Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 12/8 kur. 22-23
  • Je, Msiba wa Anga Utaangamiza Ulimwengu Wetu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Msiba wa Anga Utaangamiza Ulimwengu Wetu?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ulimwengu Unaodhibitiwa na Mungu
  • Dunia Yetu—Iliumbwa kwa Kusudi Fulani
  • Ni Nini Kitakachoipata Dunia-Sayari?
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Mungu Anaahidi Kwamba Dunia Yetu Itaokoka
    Amkeni!—2023
  • Sayari Ndogo, Nyotamkia, na Dunia—Je, Ziko Katika Mwendo wa Kugongana?
    Amkeni!—1999
  • Zawadi ya Milele Kutoka kwa Muumba
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 12/8 kur. 22-23

Maoni ya Biblia

Je, Msiba wa Anga Utaangamiza Ulimwengu Wetu?

MACHI 12, 1998, vichwa vya magazeti ya habari, televisheni, na mifumo ya kompyuta ya Internet tufeni pote ilieneza habari hizi zenye kuogofya: “Sayari ndogo ya upana wa kilometa 1.5 inaelekea kugongana na Dunia.” Wanasayansi na watu wa kawaida walitenda kwa uharaka kukagua hatari yenyewe. Upesi waastronomia wakaamua kwamba mgongano huo haungetokea.

Hata hivyo, katikati ya ghasia hiyo, habari mpya ilitokea. “Jambo lenye kutokeza zaidi kuhusu onyo hilo lisilo la kweli ni kwamba, huenda ikawa hata liwe lilikuwa lenye kuogopesha jinsi gani, watu wengi hawakuliona kuwa lenye kushangaza sana,” chasema kichapo U.S.News & World Report. “Wazo la kwamba sisi tulio Duniani twapaswa kuangalia vyombo kama hivyo—na kupanga kufanya jambo fulani kuvihusu—lingekuwa jambo la ajabu mwongo mmoja au zaidi, lakini sasa wanasayansi na hata baadhi ya wanasiasa wanafikiri kwamba ingawa ni dogo, ni la kweli.”

Waastronomia wengine huamini kwamba vyombo 2,000 hivi vya kimbingu vikubwa viwezavyo kusababisha msiba mkubwa wa tufe lote vinaruka kwa mbio sana kwenye njia ambazo hugawa mzingo wa dunia au kuja karibu nao. Hata kama kimojawapo kilicho kidogo kwa kiasi kingegonga dunia, watafiti wanasema kwamba, mlipuko ungetoshana na nguvu za silaha nyingi za nyuklia zinazolipuka wakati uleule. Matokeo ya mgongano huo yangekuwa yenye kuleta msiba mkubwa kwenye tufe letu na wakazi wake, binadamu na wanyama vilevile.

Wazo ambalo kwa kawaida halitiwi ndani ya matabiri na makisio hayo yenye kusononesha ni lile la Muumba wa ulimwengu, Yehova Mungu. (Zaburi 8:3; Mithali 8:27) Katika Biblia yeye amejulisha waziwazi mapenzi yake na kusudi lake kwa dunia na jamii ya kibinadamu. Je, ataruhusu msiba wa anga uangamize ulimwengu wetu?

Ulimwengu Unaodhibitiwa na Mungu

Kwa kuwa Yehova ndiye Muumba mweza-yote wa ulimwengu, ni jambo la kiakili kukata kauli kwamba ana uwezo wa kudhihirisha udhibiti kamili juu ya nguvu zinazoongoza magimba ya kimbingu. Mfalme Solomoni mwenye hekima alisema kwamba Yehova ‘kwa akili zake amezifanya mbingu imara.’ (Mithali 3:19) Nabii Yeremia alitangaza kwamba Mungu “kwa ufahamu wake amezitandika mbingu.”—Yeremia 51:15.

Yehova ameweka utaratibu wa sheria na nguvu zinazoongoza miendo ya magimba ya kimbingu, kutia ndani nyota, sayari, nyotamkia, na sayari ndogo. (Isaya 40:26) Hata hivyo, yaonekana kwamba yeye huruhusu nyota na sayari ziende kupitia mizunguko ya asili ya uzaliwa, uhai, na kifo cha kisitiari bila kuingilia kwake kati sikuzote. Hiyo hutia ndani migongano mingine mibaya sana ya magimba ya kimbingu. Kielelezo kimoja cha hivi majuzi ni ule mgongano wa Julai 1994 ambao vipande vya nyotamkia iitwayo Shoemaker-Levy 9 viliigonga sayari Sumbula.

Kuna uthibitisho wa kijiolojia wa miamba mikubwa kutoka anga la nje ikigonga dunia katika historia ya kabla ya binadamu. Lakini je, tukio kama hilo litatokea katika sayari yetu iliyo na watu? Mathalani, ni nini kiwezacho kutokea ikiwa sayari ndogo yenye upana wa kilometa 1.5 ingegongana na dunia? Mwastronomia Jack Hills atabiri kwamba mgongano wake ungetokeza nishati inayozidi mara milioni nyingi ya lile bomu lililoharibu kabisa Hiroshima. Kama ingepiga bahari, mawimbi yenye kujaa na kupwa yangefurika sehemu za pwani. “Mahali ambapo kulisimama majiji,” Hills asema, “kungekuwa tu na upwa tope.” Mpangilio wa matukio ulio mbaya zaidi watabiri uharibifu kabisa wa jamii ya kibinadamu. Utabiri wa siku hii ya maangamizi wafaanaje na mapenzi ya Muumba wetu kwa dunia hii? Biblia huonyesha kwamba sayari hii ni ya kipekee katika kusudi la Yehova.

Dunia Yetu—Iliumbwa kwa Kusudi Fulani

Kuhusu sayari yetu, mtunga-zaburi asema hivi: “Mbingu ni mbingu za BWANA, bali nchi [“dunia,” NW] amewapa wanadamu.” (Zaburi 115:16) Isaya amfafanua Yehova kuwa “aliyeiumba dunia . . . aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Dunia ni urithi ambao Yehova amewapa wanadamu. Na kwa kuwa Muumba wetu alikusudia binadamu wenye kumhofu Mungu wawe na wakati ujao wa milele, dunia itabaki milele iwe makao yao yenye kudumu. Zaburi 104:5 hutuhakikishia hivi: ‘[Yehova] aliiweka nchi [“dunia,” NW] juu ya misingi yake, isitikisike milele.’

Ni kweli, Mungu ameruhusu misiba kadhaa mikubwa kwenye sayari yetu, ikitokeza kifo kwa wanadamu wengi sana. Baadhi ya misiba hiyo mikubwa—kama vile vita, njaa kali, na magonjwa—yote au sehemu yake imesababishwa na pupa, upumbavu, na ukatili wa binadamu. (Mhubiri 8:9) Mingine—kama vile matetemeko ya dunia, milipuko ya volkeno, mafuriko, na dhoruba—imesababishwa na matukio ya kiasili yasiyoeleweka kikamili na wanadamu. Kinyume na kusudi la awali la Mungu, wanadamu si wakamilifu tena; ni wenye dhambi. Likiwa tokeo, kuhusu mtu mmoja-mmoja, hatuwezi wakati huu kutegemea ulinzi wa kimungu kutoka katika ile iitwayo misiba ya asili.

Hata hivyo, Yehova hakuruhusu kwa vyovyote kuwapo kwa mwanadamu duniani kutishwe vibaya. Tangu kuumbwa kwa mwanadamu, historia iliyothibitishwa haina kisa chochote cha msiba wa asili ambao ulitisha kuwapo kwa wanadamu.a

Kuokoka kwa Jamii ya Kibinadamu Kumehakikishwa

Kuanzia mwanzo wa historia ya binadamu, kusudi la Muumba wetu limekuwa kwamba mwanadamu ‘aijaze dunia na kuitiisha.’ (Mwanzo 1:28; 9:1) Yeye ameahidi kwamba “wenye haki watairithi nchi [“dunia,” NW], nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:9, 11, 22, 29) Kuhusu ahadi zake, Yehova ahakikisha hivi: “Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote.”—Isaya 46:10; 55:11; Zaburi 135:6.

Biblia haisemi kwamba haiwezekani kuwepo msiba wa kiwango kidogo wa dunia unaosababishwa na matukio ya anga. Hata hivyo, twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hataruhusu msiba wowote wa anga uzuie kusudi lake kwa dunia na wanadamu. Kwa kutegemea ahadi za Biblia, twaweza kuwa na uhakika kwamba sayari yetu itadumu ikiwa imekaliwa na watu milele—naam, itakuwa makao ya jamii ya binadamu hata wakati usiojulikana!—Mhubiri 1:4; 2 Petro 3:13.

[Maelezo ya Chini]

a Furiko la siku ya Noa lilikuwa njia ya Mungu ya utekelezaji wa hukumu, lakini Yehova alihakikisha kwamba binadamu wengine na wanyama waliokoka.—Mwanzo 6:17-21.yy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki