Vijana Huuliza . . .
Naweza Kushindaje Kuhangaikia Sana Uzito?
”Suala kubwa zaidi maishani mwangu ni kama napaswa au sipaswi kuweka malai ya mayai kwenye sandwichi yangu. Nitawezaje kufikiria kitu kingine ninapokuwa nahangaika sana kuhusu malai ya mayai? Mwishowe naamuaje? Sitatumia malai ya mayai—ina kalori nyingi sana. Ninarudi kwenye tatizo la kujinyima chakula tena.”—Jaimee.
MATATIZO ya kula huwapata mamilioni ya vijana.a Wengi wao hawakuanza wakiwa na nia ya kujinyima chakula au kuanzisha zoea la kula kupita kiasi na kutapika. Kinyume cha hilo, wengi walianza wakiwa na mradi sahili wa kupunguza uzito kidogo. Hata hivyo, kabla hawajatambua, walikuwa wamenaswa katika zoea baya la kujinyima chakula au la kula na kutapika. “Nilianza kufuatia utaratibu huu maalumu wa chakula ili kudhibiti uzito wangu, lakini sasa unanidhibiti,” asema Jaimee.
Ukiona kwamba unafikiria chakula kupita kiasi na jinsi kinavyoathiri uzito wako, waweza kufanya nini? Kwanza, tambua kwamba vijana wengine wengi wamepigana na matatizo ya kula na wakashinda! Lakini jinsi gani?
Kujitazama Mwenyewe
Vita yenye kufanikiwa dhidi ya tatizo la kula ni kukubali uhalisi wa sura yako. “Watu walio wengi wenye matatizo ya kula wana maoni yaliyopotoka kujielekea,” chasema kitabu Changing Bodies, Changing Lives. “Hawaoni miili yao kwa njia iliyo halisi na hujichambua sana, hasa sura yao.”
Kwa kweli, vijana fulani huona kwamba umbo lao la kimwili ndilo jambo la maana zaidi; kasoro yoyote huonwa kuwa msiba. “Mimi ni mnene sana siwezi kuvumilia,” asema Vicki mwenye umri wa miaka 17. “Kiuno changu ni kinene sana siwezi kuvaa kitu chochote cha kuingizwa ndani.” Hata baada ya kupoteza kilogramu 10, Vicki hakuridhika. Ama alikataa kula ama akala kupita kiasi na kutapika chakula chote alichokuwa amekila.
Kwa hakika si kosa kuhangaika kwa kiasi fulani kuhusu namna unavyoonekana. Kwa habari hii, inapendeza kuona kwamba Biblia hutoa maelezo yanayofaa kuhusu umbo la mwili na sura za wanawake na wanaume kadhaa, kutia ndani Sara, Raheli, Yusufu, Daudi, na Abigaili.b Hata Biblia husema kwamba mtunzaji wa Daudi Abishagi alikuwa “mzuri sana.”—1 Wafalme 1:4.
Kufafanua Uzuri wa Kweli
Hata hivyo, Biblia haitilii mkazo kimsingi sura au umbile la mwili. Badala yake, inatukuza “yule mtu wa siri wa moyoni.” (1 Petro 3:4) Ni yule mtu wa ndani ambaye kwa kweli humfanya mtu ama avutie ama awe mwenye kuchukiza machoni pa Mungu na wanadamu.—Mithali 11:20, 22.
Mfikirie mwana wa Mfalme Daudi, Absalomu. Biblia husema: “Basi katika Israeli wote hapakuwa na mtu hata mmoja mwenye kusifiwa kwa uzuri wake kama huyo Absalomu; tangu nyayo za miguu yake hata utosi wa kichwa chake hapakuwa na ila kwake.” (2 Samweli 14:25) Lakini, kijana huyu alikuwa mdanganyifu. Kiburi na tamaa ya makubwa ilimchochea ajaribu kujinyakulia cheo cha mfalme aliyewekwa na Yehova. Kwa hiyo, Biblia haimfafanui Absalomu kwa njia inayofaa bali humfafanua kuwa mtu mwenye kukosa uaminifu-mshikamanifu pasipo aibu na mwenye chuki ya kuua.
Uzuri wa kweli wa mtu hautegemei umbo lake la mwili. Ikiwa na sababu nzuri, Biblia husema: “Jipatie hekima; naam kwa mapato yako yote jipatie ufahamu. Atakupa neema kuwa kilemba kichwani; na kukukirimia taji ya uzuri.”— Mithali 4:7, 9.
Ingawa hivyo, kwa kukiri wazi, mara nyingi matatizo ya kula huchochewa na mambo mengine zaidi ya mtu kutoridhika na sura yake. Kitabu kimoja cha marejezo chasema hivi: “Watu wanaohangaikia sana chakula na kupatwa na matatizo ya kula kama vile kujinyima chakula, kuwa na hamu ya chakula isiyo ya kawaida, na kula kupita kiasi, kwa kawaida hawajistahi—hawana maoni yanayofaa kuhusu hadhi yao na huhisi kwamba wengine hawawathamini vilevile.”
Kuna mambo mengi yawezayo kuchangia hisia za kutojistahi. Kwa kielelezo, unapoanza kubalehe, waweza kuwa na hisia nyingi sana za kutokuwa na hakika—hasa ikiwa umekua kabla ya marika wako. Kisha, pia, vijana fulani wanalelewa katika nyumba ambapo kuna msukosuko wa daima, labda hata kutendwa vibaya kimwili au kingono. Bila kujali kisababishi, kwa kawaida kupona hutia ndani kukiri kitu kinachochochea hisia za kutojistahi. Hili lamaanisha kujistahi. Hakika, kila mtu angalau ana sifa fulani zenye kusifika. (Linganisha 1 Wakorintho 12:14-18.) Ni kweli, huenda ukakosa kuziona, lakini rafiki aliyekomaa huenda akakutajia sifa hizi.
Lakini namna gani ikiwa wahitaji kupunguza uzito kikweli kwa sababu halali za kiafya? Biblia inapendekeza kwamba tuwe “wenye kiasi katika mazoea.” (1 Timotheo 3: 11) Kwa sababu hiyo, ni bora kuepuka mazoea yanayopita kiasi katika ulaji au kufuatia mbinu za kupunguza uzito haraka. Labda njia bora ya kupunguza uzito ni kula chakula kinachofaa na kufanya mazoezi ya kutosha. “Kama ilivyo na vitu vinginevyo,” lasema gazeti FDA Consumer, “kuna njia inayofaa na isiyofaa ya kupunguza uzito. Njia isiyofaa ni kukosa kula milo, kuamua kutokula chochote bali kuishi kwa mkate na maji, kutumia tembe za kupunguza hamu ya kula, au kujilazimisha utapike.”
Uwezo wa Kuongea na Mtu Mwingine
Mfanyakazi wa huduma za jamii Nancy Kolodny alinganisha kuwa na tatizo la kula na “kuingia ndani ya mzingile ukiwa peke yako, bila ramani au dira, bila kujua mahali njia za kutokea zilipo, na bila kuwa na hakika ni lini utatoka au ikiwa utapata njia ya kutokea. . . . Kadiri utumiavyo muda mwingi ndani yake ndivyo unavyotatanishwa na kufadhaishwa ujaribupo kujiondoa.” Kwa hiyo ikiwa una dalili za kujinyima chakula au kuwa na hamu ya chakula isiyo ya kawaida, unahitaji msaada. Huwezi kujiondoa kutoka kwenye “mzingile” huo kwa kujitegemea. Hivyo mweleze mzazi au mtu mzima unayemtumaini mambo yako ya ndani. Mithali ya Biblia husema: “Rafiki hupenda sikuzote, na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.
Wengi wa Mashahidi wa Yehova wamepata uandamani wenye kutumainika miongoni mwa wazee katika kutaniko la Kikristo. Bila shaka, wazee si matabibu, na msaada wao hauwezi kuchukua mahali pa msaada wa kitiba. Hata hivyo, waangalizi Wakristo hawatapuuza “kilio cha maskini,” na shauri na sala zao zaweza kusaidia “asiyejisikia vizuri apone” kiroho.—Mithali 21:13; Yakobo 5:13-15.
Ikiwa unahisi ugumu wa kumwelezea mtu fulani mambo yako ya ndani ana kwa ana, andika mawazo yako katika barua, ukiomba jibu. Jambo la maana ni kumfunulia mtu mwingine jambo hili. “Kwa kukiri uhakika wa kwamba huwezi kushughulika na jambo hilo ukiwa peke yako tena,” aandika Nancy Kolodny, “unawajibika kumruhusu mtu mwingine akusaidie kuanzia wakati huu na kuendelea.” Aongezea: “Huenda hatua hizi zikawa ngumu kufikiria na kuchukua, lakini zinafaa, ndizo zitakazokuongoza uelekee upande unaofaa wa kutoka kwenye mzingile huo.”
Vijana Wakristo wana msaada mwingine wenye nguvu—sala. Kusali kwa Mungu si mbinu ya kiakili ya kukufanya uwe na amani ya akili. Ni mawasiliano halisi na ya maana pamoja na Muumba, anayekuelewa vizuri kuliko unavyojielewa! (1 Yohana 3:19, 20) Kwa sababu hiyo, ingawa huu si ndio wakati wa Yehova kuondoa mabaya yote, Mungu wetu mwenye upendo aweza kuongoza hatua zako ili usiangamie. (Zaburi 55:22) Kutokana na yale aliyojionea mwenyewe, mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Nalimtafuta BWANA akanijibu, akaniponya na hofu zangu zote. Maskini huyu aliita, BWANA akasikia, akamwokoa na taabu zake zote.”—Zaburi 34:4, 6.
Basi, kwa vyovyote vile, mweleze Yehova Mungu hisia zako zote za ndani kabisa. ‘Mtupie hangaiko lako lote,’ akaandika mtume Petro, “kwa sababu yeye huwajali nyinyi.” (1 Petro 5:7) Ili kujenga uthamini kwa fadhili-upendo za Yehova, kwa nini usisome kwa uangalifu Zaburi 34, 77, 86, 103, na 139? Kutafakari juu ya zaburi hizi kutaimarisha usadikisho wako kwamba Yehova ni mwaminifu-mshikamanifu na anataka ufanikiwe. Kwa kusoma Neno lake, utahisi kama Daudi aliyeandika hivi: “Wakati wowote ninapohangaika na kuwa na wasiwasi, unanifariji na kunifanya nitereme.”—Zaburi 94:19, Today’s English Version.
Uwe Mwenye Subira —Mtu Hupona Hatua kwa Hatua
Watu walio wengi wanaopata msaada wa tatizo la kula hawaponi mara moja. Mfikirie Jaimee, aliyetajwa mwanzoni. Hata baada ya kuanza kupokea msaada, aliona ugumu wa kula chakula sahili kama vile chakula cha nafaka cha kifungua-kinywa. “Ninahitaji kujiambia mwenyewe kwamba hiki kinanifaa, na ninahitaji chakula ili niishi,” asema. “Kiasi cha kijiko kimoja ninachokula kinaonekana kuwa maelfu ya kilogramu.”
Ingawa wakati mmoja Jaimee alikaribia kufa, aliamua kushinda tatizo la kufikiria chakula kupita kiasi. “Sitakufa,” akasema. “Nitapigana na tatizo hili na kulishinda. Nitashinda tatizo la kujinyima chakula. Itakuwa vigumu, lakini nitafanya hivyo.” Wewe pia unaweza kufaulu!
[Maelezo ya Chini]
[Picha katika ukurasa wa 19]
Mlo kamili na mazoezi yanayofaa yanaweza kukusaidia kudhibiti uzito wakyo