Maoni ya Mkristo Juu ya Uchumba
Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua
NDOA ni jambo linalofanywa ulimwenguni pote. Ijapokuwa huenda ishangaze watu wengi, uchumba sivyo ulivyo. Na hata katika nchi nyingi ambako unafanywa, desturi za uchumba zinatofautiana sana.
Kwa watu ambao kwao uchumba unakubaliwa kama jambo la kawaida, kutokuwako kwake katika nchi fulani huenda kukashangaza. Lakini watu waishio katika nchi ambako uchumba haufanywi nao vile vile wanaweza kushangazwa na desturi fulani katika nchi ambako unaendeshwa. Huenda hata wakaziona nyingine za desturi hizi kuwa zenye kuchukiza kidogo.
Kwa hiyo, kuliko kushikilia maoni yetu wenyewe na kudhani kwamba njia ya pekee ya kufanya mambo ndiyo namna ambavyo watu katika mahali petu wenyewe wanavyoyafanya, ni afadhali zaidi kupanua kuwaza kwetu. Hata hivyo, katika mchanganuo wa mwisho, je! siyo matokeo yanayoamua namna desturi fulani zilivyo njema au mbaya? Katika Biblia katika Mhubiri 7:8 twasoma hivi: “Heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake.” Nasi lazima tukubali kwamba katika nchi nyingi ambako uchumba ndiyo desturi, kiasi kikubwa kwa mia cha ndoa haziwi na matokeo mema bali mwisho wazo unakuwa talaka.
DESTURI ZILIZOPO
Kwa kweli, ulizo linalokupasa wewe ni: N’nini desturi iliyopo mahali uishipo? Katika nchi nyingine au majimbo wanaotazamiwa kuwa bibi-arusi na bwana-arusi hawakutani mpaka siku yao ya arusi. Mipango ya ndoa yao yote imekwisha pangwa na wengine—na wazazi wao mbali-mbali au pengine kwa njia ya mshauri anayeweza kutumiwa na wazazi au anayetazamiwa kuwa mume, nyakati nyingine. Sasa, mpango huu wa ndoa bila ya kuchumbiana kwanza huenda usipendelewe na wengi; lakini ndiyo desturi ya wengine. Na yatupasa tuangalie kwamba ni desturi tusiyoweza kuilaumu kama isiyopatana na Neno la Mungu, Biblia.
Twaiona imeonyeshwa katika ndoa ya mwana wa Ibrahimu Isaka na Rebeka, ambayo waweza kusoma juu yake katika Mwanzo sura ya 24. Nasi twasoma kwamba mwana wa Isaka Yakobo alipotaka kumwoa binti yake Labani Raheli, hakumposa yeye (Raheli) bali alifanya maposo yake kwa baba yake, akimwomba Labani aikubali ndoa hiyo. (Mwa. 29:15-20) Zaidi ya hayo, ndoa hizi za waabudu wa kweli zilifanikiwa.
Kwa kweli kuna msingi mmoja tu wa Maandiko kwa Mkristo kukataa kuoa au kuolewa chini ya mpango wa namna hiyo. Huo ndio upi? Ni ambapo mpango huo ungehitaji mtu aoe au aolewe na mtu asiyemwamini Mungu wa kweli. Yehova, wala asiye mwanafunzi wa Mwana wa Mungu, Yesu Kristo.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 7:3, 4; 1 Wakorintho 7:39; 2 Wakorintho 6:14.
Kwa hiyo, yanayosemwa katika makala ifuatayo hayakusudiwi kuuendeleza mpango wa uchumba wala kudharau desturi zilizoko katika nchi nyingi wala kuzipuza. Kuliko hivyo, yamekusudiwa yatoe mashauri yafaayo kutoka kwa Neno la Mungu, zaidi kwa vijana waishio katika nchi ambako mazoea ya namna hiyo ya uchumba yanapatikana.
NDOA ZA WASIOFIKIA UMRI WA MIAKA 20
Na ijapokuwa makala hii inayofuata imekusudiwa hasa kwa vijana, kusudi lake si kutia moyo ndoa ya mapema. Magumu yanaonyesha kwamba ndoa za watu wasiofikia umri wa miaka 20 hazielekei kufanikiwa kama ndoa ambapo mmoja au watu wote wawili wamefikia umri mkubwa zaidi, Kama vile alivyosema mchunguzi wa maendeleo ya jamii ya watu: “Uchunguzi unaonyesha kwamba, kwa jumla, ndoa za watu wasiofikia umri wa miaka 20 zinaonyeshwa na talaka nyingi au huzuni nyingi zikilinganishwa na ndoa zinazofanywa katika umri wa baadaye.”
Kwa upande mwingine, hakuna msingi wa Maandiko wa kukataza kwa ushupavu ndoa zote kati ya vijana hao. Kwa jumla, sheria za nchi zinawapa wazazi haki ya kufanya uamuzi kamili juu ya mambo yatakayokuwa bora kwa watoto wao na kuwaongoza kwenye furaha kuu na faida kwao. Huenda wakaamua waruhusu ama wasiruhusu ndoa ya wana wao na binti walio chini ya usimamizi wao. Bila shaka, magumu yaliyo mengi ya nyakati zetu na kiasi kikubwa kwa mia cha kushindwa kwa ndoa yamepaswa yawafanye kuwa waangalifu. Nayo yamepaswa yawafanye vijana wenye akili vile vile wajiangalie—kuliko ‘kuoa au kuolewa haraka haraka na kuja kujuta polepole.’ Ni upumbavu kupita katika mlango haraka haraka ati kwa sababu tu umefunguliwa, na hali hujui sawasawa kilichoko upande wa pili.
Zaidi ya yote, mtu mwenye hekima, kijana au mzee, atatafuta uongozi wa Mungu. Ndiyo, “mkabidhi [Yehova] kazi zako, na mawazo yako yatathibitika,” kwa maana “moyo wa mtu huifikiri njia yake; bali [Yehova] huziongoza hatua zake.”—Mit. 16:3, 9.