaidi. Haimwachii mwanadamu ajifasirie mwenyewe historia yake kwa kupatana na uamuzi wake au ubaguzi wake. Biblia yafafanua historia na wakati ujao katika njia ya Mungu ya kufikiri.—Isaya 55:8, 9.

Maandiko yasema juu ya matukio mema na mabaya na vilevile juu ya watu wema na wabaya. Mara nyingi somo lenye kufaa, lenye kupatana na mapenzi ya Mungu, laweza kupatikana katika masimulizi hayo. Baada ya kutaja matukio kadhaa katika historia ya Israeli la kale, mtume Paulo alimalizia hivi: “Basi mambo hayo yaliendelea kuwapata kuwa vielelezo, nayo yaliandikwa kuwa onyo kwetu sisi.” (1 Wakorintho 10:11) Yesu mwenyewe alitaja somo la historia alipowaambia wanafunzi wake: “Mkumbukeni mke wa Loti.”—Luka 17:32.

Mambo Anayoyakumbuka Mungu na Anayoyasahau

Twajifunza katika Biblia kwamba Mungu huwakumbuka watu au huwasahau kwa kutegemea matendo yao. Wale wanaotenda dhambi lakini wanatubu husamehewa na Mungu “kabisa.” (Isaya 55:7) Mwovu akitubu na ‘kuacha dhambi yake, na kutenda yaliyo halali na haki; dhambi zake zote alizozitenda, hata mojawapo haitakumbukwa juu yake.’—Ezekieli 33:14-16.

Paulo aliandika kwamba “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Waebrania 6:10) Basi, Yehova atawathawabisha wale ambao yeye awakumbuka kwa mema. Yobu mwaminifu alisali hivi: “Laiti ungenificha kuzimuni [kaburi la kawaida la wanadamu wote], . . . na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka!”—Ayubu 14:13.

Kwa kutofautisha, Mungu atashughulikia mwovu asiyetubu kupatana na maneno ambayo Yeye alimwambia Musa: ‘Nitamfuta katika kitabu changu.’ (Kutoka 32:33) Ndiyo, Mungu atawasahau waovu milele.

Hakimu wa Mwisho

Mungu ndiye Hakimu wa mwisho wa historia. (Mwanzo 18:25; Isaya 14:24, 27; 46:9-11; 55:11) Kulingana na hukumu yake bora, hatasahau ukatili mwingi ambao wanadamu wametendwa. Katika siku ya hasira yake yenye uadilifu, atawahukumu watu wote na mashirika yote yenye hatia.—Ufunuo, sura ya 18 na 19.

Miongoni mwa hao kutakuwamo mfumo wa ulimwengu wa dini isiyo ya kweli, ambao Maandiko yameupa jina la ufananisho “Babiloni Mkubwa.” Imeandikwa hivi juu yake: “Dhambi zake zimetungamana pamoja hadi mbinguni, na Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki.”—Ufunuo 18:2, 5.

Dini hizi zilitakikana zifundishe wafuasi wake kufanya yaliyo mema lakini zilishindwa. Hivyo, Neno la Mungu lasema hivi kuhusu dini yote ya kilimwengu: “Katika yeye ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wote wale ambao wamechinjwa juu ya dunia.” (Ufunuo 18:24) Kwa sababu ya kushindwa kuagiza wafuasi wao wapende watu na wanadini wenzao, dini hizo zina hatia ya damu.

Ulimwengu Mpya U Karibu!

Siku ambayo maovu yataondolewa i karibu. (Sefania 2:1-3; Mathayo 24:3, 7-14) Baada ya wakati huo, kutakuwa na wakati ambapo hakutakuwapo tena ‘ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu’ kwa wakazi wenye furaha wa dunia. (Ufunuo 21:3-5) Ukatili na mauaji ya kikatili hayatatukia tena kwa sababu utawala wa dunia hii utachukuliwa kutoka kwa wanadamu na kupewa Ufalme wa kimbingu wa Mungu utakaokuwa mikononi mwa “Mfalme wa Amani,” Yesu Kristo.—Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

Wakati huo unabii ulio katika Zaburi 46:9 utatimizwa kabisa: “[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia.” Amani hiyo itadumu milele kwa sababu, kama Isaya 2:4 linavyotabiri, “taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Hivyo Zaburi 37:11 inatabiri: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” Ndiyo, ndipo itakaposemwa kwamba “dunia yote inastarehe na kutulia; hata huanzilisha kuimba.”—Isaya 14:7.

Yote haya yamaanisha kwamba ulimwengu mpya wenye uadilifu u karibu. Na katika ulimwengu huo mpya, chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu, tukio jingine zuri ajabu litatukia—ufufuo wa wafu! Neno la Mungu lahakikisha hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.

Alipokuwa duniani, Yesu alidhihirisha jambo hilo kwa kuwafufua watu. Kwa mfano, alipomfufua msichana mmoja, masimulizi hayo yanasema: “Na mara yule mwanamwali akainuka akaanza kutembea . . . Na mara moja [watazamaji] wakapigwa na bumbuazi ya upeo wa shangwe kubwa.” (Marko 5:42) Katika ufufuo wale waliouawa katika ukatili uliofanywa na vilevile wengine ambao walikufa zamani watainuliwa kutoka kwa wafu na kupewa fursa ya kuishi milele katika dunia paradiso. (Luka 23:43) Na baada ya muda “mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17.

Ni jambo la hekima kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu, Biblia, na kufanya mapenzi yake. Ndipo Mungu atakapokukumbuka kwa mema wakati ambapo atasuluhisha kwa umilele tatizo la ukatili na kurudisha hai wanadamu walioathiriwa. Yesu alisema: “Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Mungu ataigeuza dunia hii iwe paradiso yenye amani

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mungu ataondoa athari za ukatili uliofanywa kwa kuwafufua wafu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki