Upendo Wangu kwa Dunia Utatoshelezwa Milele
Kama ilivyosimuliwa na Dorothy Connelly
Nilipokuwa msichana mdogo, niliambiwa kwamba nitaenda helo kwa sababu nilikuwa Mwenyeji wa Australia. Miaka kadhaa baadaye, katika mwaka wa 1936, nilisikiliza hotuba ya Biblia iliyorekodiwa ambayo ilizima helo na kunipa tumaini. Tumaini hilo sasa ni angavu kuliko wakati mwingine wowote. Kabla sijaeleza kwa nini iko hivyo, acheni niwaeleze jambo fulani kunihusu.
NILIZALIWA karibu mwaka wa 1911. Nasema “karibu” kwa sababu katika siku hizo Wenyeji wa Australia hawakujishughulisha na tarehe na vyeti vya kuzaliwa. Wazazi wangu walikuwa watu wenye kufanya kazi kwa bidii na wenye kumhofu Mungu. Tuliishi katika mji mdogo wa Springsure, karibu na Safu ya Milima yenye mawemawe iliyo maridadi ya Carnarvon katikati mwa Queensland, Australia.
Baba yangu alilelewa na familia ya wazungu waliokuwa wafuasi wa Katoliki ya Kiroma. Lakini, wazazi wangu Wenyeji wa Australia walikazia ndani yangu desturi zao za kienyeji na upendo kwa dunia. Tuliwinda kangaruu, emu, kasa, na nyoka na kuvua samaki na kutafuta viwavi wakubwa wanaoliwa. Lakini singekula emu kamwe. Katika familia yetu, mimi pekee nilikatazwa kwa sababu alikuwa kiwakilishi cha mungu wangu binafsi. Kulingana na mapokeo ya Wenyeji wa Australia, au “Muhula wa Ndoto,” kila mshiriki wa kabila ana kiwakilishi chake mwenyewe, na marufuku ya kula kitu hicho ilitekelezwa na familia na kabila.
Ingawa matumizi ya viwakilishi hivyo yategemea ushirikina, kutekelezwa kwa mwiko huu kulikuwa kikumbusha cha utakatifu wa uhai. Wenyeji wa Australia hawakuua ili kujifurahisha. Nakumbuka nikitetemeka kwa hasira kali ya Baba aliponipata nikiwapasua panzi waliokuwa hai nilipokuwa msichana mdogo. “Ni vibaya sana!” akasema kwa mshangao. “Je, hujui jinsi ambavyo Mungu huchukia ukatili? Je, ungefurahi kama mtu angekufanyia hivyo?”
Tulikuwa na ushirikina mwingi. Kwa kielelezo, ikiwa kitwitwi (ndege mdogo sana) alicheza karibu na nyumba yetu, iliashiria tukio baya; au ikiwa bundi aliketi kwenye kisiki kilicho karibu wakati wa mchana, tuliamini kwamba ilimaanisha mtu fulani atakufa. Ndoto fulani zilionwa kuwa zinaashiria matukio mabaya. Kwa kielelezo, maji yenye matope katika ndoto yalimaanisha kwamba mtu fulani katika familia alikuwa mgonjwa. Lakini ikiwa maji yalijaa sana matope, basi ilisemekana kwamba mtu fulani amekufa. Kweli, tulikuwa Wakatoliki, lakini hiyo haikuondoa ushirikina wetu wote wa kikabila.
Pia familia yangu ilihifadhi lugha ya Wenyeji wa Australia. Ingawa hivyo, sasa, lugha ya Wenyeji wa Australia ni mojawapo ya lugha nyingi zinazokaribia kutoweka. Bado, mimi huitumia mara kwa mara ninapozungumza na watu kuhusu Biblia. Ingawa hivyo, mara nyingi, mimi hutumia ama Kiingereza ama lugha ya hapa ya pidgin.
Mazoezi Yanayofaa ya Mapema
Nilipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, familia yetu iliishi kwenye shamba la kufuga ng’ombe karibu kilometa 30 kutoka Springsure. Kila siku ningetembea kilometa chache hadi kwenye shamba hilo ili kufanya kazi zangu za nyumbani. Mshahara wangu kwa siku ulikuwa mkebe mmoja wa maziwa na mkate. Familia yetu iliishi katika vibanda vilivyojengwa kwa maganda ya miti, ambayo ni makao ya kawaida ya Wenyeji wa Australia. Kuliponyesha, tungelala kwenye mapango yaliyokuwa karibu usiku huo. Je, niliona maisha haya sahili kuwa magumu? La. Ilikuwa ndiyo njia ya maisha ya Wenyeji wa Australia kwa karne kadhaa, na tuliikubali.
Kwa hakika, nafurahi kwamba sikuishi maisha rahisi na ya raha, na kwamba nilikuwa na wazazi wenye upendo walionipa nidhamu, wakanifanyisha kazi kwa bidii, na kunifundisha njia ya kujipatia riziki kwa kulima. Katika mwaka wa 1934, muda mfupi baada ya kuhamia eneo lililotengwa karibu na Woorabinda, Queensland, nilitoka nyumbani kwa mara ya kwanza na kuelekea upande wa magharibi kufanya kazi katika mashamba ya ng’ombe na kondoo nikiwa mjakazi. Hatimaye kazi ilinifanya nihamie mashariki, nje tu ya jiji la mwambao la Rockhampton. Hapo ndipo nilipokutana na mume wangu aliyekufa, Martin Connelly, ambaye baba yake alitoka Ireland. Tulioana katika mwaka wa 1939.
Kujifunza Kweli ya Biblia
Sikuzote niliistahi sana Biblia. Nilipokuwa kijana, mama-msimamizi wa shamba la ng’ombe angetukusanya watoto wote pamoja—Wenyeji wa Australia na wazungu—na kutusimulia hadithi kuhusu Yesu. Wakati mmoja alieleza maana ya maneno haya ya Yesu: ‘Msiwakataze watoto wadogo waje kwangu.’ (Mathayo 19:14, King James Version) Kwa mara ya kwanza tangu nilipolaaniwa kwenda motoni, nilipata tumaini.
Baadaye nilisikiliza hotuba iliyorekodiwa, iliyotajwa mwanzoni, kuwa helo si moto. Ijapokuwa hilo lilinifanya nianze kufikiri, sikukutana tena na Mashahidi wa Yehova mpaka mwaka wa 1949. Wakati huo tuliishi Emerald, zapata kilometa 250 magharibi ya Rockhampton. Mgeni wetu, R. Bennett Brickell,a alizungumza nasi kuhusu Biblia. Baadaye, nyumba yetu ikawa makao ya Ben wakati wowote alipozuru eneo letu. Sisi sote, kutia ndani Martin na watoto wetu wanne, tulimstahi sana. Martin hakupendezwa na ujumbe wa Biblia, ingawa sikuzote alikuwa mwenye fadhili na mkarimu kwa Mashahidi na hasa kwa Ben.
Ben alinipa misaada mingi ya kujifunzia Biblia, lakini kulikuwako tatizo moja—sikujua kusoma. Hivyo, kwa saburi Ben aliwasomea watoto pamoja nami Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia, na kuelezea alichokuwa akisoma. Alikuwa tofauti na makasisi kama nini, ambao baada ya kumaliza ibada zao za kidini, hawakutumia hata dakika tano kutufundisha kusoma! Ben alituonyesha kutoka kwa Biblia kwamba Shetani na roho waovu wake ndio waanzilishi wa ushirikina mwingi ambao umenasa jamii ya kibinadamu, kutia ndani watu wangu. Jinsi nilivyokuja kuyathamini maneno haya ya Yesu: “Kweli itawaweka nyinyi huru!”—Yohana 8:32.
Nilisisimuka kujifunza juu ya kusudi la Mungu la kuwa na paradiso ya kidunia kwa wale wanaomtii. Zaidi ya yote, nikaja kutamani sana ufufuo wa wafu; Mama alikuwa amekufa katika mwaka wa 1939, na Baba katika mwaka wa 1951. Sikuzote mimi hutazamia kwa hamu siku ambayo nitawakumbatia na kuwakaribisha tena kwenye dunia waliyoipenda sana. Jinsi itakavyosisimua kuwafundisha juu ya Yehova Mungu na Ufalme wake!
Mhubiri Asiyejua Kusoma na Kuandika
Ujuzi wangu juu ya Biblia ulipokua, nilitaka kuushiriki pamoja na wengine. Nilizungumza na jamaa na marafiki zangu, lakini nilitaka kupanua utumishi wangu. Kwa hiyo Ben alipokuja tena Emerald, niliwatayarisha watoto haraka haraka, na sote tukaandamana naye kwenda kuhubiri. Alinionyesha utoaji sahili na kunifundisha kumtegemea Yehova kupitia sala. Nakiri kwamba utoaji wangu haukuwa mzuri sana, lakini ulitoka moyoni mwangu.
Kwanza, niliwaambia wenye nyumba kwamba sikujua kusoma; na pili, niliwaalika kusoma mafungu ya Biblia niliyowaonyesha. Nilikuwa nimekariri mafungu hayo. Ningetazamwa kwa mshangao katika mji huu wenye wazungu wengi, lakini watu hawakuwa wajeuri. Baada ya muda, nilijifunza kusoma. Jinsi jambo hili lilivyoboresha uhakika wangu na hali yangu ya kiroho!
Mkusanyiko Wangu wa Kwanza
Katika Machi 1951, nikiwa nimeweka maisha yangu wakfu kwa Yehova, nilifikia matukio mawili muhimu maishani mwangu: ubatizo wa maji na mkusanyiko wangu wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova. Lakini hilo lilimaanisha kusafiri hadi jiji kubwa la Sydney—wazo lenye kutisha kwa msichana wa mashambani. Zaidi ya hilo sikuwa na nauli ya gari-moshi. Kwa hiyo, ningefanya nini?
Niliamua kucheza kamari ili kujipatia nauli. ‘Nafanya jambo hili kwa ajili ya Yehova,’ nikafikiri, ‘kwa hiyo kwa hakika atanisaidia nishinde.’ Baada ya kucheza mara kadhaa, nilihisi kwamba amenisaidia, kwa kuwa nilipata pesa za kutosha za safari ya kwenda na kurudi.
Ben alijua juu ya mipango yangu ya kwenda Sydney, kwa hiyo alipozuru tena, aliniuliza kama nilikuwa na pesa za kutosha. “Ndiyo!” nikajibu. “Nilipata nauli ya gari-moshi kwa kucheza kamari.” Uso wake uligeuka ukawa mwekundu, na moja kwa moja nikafahamu kwamba nilisema jambo lisilofaa. Nikijitetea kwa haraka, niliongezea: “Una shida gani? Sikuiba kamwe!”
Alipopata utulivu tena, Ben alieleza kwa njia ya fadhili kwa nini Wakristo hawachezi kamari na kuongezea, kwa uhakikishio: “Lakini si kosa lako. Sikuwa nimekwambia.”
Nahisi Kuwa Nimekaribishwa
Mkusanyiko huo wa siku nne, Machi 22-25, 1951, ulikuwa pindi yangu ya kwanza kukutana na Mashahidi wengi namna hiyo. Kwa kuwa nilimjua tu Ben na Mashahidi wachache, sikuwa na uhakika jinsi ambavyo ningepokewa. Kwa hiyo unaweza kuwazia jinsi nilivyosisimuka kukaribishwa kwa uchangamfu na wale ambao baadaye wangekuwa ndugu na dada zangu wa kiroho, ambao hawakuonyesha dalili yoyote ya ubaguzi. Nilihisi kuwa nimekaribishwa na kustarehe.
Bado naukumbuka vizuri mkusanyiko huo, hasa kwa sababu nilikuwa miongoni mwa 160 waliobatizwa katika Botany Bay. Yaonekana, nilikuwa mmoja wa Wenyeji wa Australia wa kwanza kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Picha yangu ilitokea katika gazeti la habari la Jumapili na pia kwenye filamu ya habari iliyoonyeshwa katika majumba ya sinema.
Shahidi Pekee Mjini
Mwezi mmoja baada ya kurudi kutoka Sydney, familia yetu ilihamia Mount Isa, mji ulio katika eneo la migodi katika kaskazini-magharibi ya Queensland. Kwa miaka sita tuliishi ndani ya kibanda tukiwa watunzaji wa shamba kubwa nje tu ya mji. Tulijenga kuta za kibanda chetu kwa kutumia mbao tulizokata katika miti iliyokuwa karibu. Tulitengeneza paa kwa kutumia mapipa mazee ya lami tuliyoyapasua kwa upande na kuyanyosha kuwa bapa. Martin alipata kazi katika reli, lakini ulevi wake hatimaye uliharibu afya yake. Kisha nikawa mwandaliaji wa pekee wa familia yetu. Alikufa katika mwaka wa 1971.
Kwanza, nilikuwa Shahidi pekee katika Mount Isa. Ben angezuru kila miezi sita hivi, kwa kuwa Mount Isa ilikuwa sehemu ya eneo lake kubwa la kutoa ushahidi. Ikiwa ingetukia awe mjini wakati wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo—lilikuwa tukio la pekee sana kwa Ben, kwa kuwa alikuwa na tumaini la uhai wa kimbingu—angeuadhimisha pamoja na familia yangu, nyakati fulani chini ya mti.
Kwa kawaida Ben hakuwa akikaa sana, kwa hiyo mimi na watoto tulihubiri kwa sehemu kubwa tukiwa peke yetu. Kweli, tulikuwa peke yetu; lakini roho ya Yehova ilitupa nguvu, na ndivyo na tengenezo lake lenye upendo. Waangalizi waaminifu wasafirio pamoja na wake zao walipambana na joto kali, nzi, vumbi, na barabara mbaya ili kuja Mount Isa kututia moyo, ingawa kwa miaka mingi kikundi chetu kilikuwa kidogo sana. Pia, Mashahidi kutoka kutaniko jipya la ujirani katika Darwin, zaidi ya kilometa 1,200, wangezuru pindi kwa pindi.
Kutaniko Laanzishwa
Katika Desemba 1953 kutaniko lilianzishwa katika Mount Isa. Ben aliwekwa rasmi kuwa mwangalizi, na binti yangu Ann na mimi ndio peke yetu tulioshiriki katika huduma. Lakini baada ya muda mfupi Mashahidi wengine walihamia mji huo. Eneo letu pia likaanza kutokeza mazao ya wanafunzi, kutia ndani idadi kadhaa ya Wenyeji wa Australia, baada ya muda.
Kutaniko likazidi kukua, na baada ya muda mfupi ikawa wazi kwamba tulihitaji Jumba la Ufalme la kufanyia mikutano yetu. Mnamo mwezi wa Mei 1960, baada ya kazi nyingi, tulimaliza kujenga jumba letu jipya. Katika miaka 15 iliyofuata, lilipanuliwa mara mbili. Lakini kufikia katikati ya miaka ya 1970, tulikuwa na wahubiri 120, na jumba likawa dogo kwa mara nyingine tena. Hivyo, Jumba la Ufalme zuri liwezalo kutoshea watu 250 lilijengwa, na liliwekwa wakfu katika mwaka wa 1981. Kwa sababu jengo hili lina nafasi za ziada, limetumika pia kwa mikutano mikubwa inayoitwa makusanyiko ya mzunguko.
Ukuzi Miongoni mwa Wenyeji wa Australia
Jambo lililonisisimua lilikuwa kuanzishwa katika mwaka wa 1996 kwa kikundi cha Wenyeji wa Australia na cha Wakazi wa Kisiwani ambacho hushirikiana na Kutaniko la Mount Isa. Wakazi wa Kisiwani ni Wenyeji wa Australia wanaotoka katika visiwa vilivyo karibu na bara la Australia. Lengo kuu la kikundi hiki ni kutoa ushahidi ulio bora kwa Wenyeji wa Australia, ambao wengine wao hawajihisi huru wanapokuwa na wazungu.
Kuna vikundi kama hivyo 20 vya Wenyeji wa Australia vilivyotawanyika katika Australia kote. Kwa kuongezea, makutaniko ya Wenyeji wa Australia yameanzishwa katika Adelaide, Cairns, Ipswich, Perth, na Townsville. Karibu watu 500—kutia ndani wengine wa familia yangu—huhudhuria katika vikundi hivi na makutaniko haya. Karibu asilimia 10 ya wahubiri Wenyeji wa Australia ni mapainia, au wahudumu wa wakati wote!
Nilishikwa na ugonjwa wa kisukari katika mwaka wa 1975, na kwa miaka ambayo imepita maradhi haya, ambayo huwaathiri Wenyeji wa Australia wengi sana, yameanza kunidhuru. Kusoma kumekuwa jambo gumu. Lakini, Yehova anaendelea kunitegemeza na kunipa shangwe.
Ninawashukuru wahudumu wenye ujasiri ambao wamenitumikia pamoja na familia yangu. Bidii yao thabiti, upendo wao, na hazina za kiroho walizobeba kwenye baiskeli walipovuka barabara, njia na pori zenye vumbi na ukiwa za Queensland ilituwezesha kujifunza kweli ya Biblia. Sasa nasubiri nikiwa na uhakika wakati ambapo upendo wangu kwa dunia utakapotoshelezwa milele.
[Maelezo ya Chini]
a Simulizi lenye kutokeza la maisha ya Ben Brickell lilichapishwa katika Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1972, ukurasa wa 533-536, (la Kiingereza).
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 15]
Perth
Darwin
Cairns
Townsville
Mount Isa
Rockhampton
Emerald
Springsure
Woorabinda
Ipswich
Sydney
Adelaide
Dorothy leo
[Picha katika ukurasa wa 13]
Kipindi cha mazoezi pamoja na Ben katikati ya miaka ya 1950