Ni Nini Kusudi la Mungu?
WATU wengi wanaotilia shaka kuwapo kwa Mungu mwenye nguvu zote na mwenye upendo, hujiuliza: Ikiwa Mungu yuko, kwa nini ameruhusu kuteseka kwingi na uovu mwingi katika historia yote? Kwa nini anaruhusu kuwepo kwa hali ya mambo yenye kusikitisha inayotuzunguka leo? Kwa nini hafanyi jambo fulani ili kukomesha vita, uhalifu, ukosefu wa haki, umaskini, na taabu nyingine nyingi zinazoongezeka kwa kiwango chenye kuogofya katika nchi nyingi sana duniani?
Watu fulani wanadokeza kwamba Mungu aliumba ulimwengu wote mzima, akaweka wanadamu kwenye sayari Dunia, na kisha kuwaacha wasimamie mambo yao wenyewe. Kulingana na oni hili, Mungu hangelaumiwa kwa ajili ya shida na taabu ambazo watu hujiletea kwa sababu ya pupa yao au usimamizi wa mambo usiofaa.
Hata hivyo, wengine wanapinga nadharia hiyo. Kwa kielelezo, profesa wa fizikia Conyers Herring, anayekiri kuitikadi katika Mungu, asema hivi: “Napinga wazo la kuwapo kwa Mungu ambaye zamani sana alianzisha utaratibu fulani na tangu wakati huo akaketi akiwa mtazamaji huku wanadamu wakipambana na fumbo hilo. Sababu moja inayonifanya nikatae jambo hili ni kwamba mambo ambayo nimejionea katika sayansi hayanipi sababu ya kuitikadi kwamba kuna ‘utaratibu’ wowote wa ulimwengu wote mzima ambao kwa msingi ndio ulio sahihi. Nadharia zetu za kisayansi . . . sikuzote zitaendelea kufanyiwa marekebisho makubwa zaidi, lakini nahisi uhakika kwamba sikuzote zitathibitika kuwa na kasoro. Nafikiri ni jambo lenye utimamu kuwa na imani katika kani iliyo hai ambayo hufanya maendeleo haya yawezekane sikuzote.”
Mungu Ana Kusudi
Kusudi la Mungu la awali kwa sayari Dunia lilikuwa ikaliwe na wanadamu waadilifu, waliokamilika. Nabii Isaya aliandika: “Maana BWANA, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu, ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isaya 45:18.
Badala ya kujaza watu duniani kwa kuumba mtu mmoja-mmoja, Mungu alikusudia kujaza dunia kupitia kuzaana. Adamu na Hawa walipoasi dhidi ya Mungu, uasi huo haukuzuia kusudi lake la awali, lakini ulisababisha rekebisho la lazima kwa mambo fulani ili kusudi lake kuhusu wanadamu na dunia lipate kutimizwa.
Kwa miaka ya kwanza ipatayo 6,000 ya kipindi hiki, Mungu ameruhusu mwanadamu ajitawale kwa kujitegemea pasipo mwongozo wake wa moja kwa moja. Hivyo ndivyo wazazi wetu wa awali walivyochagua kwa hiari yao wenyewe. (Mwanzo 3:17-19; Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Kuruhusiwa kujitegemea pasipo mwongozo wa Mungu na utawala ambao ungefuata wa kibinadamu badala ya utawala wa Mungu kungefichua kushindwa kwa binadamu kuelekeza hatua zake mwenyewe na kushindwa kumtawala mwanadamu mwenzake kwa mafanikio.
Bila shaka, Yehova alijua matokeo ya hili kimbele. Aliwapulizia waandishi wa Biblia wayaandike. Kwa kielelezo, nabii Yeremia aliandika: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.
Mtu mwenye hekima Solomoni alieleza juu ya matokeo yenye msiba yanayotokea wakati wanadamu wanapojaribu kuwatawala wanadamu wenzao, kama ambavyo wamefanya kwa karne nyingi. “Mambo hayo yote nimeyaona, nikatia moyo wangu katika kila kazi iliyofanyika chini ya jua. Kuna wakati ambapo mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9.
Hata hivyo, badala ya “kuketi akiwa mtazamaji huku wanadamu wakipambana na fumbo hilo,” Mungu Mweza Yote amekuwa na sababu ya kutosha kuruhusu muda kupita kwa maelfu haya ya miaka bila kuingilia kati moja kwa moja maisha ya wanadamu walio wengi.
Kusudi Zuri Limetimizwa
Miaka 6,000 iliyopita ya historia ya kibinadamu yaweza kuonekana kuwa muda mrefu inapolinganishwa na wastani wa muda wa maisha yetu unaopungua miaka 100. Lakini kulingana na ratiba ya Mungu na jinsi anavyoona kupita kwa wakati, hii miaka elfu kadhaa ni kama siku sita—muda unaopungua juma moja! Mtume Petro alieleza hivi: “Acheni jambo hili moja lisiwe likiponyoka kujali kwenu, kwamba siku moja kwa Yehova ni kama miaka elfu na miaka elfu kama siku moja.”—2 Petro 3:8.
Kisha Petro aendelea kupinga shtaka lolote la uzembe au la kukawia kwa upande wa Mungu, kwa kuongezea: “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 Petro 3:9.
Hivyo, wakati miaka iliyotengwa kando itakapomalizika, Muumba atakomesha usimamizi mbaya wa sayari yetu maridadi. Atakuwa amempa mwanadamu muda wa kutosha kudhihirisha kushindwa kwake kutawala au kukomesha vita, jeuri, umaskini, ugonjwa, na visababishi vingine vya kuteseka. Yale ambayo Mungu alionyesha wanadamu hapo mwanzoni—kwamba lazima wafuate mwelekezo wa kimungu ili wafanikiwe, yatakuwa yamethibitishwa kwa mambo halisi waliyojionea.—Mwanzo 2:15-17.
Kulingana na utimizo wa unabii wa Biblia, sasa tunaishi katika sehemu ya umalizio wa “siku za mwisho” za huu mfumo wa mambo usiomwogopa Mungu. (2 Timotheo 3:1-5, 13; Mathayo 24:3-14) Uvumilivu wa Mungu kwa wanadamu kujitawala pasipo kumtegemea na kuvumilia kwake uovu na kuteseka wakaribia kufikia kikomo. (Danieli 2:44) Karibuni, dhiki kubwa zaidi ambayo ulimwengu huu haujapata kushuhudia itatukia, ikifikia upeo kwenye “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote,” Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Vita hiyo itakayoelekezwa na Mungu haitaharibu kazi ya mikono ya Mungu, dunia, bali ‘itawaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.’—Ufunuo 11:18.
Ufalme wa Mungu wa Miaka Elfu
Kutakuwako mamilioni ya waokokaji duniani Har–Magedoni itakapokwisha. (Ufunuo 7:9-14) Unabii ulio katika Mithali 2:21, 22 utakuwa umetimizwa: “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”
Kusudi la Mungu ni kwamba kipindi cha pekee cha miaka elfu moja kitafuatia vita ya uadilifu ya Har–Magedoni. (Ufunuo 20:1-3) Kipindi hiki kitafanyiza Utawala wa Mileani wa Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, akiwa Mfalme wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu. (Mathayo 6:10) Wakati wa utawala huu wa Ufalme wenye shangwe juu ya dunia, mamilioni ya watu wasiohesabika watafufuliwa kutoka katika usingizi wao katika kifo ili kujiunga na mamilioni ya waokokaji wa Har–Magedoni. (Matendo 24:15) Wakiwa pamoja watarudishwa kwenye ukamilifu, kisha—mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo—hatimaye dunia itajaa wanaume na wanawake wakamilifu, wote wakiwa wazao wa Adamu na Hawa. Kusudi la Mungu litakuwa limetimizwa kwa utukufu na kwa mafanikio.
Naam, kusudi la Mungu ni “‘kufuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’ Na Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’” (Ufunuo 21:4, 5) Bila kukosa, kusudi hilo litatimizwa katika wakati ujao ulio karibu.—Isaya 14:24, 27.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Katika ulimwengu mpya wa Mungu, watu wataishi milele kwa furaha