Wamasora Walikuwa Nani?
YEHOVA, “Mungu wa kweli,” amehifadhi Neno lake, Biblia. (Zaburi 31:5) Lakini kwa kuwa Shetani, adui wa kweli, amejaribu kuifisidi na kuiharibu, Biblia ilitufikiaje kama ilivyoandikwa pale mwanzoni?—Ona Mathayo 13:39.
Sehemu ya jibu hilo yaweza kupatikana katika elezo la Profesa Robert Gordis: “Utimizo wa [wale] Waebrania, walioitwa Wamasora au ‘wahifadhi-desturi,’ haujathaminiwa vya kutosha. Waandishi hawa wasiotajwa majina walinakili Kitabu Kitakatifu kwa uangalifu mwingi na kwa upendo wenye kujali.” Ingawa leo hatujui majina ya wengi wa hawa wanakili, jina la familia moja ya Wamasora limerekodiwa vizuri—Ben Asheri. Je, tunajua nini kuwahusu pamoja na Wamasora wenzao?
Familia ya Ben Asheri
Ile sehemu ya Biblia iliyoandikwa mwanzoni kwa Kiebrania, mara nyingi iitwayo Agano la Kale, ilinakiliwa kwa uaminifu na waandishi wa Kiyahudi. Kutoka karne za sita hadi za kumi W.K., wanakili hawa waliitwa Wamasora. Kazi yao ilitia ndani nini?
Kwa karne nyingi Kiebrania kiliandikwa kwa konsonanti pekee, vokali zikiwekwa na msomaji. Hata hivyo, kufikia wakati wa Wamasora, matamshi yafaayo ya Kiebrania yalikuwa yakipotea kwa sababu Wayahudi wengi hawakuijua lugha hiyo vizuri. Vikundi vya Wamasora katika Babiloni na Israeli vilibuni viishara vya kuzungushia konsonanti kuonyeshea tamko na matamshi yafaayo ya vokali. Angalau mifumo mitatu tofauti ilitokezwa, lakini ule uliokuwa wenye uvutano mwingi zaidi ulikuwa ule wa Wamasora katika Tiberia, kando ya Bahari ya Galilaya, makao ya familia ya Ben Asheri.
Vyanzo vya habari huorodhesha vizazi vitano vya Wamasora kutoka kwa familia hii ya kipekee, kuanzia Asheri Mzee wa karne ya nane W.K. Wengine walikuwa Nehemia Ben Asheri, Asheri Ben Nehemia, Musa Ben Asheri, na mwishowe, Haruni Ben Musa Ben Asheri wa karne ya kumi W.K.a Wanaume hawa walikuwa watangulizi wa wale waliokamilisha ishara mbalimbali zilizoandikwa ambazo zingeeleza vizuri yale waliyoelewa kuwa matamshi yafaayo ya maandishi ya Biblia ya Kiebrania. Ili kuendeleza viishara hivyo, iliwabidi kupambanua chanzo cha mfumo wa sarufi ya Kiebrania. Hakuna mfumo wenye kueleweka wazi wa kanuni mbalimbali za sarufi ya Kiebrania uliowahi kamwe kurekodiwa. Hivyo, mtu anaweza kusema kwamba Wamasora hawa walikuwa wanasarufi wa kwanza wa Kiebrania.
Haruni, Mmasora wa mwisho wa ukoo wa familia ya Ben Asheri, alikuwa wa kwanza kurekodi na kuandika habari hiyo. Alifanya hivyo katika kitabu kiitwacho “Sefer Dikdukei ha-Te’amim,” kitabu cha kwanza cha kanuni za sarufi ya Kiebrania. Kitabu hicho kikawa msingi wa vitabu vya wanasarufi wengineo wa Kiebrania kwa karne zilizofuata. Lakini hicho kilikuwa tu zao la kando la kitabu cha maana zaidi cha Wamasora. Hicho kilikuwa kipi?
Kumbukumbu la Ajabu Lahitajiwa
Hangaiko kubwa la Wamasora lilikuwa kuweka kila neno, na kila herufi, ya maandishi ya Biblia kwa usahihi. Ili kuhakikisha usahihi, Wamasora walitumia pambizo za kando ya kila ukurasa kurekodi habari ambayo ingeonyesha badiliko lolote la maandishi yaliyofanywa kimakosa ama kimakusudi na wanakili wa wakati uliopita. Katika maandishi hayo ya pambizoni, Wamasora pia waliandika maneno yasiyo ya kawaida na michanganyiko ya maneno, wakitia alama mara kadha wa kadha ambazo yalitokea katika kitabu au katika Maandiko yote ya Kiebrania. Kwa kuwa nafasi ilikuwa ndogo, maelezo hayo yalirekodiwa kwa ufupi sana. Walitia alama neno na herufi ya katikati ya vitabu fulani, ili iwe njia ya ziada ya kulinganisha. Walifanya mengi kiasi cha kuhesabu kila herufi ya Biblia ili kuhakikisha unakili sahihi.
Katika pambizo za juu na chini ya ukurasa, Wamasora walirekodi maelezo marefu zaidi kuhusu maandishi fulani yaliyofupizwa katika pambizo za kando.b Hayo yalisaidia katika kulinganisha kazi yao. Kwa kuwa mistari haikuwa na nambari na hakukuwa na konkodansi za Biblia wakati huo, Wamasora walirejezeaje sehemu nyinginezo za Biblia ili wafanye ulinganishi huo? Katika pambizo za juu na chini, waliorodhesha sehemu ya andiko lililofanana na jingine ili kuwakumbusha mahali neno au maneno yaliyoonyeshwa yalipopatikana penginepo ndani ya Biblia. Kwa sababu ya upungufu wa nafasi, mara nyingi wangeandika neno kuu moja tu la kuwakumbusha juu ya kila mstari uliofanana na huo. Ili kufanya maandishi hayo ya pambizoni yawe yenye kutumika, ilibidi wanakili hao kuikariri karibu Biblia yote ya Kiebrania.
Orodha zilizokuwa ndefu kupita pambizo zilipelekwa kwenye sehemu nyingine ya hati hizo. Kwa mfano, maandishi ya Kimasora kando ya pambizo za Mwanzo 18:3 huonyesha herufi tatu za Kiebrania, קלד. Hiyo inalingana na nambari 134 ya Kiebrania. Katika sehemu nyingine ya hati hiyo, orodha inaonekana ikionyesha sehemu mbalimbali 134 ambapo wanakili wa kabla ya Wamasora walikuwa wameondoa kimakusudi jina Yehova kutoka kwenye maandishi ya Kiebrania, wakiweka mahali palo neno “Bwana.”c Ingawa walijua mabadiliko hayo, Wamasora hawakujipatia uhuru wa kubadili maandishi yaliyokuwa yamepitishwa kwao. Badala ya hilo, walionyesha mabadiliko hayo kwenye maandishi yao ya pambizoni. Lakini kwa nini Wamasora walikuwa na uangalifu mwingi kama huo wa kutobadili maandishi ilhali wanakili waliotangulia walikuwa wameyabadili? Je, namna yao ya itikadi ya Kiyahudi ilikuwa tofauti na ya wale waliowatangulia?
Wamasora Waliamini Nini?
Wakati wa kipindi hicho cha maendeleo ya Kimasora, Dini ya Kiyahudi ilihusika kwenye pambano kali sana la maoni. Tangu karne ya kwanza W.K., Dini ya Kiyahudi ya kirabi ilikuwa ikiendelea kupata mamlaka zaidi. Kwa kuandikwa kwa Talmud na mafasiri ya marabi, maandishi ya Kibiblia yalianza kuwa ya pili dhidi ya ufasiri wa kirabi wa sheria ya mdomo.d Kwa hiyo, kuhifadhiwa kwa uangalifu kwa maandishi ya Biblia kungaliweza kupoteza umaana wayo.
Katika karne ya nane, kikundi kilichoitwa Wakaraite kiliasi dhidi ya mwelekeo huo. Kikikazia umaana wa funzo la Biblia la kibinafsi, kilikataa mamlaka na mafasiri ya marabi na Talmud. Kilikubali maandishi ya Biblia pekee kuwa mamlaka yacho. Hiyo iliongeza uhitaji wa unakili sahihi wa maandishi hayo, na utendaji wa Kimasora ukapata nguvu mpya.
Itikadi ya ama kirabi ama ya Wakaraite ilikuwa na uvutano kadiri gani juu ya Wamasora? M. H. Goshen-Gottstein, mtaalamu wa hati za Biblia ya Kiebrania, asema: “Wamasora walikuwa na uhakika . . . kwamba walikuwa wakifuata desturi ya kale, na kuihalifu kimakusudi kungalikuwa uhalifu mbaya zaidi ambao wangeweza kutenda.”
Wamasora waliona unakili ufaao wa maandishi ya Biblia kuwa kazi takatifu. Ingawa wao wenyewe huenda wakawa walikuwa wamechochewa sana na mawazo mengine ya kidini, inaonekana kwamba kazi yenyewe ya Wamasora haikuwa na uvutano wa masuala hayo ya kidini. Yale maandishi mafupi sana ya pambizoni pekee hayakuacha nafasi yoyote ya mjadala wa kitheolojia. Maandishi ya Biblia pekee ndiyo yalikuwa hangaiko lao maishani; hawangaliyachezea-chezea.
Kunufaishwa na Juhudi Yao
Ingawa Israeli la asili halikuwa tena watu waliochaguliwa na Mungu, wanakili hawa Wayahudi walikuwa wamejitoa kabisa-kabisa kuhifadhi usahihi wa Neno la Mungu. (Mathayo 21:42-44; 23:37, 38) Matimizo ya familia ya Ben Asheri na Wamasora wengineo yameelezwa vizuri na Robert Gordis, aliyeandika hivi: “Wafanyakazi hao wanyenyekevu na wasioshindwa . . . walifanya kazi yao iliyokuwa ngumu sana bila kujulikana ya kulinda Maandishi ya Kibiblia yasipotee au kubadilishwa.” (The Biblical Text in the Making) Kama tokeo, Warekebishaji kama vile Luther na Tyndale wa karne ya 16 walipoasi mamlaka ya kanisa na kuanza kutafsiri Biblia kwa lugha za kawaida ili watu wote waisome, walikuwa na maandishi ya Kiebrania yaliyohifadhiwa vizuri ya kutumia yakiwa msingi wa kazi yao.
Kazi ya Wamasora yaendelea kutunufaisha leo. Maandishi yao ya Kiebrania yanatumika kuwa msingi wa Maandiko ya Kiebrania ya New World Translation of the Holy Scriptures. Tafsiri hiyo inaendelea kutafsiriwa katika lugha nyingi kwa mwelekeo uo huo wa kujitoa na kujali usahihi ulioonyeshwa na Wamasora wa kale. Tunafanya vema kuonyesha mwelekeo uo huo katika kutoa uangalifu kwa Neno la Yehova Mungu.—2 Petro 1:19.
[Maelezo ya chinis]
a Kwa Kiebrania “ben” humaanisha “mwana.” Hivyo Ben Asheri humaanisha “mwana wa Asheri.”
b Maandishi ya Wamasora katika pambizo za kando yanaitwa Masora Ndogo. Maandishi yaliyo katika pambizo za juu na chini yanaitwa Masora Kubwa. Orodha zilizowekwa penginepo ndani ya hati zinaitwa Masora ya Mwisho.
c Ona nyongeza 1B katika New World Translation of the Holy Scriptures With References.
d Kwa habari zaidi juu ya sheria ya mdomo na Dini ya Kiyahudi ya kirabi, ona kurasa 8-11 za broshua Je, Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?, iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa28]
Mfumo wa Matamshi ya Kiebrania
UTAFUTAJI wa njia nzuri zaidi ya kurekodi alama za vokali na alama za tamko ulidumu kwa karne nyingi miongoni mwa Wamasora. Hivyo, haishangazi kuona ukuzi unaoendelea wa kila kizazi cha familia ya Ben Asheri. Hati zilizopo zinawakilisha miundo na njia mbalimbali za Wamasora wawili tu wa mwisho wa familia ya Ben Asheri, Musa na Haruni.e Uchunguzi wa kulinganisha hati hizi waonyesha kwamba Haruni alianzisha kanuni mbalimbali juu ya mambo fulani madogo-madogo ya matamshi na viishara vilivyotofautiana na vile vya baba yake, Musa.
Ben Naftali aliishi wakati wa Haruni Ben Asheri. Ile Kodeksi ya Cairo ya Musa Ben Asheri ina fasiri nyingi hususa zilizoandikwa na Ben Naftali. Hivyo basi, ama Ben Naftali mwenyewe alifundishwa na Musa Ben Asheri ama wote wawili walihifadhi desturi ya kawaida iliyokuwa ya kale zaidi. Wasomi wengi hueleza juu ya tofauti kati ya mifumo ya Ben Asheri na Ben Naftali, lakini M. H. Goshen-Gottstein aandika hivi: “Ingekuwa sahihi kuzungumza juu ya mifumo hiyo midogo miwili ndani ya familia ya Ben Asheri na kueleza tofauti za fasiri: Ben Asheri dhidi ya Ben Asheri.” Hivyo isingekuwa sahihi kuzungumza juu ya njia moja tu ya Ben Asheri. Haikuwa tokeo la umashuhuri uliorithiwa kwamba mfumo wa Haruni Ben Asheri ukawa njia iliyokubaliwa mwishowe. Maandishi ya Haruni Ben Asheri yalipendelewa kwa sababu tu ya sifa yaliyopewa na msomi wa Kitalmud Musa Maimoni wa karne ya 12.
[Artwork—Hebrew characters]
Sehemu ya Kutoka 6:2 yenye vokali na ishara za tamko na ile isiyokuwa na kitu
[Maelezo ya Chini]
e Ile Kodeksi ya Cairo (895 W.K.), ambayo ina majina ya manabii wa kwanza na wa mwisho pekee, inatoa kielelezo cha miundo ya Musa. Zile kodeksi za Aleppo (karibu 930 W.K.) na Leningrad (1008 W.K.) zinatumika kuwa vielelezo vya miundo ya Haruni Ben Asheri.
[Picha katika ukurasa wa26]
Tiberia, kitovu cha utendaji wa Kimasora tangu karne ya nane hadi karne ya kumi
[Picha zimeandaliwa na]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.