Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • gm sura 2 kur. 12-24
  • Vita vya Biblia ili Kuishi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vita vya Biblia ili Kuishi
  • Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ni Biblia Pekee Iliyookoka
  • Watunzaji wa Lile Neno
  • Nakala Zenye Kosa
  • Watu na Lugha Zao
  • Funzo Namba 6—Maandishi-awali ya Kigiriki ya Kikristo ya Maandiko Matakatifu
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Maandiko ya Kikristo Yana Usahihi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Hicho Kitabu Kiliokokaje?
    Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
  • Funzo Namba 5—Maandishi-Awali ya Kiebrania ya Maandiko Matakatifu
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
gm sura 2 kur. 12-24

Sura 2

Vita vya Biblia ili Kuishi

Kuna visehemu vingi vya uthibitisho kuonyesha kwamba kweli kweli Biblia ni Neno la Mungu. Kila kisehemu kina nguvu, lakini vyote vinapochukuliwa pamoja, havishindiki. Katika sura hii na itakayofuata, tutazungumza juu ya kisehemu kimoja tu cha uthibitisho: historia ya Biblia ikiwa kitabu. Kweli, ni mwujiza kwamba kitabu hiki cha kutokeza kimeokoka mpaka wa leo. Fikiria mwenyewe mambo ya hakika.

1. Ni nini baadhi ya habari juu ya Biblia?

BIBLIA ni zaidi tu ya kuwa kitabu. Ni maktaba kubwa yenye vitabu 66, vingine vikiwa vifupi na vingine vikiwa virefu sana, vyenye sheria, unabii, historia, mashairi, shauri, na mambo mengine zaidi. Karne nyingi kabla ya kuzaliwa kwa Kristo, vya kwanza 39 kati ya vitabu hivyo vilikuwa vimeandikwa—hasa katika lugha ya Kiebrania—na Wayahudi, au Waisraeli waaminifu. Sehemu hii huitwa mara nyingi Agano la Kale. Vile vitabu 27 vya mwisho viliandikwa katika Kigiriki na Wakristo na hujulikana sana kuwa Agano Jipya. Kulingana na uthibitisho wa ndani na mapokeo yaliyo ya kale zaidi, vitabu hivi 66 viliandikwa katika kipindi cha miaka 1,600 hivi, kuanzia wakati Misri ilipokuwa ndilo taifa lenye kutawala na kumalizika wakati Roma ilipokuwa ikiongoza ulimwengu.

Ni Biblia Pekee Iliyookoka

2. (a) Hali ya Israeli ilikuwa nini wakati Biblia ilipoanza kuandikwa? (b) Ni nini baadhi ya vitabu vilivyotokezwa wakati wa kipindi icho hicho?

2 Miaka zaidi ya 3,000 iliyopita, wakati uandikaji wa Biblia ulipoanza, Israeli lilikuwa taifa moja dogo miongoni mwa mengi katika Mashariki ya Kati. Yehova alikuwa Mungu wao, huku mataifa yenye kuzunguka yakiwa na unamna-namna wenye kushtua wa vijimungu na vijimungu-vike. Wakati wa kipindi hicho, si Waisraeli pekee waliotokeza vitabu vya kidini. Mataifa mengine pia yalitokeza vitabu vilivyoonyesha dini yao na kanuni zao za kitaifa. Kwa kielelezo, hekaya ya Gilgameshi ya Kiakadi kutoka Mesopotamia na tenzi za Ras Shamra, zilizoandikwa katika Kiugrati (lugha iliyonenwa katika ile inayojulikana sasa kuwa Siria ya kaskazini), bila shaka zilipendwa sana na wengi. Vitabu vilivyo vingi vya wakati huo vilitia ndani pia vitabu kama Mawaidha ya Ipu-wer na Unabii wa Nefer-rohu katika lugha ya Kimisri, nyimbo za kidini za kusifu viabudiwa tofauti katika Kisumeri, na vitabu vya kiunabii katika Kiakadi.1

3. Ni nini kinachoonyesha Biblia kuwa tofauti na vitabu vinginevyo vya kidini vilivyotokezwa katika Mashariki ya Kati wakati uo huo?

3 Hata hivyo, vitabu hivyo vyote vya Mashariki-Kati, vilipatwa na mwisho ule ule. Vilisahauliwa, na hata lugha ambazo vilikuwa vimeandikwa zikatoweka. Ni katika miaka ya karibuni tu kwamba waakiolojia na wafilolojia (wataalamu wa lugha) wamejifunza juu ya kuwapo kwazo na wakagundua jinsi ya kuzisoma. Kwa upande mwingine, vitabu vya kwanza vilivyoandikwa vya Biblia ya Kiebrania vimeokoka mpaka wakati wetu wenyewe na vingali vyasomwa sana. Nyakati nyingine wasomi hudai kwamba vitabu vya Kiebrania katika Biblia vilitokana kwa njia fulani na vitabu hivyo vya kale vya kiutungaji. Lakini uhakika wa kwamba vitabu vingi kati ya hivyo vilisahauliwa ambapo Biblia ya Kiebrania iliokoka huonyesha Biblia kuwa tofauti sana.

Watunzaji wa Lile Neno

4. Ni matatizo gani makubwa ya Waisraeli ambayo huenda yalionekana yakitia kuokoka kwa Biblia katika shaka?

4 Usikosee, halikuwa jambo lenye kutarajiwa kwa maoni ya kibinadamu kwamba Biblia ingeokoka. Jumuiya zilizoitokeza zilipatwa na majaribu magumu na upinzani mkali hivi kwamba kuokoka kwayo mpaka siku yetu kwastaajabisha kweli kweli. Katika miaka ya kabla ya Kristo, Wayahudi waliotokeza Maandiko ya Kiebrania (“Agano la Kale”) walikuwa taifa dogo kwa kulinganisha. Walikaa kwa njia ya hatari katikati ya mataifa ya kisiasa yenye nguvu yaliyokuwa yaking’ang’ania ukuu. Israeli ililazimika kupigania uhai wayo dhidi ya mfululizo wa mataifa, kama vile Wafilisti, Wamoabi, Waamoni, na Waedomi. Kipindi fulani Waebrania walipokuwa wamegawanyika kuwa falme mbili, Milki ya Kiashuri yenye ukatili ilikaribia kufagilia mbali kabisa ule ufalme wa kaskazini, nao Wababuloni wakaangamiza ule ufalme wa kusini, wakiwapeleka watu kwenye uhamisho ambao ni baki tu lilirejea miaka 70 baadaye.

5, 6. Ni majaribio gani yaliyofanywa ambayo yalihatarisha kuwapo kwenyewe kwa Waebrania wakiwa kikundi tofauti cha watu?

5 Hata kuna ripoti za kuangamiza taifa zima kulikojaribiwa dhidi ya Waisraeli. Nyuma katika siku za Musa, Farao aliamuru mauaji ya watoto wao wavulana waliozaliwa karibuni. Kama agizo lake lingefuatwa, Waebrania wangalimalizwa. (Kutoka 1:15-22) Baadaye sana, Wayahudi walipokuwa chini ya mtawala Mwajemi, maadui wao walitunga hila sheria fulani ipitishwe kwa kusudi la kuwaangamiza. (Esta 3:1-15) Kushindwa kwa njama hiyo kungali kwasherehekewa katika Sikukuu ya Kiyahudi ya Purimu.

6 Bado baadaye, Wayahudi walipokuwa chini ya Siria, Mfalme Antioko 4 alijaribu sana kufanya taifa hilo lifuate Uyunani, akililazimisha lifuate desturi za Kigiriki na kuabudu vijimungu vya Kigiriki. Badala ya kufagiliwa mbali au kumezwa, Wayahudi waliokoka huku, vikundi vya kitaifa vikitoweka katika tamasha ya ulimwengu, kimoja baada ya kingine. Na Maandiko ya Kiebrania ya Biblia yaliokoka pamoja nao.

7, 8. Kuokoka kwa Biblia kulitishwaje na dhiki za Wakristo?

7 Wakristo, ambao walitokeza sehemu ya pili ya Biblia (“Agano Jipya”), walikuwa pia kikundi chenye kudhulumiwa. Yesu, kiongozi wao, aliuawa kama mhalifu wa kawaida. Katika siku za mapema baada ya kifo chake, mamlaka za Kiyahudi katika Palestina zilijaribu kuwagandamiza. Ukristo ulipoenea mpaka mabara mengine, Wayahudi waliwawinda, wakijaribu kuzuia kazi yao ya umisionari.—Matendo 5:27, 28; 7:58-60; 11:19-21; 13:45; 14:19; 18:5, 6.

8 Wakati wa Nero, mtazamo wenye uvumilio wa hapo kwanza wa mamlaka za Kiroma ulibadilika. Takito alijivunia “mateso yenye kupendeza” waliyofanyiwa Wakristo na maliki huyo mkatili, na tangu wakati wake na kuendelea, kuwa Mkristo kukawa ni kosa linalostahili kifo.2 Katika 303 W.K., Maliki Dioklesio alitenda kinyume cha Biblia moja kwa moja.a Katika jitihada ya kumaliza Ukristo, aliamuru kwamba Biblia zote za Kikristo zichomwe.3

9. Kungalitukia nini kama jitihada za kuangamiza Wayahudi na Wakristo zingalifaulu?

9 Jitihada hizo za dhuluma na kuangamiza taifa zima zilikuwa tisho halisi kwa kuokoka kwa Biblia. Kama Wayahudi wangalienda katika njia ya Wafilisti na Wamoabi au kama jitihada za mamlaka ya Kiyahudi kwanza na kisha ya Kiroma za kumaliza Ukristo zingalifanikiwa, ni nani angaliandika na kuhifadhi Biblia? Kwa furaha, watunzaji wa Biblia—kwanza Wayahudi na kisha Wakristo—hawakufagiliwa mbali, na Biblia ikaokoka. Hata hivyo, kukawa tisho jingine kubwa kama si kwa kuokoka kwa Biblia angalau kwa usahihi wa Biblia.

Nakala Zenye Kosa

10. Hapo awali Biblia ilihifadhiwaje?

10 Vingi vya vitabu hivyo vya kale vilivyotangulia kutajwa ambavyo vilisahauliwa hatimaye vilikuwa vimechongwa katika mawe au kuandikwa kwenye mabamba ya udongo yenye kudumu. Sivyo na Biblia. Hapo awali ilikuwa imeandikwa kwenye mafunjo au kwenye ngozi—vifaa vyenye kuelekea kuharibika zaidi. Kwa hiyo, hati-mkono zilizotokezwa na waandikaji wa awali zilitoweka zamani za kale. Basi, Biblia ilihifadhiwaje? Kwa taabu, maelfu yasiyohesabika ya nakala yaliandikwa kwa mkono. Hiyo ndiyo iliyokuwa njia ya kawaida ya kutokeza nakala ya kitabu kabla ya kuwasili kwa uchapaji.

11. Ni nini kisichoweza kuepukwa kitukie wakati hati-mkono zinaponakiliwa kwa mkono?

11 Hata hivyo, kuna hatari katika kunakili kwa mkono. Sir Frederic Kenyon, yule mwakiolojia mwenye kujulikana sana na mkutubi wa British Museum, alieleza hivi: “Kungali hakujaumbwa mkono na ubongo wa kibinadamu uwezao kunakili kitabu kirefu kizima bila ya vikosa. . . . Makosa yalikuwa lazima yaingie.”4 Kosa lilipoingia katika hati-mkono, lilirudiwa kufanywa wakati hati-mkono hiyo ilipokuwa msingi wa nakala za wakati ujao. Nakala nyingi zilipofanyizwa baada ya kipindi kirefu, vikosa vingi vya kibinadamu viliingia.

12, 13. Ni nani waliochukua daraka la kuhifadhi maandishi-awali ya Maandiko ya Kiebrania?

12 Kwa sababu ya maelfu mengi ya nakala za Biblia zilizofanyizwa, twajuaje kwamba utaratibu huo wa kufanyiza nyingine haukuibadili isiweze kujulikana? Basi, chukua kisa cha Biblia ya Kiebrania, “Agano la Kale.” Katika nusu ya pili ya karne ya sita K.W.K., Wayahudi waliporejea kutoka uhamisho wao wa Kibabuloni, kikundi kimoja cha wasomi Waebrania kilichojulikana kuwa Wasoferi, “waandishi,” kilikuja kuwa watunzaji wa maandishi-awali ya Biblia ya Kiebrania, na lilikuwa ni daraka lao kunakili Maandiko hayo kwa ajili ya matumizi katika ibada ya umma na ya kibinafsi. Walikuwa wanaume wenye kichocheo kikubwa, wataalamu, na kazi yao ilikuwa yenye ubora wa juu zaidi.

13 Kuanzia karne ya saba mpaka karne ya kumi ya Wakati wa Kawaida wetu, warithi wa Wasoferi walikuwa Wamasora. Jina lao hutokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “mapokeo,” na kwa msingi wao pia walikuwa waandishi waliokabidhiwa kazi ngumu ya kuhifadhi maandishi-awali ya Kiebrania ya kimapokeo. Wamasora walikuwa waangalifu sana. Kwa kielelezo, mwandishi alipaswa kutumia nakala iliyothibitishwa kwa kufaa ni asilia iwe maandishi-awali yake ya msingi, naye hakuruhusiwa kuandika chochote kutoka kumbukumbu yake. Alipaswa kuchunguza kila herufi kabla ya kuiandika.5 Profesa Norman K. Gottwald aripoti hivi: “Wazo fulani juu ya uangalifu ambao kwao walifanya wajibu wao laonyeshwa na takwa kwamba hati-mkono mpya zote zilipasa kusahihishwa na nakala zenye kasoro kutupwa mara moja.”6

14. Ni uvumbuzi gani uliofanya iwezekane kuthibitisha upokezaji wa Wasoferi na Wamasora wa maandishi-awali ya Biblia?

14 Mpitisho wa maandishi-awali kwa Wasoferi na Wamasora ulikuwa sahihi kadiri gani? Mpaka 1947 ilikuwa vigumu kujibu swali hilo, kwa kuwa hati-mkono kamili za Kiebrania za mapema zaidi zilizokuwako zilikuwa za kuanzia karne ya kumi ya Wakati wa Kawaida wetu. Hata hivyo, katika 1947, vipande vya hati-mkono vya kale sana vilipatikana katika mapango katika ujirani wa Bahari ya Chumvi, kutia ndani visehemu vya vitabu vya Biblia ya Kiebrania. Idadi fulani ya vipande ilikuwa ya tarehe ya kabla ya wakati wa Kristo. Wasomi walivilinganisha na hati-mkono za Kiebrania zilizokuwapo ili kuthibitisha usahihi wa upokezaji wa maandishi-awali. Tokeo la ulinganisho huo lilikuwa nini?

15. (a) Ni nini lililokuwa tokeo la kulinganisha hati-kunjo ya Isaya ya Bahari ya Chumvi na maandishi-awali ya Masora? (b) Twapaswa kufikia mkataa gani kutokana na uhakika wa kwamba hati-mkono fulani zilizopatikana katika Bahari ya Chumvi zaonyesha utofautiano fulani wa maandishi-awali? (Ona kielezi-chini.)

15 Kimoja cha vitabu vya mapema zaidi kilichovumbuliwa ni kitabu kamili cha Isaya, na ukaribiano wacho wa maandishi-awali na yale ya Biblia ya Masora tuliyo nayo leo wastaajabisha. Profesa Millar Burrows aandika hivi: “Nyingi za tofauti kati ya hati-kunjo ya Isaya ya Mt. Marko [iliyogunduliwa karibuni] na maandishi-awali ya Masora zaweza kuelezwa kuwa makosa ya unakiliji. Isipokuwa hayo, kwa ujumla, kuna kuafikiana kwa kutokeza, pamoja na maandishi-awali yanayopatikana katika hati-mkono za enzi za kati. Kuafikiana huko katika hati-mkono ya kale zaidi hutoa ushuhuda wenye kuhakikisha usahihi wa ujumla wa maandishi-awali ya kimapokeo.”7 Burrow aongeza hivi: “Ni jambo la kushangaza kwamba baada ya kitu kama miaka elfu moja maandishi-awali hayo yalibadilika kidogo sana.”b

16, 17. (a) Kwa nini twaweza kuwa na hakika kwamba maandishi-awali ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ni timamu? (b) Sir Frederic Kenyon alishuhudia nini juu ya maandishi-awali ya Maandiko ya Kigiriki?

16 Kwa habari ya sehemu ya Biblia iitwayo Agano Jipya, ambayo iliandikwa katika Kigiriki na Wakristo, wanakiliji walikuwa watu wenye kujitolea wenye karama tofauti na Wasoferi ambao walikuwa wataalamu waliozoezwa sana. Lakini wakiwa wanafanya kazi chini ya tisho la adhabu kutoka mamlaka, wao walichukua kazi yao kwa uzito. Na mambo mawili yatuhakikishia kwamba sisi leo tuna maandishi-awali ambayo kwa msingi ni kama yale yale yaliyoandikwa na waandikaji wa awali. Kwanza, tuna hati-mkono za tarehe ya karibu zaidi na wakati wa kuandikwa kuliko ilivyo katika kisa cha sehemu ya Kiebrania ya Biblia. Kwa kweli, kipande kimoja cha Gospeli ya Yohana ni cha nusu ya kwanza ya karne ya pili, miaka inayopungua 50 kutoka tarehe ambayo labda Yohana aliandika Gospeli yake. Pili, ile idadi yenyewe ya hati-mkono ambazo zimeokoka yatoa wonyesho mkubwa sana wa utimamu wa maandishi-awali hayo.

17 Kuhusu hilo, Sir Frederic Kenyon alishuhudia hivi: “Si kudai mno kwamba kwa mujibu wa maana yenyewe maandishi-awali ya Biblia ni hakika. Hasa ndivyo ilivyo na Agano Jipya. Idadi ya hati-mkono za Agano Jipya, za tafsiri za mapema zalo, na za manukuu yalo ya waandikaji wa kale zaidi wa Kanisa, ni kubwa sana hivi kwamba karibu ni hakika kwamba maandishi ya kweli ya kila kifungu chenye kutilika shaka yamehifadhiwa katika mojawapo hati hizi za kale. Haiwezi kusemwa hivyo juu ya kitabu kinginecho chote cha kale katika ulimwengu.”10

Watu na Lugha Zao

18, 19. Ilikuwaje kwamba Biblia haikubaki katika lugha ambazo iliandikwa hapo awali?

18 Baada ya muda mrefu, lugha za awali ambazo katika hizo Biblia iliandikwa, zilikuwa pia, kizuizi cha kuokoka kwayo. Vile vitabu 39 vya kwanza viliandikwa hasa katika Kiebrania, ulimi wa Waisraeli. Lakini Kiebrania hakijapata kujulikana sana. Kama Biblia ingalibaki katika lugha hiyo, haingalipata kamwe kuwa na uvutano nje ya taifa hilo la Kiyahudi na wageni wachache ambao wangeweza kukisoma. Hata hivyo, katika karne ya tatu K.W.K., kwa ajili ya faida ya Waebrania wenye kuishi katika Aleksandria, Misri, tafsiri ya sehemu ya Kiebrania ya Biblia ilianza katika Kigiriki. Wakati huo Kigiriki kilikuwa lugha ya kimataifa. Hivyo, Biblia ya Kiebrania ikapatikana kirahisi kwa wasio Wayahudi.

19 Ulipofika wakati wa sehemu ya pili ya Biblia kuandikwa, Kigiriki kilikuwa kingali kikitumiwa sana, kwa hiyo vile vitabu 27 vya mwisho vya Biblia viliandikwa katika ulimi huo. Lakini si kila mtu angeweza kuelewa Kigiriki. Kwa hiyo, tafsiri za sehemu za Kiebrania na Kigiriki pia za Biblia upesi zikaanza kuonekana katika lugha za kila siku za karne hizo za mapema, kama vile Kisiria, Kikopti, Kiarmenia, Kigeorgia, Kigothi, na Kiethiopia. Lugha rasmi ya Milki ya Kiroma ilikuwa Kilatini, na tafsiri za Kilatini zilifanyizwa katika idadi nyingi hivi kwamba ikawa lazima “tafsiri yenye kuidhinishwa” itolewe. Hiyo ilikamilishwa karibu 405 W.K. na ikaja kujulikana kuwa Vulgate (maana yake “yenye kupendwa na wengi” au “ya umma”).

20, 21. Vizuizi vya kuokoka kwa Biblia vilikuwa vipi, na ni kwa nini vilishindwa?

20 Hivyo, ijapokuwa vizuizi vingi, Biblia iliokoka mpaka karne za mapema za Wakati wa Kawaida wetu. Wale walioitokeza walikuwa wachache wenye kudharauliwa na kunyanyaswa ambao waliishi maisha magumu katika ulimwengu wenye uadui. Ingaliweza kupotoshwa vibaya sana kwa urahisi katika kuinakili, lakini sivyo. Zaidi ya hayo, iliponyoka hatari ya kupatikana kwa watu walionena lugha fulani fulani tu.

21 Kwa nini ilikuwa vigumu mno kwa Biblia kuokoka? Biblia yenyewe yasema: “Ulimwengu wote mzima unakaa katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW) Kwa sababu hiyo, tungetazamia ulimwengu uwe wenye uadui kwa kweli iliyotangazwa, na ndivyo imekuwa. Basi, ni kwa nini Biblia iliokoka ambapo vitabu vingine vingi ambavyo havikukabili magumu ayo hayo vilisahauliwa? Biblia hujibu pia. Yasema: “Neno la Bwana [Yehova, NW] hudumu hata milele.” (1 Petro 1:25, NW) Ikiwa Biblia ni Neno la Mungu kweli kweli, hakuna uwezo wa kibinadamu unaoweza kuiangamiza. Na mpaka karne hii ya 20, imekuwa hivyo.

22. Ni badiliko gani lililotukia mapema katika karne ya nne ya Wakati wa Kawaida wetu?

22 Hata hivyo, katika karne ya nne ya Wakati wa Kawaida wetu, jambo fulani lilitukia ambalo hatimaye likatokeza mashambulizi mapya juu ya Biblia na likabadili sana mwendo wa historia ya Ulaya. Miaka kumi tu baada ya Dioklesio kujaribu kuangamiza nakala zote za Biblia, sera ya milki hiyo ilibadilika na “Ukristo” ukawa halali. Miaka kumi na miwili baadaye, katika 325 W.K., maliki mmoja Mroma alisimamia Baraza la “Kikristo” la Nisea. Ni kwa nini iliyoonekana kuwa hatua nzuri hivyo ikaja kuwa hatari kwa Biblia? Tutaona katika sura inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Katika kichapo hiki, badala ya “A.D.” na “B.C.” ambavyo ni vifupisho vinavyotumiwa na wengi, “W.K.” (Wakati wa Kawaida) na “K.W.K.” (kabla ya Wakati wa Kawaida) ambavyo ndivyo sahihi zaidi vyatumiwa.

b Si hati-mkono zote zilizopatikana kwenye Bahari ya Chumvi zilizoafikiana kabisa na maandishi-awali ya Biblia yaliyopo. Nyingine zilionyesha utofautiano mkubwa wa maandishi-awali. Hata hivyo, tofauti hizo hazimaanishi kwamba maana ya msingi ya maandishi-awali imepotoshwa. Kulingana na Patrick W. Skehan wa Catholic University of America, nyingi zawakilisha “kufanyiza tena [kwa maandishi-awali ya Biblia] kwa msingi wa sababu nzuri yayo yenyewe iliyomo, hivi kwamba umbo lapanuliwa lakini maana yabaki ile ile . . . Mtazamo wa msingi ni wa heshima nyingi kabisa kwa ajili ya maandishi-awali yaliyoonwa kuwa matakatifu, mtazamo wa kueleza (kama ambavyo sisi tungesema) Biblia kwa kutumia Biblia katika mpitisho ule ule wa maandishi-awali yenyewe.”8

Mwelezaji mwingine aongeza hivi: “Ijapokuwa ukosefu wote wa uhakika, ukweli mkubwa ungali kwamba maandishi-awali kama tulivyo nayo sasa, kwa ujumla, yawakilisha kwa kadiri kubwa maneno yale yale ya watungaji walioishi, baadhi yao, karibu miaka elfu tatu iliyopita, nasi hatuhitaji kuwa na shaka nzito juu ya idadi ya mabadiliko ya maandishi-awali kuwa yaathiri thamani ya ujumbe ambao Agano la Kale latupa.”9

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

Maandishi-awali ya Biblia Yaliyothibitishwa Kabisa

Ili kuthamini jinsi maandishi-awali ya Biblia yalivyothibitishwa, twapaswa tu kuyalinganisha na sehemu fulani tu ya vitabu ambavyo vimetujia toka kale: maandishi bora sana ya Wagiriki na Waroma. Kwa kweli, vingi vya vitabu hivyo viliandikwa baada ya Maandiko ya Kiebrania kukamilishwa. Katika kumbukumbu hakuna majaribio ya kuangamiza taifa zima la Wagiriki au Waroma, na vitabu vyao havikuhifadhiwa chini ya mnyanyaso. Hata hivyo, angalia maelezo ya Profesa F. F. Bruce:

“Kwa ajili ya Gallic War cha Kaisari (kilichotungwa kati ya 58 na 50 B.C.) kuna hati-mkono kadhaa za kale, lakini ni tisa au nane tu zilizo nzuri, na ya kale zaidi ni ya miaka 900 hivi baada ya siku ya Kaisari.

“Kati ya vile vitabu 142 vya historia ya Kiroma ya Livy (59 B.C.-A.D. 17), ni 35 tu vilivyookoka; vyajulikana kwetu kutokana na hati-mkono zisizozidi ishirini ambazo hazina maana, moja tu kati yazo, na ikiwa na vipande vya Vitabu 3-6, ndiyo ya kale kufikia karne ya nne.

“Kati ya vile vitabu kumi na vinne vya Histories vya Takito (c. [karibu] A.D. 100) ni vinne na nusu tu vilivyookoka; kati ya vile vitabu vyake kumi na sita vya Annals, kumi vimeokoka vikiwa kamili na viwili vikiwa sehemu. Maandishi-awali ya visehemu hivyo vya kale ya vitabu vyake vya kihistoria hutegemea kabisa hati-mkono mbili, moja ya karne ya tisa na nyingine ya ile ya kumi na moja. . . .

“Historia ya Thucydides (c. [karibu] 460-400 B.C.) yajulikana kwetu kutokana na hati-mkono nane, ile ya mapema zaidi ikiwa ni ya c. [karibu] A.D. 900, na visehemu vichache vya mafunjo, vya karibu mwanzo wa kipindi cha Kikristo.

“Ni hali moja na Historia ya Herodoto (c. [karibu] 488-428 B.C.). Hata hivyo hakuna msomi yeyote wa vitabu vilivyo bora ambaye angeweza kusikiliza hoja ya kwamba uasilia wa Herodoto au Thucydides watilika shaka kwa sababu hati-mkono za mapema zaidi za vitabu vyao vyenye mafaa yoyote kwetu ni vya miaka 1,300 baada ya vile vya awali.”—The Books and the Parchments, ukurasa 180.

Linganisha hili na uhakika wa kwamba kuna maelfu ya hati-mkono za sehemu mbalimbali za Biblia. Na hati-mkono za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zarudi nyuma kufikia miaka mia moja wakati wa uandikaji wa vitabu vya awali.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Waebrania walikuwa taifa dogo lililotishwa daima na mataifa yenye nguvu zaidi. Mchongo huu wa kale waonyesha Waebrania fulani wakipelekwa utumwani na Waashuri

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kabla ya kuwasili kwa uchapaji, Maandiko yalinakiliwa kwa mkono

[Picha katika ukurasa wa 16]

Nero alifanya kuwa Mkristo kuwe kosa la kustahili kifo

[Picha katika ukurasa wa 21]

Utafiti wa kunjo la Bahari ya Chumvi ulithibitisha kwamba kitabu hiki kilikuwa karibu kimebaki bila kubadilishwa kwa kipindi cha miaka zaidi ya 1,000

[Picha katika ukurasa wa 23]

Maliki Dioklesio alishindwa katika jitihada zake za kuangamiza Biblia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki