Hati-Mkono ya Biblia ya Kiebrania Iliyo Kiolezo
KABLA ya uvumbuzi wa Hati-Kunjo za Bahari ya Chumvi katika 1947, hati-mkono za Biblia ya Kiebrania za mapema zaidi kujulikana—licha ya vijipande vichache—zilikuwa za tangu mwisho-mwisho wa karne ya 9 hadi karne ya 11 W.K. Hiyo haizidi miaka elfu moja iliyopita. Je! hiyo yamaanisha kwamba kabla ya 1947 maandishi-awali ya Kiebrania ya Biblia hayakujulikana? Na kwa nini kulikuwako hati-mkono za Kiebrania za kale chache sana?
Kwa kuzungumzia swali hilo la mwisho kwanza, chini ya mfumo wa Kiyahudi uliokubaliwa, hati-mkono yoyote ya Biblia ya Kiebrania iliyoonwa kuwa imechakaa sana kuweza kutumiwa zaidi ilifungiwa mbali katika geniza (chumba cha kuhifadhia vitu katika sinagogi). Baadaye, hati-mkono hizo zilizochakaa zilizokuwa zimekusanywa zilitolewa nje na kuzikwa. Wayahudi walifanya hivyo ili kuyazuia Maandiko yao yasichafuliwe au kutumiwa vibaya. Kwa nini? Kwa sababu yalikuwa na Tetragramatoni, herufi za Kiebrania zilizowakilisha lile jina takatifu la Mungu, linaloonyeshwa kwa kawaida katika Kiswahili kuwa “Yehova.”
Lile “Taji”
Kwa kadiri kubwa zaidi, maandishi-awali ya Kiebrania ya kale yamepitishwa kwa uaminifu kutoka nyakati za mapema zaidi. Kwa mfano, kumekuwako hati-mkono ya Kiebrania yenye maana, iitwayo Keter, lile “Taji,” ambayo mwanzoni ilikuwa na Maandiko ya Kiebrania yote, au “Agano la Kale.” Ililindwa katika sinagogi la zamani zaidi la jumuiya ndogo ya kale ya Wayahudi walioishi katika Aleppo, Siria, ambao ni mji wenye Waislamu wengi. Mapema zaidi, hati-mkono hiyo ilikuwa imeachiwa Wayahudi Wakaraite katika Yerusalemu, lakini ilitekwa katika 1099, na Wapiganaji Vita vya Krusedi. Baadaye, hati-mkono hiyo ilipatikana tena na kupelekwa Old Kairo, Misri. Iliwasili Aleppo kufikia angalau karne ya 15 na baadaye ikajulikana kuwa Kodeksi ya Aleppo. Hati-mkono hiyo, iliyokuwa ya tarehe ya nyuma kufikia angalau 930 W.K., ilionwa kuwa taji la uanachuo wa Masora, kama vile jina layo hudokeza. Ni mfano mzuri wa kuonyesha uangalifu uliotolewa katika kupisha maandishi-awali ya Biblia na kwa kweli, ilikuwa hati-mkono ya Kiebrania iliyo kiolezo.
Katika nyakati za kisasa zaidi, watunzaji wa hati-mkono hiyo yenye kutokeza, wakihofu kishirikina kuchafuliwa kwa kitu chao kitakatifu, walikuwa hawaruhusu kichunguzwe na wanachuo. Isitoshe, kwa kuwa ni ukurasa mmoja tu uliopata kupigwa picha, nakala ilikuwa haiwezi kutangazwa kwa chapa ili ichunguzwe.
Waingereza walipoondoka Palestina katika 1948, ghasia zilitokea katika Aleppo dhidi ya Wayahudi. Sinagogi lao lilichomwa; kodeksi hiyo yenye thamani ku-bwa ilipotea ikadhaniwa kwamba ilikuwa imeharibiwa. Kwa hiyo, lilikuwa jambo la kushangaza kama nini, miaka kumi hivi baadaye, kupata kujua kwamba karibu robo tatu yayo ilikuwa imeokoka na kutolewa nje ya Siria kisiri kupelekwa hadi Yerusalemu! Katika 1976 chapa-nakili nzuri yenye nakala 500 zenye rangi kamili ilitolewa hatimaye.
Kazi ya Mstadi
Kwa nini hati-mkono hiyo ni ya maana sana? Kwa sababu maandishi-awali yayo ya kwanza hasa ya kikonsonanti yalisahihishwa na kutiwa alama za vituo kufikia yapata 930 W.K. na Aaron ben Asher, mmoja wa wale wanachuo mashuhuri waliozoezwa katika kunakili na kupitisha Biblia ya Kiebrania. Kwa hiyo ilikuwa kodeksi iliyo kiolezo, ikiwekea kiwango nakala za wakati ujao zilizofanywa na waandishi waliokuwa na ustadi mdogo zaidi.
Mwanzoni ilikuwa na folio 380 (kurasa 760) na iliandikwa kwa ujumla katika safu tatu kwenye kurasa za ngozi. Sasa ina folio 294 na inakosa sehemu kubwa ya Pentateuki na sehemu yayo ya mwisho, iliyokuwa na Maombolezo, Wimbo Ulio Bora, Danieli, Esta, Ezra, na Nehemia. Inatajwa kuwa “Al” katika New World Translation of the Holy Scriptures—Reference Bible (Yoshua 21:37, NW, kielezi-chini). Moses Maimonides (aliyeonyeshwa hapa), mwanachuo Myahudi mashuhuri wa enzi za kati wa karne ya 12 W.K., aliitamka Kodeksi ya Aleppo kuwa bora zaidi ya yoyote aliyopata kuona.a
Maandishi-awali ya Kiebrania yaliyonakiliwa kwa mkono kutoka karne ya 13 kupitia karne ya 15 yalikuwa yenye kuchanganyika yaliyotolewa kutoka familia mbili kuu za Masora, ile ya Ben Asher na ile ya Ben Naphtali. Katika karne ya 16, Jacob ben Hayyim alitokeza maandishi-awali ya Biblia ya Kiebrania iliyochapishwa yaliyochukuliwa kutoka mapokeo hayo yaliyochanganyika, na hayo yakawa ndiyo msingi wa karibu Biblia zote za Kiebrania kwa muda wa miaka 400 iliyofuata.
Kukiwa na ile chapa ya tatu katika 1937 ya Biblia Hebraica (maandishi-awali ya Kiebrania yaliyochapishwa), mapokeo ya Ben Asher yalichunguzwa kwani yalikuwa yamehifadhiwa katika hati-mkono iliyowekwa katika Urusi, iliyojulikana kuwa Leningrad B 19A. Hiyo Leningrad B 19A ni ya tarehe kutoka 1008 W.K. Chuo Kikuu cha Kiebrania katika Yerusalemu kinapanga kutangaza kwa chapa maandishi-awali ya Kiebrania ya Aleppo kwa ukamili kwa muda fulani wa wakati, pamoja na maandishi kutoka hati-mikono na tafsiri nyinginezo zote zenye maana, kutia na Hati-Kunjo za Bahari ya Chumvi.
Maandishi-awali ya Biblia tunayotumia leo ni yenye kutegemeka. Yalipuliziwa roho kimungu na yalipitishwa kwa muda wa karne kadhaa zilizopita na waandishi wenye kunakili waliofanya kazi kwa ustadi wenye uangalifu mwingi. Uangalifu mwingi wa wanakili hao huonekana kwa habari ya kwamba milinganisho kati ya hati-kunjo ya Isaya iliyopatikana kando ya Bahari ya Chumvi katika 1947 na maandishi-awali ya Masora huonyesha tofauti chache kwa jinsi ya kushangaza, hata ingawa Hati-Kunjo ya Bahari ya Chumvi ni ya zamani zaidi ya miaka elfu moja kuliko Biblia za Masora zilizoko. Isitoshe, kwa kuwa sasa Kodeksi ya Aleppo inapatikana kwa wanachuo, itaandaa sababu nyingine zaidi ya kuwa na uhakika katika uasilia wa maandishi-awali ya Maandiko ya Kiebrania. Kwa kweli, “neno la Mungu wetu litasimama milele.”—Isaya 40:8.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa miaka kadhaa wanachuo fulani walitilia shaka kwamba Kodeksi ya Aleppo ilikuwa hati-mkono iliyotiwa alama za vituo na Ben Asher. Hata hivyo, kwa kuwa kodeksi hiyo imepatikana ili iweze kuchunguzwa, ushuhuda umetokea wa kwamba hiyo ndiyo hati-mkono hasa ya Ben Asher iliyotajwa na Maimonides.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 28]
Bibelmuseum, Münster
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 29]
Jewish Division/The New York Public Library/Astor, Lenox, and Tilden Foundations