Mageuzi Si Jambo la Hakika
Kura za maoni zaonyesha kwamba Wamarekani wengi huamini kwamba wanadamu wa kwanza waliumbwa moja kwa moja na Mungu na si kupitia njia ya mageuzi kutoka kwenye namna fulani za uhai wa kikale. Lakini kwa nini walimu wengi wa sayansi huko Marekani hukuza mageuzi yasiyo ya kiakili na ya kinasibu kuwa jambo la hakika? Sababu moja ni kwamba “Wafuasi wa nadharia ya Darwin . . . husimamia idara za sayansi katika vyuo vikuu vingi,” asema Phillip E. Johnson profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha California, Berkeley.
Johnson asema hivi: “Katika visa fulani maprofesa wa biolojia wamekatazwa kuwaambia wanafunzi kwamba kuna sababu halali za kushuku dai la kwamba mfululizo usiohitaji akili ungeumba na uliumba maajabu ya biolojia.”
Mwanasayansi na mhandisi Murphy O’Dean asema hivi: “Badala ya kutupilia mbali nadharia ambayo si hakika, mwelekeo wa ‘sayansi ya mageuzi’ umekuwa imani thabiti kwamba ‘lazima mageuzi yawe kweli.’” Uthibitisho unaohitilafiana na ukosefu wa uthibitisho na uthibitisho ama hupuuzwa ama huelezwa vinginevyo.
Kwa nini? Michael Behe, mwanabiolojia wa molekuli, asema hivi katika kitabu Darwin’s Black Box: “Watu wengi, kutia ndani wanasayansi mashuhuri na wenye kuheshimiwa, hawataki kuamini kwamba kuna kitu fulani kilicho nje ya ulimwengu. Hawataki mtu aliye na uwezo upitao wa kibinadamu aathiri ulimwengu.” Lakini sayansi ya kweli haipuuzi uthibitisho unaohitilafiana ili kuendeleza mawazo yanayopendwa. Wala si wanasayansi wote waaminio mageuzi.
Gazeti la Brazili Veja lilimwuliza Carlo Rubbia, mshindi wa Tuzo la Nobeli la Fizikia, “Je, waamini katika Mungu?” Ingawa hakukiri Mungu halisi, alikiri hivi: “Kadiri uchunguzavyo ulimwengu, ndivyo uonavyo kwamba kuna utaratibu mkubwa sana katika vitu vyote. Kuna akili kubwa sana hivi kwamba kwa kuchunguza tu mambo ya asili nafikia mkataa wa kwamba kuna Muumba.”
Maoni yake hutukumbusha maneno ya mtume Paulo kuhusu Mungu: “Sifa zake zisizoonekana zaonwa waziwazi tangu uumbaji wa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zafahamiwa kwa vitu vilivyofanywa, hata nguvu zake za milele na Uungu.”—Waroma 1:20.