Haki za Kibinadamu kwa Wote—Uhalisi wa Ulimwenguni Pote!
“NI NINI kisababishi kikuu cha ukiukaji wa haki za kibinadamu?” wakili mmoja mwenye uzoefu wa haki za kibinadamu aliulizwa swali hili. Wakili huyo alijibu, “pupa.” “Pupa ya kutaka mamlaka ya kisiasa na kiuchumi.” Na kwa kuwa pupa husitawi katika akili za binadamu, ukiukaji wa haki za kibinadamu hatimaye huonyesha hali ya akilini. Kisababishi kingine ni utukuzo wa taifa. Falsafa ya nchi yangu kwanza huchochea ukiukaji wa haki za kibinadamu. Kwa hiyo haki za kibinadamu zitapatikana tu ‘ikiwa kutakuja serikali ya ulimwengu itakayokuwa na uwezo wa kuchukua hatua imara,’ asema profesa wa sheria na uchumi wa Uholanzi Jan Berkouwer.
Yaani, ili haki za kibinadamu ziweze kupatikana tufeni pote, angalau mambo mawili yapasa kutokea kwanza: badiliko la akili na badiliko la serikali. Je, ni kufikiri kuzuri kutarajia mambo haya yatukie?
Sababu Yenye Mambo Mawili kwa Badiliko
Huku Mwongo wa Elimu ya Haki za Kibinadamu wa UM ukikaribia kuingia mwaka wake wa tano, kwa miongo mingi programu ya kimataifa ya elimu isiyokuwa ya serikali tayari imekuwa ikifaulu kubadili akili za mamilioni ya watu. Tokeo ni kwamba watu hawa sasa wanawatendea wanadamu wenzao kwa adhama. Programu hii inayotekelezwa na Mashahidi wa Yehova, inatenda katika zaidi ya nchi 230. Kwa nini inafanya kazi?
Jambo moja ni kwamba, programu hii ya elimu ya Biblia hupanua uelewevu wa watu kuhusu chanzo cha haki za kibinadamu. Azimio kwa Wote la Haki za Kibinadamu lasema kwamba mwanadamu ana haki kwa sababu ana uwezo wa kufikiri na kufuatia adili.
Lazima mwanadamu awe alipokea uwezo wake wa kufikiri kutoka chanzo cha juu zaidi. (Ona sanduku “Chanzo cha Haki za Kibinadamu,” kwenye ukurasa wa 13.) Kutambua chanzo hiki cha juu cha kimungu hutokeza sababu yenye nguvu ya kumheshimu mwanadamu mwenzako. Kisha unawatendea wengine kwa adhama si kwa sababu tu dhamiri yako inakusukuma ufanye hivyo bali, la maana zaidi, kwa sababu ya heshima na upendo wako kwa Muumba hukusukuma utendee uumbaji wake kwa adhama. Mfikio huu wenye sababu mbili wategemea maneno ya Yesu Kristo: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote” na, “Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:37-39) Mtu anayemheshimu sana Muumba hangekiuka kamwe haki za mwenzake kwa sababu ni urithi kutoka kwa Mungu. Mkiukaji wa haki za kibinadamu ni mpokonyaji wa urithi huo.
Elimu Inayotokeza Mabadiliko
Programu hii ya elimu ya Biblia ya Mashahidi wa Yehova ina matokeo kadiri gani katika kupunguza ukiukaji wa haki za kibinadamu? Njia bora ya kujibu swali hilo ni kutazama matokeo ya programu hiyo, kwa kuwa Yesu alisema, “hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kwa kazi zayo.”—Mathayo 11:19.
Mwandiko unaojulikana vizuri kwenye ukuta wa Jengo la Umoja wa Mataifa katika New York City wasema hivi: “Watafua panga zao ziwe majembe. Na mikuki yao kuwa miundu: Taifa halitainua upanga dhidi ya taifa lingine. Wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Kwa nukuu hili kutoka kitabu cha Biblia cha Isaya sura ya 2, mstari wa 4, tafsiri ya King James Version, UM wataja njia kubwa ya kupunguza ukiukaji mkubwa sana wa haki za kibinadamu—kukomesha vita. Kwani, vita ni ‘kinyume cha haki za kibinadamu,’ kama kielezavyo kichapo kimoja cha UM.
Programu ya elimu ya Mashahidi wa Yehova yaenda hatua zaidi ya wazo la kuandika maneno ya Isaya kwenye ukuta wa mawe. ‘Inaandika’ maneno ya Isaya katika mioyo ya wanadamu. (Linganisha Waebrania 8:10.) Jinsi gani? Programu hiyo huondoa vizuizi vya kijamii na kikabila na kuondoa utukuzo wa kitaifa kwa kufundisha maoni ya Biblia kuhusu jamii: Kuna jamii moja tu—jamii ya kibinadamu. (Matendo 17:26) Wale walioandikishwa katika programu hiyo wanasitawisha tamaa ya ‘kuwa waigaji wa Mungu,’ ambaye Biblia husema hivi kumhusu: “[Yeye] si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.”—Waefeso 5:1; Matendo 10:34, 35.
Likiwa tokeo la elimu hii inayotegemea Biblia, mamilioni ya watu leo ‘hawajifunzi vita tena kamwe.’ Badiliko la akili na moyo limetukia. Na badiliko hilo hudumu. (Ona sanduku “Elimu kwa Ajili ya Amani,” kwenye ukurasa wa 14.) Kwa sasa, zaidi ya watu 1,000 kila siku kwa wastani hukamilisha mitaala ya msingi ya kujifunza inayofanywa na Mashahidi wa Yehova na kujiunga na kundi hili la amani la ulimwenguni pote.
Badiliko hili la akili ni thabiti kadiri gani na uamuzi unaofuatia wa kuheshimu haki za kibinadamu kwa kutoshiriki katika vita? Ni lenye nguvu sana. Kwa kielelezo: Kina cha Mashahidi cha kustahi haki za kibinadamu kilijaribiwa vikali wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, hasa katika Ujerumani ya Nazi. Mwanahistoria Brian Dunn alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova hawakupatana na itikadi ya Wanazi. Kipingamizi kikubwa zaidi kwa Wanazi kilikuwa msimamo wao wa kutokuwamo katika mambo ya kisiasa. Hili lilimaanisha kwamba hakuna mwamini ambaye angebeba silaha.” (The Churches’ Response to the Holocaust) Katika A History of Christianity, Paul Johnson alisema: “Wengi walihukumiwa kifo kwa kukataa kujiunga na utumishi wa kijeshi . . . , au waliishia Dachau au makao ya wenye kurukwa akili.” Ijapokuwa hivyo, walisimama imara. Mwanasoshiolojia Anna Pawełczyńska aliwafafanua Mashahidi hao kuwa “kikundi kidogo sana chenye nguvu za [adili] za daima katika taifa lililotishwa.”
Ebu wazia tu kungekuwa na upungufu mkubwa kama nini wa ukiukaji wa haki za kibinadamu ulimwenguni pote ikiwa watu wote wangechukua msimamo huo leo na ‘kutojifunza vita tena kamwe’!
Serikali ya Ulimwengu—‘Je, Ni Ndoto Tu’?
‘Ni vigumu kubadili akili, lakini kuunda serikali ya ulimwengu ni ndoto tu,’ ndivyo alivyosema mfanyakazi mmoja wa UM. Na kwa kweli, uhakika wa kwamba mataifa hayajawa tayari kusalimisha enzi zao kwa UM, au kwa shirika lolote, wakazia mkataa huu. Hata hivyo, wale wanaopuuza wazo la serikali ya ulimwengu, asema Profesa Berkouwer, “wana wajibu wa kuonyesha njia nyinginezo za kutatua matatizo ya ulimwengu. Hata hivyo, utatuzi-badala haupatikani.” Hakuna utatuzi wa kibinadamu. Lakini kuna utatuzi unaozidi nguvu za kibinadamu. Ni gani huo?
Kama vile Biblia ionyeshavyo kwamba Muumba ndiye chanzo cha mambo yaliyo msingi wa haki za kibinadamu, pia inatujulisha kwamba ndiye chanzo cha serikali ya ulimwengu ambayo inazitokeza. Serikali hii ya kimbingu haionekani lakini ni halisi. Kwa kweli, mamilioni ya watu, labda pasipo kujua, wanasali kwa serikali hii ya ulimwengu wanaposema ile inayoitwa kwa kawaida Sala ya Bwana: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:10) Kiongozi aliyechaguliwa na Mungu wa serikali hiyo ya Ufalme ni Mkuu wa Amani, Yesu Kristo.—Isaya 9:6.
Serikali hii ya ulimwengu itafaulu katika kutokeza utamaduni wa kweli wa tufeni pote wenye haki za kibinadamu zitakazodumu kwa kuondoa vita milele. Biblia inatabiri: “[Muumba] avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.”—Zaburi 46:9.
Jambo hili litatukia haraka kadiri gani tufeni pote? Programu ya kujifunza Biblia inayoandaliwa na Mashahidi wa Yehova inatia ndani jibu lenye kuridhisha kwa swali hili. Twakutia moyo ufahamu programu hii.a Ikiwa unahangaikia haki za kibinadamu, hutatamaushwa.
[Maelezo ya Chini]
a Ukipenda kupokea habari zaidi kuhusu programu hii ya elimu ya Biblia, wasiliana na wachapishaji wa gazeti hili au Mashahidi wa Yehova katika jumuiya yenu. Programu hii inatolewa bila malipo.
[Sanduku katika ukurasa wa 13]
Chanzo cha Haki za Kibinadamu
Kifungu cha 1 cha Azimio kwa Wote la Haki za Kibinadamu chasema kwamba “wanadamu wote wanazaliwa wakiwa huru na sawa katika hadhi na haki.” Hivyo, haki za kibinadamu zinafafanuliwa kuwa haki ya uzaliwa ambayo hupitishwa kutoka kwa wazazi hadi kwa watoto, kama vile tu mto hupeleka maji kwa watu wanaoishi kandokando ya kingo zake. Ni wapi ulipoanzia mto huu wa haki za kibinadamu?
Kulingana na Azimio kwa Wote, wanadamu wana haki kwa sababu “wamepewa uwezo wa kusababu na dhamiri.” Kichapo kimoja cha UM chaeleza hivi: “Kwa sababu mwanadamu ni kiumbe kiwezacho kusababu na kufuatia maadili, yeye ni tofauti na viumbe vingine vilivyoko duniani na kwa hiyo anapaswa kuwa na haki na uhuru fulani ambao viumbe vingine haviwezi kufurahia.” (Italiki ni zetu.) Hivyo, kuwa na uwezo wa kusababu na kuwa na dhamiri kunasemekana kuwa msingi wa kupata haki za kibinadamu. Mambo yakiwa namna hiyo, chanzo cha uwezo wa kusababu na dhamiri ya mwanadamu ndicho chanzo pia cha haki zake za kibinadamu.
Kwa wapiganiaji wa haki za kibinadamu wanaoamini nadharia ya mageuzi, taarifa ya kwamba haki za kibinadamu zinahusiana na uwezo wa kusababu na dhamiri hutokeza ugumu. Kitabu chenye kuunga mkono mageuzi Life Ascending chakiri: “Tunapojiuliza kwa nini utaratibu wa [mageuzi] . . . ungeweza kutokeza sifa kama vile kupenda uzuri na kweli, huruma, uhuru, na zaidi ya yote, kina cha mtazamo wa kibinadamu, tunatatanika.” Na kwa kufaa. Kwa vyovyote, kusisitiza kwamba uwezo wa mwanadamu wa kusababu na wa dhamiri unatokana na wazazi wa kale walio duni wasioweza kusababu na wasio na dhamiri ni sawa na kusema kwamba mto huchipuka kutoka kwenye kisima kisichokuwa na maji.
Kwa kuwa uwezo wa mwanadamu wa kusababu na wa dhamiri hauwezi kutoka kwa chanzo kilicho duni kuliko wanadamu, lazima uwezo huu utokane na chanzo kinachozidi uwezo wa kibinadamu. Ni wanadamu tu walio na sifa zinazohusiana na haki za kibinadamu—kusababu na dhamiri—kwa sababu tofauti na wanyama, wanadamu waliumbwa kwa “mfano” wa Mungu, yaeleza Biblia. (Mwanzo 1:27) Kwa hiyo, kama kisemavyo kitabu Human Rights—Essays on Justification and Applications, jibu halali kwa swali kwa nini watu wana haki za kiadili ni kwamba “wana thamani ya kiasili au adhama au wao ni . . . watoto wa Mungu.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]
Elimu kwa Ajili ya Amani
Miaka kadhaa iliyopita, vita ilipokuwa ikigawanya Wabalkani, Branko alikuwa anatumika akiwa mlinzi mwenye silaha katika kliniki moja iliyokuwa sehemu ya Kroatia katika Bosnia.b Daktari fulani huko alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, na usiku mmoja alimweleza Branko alichokuwa amejifunza kutokana na funzo hili. Kile alichosikia Branko kilimfanya aache silaha zake. Wakati fulani baadaye, baada ya kuhamia nchi fulani ya Ulaya, Branko alihudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova, na hapo akakutana na Slobodan.
Slobodan alitoka Bosnia pia. Alikuwa ameshiriki katika vita hiyohiyo kama vile Branko—lakini katika upande wa adui. Slobodan alikuwa amepigania Waserbia dhidi ya Wakroatia. Wakati watu hawa wawili walipokutana, tayari Slobodan alikuwa Shahidi wa Yehova, na alijitolea kujifunza Biblia pamoja na Branko, adui wake wa zamani. Funzo lilipoendelea, upendo wa Branko kwa Muumba, Yehova, ulikua. Baada ya muda mfupi akaamua kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.c
Slobodan mwenyewe alikuwa Shahidi pia kwa msaada wa adui wake wa zamani. Jinsi gani? Naam, baada ya kuondoka kwenye eneo la vita katika Bosnia, Slobodan alitembelewa na Mujo, ambaye pia alitoka Bosnia lakini aliyelelewa katika dini iliyokuwa tofauti sana na ya Slobodan. Ikawa kwamba Mujo alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ingawa walikuwa maadui, Slobodan alikubali pendekezo la Mujo la kujifunza Biblia pamoja naye, na baadaye akachukua hatua ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Ni nini kilichosababisha wanaume hawa washinde chuki kali ya kikabila na kubadilika kutoka kuwa maadui hadi kuwa marafiki? Kupitia funzo lao la Biblia, walikuza upendo kwa Yehova. Baada ya hilo, walikuwa tayari ‘kufundishwa na Mungu kupendana.’ (1 Wathesalonike 4:9) Kama vile Profesa Wojciech Modzelewski alivyosema kuhusu Mashahidi wa Yehova kwa ujumla, “sababu ya msingi kwa msimamo wao wenye amani ni wazo la kufuata kwa sasa kanuni zilizofunuliwa katika Biblia.”
[Maelezo ya Chini]
b Majina yote yaliyotajwa katika sanduku hili yamebadilishwa.
c Baadaye, Branko alipendezwa kujua kwamba daktari aliyezungumza naye mara ya kwanza alikuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova vilevile.
[Picha katika ukurasa wa 11]
Badiliko la akili na serikali—je, litapata kutokea?
[Hisani]
U.S. National Archives photo
[Picha katika ukurasa wa 12, 13]
Elimu inayotegemea Biblia inatokeza badiliko zuri la akili