Sura ya 19
Matembezi ya Wavulana Pamoja na Wasichana na Uchumba
1-4. (a) Ni tangu wakati gani katika siku zetu matembezi ya wavulana pamoja na wasichana yamekuwa mazoea, ya watu wengi? (b) Huenda ndoa zikapangwa namna gani mahali ambako si desturi wavulana kutembea pamoja na wasichana? (c) Mwishowe, ni nini linaloonyesha uzuri au ubaya wa desturi hizo?
KILA mtu wa kawaida ataka afurahie sana maisha. Biblia yaonyesha kwamba hili ni jambo linalofaa, ikitaja furaha kuwa mojawapo la ‘matunda’ ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Vijana wengi, sana sana katika nchi za Wazungu, wanatazamia matembezi ya wavulana pamoja na wasichana kama njia kuu ya kupata furaha. Mara, nyingi wavulana wanapanga kushinda na msichana bila mtu mwingine wa kuwalinda, na wasichana ni vivyo hivyo. Ni nini linaloweza kusemwa juu ya jambo hilo?
2 Labda utadhani si vibaya wavulana kutembea pamoja na wasichana na wasichana kutembea pamoja na wavulana kwa kuwa desturi hiyo inafuatwa sana mahali pengi. Hata hivyo sivyo imekuwa sikuzote, kama kitabu The Family in Social Context kinavyoeleza: “Kama tunavyojua, labda matembezi ya wavulana pamoja na wasichana yalitokea baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu.” Walakini, katika nchi nyingi matembezi ya wavulana pamoja na wasichana hayajawa desturi hata kidogo. Kwa kweli huenda wanaotazamiwa kuwa bwana-arusi na bibi-arusi wasionane mpaka wakati wa arusi yao. Mipango ya ndoa yao inafanywa na wazazi wao, au labda na “mshenga” au rafiki ya mtu anayefunga ndoa.
3 Bila shaka, ikiwa unaishi katika nchi ambamo matembezi ya wavulana pamoja na wasichana na uchumba yanakubaliwa kuwa kawaida, huenda kutokuwako kwa desturi hizo katika nchi fulani likaonekana kuwa jambo gumu kufahamu. Lakini watu wanaoishi katika nchi hizo huenda nao wakaona vivyo hivyo desturi za nchi yako kuwa ngumu. Huenda wakaona matembezi ya wavulana pamoja na wasichana na uchumba kuwa jambo la upumbavu, au hata jambo linalochukiza sana. Msichana mmoja Mhindi alimweleza Mzungu ambaye ni mshauri wa ndoa hivi: “Tungewezaje kujua tabia ya mvulana tuliyekutana tukafanya urafiki naye? Sisi ni wachanga na hatuna ujuzi. Wazazi wetu ni watu wazima na wenye hekima kuliko sisi, nao hawadanganywi vyepesi kama sisi. . . . Ni jambo la maana sana mwanamume anayenioa awe anayefaa. Kama ingenipasa nijitafutie mwenyewe, ningeweza kukosea vyepesi sana.”
4 Basi, inafaa kupanua mawazo yako mahali pa kuwa na maoni madogo na kudhani kwamba desturi peke yake zinazofaa ni zile za watu walio katika nchi yako mwenyewe. Ingawaje, mwishowe ni matokeo ndiyo yanayoonyesha uzuri na ubaya wa desturi fulani. Tunasoma katika Biblia katika Mhubiri 7:8 hivi: “Heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake.” Na inatupasa tukubali kwamba katika nchi nyingi ambako ni desturi wavulana kutembea pamoja na wasichana na kufanya uchumba, kadiri kubwa ya ndoa hazifanikiwi bali matokeo yake yanakuwa talaka.
BASI, NAMNA GANI MATEMBEZI YA WAVULANA PAMOJA NA WASICHANA?
5-8. (a) Yanayosemwa katika Mhubiri 11:9, 10 yanatusaidiaje tuwe na maoni makubwa juu ya mwenendo wetu? (b) Ni kwa sababu gani vijana wengi wanataka matembezi ya wavulana pamoja na wasichana?
5 Ikiwa wewe unapenda kuamini mambo baada ya kupewa sababu, hutataka ufikirie matokeo ya muda tu ya matembezi ya wavulana pamoja na wasichana bali vilevile matokeo ya muda mrefu zaidi. Muumba wetu anatusaidia tuyatazame mambo kwa maoni hayo ya muda mrefu. Yeye anataka tupate mambo yatakayotuletea furaha ya kweli na inayoendelea. Kwa hiyo anatusihi katika neno lake hivi: “Wewe, kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako, ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako; lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote Mungu atakuleta hukumuni. Kwa hiyo ondoa majonzi moyoni mwako, nawe uuondoe ubaya mwilini mwako; kwa maana ujana ni ubatili, na utu uzima pia.” (Mhubiri 11:9, 10) Maana ya hayo ni nini?
6 Maana yake ni kwamba Muumba ataka ufurahie ujana wako, lakini vilevile, usiufuate mwenendo utakaoharibu maisha yako mwishowe. Kwa huzuni inatukia hivyo mara nyingi, kama mwandikaji wa nyakati hizi alivyosema: “Sehemu kubwa zaidi ya wanadamu wanatumia miaka yao ya kwanza kuifanya miaka yao ya mwisho kuwa yenye kusikitisha.” Wewe hutaki hilo likupate, sivyo? Wala Mungu hataki likupate. Hata hivyo Biblia inaonyesha vilevile hapo katika Mhubiri kwamba Mungu atawahukumu vijana kwa kadiri ya matendo yao. Ujana wao hautawaepusha wasipate matokeo ya mwendo wanaochagua.
7 Yote hayo yanapasa sana matembezi ya wavulana pamoja na wasichana. Namna gani? Basi, jiulize mwenyewe: “Kwa nini nataka kutembea pamoja na wasichana au na wavulana? Ninatafuta nini ambalo nisingeweza kufurahia, kwa mfano, kama sehemu ya kikundi? Ni kwa nini nataka kutembea na msichana au na mvulana?” Je! si kwa sababu tu ya kujiona ukivutwa sana na wasichana au na wavulana? Hii inaonwa hivyo kwa sababu kwa kawaida uvutano wa kimwili unamfanya mtu atamanike na kuwa mtu wa kutembea pamoja naye.
8 Vijana wengi wanaotembea na wasichana au na wavulana hawafikirii sana kuoa au kuolewa sasa, wala si kwamba wangetaka mtu yule wanayefanya matembezi pamoja naye awe mwenzi wa ndoa. Mahali pengi ambapo inaonwa kuwa desturi wavulana kutembea pamoja na wasichana inaonwa kuwa namna ya tafrija tu, njia ya kufurahia jioni au mwisho wa juma. Na kwa kuwa hawataki waonwe kuwa “tofauti,” watu wengine wanatembea pamoja na wasichana au na wavulana kwa sababu wengine wa rika zao wanafanya hivyo. Hata hivyo, hakuna shaka kwamba matembezi ya wavulana pamoja na wasichana yanaweza kuongoza kwenye “majonzi,” hata kwenye “ubaya.” Na tuangalie ni kwa sababu gani yanaweza.
MATOKEO YA KUGUSANA MIILI
9-11. (a) Wavulana na wasichana wanagusana miili namna gani wanapotembea pamoja? Kwa sababu gani kufanya hivyo kwaweza kuleta mazoea mabaya? (b) Ni kwa sababu gani huenda jambo hilo likamletea mtu asiyeoa au asiyeolewa wasiwasi? (c) Ikiwa kugusana miili kunaongoza kwenye uasherati, kunawezaje kutokeza ubaya wa namna nyingi?
9 Mara nyingi, matembezi ya wavulana pamoja na wasichana yanatia ndani kugusana kwa miili —kushikana mikono, kubusu, au hata kufanya zaidi ya hayo. Kwanza, huenda kugusa mkono wa mtu mwingine kukapendeza sana, kukimfanya mtu aone raha. Lakini kikipita kitambo kidogo huenda raha yake ikaisha. Huenda mara nyingine kufanya zaidi ya hilo kukapendeza, kama vile kubusu. Lakini vilevile, hapo ndipo huenda raha ya kufanya hivyo ikaisha. Kwa sababu gani iko hivyo?
10 Kwa sababu panapokuwa na nyege, inakuwa sehemu ya mfululizo wa matukio yanayokusudia kutokeza jambo fulani halisi. La kwanza katika mfululizo huo ni kule kugusa kwanza. La mwisho katika mfululizo huo ni kufanya ngono, ambayo Neno la Mungu linaonyesha kwamba ni ya watu waliofunga ndoa peke yao. Kila jambo linalofanywa kati ya hayo laweza kuelekeza kwenye jambo hilo la mwisho. Hivyo, basi, ikiwa wewe hujaoa au hujaolewa, je! ni hekima kuanza na jambo hilo la kwanza, au lo lote la mengine yanayoongoza mwishowe kwenye kufanya ngono? Inaelekea kufanya hivyo kutaleta “majonzi.” Kwa sababu gani? Kwa sababu mwili wako utajiweka tayari kwa jambo fulani usilopaswa kupokea sasa, yaani, ngono. Kuamsha nyege za kufanya ngono bila kuzitosheleza kwaweza kutokeza mapingamizi na wasiwasi.
11 Uasherati hautamaliza “majonzi” hayo. Mahali pake, unaweza kuongoza kwenye “ubaya.” Namna gani? Kwa njia nyingi. Unaweza kutokeza ugonjwa wa kisonono na kaswende. Msichana anaweza kuwa na mimba kisha mvulana na msichana huyo walazimike kuoana, jambo ambalo hawajawa tayari kufanya, likiharibu furaha yao ya wakati ujao. Au huenda kijana huyo wa kiume akakataa kumwoa msichana, naye itampasa kumlea mtoto peke yake pasipo mume. Au huenda msichana akashawishwa atoe mimba, jambo ambalo Biblia inaonyesha kuwa uuaji. Je! huu sio “ubaya”? Huenda ukakaza moyo kwamba matembezi ya wavulana pamoja na wasichana hayatakuletea matokeo hayo. Lakini wengi waliokuwa wemekaza mioyo kama wewe wasipatwe na mambo hayo, wamepatwa na masumbufu hayo mwishowe. Basi, ulizo linarudi juu ya kama uko tayari kufunga ndoa au sivyo.
MAENDELEO YAKO MWENYEWE
12, 13. Matembezi ya wavulana pamoja na wasichana yanaweza kuzuia maendeleo ya mtu namna gani? Basi, ni uhusiano (ushirika) wa namna gani unaoweza kufaa zaidi?
12 Hata ikiwa matembezi ya wavulana na wasichana hayaongozi moja kwa moja kwenye “ubaya,” yanaweza kuleta shida nyingine. Shida moja ni kwa vile yanavyoelekea upesi sana kukufanya upendezwe na mtu mmoja tu. Huu ndio wakati unapoweza kufaidika zaidi na ushirika wa watu wa namna mbalimbali ili upate maendeleo ya kukomaa kwako kwa moyoni. Ikiwa wewe ni kijana wa kiume anayekua, sababu gani usikaze fikira zako kwanza juu ya kuwa mwanamume kweli kweli kufanya urafiki na wanaume wengine wanaoheshimu yaliyo mema? Unaweza kujifunza kwao tabia na njia za kiume. Ikiwa wewe ni msichana anayekua, sababu gani usipendezwe kwanza na maendeleo ya kuwa mwanamke wa kweli, ukifaidika na ushirika wa wale walio wanawake kweli na wanaoweza kukusaidia usitawishe tabia na njia njema za wanawake? Kwa kweli matembezi ya wavulana pamoja na wasichana yanazuia na kupunguza maendeleo hayo.
13 Kabla matembezi ya wavulana na wasichana hayajawa desturi ya watu wengi, vijana walikuwa na mambo mengi ya kuwafurahisha. Wewe vilevile waweza kuwa nayo. Unaweza kuona furaha ya kweli katika kuongea, kujifunza, kusitawisha ujuzi fulani, kufanya kazi ndogondogo, kucheza michezo, kutembelea mahali fulani na kutazama vitu. Nawe waweza kuona furaha kubwa kwa kufanya mambo hayo pamoja na mwanamume mwenzako au pamoja na kikundi cha watu. Utaona mara nyingi kwamba kadiri unavyoshirikiana na watu mbalimbali—wengine wakiwa rika lako, wengine watu wazima, na wengine wachanga zaidi —ndivyo utakavyokuwa na furaha zaidi.
NI WAKATI GANI UNAOFAA ZAIDI KUOA AU KUOLEWA?
14, 15. (a) Unadhani ndoa za vijana wenye umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa zinafaa? (b) Wazazi wana daraka la kufanya nini wakati watoto wao wanapotaka kuoa au kuolewa?
14 Walakini, unakuja wakati ambao kwa kawaida kijana anataka kuoa au kuolewa. Ni wakati gani unaofaa zaidi kufanya hivyo—wakati ungali una umri kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa? Kwa kawaida sivyo, maana mambo yanayotokea yanaonyesha kwamba ndoa nyingi za vijana wenye umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa hazifanikiwi kama ndoa zile ambazo mtu mmoja au wote wawili wamefikia umri wa kukomaa zaidi. Kama mtu mmoja anayechunguza habari za usitawi wa jamii alivyoeleza: “Uchunguzi unaonyesha kwamba, kwa jumla, ndoa za vijana wenye umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa zinajaa talaka nyingi au huzuni zikilinganishwa na ndoa za umri ulio zaidi ya huo.”
15 Kwa upande mwingine, hakuna msingi wa Maandiko wa kukataza ndoa zote katikati ya vijana hao bila sababu inayofaa. Kwa kawaida, sheria za nchi zinawapa wazazi haki ya kutumia busara yao ya kukomaa kuamua wanayoona yatawafaa zaidi sana watoto wao na kuwaletea furaha iliyo kubwa zaidi na kuwapa faida. Huenda wakaamua kuwaruhusu ama kutowaruhusu wanao au binti zao walio chini ya ulinzi wao kuoa au kuolewa. Bila shaka, matatizo (magumu) mengi ya nyakati zetu na wingi wa ndoa zinazovunjika ni sababu ya kutosha kwao kuwa waangalifu. Na inatosha vilevile kuwafanya vijana wenye akili wawe waangalifu, mahali pa kufanya ndoa haraka haraka kisha kusikitika mwishowe. Ni jambo la upumbavu kuingia haraka haraka katika mlango kwa sababu tu uko wazi, hali hujui sawasawa kilichoko upande mwingine.
KUCHAGUA MTU WA KUOANA NAYE
16-19. (a) Mahali ambako mvulana na msichana wanaruhusiwa kuchumbiana, matumizi ya kanuni iliyo katika Wagalatia 5:13 yatakuwa yenye faida namna gani? (b) Mradi wa uchumba umepaswa uwe nini? Kwa hiyo wale wanaofanya uchumba huo wamepaswa wajiweke tayari kufanya nini? (c) Kwa sababu gani ni faida yako umjue mtu mkiwa pamoja na watu wengi, kuliko kuwa peke yenu?
16 Mahali pengine kijana wa kiume anaruhusiwa kuwa pamoja na msichana wakati anapokuwapo hata mmoja wa wazazi, au mtu mzima mwingine. Walakini, katika nchi za Wazungu huenda mara nyingi vijana hao wakawa pamoja bila mtu mzima wa kuwaangalia. Basi, katika nchi ambako uhuru mkubwa kama huo unaruhusiwa, ulizo ni hili, kijana aweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba uchumba utaongoza kwenye ndoa yenye furaha na yenye kufanikiwa kweli kweli?
17 Sikuzote uhuru unaleta daraka. Hivyo, ikiwa hilo ndilo tatizo (taabu) lako, itakufaa uikumbuke kanuni nzuri iliyoandikwa katika Biblia katika Wagalatia 5:13. Bila shaka hapo mtume Paulo alikuwa akisema habari ya uhuru wa kiroho ambao Ukristo uliletea wale walioukubali kwa moyo. Lakini kanuni hiyo inapasa uhuru wa aina yo yote, sana sana tukitaka ulete matokeo mema na kibali ya Mungu tunapoutumia. Mtume anaandika “Maana ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwill, bali tumikianeni kwa upendo.” Kumpenda Mungu na kupenda jirani yetu kweli kweli, kutia na mtu tunayechumbiana naye, kutatusaidia tuepuke kutumia uhuru wo wote tulio nao katika njia ya choyo na yenye kuumiza.
18 Kwa kufaa, uchumba umepaswa ufanywe kwa kusudi la ndoa. Kwa hiyo, uchumba usianze kabla mtu hajawa tayari kutwaa madaraka ya ndoa. Bila shaka, huwezi kujua pale mwanzoni kama wataka au hutaki kuoa au kuolewa na mtu. Basi ni jambo la busara kutokuwa na haraka ya kumfikiria mtu mmoja ye yote. Lakini hii siyo sababu ya kuendeleza uchumba kwa muda mrefu hata unakuwa wa kufanyiana mahaba (mapenzi) tu na kutiana nyege bila kusudi la kuoana.
19 Hata ikiwa ‘unapendezwa’ na mtu fulani, lingekuwa jambo la busara kujaribu kushirikiana kwa muda na mtu huyo mkiwa pamoja na watu wengi, katika kazi za watu wengi. Kwa sababu gani? Kwa sababu, katika hali hizo, mara nyingi unaweza kujua vizuri tabia za mtu huyo. Hii ni kwa sababu sisi sote tunaelekea kuwa namna ile ile bila kukazwa na maoni ya kwamba kuna mtu anayetuchunguza sana. Lakini watu wawili wanapojitenga mbali na watu wengi, tangu wakati huo maelekeo ya asili yanamfanya mtu atake kuwa kama mtu mwingine anavyotaka awe, hata kupenda vitu anavyopenda na kuchukia vitu anavyochukia. Mara nyingine hii inaweza kuficha tabia za mtu huyo. Wanapokuwa wawili, upesi mwanamume na mwanamke wanaweza vilevile kuvutwa sana na mahaba (mapenzi) hata waanze kutazamana kwa matumaini mazuri sana. Mwanamume na mwanamke wakioana kwa sababu ya kuvutwa na mahaba hayo, mara nyingi wanakuja kujua mwishowe kwamba wako katika matatizo (magumu).
20-22. (a) Ni kwa sababu gani ni jambo la maana kuanza uchumba bila kufanya mchezo? (b) Ni mambo gani unayoweza kujua juu ya mtu unayetazamia kuoana naye wakati wa uchumba? Zaidi ungetaka kuona mchumba wako akiwa na sifa gani?
20 Kwa kawaida, mwanamume ndiye anayeanza uchumba kwa kuonyesha anapendezwa na mwanamke. Ikiwa mwanamume huyo anasema kweli na hafanyi mchezo, mwanamke ana haki ya kusadiki kwamba bila shaka mwanamume huyo anakusudia kumwoa. Halafu? Basi, hapo mwanamke anakuwa na daraka la kujiuliza kama anasadiki ya kwamba angeweza kufikiria kuolewa na mwanamume huyo. Akiwa na hakika sana kwamba hangefikiria kuolewa naye, hapo halingekuwa tendo la fadhili amruhusu mwanamume ampende sana. Wasichana wengine wamekuwa na nia ya kuchumbiwa ili waonyeshe tu kwamba wanajulikana sana au wanafaa, wakitumaini kwamba sasa vijana wengine wa kiume wangewapendelea. Vijana wengine wa kiume wamefanya kama hivyo, wakidhani wanaweza kufanya upuzi, na kujifurahisha kisha waache kabla mambo hayajawa mazito sana. Lakini mtu akitumia uhuru wake kwa choyo hivyo anaweza kuleta mambo makubwa ya kuchukiza kweli kweli, yanayoweza kuchukua miezi hata miaka, ili yaondolewe.
21 Njia ya pekee ambayo uchumba waweza kuleta faida ni kuutumia bila choyo. Unaweza kutoa nafasi ya kujuana sana na mtu ambaye unafikiria kuishi naye muda mwingine wa maisha. Ikitegemea unyofu ambao mtu anamwonyesha mwenzake, kila mmoja anaweza kujua mambo ambayo mwenzake anapenda na asiyopenda, anaweza kujua kanuni, mazoea na maoni, ndiyo, hasira na nia za mwenzake na anavyotenda yanapotokea matatizo au magumu. Una haki ya kutaka kujua mambo haya: Je! yeye ni mwenye fadhili, ni mkarimu na anafikiria wengine? Je! anaheshimu wazazi na watu ambao ni wazima kuliko yeye? Je! anaonekana sawa kuwa mwenye kiasi na unyenyekevu, au ni mtu mwenye majivuno, mwenye kichwa kikubwa? Je! ninaona akijiweza na kuwa mwenye kusawazika, au mahali pake, naona udhaifu na tabia za kitoto, labda kufutuka (kuona uchungu) au hata kuwa na hamaki? Kwa kuwa kazi ni sehemu kubwa ya maisha, namna gani ishara za uvivu, kutokuaminika au moyo wa kuponda fedha? Namna gani mipango ya wakati ujao? Je! watoto wanahitajiwa au mnapendezwa na kazi fulani ya pekee? Katika makala iliyo na kichwa hiki “Vionyo vya Hatari ya Uchumba,” mwandikaji mmoja anaeleza hivi: “Uchunguzi wetu juu ya watu waliochumbiana na watu waliooana wakawa na furaha na wale wasiokuwa na furaha ulivumbua kwamba wale wasio na furaha ni wale ambao hawakupatana sana juu ya miradi na kanuni za maisha.”
22 Zaidi ya yote, imekupasa ujue makusudi ya Mungu yanavyolingana na mapendezi na mipango ya mwenzako. Ndiyo, mkiisha kupanga mambo yote, sasa ninyi wawili mnafaana namna gani? Ikiwa pana tofauti kubwa sana, usijipumbaze kwa kudhani kwamba ndoa itakuja kuziondoa. Huenda matata yanayoletwa na tofauti hizo yakafanywa kuwa mengi hata zaidi.
MWENENDO UNAOHESHIMIKA WAKATI WA UCHUMBA
23-26. (a) Maoni yako ni nini juu ya kushikana mikono, kupigana busu (kubusu) na kukumbatiana kwa mwanamume na mwanamke wanaokusudia kuoana? (b) Huenda mtu akawa mwenye hatia ya “mwenendo mpotovu” na “uchafu” namna gani? Sababu gani ni jambo la maana kuepuka mambo hayo? (Wagalatia 5:19, 21)
23 Katika nchi ambazo wazazi wanaruhusu waliochumbiana kushirikiana bila kuwa na mtu wa kuwaangalia, mara nyingi mwanamume na mwanamke wanaanza kuonyeshana mahaba kama vile kushikana mikono, kupigana busu (kubusu), hata kukumbatiana. Bila shaka, wazazi wanao wajibu wa kufundisha wana na mabinti zao kanuni wanazotaka ziongoze mwenendo wao. Wazee katika kundi la Kikristo wanaweza kuelekeza fikira za vijana kwenye kanuni za uongozi zinazopatikana katika Neno la Mungu, na mtu ye yote anayetaka sana kufuata mwenendo huo wenye hekima katika maisha atatii shauri hilo kwa nia na kwa furaha.
24 Biblia inakataza kabisa uasherati ambayo maana yake ni ngono inayofanywa na watu wasiofunga ndoa na watu waliochumbiana, inaonya vilevile juu ya mwenendo usio wa adili na juu ya “uchafu” unaoweza kutukia wakati wa uchumba. (Wagalatia 5:19-21) Wanaume na wanawake wo wote wanaotii maonyo hayo wataepuka kupata huzuni nyingi wala hawatasumbuka sana wanapokumbuka mwendo fulani mbaya waliokuwa nao zamani. Lakini mwenendo mchafu kulingana na kanuni za Biblia ni nini? Waweza kutia ndani nini?
25 Kushikana mikono kunaweza kuwa wonyesho safi wa mapenzi kati ya watu wanaofikiria kuoana. Kweli, kushikana mikono kunaamsha tamaa, lakini hilo ni jambo la kawaida wala si nyakati zote linapokuwa baya. Hata kumwona tu mtu unayefikiria kuoana naye kwaweza vilevile kuamsha tamaa, ‘kuufanya moyo upige-pige haraka zaidi.’ (Wimbo wa Sulemani 4:9, New World Translation ya Kiingereza) Hata hivyo, ni lazima tukumbuke ya kwamba kulingana na tabia ya kibinadamu, kugusana kwa miili kunaongeza nyege za mwanamume na mwanamke. Basi, kwa sababu ya kujua yanayoweza kutokea kwa kugusana miili, huenda watu wengine wakaona ni afadhali wasiwe wakigusana miili kabisa wakati wa uchumba. Kusiwe mtu wa kudharau wala kupuza maoni ya dhamiri yao.
26 Kubusu vilevile kunaweza kuwa wonyesho safi wa mapenzi kati ya watu wanaofikiria kuoana —au huenda usiwe. Basi, ulizo ni hili, Nyege zinaamka kadiri gani? Kubusu kunaweza kuamsha nyege kwa kadiri ya kufanya mwanamume na mwanamke wawashwe sana hata watake kufanya ngono. Kuamshwa nyege kunaweka mwanamume na mwanamke tayari kufanya ngono, lakini kulingana na sheria ya Mungu, pendeleo hilo ni la watu waliofunga ndoa peke yao. Mwanamume na mwanamke wakipuza sheria ya Mungu na kushiriki mwenendo unaoamsha nyege kwa makusudi, kwamba ni kwa kushikana-shikana viungo vya uzazi au kwa njia nyingine, wana hatia ya “uchafu” na ya “mwenendo mpotovu.”
27-30. Kuna sababu gani za kuepuka mwenendo wa kuamsha nyege kabla ya ndoa?
27 Haitupasi tujidanganye wenyewe. Tukijua kwamba hatujiwezi katika mambo hayo, basi tusihatirishe matumaini yetu ya wakati ujao wala yale ya mwenzetu kwa kuchezea mambo hayo. Je!
ungeendesha motokaa kutelemka kilima katika barabara inayopotokapotoka ikiwa ungejua kwamba breki zake si nzuri? Wakati wa kukaza nia yako na kufikiria mambo hayo ni kabla hujaanza, si ukiisha kuanza. Tamaa za mwili zikiisha kuanza kuamka, kwa kawaida ni vigumu sana kuzuia matokeo yazo. Wale wanaoruhusu nyege ziongezeke ndani yao hata watamani kufanya ngono na hali hawajafunga ndoa, wanajiletea wenyewe wasiwasi na mapingamizi. Ni kama kusoma kitabu chenye hadithi yenye kupendeza sana halafu kukuta kwamba sura ya mwisho imeondolewa.
28 Wale wanaokuwa na mwenendo bora wakati wa uchumba watakuwa na mwanzo mzuri wa ndoa kushinda wale wanaovutwa na nyege na kuzidi kufanya mahaba. Msichana atamheshimuje mtu ambaye hajizuii? Lakini mvulana anayejizuia na kukaza moyo anajipatia heshima. Ndivyo ilivyo na msichana. Zaidi yampasa yeye afahamu kwamba, ijapokuwa nyege zake zinachukua muda mrefu kuamka, ni tofauti kwa mwanamume. Mwanamume anaweza kuamshwa nyege vyepesi na kwa haraka.
29 Kuvutwa na nyege za mara kwa mara zinazoongezeka kunaweza kuongoza mtu kwenye ndoa ya mapema zaidi. Kitabu kinachoitwa Adolescence and Youth chasema: “Mara nyingi mwanzo wa uchumba hauwi wa kuwazia tu. Huenda wakati huo ndoa ikamfanya mtu atazamie mambo mengi kuliko ambavyo ndoa yo yote ingeweza kutimiza. Kwa kawaida uchumba unaochukua muda mrefu unatoa nafasi ya kumfahamu mwenzako vya kufaa zaidi ili kuwe ndoa yenye ufahamiano.” Uchumba wa mtu ukichukua muda mrefu ni lazima ajizuie, ama sivyo huenda nyege zikaongezeka mapema sana hata iwe hatari sana.
30 Nyege zikiruhusiwa ziamke sana wakati wa uchumba, huenda yakatokea vilevile mashaka baada ya ndoa. Huenda mume na mke wakaanza kuwaza hivi, Je! kweli tulioana kwa sababu ya upendo? Au tulioana kwa sababu ya kuwashwa nyege tu? Je! nilimchagua mwenzangu kwa hekima? Huenda msichana vilevile akaelekea kuona shaka juu ya ukweli wa upendo wa mumewe, akiwaza kwamba labda alimwoa kwa sababu ya kutamani mwili wake tu na si kwa sababu ya jinsi alivyo kama mtu.
31, 32. Ni jambo gani linaloweza kusaidia mwanamume na mwanamke waepuke mwenendo wa kuamsha nyege ambao ungeharibu uchumba wao?
31 Basi, jilindeni wenyewe na kuilinda furaha yenu ya wakati ujao kwa kuepuka hali zinazoamsha nyege. Mahali pasipo na watu na penye giza hapatawasaidia mwe na uchumba unaoheshimika. Wala hali za kushinda muda mrefu mkiwa peke yenu kunapokuwa hakuna jambo jingine la kufanya isipokuwa kupeana mahaba hayo, hazitasaidia. Lakini furaha nyingi na zilizo safi zaweza kuonwa kwa kula chakula pamoja katika mkahawa au kutembelea nyumba fulani yenye vitu vya makumbusho au mahali fulani pa kwenu panapopendeza na pana mambo mazuri. Ijapokuwa mnafurahia maono ya kuwa na faragha kwa sababu hampo pamoja na watu mnaojuana nao, mtaona usalama wa kwamba hamkutengwa kabisa na watu wengine.
32 Vilevile, mahali pa kufikiria tu mambo ambayo mnakosa kwa kujizuia, fikirieni mnayotayarisha kufanya wakati ujao. Kisha, miaka yote itakayokuja, mtaweza kuukumbuka uchumba wenu, si kwa kuuchukia wala kusikitika, bali kwa furaha na uradhi.