Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • lfs makala 14
  • Yehova Alinisaidia Nimpe Kilicho Bora Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Alinisaidia Nimpe Kilicho Bora Zaidi
  • Masimulizi ya Maisha ya Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nachochewa na Bidii ya Mama Yangu
  • Natiwa Moyo na Mashirika Mazuri
  • Naalikwa Gileadi, Kisha Taiwan
  • Tunajifunza Kichina
  • Nasaidiwa na Mwandamani Mpya
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Walijitoa Wenyewe kwa Hiari​—Nchini Taiwan
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Jinsi Siku Ilivyo Katika Maisha ya Misionari
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Masimulizi ya Maisha ya Mashahidi wa Yehova
lfs makala 14
Terry Reynolds.

TERRY REYNOLDS | SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Alinisaidia Nimpe Kilicho Bora Zaidi

Ndugu wa kiroho mwenye umri mkubwa aliyeitwa Cecil alinipatia Biblia nilipokuwa na umri wa miaka 14. Hiyo ndiyo Biblia aliyoitumia katika funzo lake la kibinafsi, kwa hiyo ilikuwa na maandishi aliyoandika pambizoni. Niliiona ‘hiyo kuwa zawadi bora sana!’

Ndugu Cecil alikuwa mnyenyekevu sana na aliwajali watu wengine. Mfano wake na ule wa mama yangu na wa ndugu na dada wengine waaminifu kutanikoni, ulichochea ndani yangu ‘hamu ya kutenda,’ au ya kumpa Yehova kilicho bora. (Wafilipi 2:13) Acheni niwasimulie hadithi yangu.

Nachochewa na Bidii ya Mama Yangu

Nilizaliwa mwaka wa 1943. Wazazi wangu waliishi katika shamba lililokuwa karibu na jiji la pwani la Bundaberg katika eneo ambako miwa inakuzwa, huko Queensland, Australia. Wenyeji wa huko walikuwa na zoea la kwenda mjini kila Jumamosi jioni ili kukutana na marafiki. Pindi moja kama hiyo mwaka wa 1939, wazazi wangu walikutana na mapainia wawili (wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova) ambao walizungumza nao kuhusu Biblia. Wazazi wangu walipendezwa sana na mambo waliyojifunza, na baada ya muda wakawa Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu hiyo, mimi na dada yangu Jean, tulilelewa katika nyumba ya Kikristo. Hata hivyo, kwa kusikitisha, Baba alianguka akiwa nyumbani na kufa. Nilikuwa na umri wa miaka saba tu nami nilishtuka sana. Bado nakumbuka vizuri kwamba alikuwa mwanamume mwenye bidii na mcheshi. Natamani sana kumwona akifufuliwa na nipate kumjua vizuri.​—Matendo 24:15.

Mama yangu alikuwa mwenye fadhili na usawaziko. Alituruhusu tueleze waziwazi mambo tuliyopenda na tusiyopenda. Lakini ilipohusu kanuni za Biblia na ibada ya Yehova, mama alikuwa thabiti. Tulihudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Mama alituonya mimi na Jean tusitumie wakati mwingi na watoto ambao si Mashahidi baada ya shule. (1 Wakorintho 15:33) Ninapokumbuka hilo sasa, ninathamini sana msimamo wake imara.

Nilipokuwa na umri wa miaka 14

Mama alikuwa mhubiri wa Ufalme mwenye bidii, mara nyingi alitumikia akiwa painia wa likizo (sasa ni painia-msaidizi.) Nakumbuka alitembelea zaidi ya familia 50 kwa ukawaida ili kuzipelekea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Hata alipozeeka na kuwa dhaifu, hakuacha kuwahangaikia watu waliopendezwa na kweli. Kwa sababu aliwapenda wengine, na hasa watoto wake, tulimpenda na tulijaribu kumwiga. Katika mwaka wa 1958, nikiwa na umri wa miaka 14, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

Natiwa Moyo na Mashirika Mazuri

Baada ya muda mfupi, kijana kutanikoni kwetu aliyeitwa Rudolf, mwenye umri wa miaka 20 hivi, alibatizwa. Alikuwa amehamia kutoka Ujerumani. Jumamosi asubuhi, mara nyingi mimi na Rudolf tuliwahubiria watu ambao walikuwa wameketi kwenye magari yao wakiwasubiri watu wa familia waliokuwa wameingia madukani.

Rudolf alikuwa ndugu mwenye bidii, naye alinialika tufanye upainia wa likizo wakati wa likizo za shule. Pindi moja, tulihubiri kwa majuma sita katika jiji la Gladstone, karibu kilomita 190 kaskazini mwa Bundaberg. Jitihada za Rudolf za kunisaidia na shangwe niliyopata nilipokuwa nikifanya upainia wa likizo zilinichochea kuwa painia wa kawaida. Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilifikia lengo hilo, na nikaazimia kufanya utumishi wa wakati wote uwe kazi yangu ya maisha.

Mgawo wangu wa kwanza wa upainia ulikuwa katika jiji la Mackay, kwenye pwani ya kaskazini ya Bundaberg karibu na lile Tumbawe Kubwa la Australia. Baada ya mwaka mmoja hivi, nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilipewa mgawo wa kuwa painia wa pekeea katika eneo la kijijini la Australia lisilo na watu wengi. Painia mwenzangu alikuwa mtiwa-mafuta, aliitwa Bennett (Ben) Brickell, ambaye alinizidi umri kwa miaka 30.b Lilikuwa pendeleo kubwa sana kufanya kazi pamoja na painia mwenye uzoefu mwingi, ambaye wengi walimwita painia wa mapainia!

Nikimhubiria mwanamke ambaye ni Mwenyeji wa Asili wa Australia katika eneo la mbali, mwaka wa 1963

Eneo letu la kaskazini-magharibi mwa Queensland lilikuwa katika Eneo la Ghuba, yaani, eneo lililopakana na Ghuba ya Carpentaria. Wakati huo, mimi na Ben ndio tuliokuwa Mashahidi pekee katika eneo hilo lenye watu wachache. Nyakati nyingine ilituchukua saa nyingi kuendesha gari kutoka nyumba moja hadi nyumba jirani. Wakati wa safari hizo ndefu kwenye barabara zenye vumbi, mara nyingi Ben alinisimulia mambo aliyojionea zamani katika huduma. Masimulizi yake yalitia ndani kuhubiri kwa kutumia magari yenye vipaza sautic wakati wa Vita vya Ulimwengu vya Pili, wakati ambapo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku nchini Australia.

Ndugu mmoja (kulia) na mimi (katikati) tukiongoza funzo la Biblia katika eneo la mbali

Baada ya kuhubiri siku nzima, tulipiga kambi kwenye sehemu nzuri karibu na barabara.d Ili kutayarisha chakula cha jioni, tulikusanya kuni na kuwasha moto. Kitanda changu kilikuwa cha karatasi isiyopenyeza maji niliyotandika chini, blanketi kadhaa, na mto. Bado nakumbuka woga niliohisi kumwelekea Yehova nilipotazama anga lililojaa nyota zilizoonekana vizuri bila kuathiriwa na mwanga wa taa za umeme.

Katika eneo la mbali kama hilo, ni hatari sana kuharibikiwa na gari. Pindi moja ekseli ya gari letu ilivunjika. Siku hiyo kulikuwa na joto kali, na hatukuwa na maji ya kutosha. Ili kupata ekseli nyingine, Ben aliomba lifti ili kwenda mji wa Cloncurry. Nilisubiri hapo kwenye gari kwa siku tatu. Kila siku magari machache yalipita, na kwa fadhili madereva walinipa maji. Pia, mtu mmoja alinipa kitabu kilichoraruka-raruka. Akasema: “Rafiki, kisome, huenda kikakusaidia.” Nilishangaa kwa sababu licha ya kwamba kitabu hicho hakikuwa kimechapishwa na tengenezo letu, kilizungumzia mambo ambayo Mashahidi wa Yehova walipitia katika kambi za mateso za Wanazi!

Ben nami tulifanya upainia pamoja kwa karibu mwaka mmoja. Aliniambia hivi kabla ya kuniaga, “Ndugu yangu, endelea kupigana ili udumishe uaminifu wako.” Mfano wake wa bidii na ujitoaji kimungu ulinifanya niazimie hata zaidi kubaki katika utumishi wa wakati wote.

Naalikwa Gileadi, Kisha Taiwan

Baada ya kufanya upainia katika eneo hilo la mbali kwa miaka kadhaa, nilialikwa kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Mgawo huo ulihusisha kutumia juma moja au zaidi na kila kutaniko na vikundi vilivyo mbali katika mzunguko. Niligawiwa mizunguko minne kwa miaka kadhaa. Ilitia ndani makutaniko huko Queensland na New South Wales. Kisha, katika mwaka wa 1971, nikapata pendeleo ambalo sikutarajia la kuhudhuria darasa la 51 la Gileadi, shule ya wamishonari ya Mashahidi wa Yehova iliyoko huko New York. Mtaala huo wenye kina wa funzo la Biblia na ushirika wenye kujenga pamoja na wanafunzi na walimu ulinisaidia kujitayarisha kwa ajili ya mgawo wangu uliofuata, yaani, kazi ya umishonari nchini Taiwan.

Terry pamoja na wahitimu wenzake wa darasa la 51 la Gileadi Septemba mwaka wa 1971.

Darasa langu la Gileadi

Washirika tisa wa darasa letu walipewa mgawo wa kwenda Taiwan, kutia ndani Ian Brown, kutoka New Zealand, naye akawa mwandamani wangu wa umishonari. Hatukujua chochote kuhusu Taiwan. Hata hatukujua nchi hiyo ilikuwa wapi hadi tulipoangalia ramani.

Kulikuwa na tofauti kubwa sana kati ya eneo nililohubiri huko Queensland na Taiwan! Changamoto yetu ya kwanza kubwa ilikuwa ni kujifunza lugha ya Kichina. Kwa muda fulani, sikuelewa chochote kilichokuwa kikisemwa kwenye mikutano, ambayo ndiyo chanzo kikuu cha kitia moyo cha kiroho. Wala sikuweza kuwasiliana vizuri na ndugu na dada zangu. Hali hiyo ilinisaidia mimi na Ian kuelewa kwa nini ilifaa tukapata mazoezi na ujuzi mwingi sana huko Gileadi. Ujuzi huo pamoja na funzo la Biblia la kibinafsi na sala za kutoka moyoni, zilitusaidia twendelee kuwa imara. Na hata ingawa hatungeweza kuwasiliana vizuri pamoja na ndugu na dada zetu, tulitiwa moyo sana na upendo wao kwetu na kwa Yehova.

Ramani ya Australia na mashariki ya Asia, imetiwa alama kwenye maeneo ambayo Terry aliwahi kuishi na kuhubiri, yanayotia ndani: Taipei, Taiwan; Ghuba la Carpentaria, Cloncurry, Mackay, Gladstone, na Bundaberg huko Queensland, Australia; na New South Wales, Australia.

Tunajifunza Kichina

Baada ya kufika Taiwan, wamishonari wote walipewa masomo ya Kichina kwa muda mfupi sana. Mwalimu wetu alikuwa dada kutoka Australia aliyeitwa Kathleen Logan,e aliyekuwa amehitimu kutoka darasa la 25 la Gileadi. Tulijifunza lugha hiyo kwa bidii sana. Na tulitumia haraka iwezekanavyo mambo tuliyojifunza, kama tulivyoagizwa. Mimi na Ian tulikariri jinsi ambavyo tungehubiri katika siku yetu ya kwanza. Tulipokuwa tukienda kwenye eneo, tulikubaliana ni nani ambaye angekuwa wa kwanza kuzungumza mlangoni. Kwa kuwa mimi ndiye niliyekuwa mkubwa kwa umri, nilimtania na kumwambia kwamba yeye ndiye angeongea kwanza. Kwenye nyumba ya kwanza mwenye nyumba alikuwa mwanamume wa Kichina. Alisikiliza kwa subira Ian alipozungumza kwa mchanganyiko wa Kichina na wa Kiingereza. Kisha, akatushangaza alipotuuliza kwa Kiingereza sanifu, tulikuwa tunataka nini! Tulizungumza kwa muda fulani, kisha mwishoni mwa mazungumzo yetu akatutia moyo twendelee kujitahidi kujifunza lugha. Maneno yake yenye fadhili yalituchochea ‘kuendelea kung’ang’ana, kama vile ambavyo Ben alisema.

Eneo letu lilikuwa sehemu kubwa sana ya jiji la Taipei. Lilikuwa eneo jipya kwa sababu ni Mashahidi wachache sana walioishi huko wakati huo. Hilo halikutuvunja moyo kwa hiyo, tulianza kuhubiri kwa bidii hata zaidi. Siku hizo, tuliwaachia watu magazeti mengi sana kwa mwezi. Hata hivyo, baadhi ya watu walichukua magazeti ili tu kujua sisi ni akina nani na kile tulichokuwa tunasema! Hata hivyo, tulifanya yote tuliyoweza kueneza mbegu ya Ufalme, tukiwa na uhakika kwamba nyingine zitatia mizizi ndani ya mioyo ya watu.

Nasaidiwa na Mwandamani Mpya

Terry na Wen-hwa wakiwa na baiskeli zao.

Mimi na Wen-hwa katika huduma, mwaka wa 1974

Katika kipindi hiki cha huduma yangu, nilianzisha urafiki na dada mwenyeji wa Taiwan anayeitwa Wen-hwa. Alipenda ukweli na alitaka kusaidia wenyeji wanufaike na ujumbe wa Biblia kama yeye. Kwa hiyo, aliwasaidia wamishonari wengi, kutia ndani mimi, kuboresha ustadi wetu wa lugha. Nilimpenda dada huyo mkomavu na tukafunga ndoa mwaka wa 1974.

Wen-hwa aliwasaidia wamishonari wawe na matokeo zaidi katika huduma. Kwa mfano, alitusaidia kujifunza lugha kwa kutusaidia tuelewe desturi na njia ya kufikiri ya watu wa Taiwan. Na alitusaidia tubadili utangulizi wetu upatane na eneo, ambalo lilikuwa limejaa Wabudha na Watao. Watu waliabudu mababu waliokufa, na wengi wao hawakuwa wamewahi kusoma Biblia wala hata kuiona. Kwa hiyo, katika mahubiri yetu tulikazia kuhusu Muumba—kwamba jina lake ni Yehova na pia kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba yuko. Kwa mfano, ikiwa mkulima au mvuvi angesema: “Tunategemea mbingu ili tupate chakula,” tungejibu hivi: “Ni nani ambaye huandaa chakula chote? Je, si Mungu ambaye ndiye mwenye nguvu zote, aliyeumba vitu vyote, na ambaye anastahili ibada yetu?”

Nikiwa na Wen-hwa, mwaka wa 1975

Kadiri muda ulivyopita, jitihada zetu zilithawabishwa. Mbegu ya Ufalme ilipata udongo mzuri katika mioyo ya watu waliokuwa tayari kuukubali. Baadhi ya wanafunzi hao wa Biblia walijitahidi sana kushinda imani za uwongo zilizokita mizizi na desturi zisizo za kimaandiko. Lakini kwa msaada wa wamishonari na ndugu wa eneo hilo, walifaulu na maisha yao yaliboreka sana. (Yohana 8:32) Baadaye ndugu wengi walistahili kuwa wazee na watumishi wa huduma kutanikoni, na ndugu na dada wengi walijiunga na utumishi wa wakati wote, kutia ndani kutumikia katika ofisi ya tawi ya Taiwan, au Betheli.

Kuanzia mwaka wa 1976, nilipata pendeleo la kutumikia katika Halmashauri ya Tawi ya Taiwan huku nikiendelea kutumikia nikiwa mmishonari shambani. Mwaka wa 1981, mimi na Wen-hwa tulialikwa Betheli, na nikaendelea kutumikia katika halmashauri ya tawi kwa miaka mingi. Sasa miaka 60 imepita tangu nilipojiunga na utumishi wa wakati wote. Nimetumia miaka zaidi ya 50 kati ya hiyo nikiwa Taiwan, na karibu miaka 50 nikiwa pamoja na mke wangu mpendwa. Mwandamani wangu wa zamani na rafiki yangu Ian Brown, alibaki hapa katika utumishi wa wakati wote hadi alipokufa mwaka wa 2013.

Nikiwa kazini katika ofisi yangu nchini Taiwan, 1997

Mimi na Wen-hwa tunajaribu kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Betheli, katika kutaniko letu la lugha ya Kichina, na katika huduma. Tunamshukuru Yehova kwa mapendeleo hayo yenye thamani. Alinipa hamu na nguvu ya kumtumikia kwa moyo wote nilipokuwa kijana, na anaendelea kutufanyia hivyo mimi na Wen-hwa hata uzeeni.

Wen-hwa naTerry leo.

a Painia wa pekee ni mhudumu wa wakati wote aliyejitolea kutumwa mahali ambapo ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova inaamua kuna uhitaji wa walimu wa Biblia.

b Simulizi la maisha la Bennett Brickell lilichapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1972 (la Kiingereza).

c Magari yenye vipaza sauti yalikuwa na vikuza sauti nje ambavyo vingefanya ujumbe wa Ufalme usikike mtu akiwa mbali.

d Ili kuona akina ndugu wakihubiri katika Nchi ya Ghuba, tazama video Kuhubiri Katika Eneo la Mbali—Australia.

e Simulizi la maisha la Harvey na Kathleen Logan lilichapishwa kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 2021.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki