Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 5/15 kur. 26-28
  • Ni Nini Mwandiko wa Kimasora?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nini Mwandiko wa Kimasora?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Neno la Yehova
  • Mlango wa Makosa Ulifunguka Kidogo
  • Majaribio ya Kuondoa Makosa
  • Je, Twaweza Kupata Mwandiko wa Kimasora Ulio “Safi”?
  • Wamasora Walikuwa Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Jinsi Ulivyotayarishiwa Maandiko ya Kiebrania
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Hati-Mkono ya Biblia ya Kiebrania Iliyo Kiolezo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Funzo Namba 5—Maandishi-Awali ya Kiebrania ya Maandiko Matakatifu
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 5/15 kur. 26-28

Ni Nini Mwandiko wa Kimasora?

HATA uwe unasoma Biblia katika lugha gani, yaelekea sehemu ya kitabu hicho ilitafsiriwa moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja kutoka kwa mwandiko wa Kimasora, ambao ni Maandiko ya Kiebrania, au “Testamenti ya Kale.” Kwa hakika kulikuwa na zaidi ya mwandiko mmoja wa Kimasora. Kwa hiyo ni upi uliochaguliwa, na kwa nini? Kwa kweli, ni nini mwandiko wa Kimasora, nasi twajuaje kwamba unategemeka?

Neno la Yehova

Uandikaji wa Biblia ulianza kwenye Mlima Sinai katika 1513 K.W.K. Kutoka 24:3, 4 latuambia hivi: “Musa akaenda akawaambia watu maneno yote ya BWANA, na hukumu zake zote; watu wote wakajibu kwa sauti moja, wakasema, Maneno yote aliyoyanena BWANA tutayatenda. Basi Musa akayaandika maneno yote ya BWANA.”

Maandiko ya Kiebrania yaliendelea kurekodiwa kwa zaidi ya miaka elfu moja, tangu 1513 K.W.K. hadi karibu 443 K.W.K. Kwa kuwa waandikaji walikuwa wamepuliziwa na Mungu, ni jambo la kupatana na akili kwamba yeye angeelekeza mambo ili ujumbe wake uhifadhiwe kwa uaminifu. (2 Samweli 23:2; Isaya 40:8) Lakini, je, hilo lamaanisha kwamba Yehova angezuia makosa yote ya kibinadamu ili hata herufi moja isingebadilishwa nakala zilipokuwa zikifanyizwa?

Mlango wa Makosa Ulifunguka Kidogo

Ingawa wanaume wenye staha ya kina kwa Neno la Mungu walilinakili tangu kizazi hadi kizazi, kadiri fulani ya makosa ya kibinadamu yalipenya katika hati-mkono. Waandikaji wa Biblia walipuliziwa, lakini wanakili hawakufanya kazi zao wakiwa wamepuliziwa kimungu.

Baada ya kutoka uhamisho wa Babiloni katika 537 K.W.K., Wayahudi walianza mtindo mpya wa kuandika uliotumia herufi za mraba walizojifunza Babiloni. Badiliko hilo kubwa lilitokeza tatizo la asili la kwamba herufi fulani zilizofanana zingeweza kukosewa na nyingine. Kwa kuwa Kiebrania ni lugha inayotegemea konsonanti, huku sauti za vokali zikiongezwa na msomaji kwa kutegemea uelewevu wake wa muktadha, badiliko la konsonanti moja lingeweza kwa urahisi kubadili maana ya neno. Hata hivyo, mara nyingi makosa hayo yangetambulika na kusahihishwa.

Wayahudi wengi zaidi hawakurudi Israeli baada ya kuanguka kwa Babiloni. Hivyo, masinagogi yakawa vitovu vya mambo ya kiroho vya jumuiya za Kiyahudi kotekote Mashariki ya Kati na Ulaya.a Kila sinagogi lilihitaji nakala za makunjo ya Maandiko. Kadiri nakala zilipoongezeka, ndivyo uwezekano wa wanakili kufanya kosa ulivyoongezeka.

Majaribio ya Kuondoa Makosa

Kuanzia karne ya kwanza W.K., waandishi katika Yerusalemu walijaribu kuweka mwandiko wa msingi ambao makunjo yote ya Maandiko ya Kiebrania yangerekebishiwa. Na bado, hakukuwa na utaratibu hususa wa kutofautisha kati ya uawali wa mwandiko na hati-mkono zenye makosa ya wanakili. Tangu karne ya pili W.K. na kuendelea, mwandiko wa kikonsonanti wa Maandiko ya Kiebrania ulionekana kuwa umesanifishwa kwa kadiri fulani, ingawa haukuwa umepewa mamlaka kamili. Manukuu ya Maandiko ya Kiebrania yaonekanayo katika Talmud (iliyokusanywa kati ya karne za pili na sita W.K.) mara nyingi huonyesha chanzo tofauti na kile kilichokuja baadaye kuitwa mwandiko wa Kimasora.

Neno “pokeo” katika Kiebrania ni ma·soh·rahʹ au ma·soʹreth. Kufikia karne ya sita W.K., wale waliolinda pokeo la kunakili kwa usahihi Maandiko ya Kiebrania walikuja kuitwa Wamasora. Nakala walizofanyiza hurejezewa kuwa miandiko ya Kimasora. Ni nini lililokuwa jambo la kipekee kuhusu kazi yao na miandiko waliyotayarisha?

Kiebrania kilikuwa kimefifia kuwa lugha ya kitaifa iliyotumika, na Wayahudi wengi hawakukifahamu tena. Kwa hiyo, uelewevu wa mwandiko wa Kibiblia wa kikonsonanti ulikuwa hatarini. Ili kuulinda, Wamasora walisitawisha mfumo wa vokali zilizowakilishwa na nukta ama vistari. Hizo ziliwekwa juu na chini ya konsonanti. Wamasora pia walisitawisha mfumo tata wa alama zilizotumika kuwa namna ya vituo na vilevile kuwa mwongozo wa utamkaji sahihi zaidi.

Mahali ambapo Wamasora walihisi kwamba mwandiko ulikuwa umebadilishwa au kunakiliwa kimakosa na vizazi vya awali vya waandishi, badala ya kubadili mwandiko, walitia maandishi katika pambizo za kando. Wao waliandika mifanyizo isiyo ya kawaida ya maneno na ukawaida ambao maneno hayo yalitokea katika kitabu fulani hususa au katika Maandiko ya Kiebrania yote. Maelezo zaidi ya kusaidia wanakili katika kuchunguza milinganisho yaliandikwa pia. Mfumo wa “herufi” zilizofupishwa ulisitawishwa ili kurekodi habari hii kwa ufupi sana. Katika pambizo za juu na chini, aina fulani ya konkodansi ndogo iliorodhesha sehemu za mistari iliyohusiana ambayo ilikuwa imefafanuliwa katika habari zilizo pambizoni.

Mfumo ujulikanao zaidi uliboreshwa na Wamasora katika Tiberia, kando ya Bahari ya Galilaya. Familia za Ben Asheri na Ben Naftali wa karne za tisa na kumi W.K., yawezekana Wakaraite, hasa zilikuja kuwa mashuhuri sana.b Ingawa kulikuwa na tofauti kati ya njia za kutamka maneno na vilevile maandishi ya pambizoni ya vikundi hivyo viwili, konsonanti za miandiko yao zatofautiana mara chache kuliko kumi katika Maandiko ya Kiebrania yote.

Vikundi vyote viwili vya Wamasora, kile cha Ben Asheri na Ben Naftali, vilichangia sana usomi wa mwandiko katika wakati wao. Baada ya Maimonidi (Msomi mmoja mashuhuri wa Talmud wa karne ya 12) kusifu mwandiko wa Ben Asheri, wengine waliupendelea kabisa. Hiyo ilifikia hatua ya kwamba hakuna hati-mkono za Ben Naftali ziwezazo kupatikana leo. Yote yanayobaki ni orodha za tofauti zilizokuwa kati ya vikundi hivyo viwili. Kumbe, maelezo ya Maimonidi yalihusika na mtindo, kama vile nafasi zilizopo kati ya mafungu, na si mambo ya maana zaidi ya usahihi wa kupitishwa kwa mwandiko.

Je, Twaweza Kupata Mwandiko wa Kimasora Ulio “Safi”?

Kuna ubishi mwingi miongoni mwa wasomi kuhusu ni kodeksi gani ipatikanayo leo iliyo mwandiko “safi” wa Ben Asheri, kana kwamba huo utatupa mwandiko “wa kweli” wa Kimasora. Kwa kweli, hakujapata kuwa na mwandiko wa Kimasora ulio wa kipekee, “safi,” na wenye mamlaka. Badala ya hivyo, kumekuwa na miandiko mingi ya Kimasora, kila mmoja ukiwa tofauti kidogo na mwingine. Kodeksi zote zinazopatikana leo ni miandiko iliyochanganyikana, ikiwa na maelezo ya Ben Asheri na ya Ben Naftali.

Jukumu linalokabili mtafsiri yeyote wa Maandiko ya Kiebrania leo ni gumu sana. Ni lazima afahamu si tu mwandiko wa Kiebrania bali pia mambo mengine ya badala ambapo mwandiko huenda ulibadilishwa kupitia kosa la mnakili au kwa sababu nyingine. Ingawa miandiko mingi ya Kimasora hutumika ikiwa msingi, anahitaji kuchunguza vyanzo vingine halali ambavyo vingeweza kwa njia ifaayo kutokeza fasiri za zamani zaidi na labda zilizo sahihi zaidi za mwandiko wa kikonsonanti.

Katika utangulizi wa kitabu chake The Text of the Old Testament, Ernst Würthwein aeleza: “Tukabilipo fungu gumu hatuwezi kukusanya tu maelezo mbalimbali na kuchagua lile linaloonekana kutoa suluhisho rahisi zaidi, nyakati nyingine tukipendelea mwandiko wa Kiebrania, nyakati nyingine Septuagint, na bado nyakati nyingine Targum ya Kiaramu. Ushahidi wa miandiko yote hautegemeki kwa kiwango kilekile. Kila mmoja una namna yao na historia yao ya kipekee. Ni lazima tufahamu hayo ikiwa tunatumaini kuepuka masuluhisho yasiyotosheleza au yasiyofaa.”

Tuna msingi imara wa kuwa na hakika kamili kwamba Yehova amehifadhi Neno lake. Kwa jitihada za pamoja za wanaume wengi wanyoofu katika karne zilizopita, hali, yaliyomo, na hata mambo madogo-madogo ya ujumbe wa Biblia yanapatikana kwa urahisi. Mabadilisho yoyote madogo-madogo katika herufi au neno hayajaathiri uwezo wetu wa kuelewa Maandiko. Sasa, swali muhimu ni, Je, tutaishi kwa kupatana na Neno la Mungu, Biblia?

[Maelezo ya chinis]

a Kwa kuwa Wayahudi wengi waliokuwa nje ya Israeli hawakuwa tena wasomaji wenye ufasaha wa Kiebrania, jumuiya hizo za Kiyahudi kama ile iliyokuwa katika Aleksandria, Misri, upesi ziliona uhitaji wa tafsiri za Biblia katika lugha zao. Ili kusuluhisha uhitaji huo, fasiri ya Septuagint ya Kigiriki ilitayarishwa katika karne ya tatu K.W.K. Fasiri hii baadaye ingekuwa chanzo muhimu sana cha kufanyia mlinganisho.

b Karibu na mwaka 760 W.K., kikundi cha Kiyahudi kilichoitwa Wakaraite kilisisitiza kushika zaidi Maandiko. Wakikataa mamlaka ya warabi, “Sheria ya Mdomo,” na Talmud, wao walikuwa na sababu kubwa zaidi ya kulinda mwandiko wa Biblia kitaratibu. Familia fulani katika kikundi hiki zilikuja kuwa wanakili wa Kimasora walio stadi sana.

[Picha katika ukurasa wa26]

Kodeksi ya Aleppo ina mwandiko wa Kimasora

[Hisani]

Bibelmuseum, Münster

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki