Vijana Huuliza . . .
Naweza Kudumishaje Uchumba wa Mbali?
“Nilikuwa tu nimetoka kusindikiza kwenye hoteli kikundi kimoja cha wajumbe waliokuwa wakihudhuria mkusanyiko mmoja wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova. Nilikuwa karibu kwenda nyumbani, lakini kikundi kingine kikaingia wakati huo. Basi nikasimama ili niongee nao, nikakutana na Odette. Ikatukia kwamba tukakutana tena baadaye juma hilo. Tukaamua kuwasiliana kwa barua, na baada ya miaka kadhaa ya kufahamiana kwa barua, tulianza kuchumbiana.”—Tony.
ULIMWENGU umekuwa mdogo. Katika miongo ya majuzi usitawishaji wa gharama za chini za usafiri wa ndege, mfumo wa simu unaounganisha dunia, huduma za upesi za kupeleka barua, na Internet zimetokeza uwezekano mpya wa mambo ya mahaba. Na kwa njia nyingi wazo la kufanya uchumba na mtu aliye mamia au hata maelfu ya kilometa mbali laweza kuonekana kuwa la kusisimua—hasa kama matazamio ya ndoa hayaonekani kwenu.
Kwa wenzi fulani, uchumba wa mbali umethibitika kuwa baraka. “Tumekuwa na ndoa yenye furaha kwa miaka 16,” asema Tony. Huenda wengine hata wakabisha wakisema kwamba uchumba wa mbali una manufaa za kuruhusu wenzi wajuane bila kupotoshwa na uvutio wa kimwili. Ingawa hivyo, hata manufaa zake ziweje, mahaba ya mbali hutokeza magumu ya pekee.
Kupata Kujuana
Inafaa zaidi kumjua kadiri uwezavyo mtu unayefikiria kufunga ndoa naye. Hata hivyo, kama asemavyo mume mmoja aitwaye Frank kuhusu ayajuayo binafsi, “si rahisi kumjua yule mwingine alivyo kabisa, ‘mtu wa siri wa moyoni.’” (1 Petro 3:4) Mkristo mwingine aitwaye Doug aliyefanya uchumba wa mbali akiri hivi: “Nikikumbuka yaliyopita, natambua kwamba hatukuwa tumejuana vizuri.”
Je, kweli yawezekana kumjua mtu mwingine anayeishi umbali wa mamia au maelfu ya kilometa? Naam, lakini jambo hilo laweza kuhitaji jitihada nyingi. “Hatukuwa na fedha za kupigiana simu, kwa hiyo tuliandikiana barua mara moja kwa juma,” asema Doug. Hata hivyo, Joanne na Frank, waliona kwamba haitoshi tu kuandika barua. “Mwanzoni tuliandika barua na kujaribu simu,” asema Joanne. “Kisha Frank akanitumia tepu-rekoda ndogo. Tulikuwa tukirekodi tepu mpya kila juma.”
Ufuatiaji wa Haki, Ndio Njia Pekee
Hata kama unatumia njia ipi ya mawasiliano, ni jambo la maana kufuatia haki. “Ukidanganya, baadaye itajulikana na utaharibu uhusiano,” ndivyo anavyoona mke mmoja Mkristo aitwaye Ester. “Fuatieni haki mtu na mwenzake. Uwe mfuatiaji-haki kujihusu. Kama hukubali jambo fulani, usilipuuze. Lizungumzieni.” Mtume Paulo atoa shauri zuri: “Semeni kweli kila mmoja wenu pamoja na jirani yake.”—Waefeso 4:25; linganisha Waebrania 13:18.
Ni masuala gani ambayo utahakikisha mnayazungumzia? Wenzi wote wanaochumbiana wanahitaji kuzungumzia mambo kama vile miradi, watoto, mambo ya kifedha, na afya. Hata hivyo, kuna mambo ambayo huenda yakahitaji kukaziwa uangalifu mahususi. Kwa mfano, itambidi mmoja wenu, au nyote wawili, kuhama ikiwa mtafunga ndoa. Je, uko tayari na waweza kufanya hivyo, kiakili na kihisia-moyo? Wajuaje? Je, umepata kuhama awali au kuwa mbali na familia yako kwa vipindi virefu? Yule ambaye angekuwa mume wa Joanne alitaka wote wawili watumikie katika makao makuu ya Watch Tower Society, wachapishaji wa gazeti hili. “Aliniuliza kama naweza kuishi katika chumba kidogo, na fedha chache,” akumbuka Joanne. “Ilitubidi tuzungumzie jambo hilo kwa uzito.”
Ikiwa uchumba wahusu mtu wa nchi nyingine, je, uko tayari kufuata utamaduni mwingine? “Je, kila mmoja wenu tayari anafurahia utamaduni wa mwenzake siku kwa siku?” auliza Frank. “Zungumzieni mambo hayo ya maana mnapoanza kuchumbiana. Mnapogundua hayo mapema, ni afadhali—kabla hamjajiingiza sana kihisia-moyo na kifedha.” Naam, kuishi kila siku katika utamaduni mwingine ni tofauti na kuwa mtalii kwa siku chache. Je, utahitaji kujifunza lugha nyingine? Je, utaweza kufaana na mabadiliko makubwa ya hali za maisha? Kwa upande mwingine, je, huenda ikawa kwamba unavutiwa na utamaduni na labda huvutiwi na mtu huyo hasa? Yaelekea uvutio huo utaisha baada ya muda fulani. Lakini ndoa hufunga watu wawili pamoja daima.—Mathayo 19:6.
Tony aeleza: “Najua msichana mmoja aliyeolewa na Mkaribea fulani. Lakini aliona maisha ya kisiwani kuwa magumu. Sikuzote kulikuwa na joto, akawa mgonjwa. Chakula kilikuwa tofauti, na alitamani familia yao sana. Kwa hiyo, walijaribu kuishi katika nchi alikozaliwa. Lakini mume wake alihisi kwamba mtindo wa maisha huko ulikuwa wa kufuatia vitu vya kimwili sana, naye alitamani ule ukaribu aliokuwa akifurahia miongoni mwa familia yao na jirani zake. Sasa wametengana; mume anaishi katika nchi alikozaliwa, na mke katika nchi yao. Watoto wao wawili wanakosa upendo na uangalifu wa wazazi wote wawili.”
Kufunga ndoa na mtu anayeishi mbali sana, labda utamaduni mwingine, hutokeza magumu mengine. Je, umejiandaa kwa ajili ya gharama za ziada za kusafiri na za kuwasiliana? Lydia akumbuka hivi: “Phil alikuwa akifanya mzaha kwamba ilitubidi tufunge ndoa upesi kwa sababu bili zake za simu zilikuwa kubwa sana, lakini sasa twalazimika kulipia simu ambazo sisi humpigia mama yangu!” Vipi watoto wakianza kutokea? Wengine hukua bila kuwajua jamaa zao, wakishindwa hata kuongea nao kwenye simu kwa sababu ya tofauti za lugha! Hiyo si kusema kwamba matatizo hayo hayawezi kushindwa. Lakini mtu apaswa kuhesabu gharama ya kuingia katika ndoa ya aina hiyo.—Linganisha Luka 14:28.
Kwa Kweli Yeye Yukoje?
Waweza kujuaje kama kwa kweli rafiki yako ni mnyoofu na mwenye kusema wazi? “Kila mti mwema hutokeza matunda bora,” lasema andiko la Mathayo 7:17. Ana matendo ya aina gani? Je, anatenda kupatana na maneno yake? Je, maisha yake ya wakati uliopita yanapatana na miradi yake ya wakati ujao? “Mambo ya kwanza ambayo tulipata kujua kati yetu ni miradi ya kiroho,” aeleza Ester. “Yeye alikuwa ametumikia akiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote kwa miaka minane, na jambo hilo lilinipa uhakika wa kwamba alikuwa akisema kweli juu ya kuendelea.”
Lakini tuseme mchumba wako anaonekana kuwa mwenye kukwepa-kwepa. Usipuuze jambo hilo na kutumaini tu kwamba matokeo yatakuwa mazuri. Chunguza kwa undani! Uliza KWA NINI? Mithali moja yasema hivi: “Mashauri ya moyoni ni kama kilindi; lakini mtu mwenye ufahamu atayateka.” (Mithali 20:5) “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo,” yaonya mithali nyingine.—Mithali 14:15.
Uso kwa Uso
Bado, huwezi kujifunza mengi sana kuhusu mtu kupitia barua au simu. Kwa kupendeza, mtume Yohana aliandikia ndugu zake Wakristo barua kadhaa. Ingawa barua hizi ziliimarisha zaidi kifungo cha shauku kati yao, Yohana alisema: “Ijapokuwa nina mambo mengi ya kuwaandikia nyinyi, sitaki kufanya hivyo kwa karatasi na wino, lakini ninatumaini kuja kwenu na kusema pamoja nanyi uso kwa uso.” (2 Yohana 12) Vivyo hivyo, hakuna kitu kinachoshinda kutumia wakati pamoja na mtu binafsi. Huenda hata ikafaa mmoja wenu kuhama kwa muda ili mweze kukaribiana. Kufanya hivyo pia kutaruhusu yule mwenye kuhama ahisi halihewa na hali za kuishi za kule ambako huenda kukawa makao yake mapya.
Mwaweza kutumiaje vizuri wakati wenu pamoja? Fanyeni mambo yanayoonyesha sifa za kila mmoja wenu. Jifunzeni Neno la Mungu pamoja. Chunguzeni jinsi kila mmoja wenu anavyoshiriki kwenye mikutano ya kutaniko na katika huduma. Fanyeni kazi za nyumbani za kawaida pamoja, kama vile usafi na ununuzi. Kuona jinsi mwenzako anavyojiendesha anapokuwa na mkazo akiwa na shughuli nyingi kwaweza kukujulisha mengi.a
Pia mwapaswa kutumia wakati pamoja na wale wanaotarajiwa kuwa wakwe. Tafuta kujenga uhusiano mzuri pamoja nao. Kwani, nyinyi wawili mkifunga ndoa, watakuwa familia yenu. Je, wawajua? Je, mwapatana? Joanne ashauri hivi: “Ikiwezekana, ni vizuri familia zote mbili zikutane.” Tony aendelea kusema hivi: “Jinsi rafiki yako aitendeavyo familia yao mwenyewe ndivyo atakavyokutendea wewe.”
Iwe wachumbia uso kwa uso au kwa njia ya simu na barua, epuka kuharakisha kufanya maamuzi yako. (Mithali 21:5) Ikionekana kwamba haitawezekana mfunge ndoa, basi litakuwa jambo la hekima kuzungumzia kuvunja uchumba. (Mithali 22:3) Kwa upande mwingine, huenda ikawa tu ni wakati mwingi zaidi unaohitajiwa kwa ajili ya mawasiliano manyoofu na ya kweli.
Yaweza kuwa vigumu kufanya uchumba wa mbali, lakini waweza kuthawabisha pia. Kwa vyovyote vile, ni jambo la kufikiriwa kwa uzito. Usiharakishe mambo. Mpate kujuana. Kisha, mkiamua kufunga ndoa, uchumba wenu utakuwa wakati wenye thamani, bali si wa kusikitikia.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi juu ya uchumba, ona kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, ukurasa wa 255-260, kilichochapishwa na Watchtower Bible na Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Hakikisha mwazungumzia mambo kama vile miradi, watoto, na mambo ya kifedha mnapoanza uchumba