Dini Katika Poland ya Leo
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA POLAND
WATU wa Poland wamejulikana ulimwenguni kote kuwa watu wenye kushika dini sana. Kwa kweli, asilimia 95 ya Wapoland hudai kuwa wafuasi wa Katoliki ya Kiroma.
Sherehe za kidini huchukuliwa kwa uzito sana katika nchi hii nazo ni sehemu kuu za desturi za kitaifa. Hasa katika sehemu za mashambani, sikukuu za kidini zaweza kuvutia sana na kuwa zenye shangwe sana, huku washiriki wakivalia mavazi ya kidesturi na watu wakicheza michezo.
Vyombo vya habari hutangaza matukio kama hayo, na vilevile safari za kwenda kwenye sehemu za ibada zilizo maarufu na misafara ya kidini. Ubatizo, ndoa za kanisa, na sherehe za somo watakatifu na Sakramenti hustahiwa sana.
Mnamo 1978, Karol Wojtyła, kutoka Poland, akawa Papa John Paul wa Pili. Jambo hilo lilichochea hata zaidi dini ya Katoliki katika Poland. Halaiki za watu humkaribisha papa huyo wakati wowote azurupo nchi yake ya uzaliwa.
Utendaji huo wote wa kidini waweza kufanya watu walio nje ya Poland wafikirie kwamba Wapoland wana imani yenye nguvu sana ambayo imedhihirishwa peupe. Lakini, nchini Poland viongozi wa Katoliki na watazamaji wengine huhangaikia mitazamo inayobadilika na tabia za idadi inayozidi kukua za washiriki wa kanisa.
Maoni ya Wapoland
Wawakilishi maarufu wa makasisi wa Katoliki ya Poland pamoja na waandishi wa habari na watafiti wa mambo ya kijamii wana maoni tofauti juu ya hali ya dini ya Katoliki katika Poland ya leo. Kwa hali inayoongezeka zaidi, viongozi wanazidi kutoa taarifa zenye nguvu dhidi ya uhalifu unaoongezeka, kuzorota kwa maadili, na kupungua kwa upendezi kwa mafundisho na matendo ya kanisa. Jambo kuu la mazungumzo hayo latia ndani swali, Namna ya ibada ya Katoliki ya Kiroma inaathirije maisha ya watu ya kila siku?
Kwa mfano, Askofu-Mkuu wa Poland Józef Glemp alitaja kwamba watu wanazidi kufuatia mambo ya kilimwengu naye alitaja kwamba kuna uhitaji wa kupinga kuenea kwa upagani wa kisasa unaopata nchi hiyo. Katika gazeti la Katoliki Ład, mwandikaji Wojciech Chudy alichunguza sana hali hiyo. Alisema: ‘Ni lazima tulifikirie suala ambalo limekuwa likiwasumbua kwa miaka mingi makasisi, wataalamu wa kijamii, na wataalamu wa kiakili ambao wanahusika na dini kwa miaka kadhaa—kujua mgawanyiko dhahiri kati ya maisha ya kidini na maisha ya kila siku. Unasikiliza hotuba, lakini punde tu utokapo nje ya kanisa, unasahau kabisa ulimwengu wa Mungu. Unaingia katika ulimwengu mwingine, ambamo unaendesha maisha yako kana kwamba Mungu hayuko kamwe.’
Askofu-Mkuu Henryk Muszyński, naibu-msimamizi wa Baraza la Maaskofu, aendelea kusema: “Gospeli haijaweza kutubadilisha kindani. Wapoland ni Wakristo kwa jina tu. Mtu hawezi kukanusha jambo la kwamba watu wengi huuona Ukristo kuwa desturi badala ya kuwa dini.”
Maadili Yaliyobadilika—Mwenendo Uliobadilika
Maneno kama hayo yanaonyesha kwamba wawakilishi mashuhuri wa kanisa wana wasiwasi juu ya mabadiliko makubwa ambayo yametokea kuhusu maadili na mwenendo wa umma. Sababu moja ni kwamba, ule ujitoaji wa awali wa kidini waonekana kama unabadilishwa na mahangaiko mengine.
Kwa mfano, katika uchunguzi mmoja wa kijamii, Wapoland walitanguliza familia katika maisha zao, ikifuatiwa na unyoofu, haki, fadhili, na kutegemeka. Mambo yahusuyo Mungu na dini yalikuwa namba 16. Tokeo la jambo hili ni kupunguka kwa hudhurio la kanisa, hata miongoni mwa wale wanaodai kuwa waamini.
Maaskofu wa Poland pia wana wasiwasi kuhusu takwimu zinazoonyesha kupuuzwa sana kwa mafundisho ya kanisa. Kwa mfano, katika uchunguzi uliohusu mambo ya kidini uliofanywa na Irena Borowik wa Chuo Kikuu cha Jagielloński, ni asilimia 50 pekee ya watu waliojibu waliosema kwamba wanaamini uhai huendelea baada ya kifo, asilimia 47 walifikiri kwamba makasisi wanapaswa kuruhusiwa kufunga ndoa, na asilimia 64 walikubali kwamba ni sawa kupata talaka.
Uchunguzi mwingine, uliochapishwa katika gazeti Wprost, ulionyesha kwamba “asilimia 69 ya Wapoland hushutumu katazo la kanisa la kutumia mbinu za kuzuia uzazi, asilimia 56 walipinga marufuku juu ya utoaji wa mimba, na asilimia 54 walikubali kuwa ni sawa kufanya ngono kabla ya ndoa.” Takwimu hizo zinaonyesha migawanyiko ya wakati huu ndani ya kanisa.
Kanisa lilipata staha sana katika miongo miwili iliyopita kwa sababu ya kupinga Wakomunisti. Lakini, sasa, hali ya kanisa ya kuendelea kujihusisha na masuala ya kisiasa na ya kijamii yaonekana kuwa inatokeza uhasama, jambo linalosababisha hata migawanyiko mikubwa zaidi kati ya washiriki wa kanisa na viongozi wa kanisa.
Kuna Suluhisho Gani Halisi?
Kabla ya mabadiliko ya kihistoria ya kisiasa ya mwaka wa 1989, kanuni fulani hususa za mwenendo zilikuwa zimewekwa na serikali. Nyingi za kanuni hizo sasa hazipo. Mfumo mpya wa kisiasa sasa umeleta demokrasia na uhuru wa kibinafsi na vilevile jitihada za kung’ang’ana katika uchumi wa soko-huru. Wengi wanahisi kwamba Wapoland hawakuwa tayari kabisa kwa badiliko kubwa kama hilo. Ni nini kilichokosekana?
Kuokoka kimaadili na kiroho katika ulimwengu wa leo kunahitaji imani inayotegemea kitu chenye nguvu zaidi kuliko mazoea au sherehe za kidini. Ni lazima kila mtu apate imani ambayo imetegemea kabisa ujuzi na uelewevu wa Neno la Mungu, Biblia.
Hivi majuzi, Papa John Paul wa Pili mwenyewe alikiri kwamba kuna uhitaji wa Wakristo kuwa wasomaji wa kawaida wa Maandiko Matakatifu. Aliwaomba watu “wasitawishe mawasiliano zaidi na ya kawaida na Neno la Mungu.” Aliongezea: “Kujifunza kusoma Andiko Takatifu ni jambo la msingi kwa kila mwamini: ndiyo hatua ya kwanza, ambayo huendelezwa kwa kutafakari, na kwa sala yenye bidii.” Papa alitia moyo “kila mtu ambaye ametafuta kweli . . . ajilishe kila siku kwa mkate wa Neno la Mungu la Uhai.”
Karne 19 zilizopita, muda mrefu kabla ya maisha kuwa na hekaheka nyingi na kukosa uthabiti kama yalivyo sasa, Yesu Kristo alimwomba Mungu alinde wanafunzi wake dhidi ya mavutano yenye kudhoofisha kiroho yaliyowazunguka. Alisali hivi: “Watakase kwa njia ya ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Na sababu ya kwamba Biblia “ndiyo kweli” ni kwamba hiyo ni Neno la Mungu, wala si la mwanadamu. Mtume Paulo aliandikia kutaniko moja: “Mlipopokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.
Kwa sababu Biblia ni “Neno la Mungu” na “ni kweli,” inaweza kuandaa kile tunachohitaji ili kujiimarisha katika ulimwengu huu wenye kufuatia mambo ya kilimwengu. Biblia yasema: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.
Watu wengi walio wanyoofu na wenye akili nchini Poland na ulimwenguni pote wanapata kwamba funzo la kibinafsi la Biblia huandaa msingi thabiti kwa imani katika Mungu na kusudi lake. Ni aina hii ya imani inayowapa nguvu ili waishi kikweli maisha ya Kikristo katika ulimwengu huu wa leo unaozidi kufuatia mambo ya kilimwengu.
[Blabu katika ukurasa wa 16]
“Wapoland ni Wakristo kwa jina tu.”—Askofu-Mkuu mmoja wa Poland
[Blabu katika ukurasa wa 17]
Mafundisho ya kanisa yamepuuzwa sana
[Ramani katika ukurasa wa 15]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
POLAND