Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 2/15 kur. 20-23
  • Jinsi Ulivyotayarishiwa Maandiko ya Kiebrania

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Ulivyotayarishiwa Maandiko ya Kiebrania
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KAZI YA “MASOFERIMU”
  • MAANDISHI YA WAYAHUDI WALIOITWA “WAMASORETI”
  • USAHIHI WAHAKIKISHWA NA HATI ZINAZOITWA “DEAD SEA SCROLLS”
  • Ni Nini Mwandiko wa Kimasora?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Hicho Kitabu Kiliokokaje?
    Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
  • Funzo Namba 5—Maandishi-Awali ya Kiebrania ya Maandiko Matakatifu
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vita vya Biblia ili Kuishi
    Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 2/15 kur. 20-23

Jinsi Ulivyotayarishiwa Maandiko ya Kiebrania

INAELEKEA wewe una nakala ya lugha yako mwenyewe ya Maandiko ya Kiebrania, ambayo sana-sana yanaitwa “Agano la Kale.” Sehemu hiyo ya Kiebrania ya Biblia Takatifu ina sura chache na mistari iliyoandikwa mbali mbali katika lugha ya Kiaramu. Maandiko ya Kiebrania yalimalizwa kuandikwa zaidi ya miaka 2,400 iliyopita.

Je! unaweza kuwa na hakika kwamba nakala ya Maandiko ya Kiebrania uliyo nayo ina mambo yale yale yaliyoandikwa hapo kwanza? Watu wengine wanaona kwamba maandiko yaliyoandikwa kwa lugha ya kwanza kabisa yamebadilika kwa sababu yamenakiliwa mara nyingi kwa muda wa maelfu ya miaka. Lakini je! kweli maandiko hayo yamebadilika? Inapendeza kuangalia habari fulani kubwa zinazohusu jinsi maandiko hayo yameendelea kuwako karne zote hizo.

Tangu pale pale mwanzoni wakati Biblia ilipokuwa ikiandikwa, jitihada zilifanywa ili kulihifadhi Neno la Mungu. Maandiko yanasema kwamba Musa aliwaamuru Walawi wakiweke “chuo hiki cha torati” kwa faida ya vizazi ambavyo vingefuata. (Kum. 31:25, 26) Wafalme wa Israeli waliagizwa na Mungu wajifanyie “nakala ya torati hii” walipokalia kiti cha enzi.​—Kum. 17:18.

Baadaye, kukawa na uhitaji mkubwa wa nakala za Maandiko ya Kiebrania wakati wa Ezra, kuhani ambaye alifuatana na Wayahudi wengine kutoka Babeli kwenda Yerusalemu mwaka wa saba wa kutawala kwa Artashasta Mfalme Mwajemi (468 K.W.K.). (Ezra 7:1-7) Maelfu ya Wayahudi walikuwa wameamua kubaki Babeli, na wengine walikuwa wametawanyika kwa sababu ya kuhama na kwenda biasharani. Majumba ya kukusanyikia yaliyoitwa masinagogi yalijengwa mahali mbalimbali, basi ikawa lazima waandishi wanakili kwa mkono hati za Biblia za kutumiwa katika majumba hayo. Ezra mwenyewe anatajwa kuwa “mwandishi mwepesi katika sheria ya Musa” na “mwandishi wa maneno ya amri za [Yehova], na wa sheria zake alizowapa Israeli.”​—Ezra 7:6, 11.

KAZI YA “MASOFERIMU”

Tangu siku za Ezra, wenye kunakili Maandiko ya Kiebrania walijulikana kama “masoferimu.” Mapokeo ya kale sana ya ualimu wa Kiyahudi yanaonyesha jina hilo lilihusiana na neno la Kiebrania la kitendo (sa·pharʹ), lililo na maana ya “kuhesabu,” ! nayo yanasema: “Wanafunzi wa kwanza waliitwa Sof’rim, kwa sababu walihesabu herufi zote katika Torah,” yaani, vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Uangalifu huo mwingi sana ulifanya Maandiko ya Kiebrania yatayarishwe kwa usahihi mwingi.

Bila shaka, ni wazi kwamba makosa fulani yangetokea katika Biblia, katika maandiko ya Kiebrania, kwa sababu ya kunakiliwa muda wa karne nyingi. Hata kuna ushuhuda wenye kuonyesha kwamba masoferimu walibadili mambo machache kwa makusudi. Kwa mfano, baada ya muda mwingi kupita, wenye kunakili wameonyesha mahali 134 ambapo masoferimu walibadili maandishi ya kwanza ya Kiebrania yakasema Adonay [“Bwana”] badala ya kutaja jina la Mungu mwenyewe YHWH [“Yehova”]. Hata hivyo, lilikuwa jambo zuri waandishi hao wakaonyesha mahali ambapo watu hao walifanya mabadiliko ili wanafunzi wa baadaye waweze kujua jinsi maandishi ya kwanza yalivyokuwa.

Kulingana na mapokeo ya Kiyahudi, jitihada nyingi sana zilifanywa kabla ya hekalu la ibada ya Mungu katika Yerusalemu kuharibiwa mwaka 70 W.K. ili kurudia kuandika mambo jinsi maandishi ya kwanza ya Biblia, katika Kiebrania, yalivyokuwa yakisema. Kuhusu hilo, Robert Gordis anaandika yafuatayo katika The Biblical Text in the Making: “Wenye kutunza maandishi ya Biblia walipata hati moja ya kale iliyoandikwa kwa uangalifu mwingi sana halafu wakaifanya iwe msingi wa kazi yao. Waliifanya ikawa ndiyo nakala iliyopaswa kutegemewa baada ya hapo wakati wa kufanya nakala zote rasmi na wakati wa kusahihisha hati zote za watu bi nafsi. “

Vitabu vya waalimu wa Kiyahudi vinataja nakala ya Kiebrania ya Pentateuch (vitabu vitano vya kwanza vya Biblia) inayojulikana kama “Kitabu cha Kukunja cha Hekalu peke yake,” nayo ilitumiwa kama kielelezo cha kusahihishia nakala mpya. Vilevile vinataja “wasahihishaji wa vitabu vya Biblia katika Yerusalemu” waliopokea mishahara yao kutokana na hazina ya Hekalu.

MAANDISHI YA WAYAHUDI WALIOITWA “WAMASORETI”

Hapo kwanza hati za Kiebrania za Biblia ziliandikwa kwa kutumia konsonanti (herufi bubu) peke yake. Alfabeti ya Kiebrania haina vokali kama zile zetu, a, e, i, o, u. Lakini ukiangalia Biblia ya Kiebrania iliyochapwa leo, utaona kwamba juu ya kila neno, chini yake, au katikati yake mna nukta (.), vistari vilivyolala (​—⁠) na alama nyingine. Kwa sababu gani viliongezwa katika Maandiko ya kwanza ya Kiebrania? Ni kwa sababu maneno mengi ya Kiebrania yaliyoandikwa kwa kutumia konsonanti peke yake yanaweza kutamkwa kwa njia mbalimbali, huku yakiwa na maana mbalimbali. Zile vokali na alama za kutia mkazo zinasaidia kufanya kila neno litamkwe kama ilivyo desturi.

Vokali hizo na alama hizo za kutia mkazo zilitayarishwa na watu wenye ujuzi mwingi wa kunakili walioishi kame ya sita mpaka ya kumi W.K. Waandishi hao walikuja kujulikana kama baalei hamasoreth (“wastadi wa mapokeo”), au “Wamasoreti.” Kwa hiyo maandishi ya Kiebrania yenye vokali yanaitwa maandishi “ya Kimasoreti.”

Wamasoreti hawakubadili kitu wakati wa kunakili hati za Kiebrania za Biblia. Walichunguza mitungo yote ya maneno yasiyo ya kawaida, wakaandika maelezo kuhusu maneno hayo katika mapambizo (sehemu za kando) ya hati za Kimasoreti. Maelezo hayo yanaitwa “masorah.” Maelezo yaliyofupizwa sana, yanayojulikana kama “masorah ndogo,” yamo katika mapambizo kando ya maandishi ya kwanza ya Kiebrania ya Biblia. Mapambizo ya juu na chini ndiyo yenye ile “masorah kubwa,” ambayo ni nyongeza ya ile masorah ndogo. Mwishoni mwa hati fulani za Kimasoreti kuna “Masorah ya mwisho” iliyo kama fahirisi yenye maneno ya maana zaidi yaliyotumiwa.

Maelezo hayo yanaonyesha kwamba Wamasoreti walijifunza mambo mengi sana kwa sababu ya kuhifadhi maandishi ya kwanza ya Biblia kwa uaminifu. Kulingana na maneno ya Robert Gordis, “walihesabu herufi za Maandiko, wakajua herufi na mstari uliokuwa katikati kabisa ya Torah [Pentateuch au vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, wakahesabu wakajua herufi iliyokuwa katikati kabisa ya Biblia nzima, wakakusanya orodha ndefu ya maneno ya Biblia ya namna ya pekee na yasiyotumika sana, wakaonyesha mara ambazo maelfu ya maneno ya Biblia yanapatikana na jinsi yanavyotumika​—nao walifanya mambo hayo yote ili kulinda Maandiko yasichezewe-chezewe na kuzuia waandishi wasiingize mabadiliko katika maandiko ya kwanza yenye kukubalika.”

Kwa mfano, ile masorah ndogo inasema kwamba lile neno la kwanza la kitabu cha Mwanzo, yaani, bereshithʹ (linalotafsiriwa mara nyingi kuwa: “Hapo mwanzo”), linapatikana mara tano katika Biblia, na tatu kati ya mara hizo linapatikana mwanzoni mwa mstari. Katika karibu kila ukurasa wa hati za Biblia za Kimasoreti, maneno mengi yametiwa alama pambizoni kwa herufi ya Kiebrania inayoitwa lamedh (ל). Herufi hiyo (inayolingana na “l” yetu) ni kifupi cha neno leit, neno la Kiaramu lililo na maana ya “hakuna.” Nayo inaonyesha kwamba neno hilo linalopatikana mahali hapo halipatikani mahali penginepo pote. Kuhusu masorah, Ernst Wurthwein anaeleza yafuatayo katika The Text of the Old Testament:

“Mara nyingi sisi tunadhani maelezo hayo ya Kimasoreti hayana maana, ni ya upuzi wala hayana kusudi. Lakini lazima tukumbuke kwamba yaliandikwa kwa sababu ya kutaka sana kulinda maandishi ya kwanza na kuzuia waandishi wasiongeze makosa kwa makusudi au kwa sababu ya uzembe, . . . Masora inahakikisha kwamba maandishi ya kwanza yalinakiliwa tena kwa usahihi kabisa, na yanastahili tuyaheshimu, ingawa nyakati zote kuna wasiwasi wa kudhani kwamba maana ya maandishi ya kwanza imekosa kufahamika kwa sababu ya kufuata sana neno kwa neno.”

USAHIHI WAHAKIKISHWA NA HATI ZINAZOITWA “DEAD SEA SCROLLS”

Eneo la Bahari ya Chumvi limechunguzwa vikapatikana vitabu vingi sana vya kukunja vya Kiebrania vilivyoandikwa kabla ya mwanzo wa Wakati wa Kawaida Vinaonekana kuwa namna gani vikilinganishwa na hati za Kimasoreti zilizotayarishwa miaka elfu moja au zaidi baadaye?

Katika uchunguzi mmoja, sura ya 53 ya Isaya ilichunguzwa jinsi ilivyo katika kitabu cha kukunja kinachoitwa “Dead Sea Scroll of Isaiah,” kilichonakiliwa karibu na mwaka 100 K.W.K., na vilevile katika maandishi ya kwanza ya Kimasoret: Norman L. Geisler na William E. Nix wanaeleza matokeo ya uchunguzi huo katika kitabu A General Introduction to the Bible:

“Kati ya maneno 166 yaliyo katika Isaya 53, herufi kumi na saba tu ndizo zinazotiliwa mashaka. Kumi kati ya herufi hizo zimeendelezwa vibaya tu, kwa hiyo hazibadili maana. Herufi nyingine nne ni mabadiliko madogo yaliyofanywa kwa jinsi tofauti, kwa mfano matumizi ya viungo vya maneno au conjunctions. Halafu herufi tatu zilizobaki zimo katika neno ‘nuru,’ lililoongezwa katika mstari wa 11, nalo halibadili sana maana. . . . Kwa hiyo, katika sura moja hiyo yenye maneno 166, neno moja tu (herufi tatu) ndilo linalotiliwa mashaka baada ya miaka elfu moja ya kunakili​—nalo neno hilo halibadili sana maana ya kifungu hicho.”

Kitabu kingine kinasema kwamba kitabu hicho cha kukunja pamoja na nakala nyingine yenye sehemu za Isaya zilizopatikana karibu na Bahari ya Chumvi “zimelingana neno kwa neno na Biblia ya kawaida ya Kiebrania tuliyo nayo, kwa kiasi cha 95 kwa mia. Ile tofauti ya kiasi cha 5 kwa mia imesababishwa hasa na makosa madogo ya kalamu na kutofautiana kwa njia za kuendeleza maneno.”

Basi, unaposoma Maandiko ya Kiebrania unaweza kuwa na hakika kwamba Biblia yako inategemea maandishi ya Kiebrania yanayoeleza kwa usahihi mawazo ya waandikaji walioongozwa na Mungu. (2 Tim. 3:16) Utaalamu wa kunakili kwa uangalifu mwingi sana muda wa maelfu ya miaka umehakikisha vile Mungu alivyotabiri zamani za kale: “Majani yakauka, ua lanyauka; bali neno la Mungu wetu litasimama milele.”​—Isa. 40:8.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Maandishi ya Kimasoreti ya Mambo ya Walawi 10:16. Ule mviringo mdogo sana ulio juu ya neno la Kiebrania (mshale wa kushoto) unaonyesha maelezo ya pambizoni (mshale wa kulia), yanayosema: “Neno lililo katikati ya Pentateuch”

[Picha katika ukurasa wa 22]

Huu ni mwanzo wa kitabu cha Isaya katika Hati inayoitwa “Dead Sea Scroll” ya mwaka 100 K.W.K. (juu) na katika Hati ya Leningrad ya mwaka 1000 W.K. (kushoto). Ingawa hati hizo mbili zimeachana kwa miaka 1,100, zinapatana karibu kila neno

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki