Vijana Huuliza . . .
Je, Nina Tatizo la Kula?
“Nyakati nyingine ninapoketi ili nile, mimi hushikwa na woga na kuanza kutetemeka. Mimi huhofia kwamba nitanenepa. Mimi hujiambia, ‘Ninapaswa kupunguza kilo nyingine mbili.’”—Melissa.a
“Nataka niwe mwenye kuvutia, na naogopa sana kunenepa. Lakini sitaki yeyote ajue kwamba mimi hujitapisha baada ya kula. Ni jambo lenye kuaibisha sana.”—Amber.
“Mimi hujiambia: ‘. . . Leo nitafanya vizuri zaidi. . . ’ Baadaye mchana, katika pindi nisiyoweza kujizuia, mimi hula chakula kingi mno kwa muda mfupi. Kisha najihisi mwenye hatia, nami hutamani kufa.”—Jennifer.
UNATAKA kuwa mwenye kuvutia, na hilo ni jambo la kawaida. Unataka kufarijiwa unapokuwa na wasiwasi au unapovunjika moyo. Hilo pia si kosa. Lakini iwapo hali yako ni kama ya wasichana watatu walionukuliwa hapa, huenda una tatizo. Hata hivyo, hauko peke yako. Ukweli ni kwamba mamilioni ya vijana, hasa wasichana, wana matatizo ya kula.b
Acheni tuzungumzie kifupi ugonjwa wa kujinyima chakula, ugonjwa wa kula na kujitapisha, na ugonjwa wa kula kupita kiasi. Kila moja ya matatizo hayo huwa na dalili zake za pekee, lakini yote yanahusiana na mtazamo usio wa kawaida kuelekea chakula. Ukihisi hali yako inafanana na mojawapo ya hali zifuatazo, uwe na hakika kwamba kuna msaada. Unaweza kupona!
Maelezo Mafupi
◼ UGONJWA WA KUJINYIMA CHAKULA. Hata awe mwembamba kadiri gani, msichana aliye na ugonjwa huo anapojiangalia kwenye kioo, yeye hujiona kuwa mnene kupita kiasi. Ili apunguze uzito, msichana huyo atachukua hatua zinazopita kiasi. “Nilianza kuhesabu kila mara kiasi cha kalori katika chakula changu,” anasema msichana aliyekuwa na ugonjwa huo. “Nilipanga kwa makini chakula ambacho ningekula kila juma, mara kwa mara sikula, nami nilifanya mazoezi mengi nilipofikiri kwamba nimekula chakula chenye kalori nyingi mno. Nilimeza dawa za kuharisha mara sita kwa siku.”
Punde si punde, dalili za ugonjwa huo huanza kuonekana. Dalili ya kawaida ni kupunguza uzito, lakini mgonjwa anaweza kupoteza nywele, kuwa na ngozi kavu, kuwa mchovu, na mifupa yake inaweza kudhoofika. Huenda akapata hedhi katika pindi zisizo za kawaida au hata kukosa kuipata kwa miezi kadhaa mfululizo.
Huenda ikaonekana kwamba dalili hizo hazidhuru, lakini tambua jambo hili—Ugonjwa wa kujinyima chakula ni hatari kwa uhai. Uchunguzi mmoja ulionyesha kuwa baada ya muda, kufikia asilimia 10 ya watu walio na ugonjwa huo hufa kutokana nao, na mara nyingi hilo hutokea mfumo fulani wa mwili unaposhindwa kufanya kazi au mtu anapokuwa na matatizo mengine yanayohusiana na kukosa lishe.
◼ UGONJWA WA KULA NA KUJITAPISHA. Badala ya kukataa kula, msichana aliye na ugonjwa huu hula chakula chenye kalori zinazoweza kufikia hata 15,000 katika kipindi cha saa mbili tu! Kisha hujitapisha, hutumia dawa za kuharisha, au za kumfanya mtu akojoe.
Kwa kawaida msichana aliye na tatizo hilo hula kwa siri chakula kingi mno. “Nilipotoka shuleni na kufika nyumbani kabla ya mtu mwingine yeyote, ningekula chakula kingi mno,” anasema msichana mmoja. “Nilificha sana tatizo langu.” Hata hivyo baada ya kula, angejihisi mwenye hatia. “Nilisikitishwa sana na hali yangu,” anasema, “lakini nilijua ninaweza kubadili hali yangu kwa urahisi. Ningejitapisha kisha ningetulia na kuhisi ninajiweza.”
Hata ikiwa kuondoa chakula tumboni kuna faida fulani, zoea hilo ni hatari. Matumizi mabaya ya dawa za kuharisha hudhoofisha utando wa utumbo nao unaweza kufura au kupata maambukizo. Kujitapisha mara nyingi kunaweza kumaliza maji mwilini, kuozesha meno, kuharibu umio, na hata kusababisha matatizo ya moyo.
◼ UGONJWA WA KULA KUPITA KIASI. Kama mtu aliye na ugonjwa wa kula na kujitapisha, kwa kawaida msichana aliye na ugonjwa huu hula chakula kingi mno. Tofauti iliyopo ni kwamba hatakiondoa tumboni. Huenda hilo likamfanya anenepe kupita kiasi. Hata hivyo, baada ya kula kupita kiasi, baadhi ya wasichana hujinyima chakula au hufanya mazoezi makali. Msichana akidumisha uzito wake kwa njia hiyo, nyakati nyingine huenda watu wa familia na marafiki wasitambue ana tatizo.
Msichana aliye na ugonjwa wa kujinyima chakula au kula na kujitapisha ana maoni yasiyofaa kuelekea chakula, hali kadhalika msichana aliye na ugonjwa wa kula kupita kiasi. Msichana mmoja anasema hivi kujihusu na kuwahusu wagonjwa wengine, “Chakula ni kama rafiki yetu wa kibinafsi na wa siri, na labda rafiki yetu wa pekee.” Mwingine anasema: “Unapokuwa ukila kupita kiasi, mambo mengine yote si muhimu. Kilicho muhimu ni chakula tu, kinafariji, na unapomaliza kula unajihisi mwenye hatia na unavunjika moyo.”
Hata bila kuondoa chakula tumboni, kula kupita kiasi ni zoea hatari. Anaweza kupata kisukari, kupanda kwa shinikizo la damu, ugonjwa wa moyo, na magonjwa mengineyo. Pia anaweza kutatizika sana kihisia.
Je, Unaweza Kuwa na Mojawapo ya Matatizo Hayo?
Bila shaka, watu wengi wanaotaka kupunguza uzito na kuwa na afya hawana matatizo ya kula. Hata hivyo, baada ya kufikiria habari iliyo juu, huenda ukajiuliza ikiwa mazoea yako yatakuletea matatizo hayo. Jiulize:
◼ Je, ninaonea aibu mazoea au vitabia vyangu vinavyohusiana na chakula?
◼ Je, ninaficha mazoea yangu ya kula ili wenzangu wasiyagundue?
◼ Je, chakula kimekuwa kitu muhimu zaidi maishani mwangu?
◼ Je, mimi hujipima uzito zaidi ya mara moja kwa siku?
◼ Je, niko tayari kujihatarisha ili nipunguze uzito?
◼ Je, nimewahi kujitapisha, kutumia dawa za kuharisha, au za kumfanya mtu akojoe?
◼ Je, mazoea yangu ya kula yameathiri uhusiano wangu na wengine? Kwa mfano, je, mimi hupendelea kujitenga na wengine ili nile na kuondoa chakula tumboni kwa siri?
Iwapo majibu yako kwa maswali hayo yanaonyesha una tatizo, jiulize hivi:
◼ Je, kwa kweli ninafurahia kuishi hivi?
Unaweza kufanya nini kuhusu hali hiyo?
Chukua Hatua Sasa!
Hatua ya kwanza ni kukubali wewe binafsi kwamba una tatizo. “Baada ya kufikiria jambo hilo,” anasema Danielle, “niligundua nina hisia na mazoea kama ya wasichana walio na ugonjwa wa kujinyima chakula. Nilihofia kukubali kuwa nilikuwa nikifanya yaleyale waliyokuwa wakifanya.”
Pili, sali kwa Yehova kuhusu tatizo lako.c Mwombe akusaidie kufahamu kinachosababisha tatizo lako ili ulishinde. Unaweza kusali hivi kama Daudi: “Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza, na uniongoze katika njia ya mpaka wakati usio na kipimo.”—Zaburi 139:23, 24.
Kwa upande mwingine, huenda ukagundua kwamba unasita kuyaacha mazoea yako ya kula. Huenda yamekolea sana, yakawa kama uraibu. Unapaswa kusali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Danielle alihitaji kufanya hivyo hasa. “Mwanzoni,” anakubali, “sikutaka kushinda tatizo langu. Hivyo, nilihitaji kusali ili niwe na tamaa nzuri.”
Tatu, zungumza na mzazi au mtu mwingine mzima anayeweza kukusaidia. Watu wazima wanaojali hawatakuaibisha. Badala yake, watajitahidi kumwiga Yehova, ambaye Biblia inasema hivi kumhusu: “Hakudharau wala kuchoshwa na mateso ya mwenye kuteseka; naye hakumficha uso wake, naye alipomlilia amsaidie alisikia.”—Zaburi 22:24.
Kwa kweli, si rahisi kushinda tatizo hilo. Msaada wa wataalamu unahitajiwa katika visa fulani.d Lililo muhimu ni kuchukua hatua. Hilo ndilo jambo ambalo msichana mmoja, aliyekuwa na ugonjwa wa kula na kujitapisha, aliazimia kufanya. “Siku mmoja,” anasema, “nilitambua kwamba zoea la kujitapisha lilikuwa likinitawala. Lakini sikuwa na hakika kuwa ninaweza kulishinda. Hatimaye, nikafanya jambo gumu zaidi nililowahi kufanya. Niliomba msaada.”
Unaweza kufanya vivyo hivyo!
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.
b Kwa kuwa idadi kubwa ya wale walio na matatizo ya kula ni wanawake, katika makala hii tunarejelea wenye matatizo kuwa wanawake. Hata hivyo, kanuni nyingi zilizozungumziwa zinawahusu wanaume pia.
c Unapofadhaika, unaweza kujihakikishia kwamba Yehova mwenyewe atakutunza kwa kutafakari maandiko kama haya yafuatayo: Kutoka 3:7; Zaburi 9:9; 34:18; 51:17; 55:22; Isaya 57:15; 2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:6, 7; 1 Petro 5:7; 1 Yohana 5:14.
d Wakristo wanapaswa kuhakikisha matibabu yoyote wanayokubali hayapingani na kanuni za Biblia.
MAMBO YA KUFIKIRIA
◼ Je, unafikiri una tatizo la kula? Ikiwa ndivyo, unaweza kumwendea nani ili akusaidie?
◼ Unaweza kumsaidiaje rafiki ambaye ana tatizo la kula?
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
“Ninafikiri una tatizo ...”
Mshiriki wa familia yako au rafiki akikuambia hivyo, epuka kujitetea. Tuseme rafiki yako amegundua kwamba nguo yako imeanza kufumuka upande wa nyuma. Je, hungemshukuru kwa kukujulisha kabla nguo yako haijafumuka kabisa? Biblia inasema: “Yuko rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.” (Methali 18:24) Mtu fulani anapokutajia kuhusu tatizo ambalo huenda unalo, mtu huyo huwa rafiki wa aina hiyo!
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]
“Nilitamani sana kuwa mwembamba”
“Nilianza kupunguza uzito. Kisha magego yangu yakang’olewa, na hivyo singeweza kula. Hilo lilinifanya niwe na ugonjwa wa kujinyima chakula. Nilihangaikia sana sura yangu. Nilihisi sikuwa mwembamba vya kutosha. Uzito wangu wa chini zaidi ulishtua. Niliudhuru mwili wangu vibaya sana! Sasa kucha zangu haziwezi kukua. Niliathiri uwezo wangu wa kiasili wa kutambua wakati. Niliharibu mimba mara nne. Nimeacha kupata hedhi ingawa bado ni mapema, nao mfumo wangu wa kuyeyusha chakula una matatizo. Pia nina ugonjwa wa kufura utumbo mkubwa. Hayo yote yamenipata kwa sababu nilitamani sana kuwa mwembamba.”—Nicole.
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
Ukitumbukia tena kwenye tatizo
Unaweza kushinda mazoea yako ya kula, lakini uyarudie majuma au miezi kadhaa baadaye. Hilo likitukia, usife moyo. Biblia inakubali kwamba, “huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba.” (Methali 24:16) Kuteleza si kuanguka. Badala yake, kunaonyesha tu uhitaji wa kuimarisha azimio lako, wa kutambua ishara zinazoonyesha unaelekea kurudia tena zoea lako, na wa kuzungumza tena waziwazi na mtu anayeweza kukutegemeza.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]
Soma kuhusu tatizo hilo
Ikiwa una tatizo la kula, ingefaa usome kulihusu. Kadiri unavyoyajua ndivyo itakavyokuwa rahisi kukabiliana nayo. Huenda ukanufaika kusoma habari nzuri iliyo katika Amkeni! la Januari 22, 1999, ukurasa wa 3-12, na la Aprili 22, 1999, ukurasa wa 13-15.
[Sanduku katika ukurasa wa 21]
TAARIFA KWA WAZAZI
Unaweza kufanya nini ikiwa binti yako ana tatizo la kula? Kwanza, soma kwa makini makala hii na marejeo yaliyoonyeshwa katika maelezo ya chini kwenye ukurasa wa 20. Jitahidi kuelewa kinachomfanya awe na tabia hiyo.
Imeonekana kwamba wengi kati ya wale walio na matatizo hayo, wanajidharau nao hutarajia ukamilifu, na hivyo hujiwekea viwango vya juu kupita kiasi. Hakikisha kwamba humfanyi binti yako awe na tabia hizo. Msifu. (Isaya 50:4) Na ili uweze kushinda mwelekeo wa kutarajia ukamilifu, acha ‘usawaziko wako ujulikane.’—Wafilipi 4:5.
Pia chunguza mtazamo wako mwenyewe kuhusu chakula na uzito wa mwili. Je, yawezekana kwamba bila kujua umekazia mambo hayo kupita kiasi, iwe kwa maneno au kwa matendo yako? Kumbuka, vijana huhangaikia sana sura yao. Hata kufanya mzaha kuhusu “unene wa mtoto mdogo” au wa kijana anayeanza kubalehe kunaweza kumhangaisha sana kijana.
Baada ya kufikiria kwa makini na kusali kuhusu jambo hilo, zungumza na binti yako kwa upendo.
◼ Fikiria sana jambo unalotaka kusema na wakati wa kulisema.
◼ Mweleze waziwazi kinachokuhangaisha na kwamba unatamani kumsaidia.
◼ Usishangae akijitetea mwanzoni.
◼ Sikiliza kwa subira.
Jambo muhimu zaidi ni kujitahidi sana kumsaidia binti yako ashinde tatizo lake. Husisha familia nzima katika jitihada za kumsaidia!
[Picha katika ukurasa wa 21]
Huenda ikakubidi kusali kuhusu tamaa yako ya kufanya marekebisho