Matatizo ya Kula—Ni Nini Kinachoweza Kusaidia?
IKIWA binti yako ana tatizo la kula, anahitaji msaada. Usiahirishe mambo ukidhani kwamba tatizo hilo litaisha lenyewe. Tatizo la kula ni ugonjwa ulio tata, unaohusisha mwili na hisia-moyo.
Bila shaka, wataalamu wametoa matibabu mengi yenye kutatanisha kwa matatizo ya kula. Wengine hupendekeza utibabu. Wengine huunga mkono matibabu ya kisaikolojia. Wengine husema kwamba kuunganisha aina zote mbili za matibabu huwa na matokeo zaidi. Kisha kuna mashauri ya familia, ambayo wengine husema ni ya maana hasa ikiwa mwenye tatizo hilo angali anaishi nyumbani.a
Ingawa huenda wataalamu wakatofautiana katika mfikio wao, wengi huafikiana kwa angalau jambo moja: Matatizo ya kula hayahusishi chakula tu. Acheni tuchunguze baadhi ya masuala yenye kina kirefu ambayo hasa yanahitaji kushughulikiwa mtu fulani anaposaidiwa apone kutokana na kujinyima chakula au kuwa na hamu ya chakula isiyo ya kawaida.
Maoni Yaliyosawazika juu ya Umbo la Mwili
“Niliacha kununua kabisa magazeti ya mitindo ya mavazi nilipokuwa na umri wa miaka 24 hivi,” asema mwanamke mmoja. “Kujilinganisha na vigezo kulileta madhara makubwa na makali sana.” Kama ilivyozungumziwa tayari, vyombo vya habari vyaweza kupotosha maoni ya msichana kuhusu urembo. Kwa kweli, mama mmoja mwenye binti aliye na tatizo la kula asema juu ya “usambazaji usioisha katika magazeti yetu ya habari na matangazo ya biashara ya televisheni ya kuwa mwembamba, mwembamba, mwembamba.” Yeye asema: “Mimi na binti yangu tunapenda kuwa wembamba, lakini tunahisi mbano wa mambo mengi wa wakati uleule hufanya hangaiko la kuwa mwembamba liwe jambo la maana zaidi maishani, la kutangulizwa.” Kwa wazi, kupona kutokana na matatizo ya kula kwaweza kuhitaji maoni mapya kuhusu kinachohusika katika urembo wa kweli.
Biblia yaweza kusaidia katika habari hii. Mtume Mkristo Petro aliandika: “Msiache urembo wenu uwe ule wa kusuka nywele kwa nje na wa kuvalia madoido ya dhahabu au kuvalia mavazi ya nje, bali acheni uwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vao lisilofisidika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.”—1 Petro 3:3, 4.
Petro anasema kwamba tunahitaji kuhangaikia zaidi sifa za ndani kuliko sura ya nje. Kwa kweli, Biblia inatuhakikishia: “BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Jambo hili hufariji, kwa kuwa ingawa hatuwezi kubadili mambo fulani kuhusu maumbile yetu, sikuzote twaweza kuboresha utu wetu.—Waefeso 4:22-24.
Kwa kuwa matatizo ya kula yanaweza kusitawi katika mazingira ya watu wasiojistahi, huenda ukahitaji kujichunguza tena mwenyewe. Kweli, Biblia hutuambia tusijifikirie wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri. (Waroma 12:3) Lakini pia hutuambia kwamba hata shore mmoja ana thamani machoni pa Mungu, ikiongezea: “Nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” (Luka 12:6, 7) Hivyo, Biblia yaweza kukusaidia usitawishe kujistahi kunakofaa. Uthamini mwili wako, na utautunza.—Linganisha Waefeso 5:29.
Lakini vipi ikiwa kwa kweli unahitaji kupunguza uzito? Labda kufuatia miiko fulani ya milo inayofaa na mazoezi yatasaidia. Biblia husema kwamba “mazoezi ya kimwili ni yenye manufaa,” hata ikiwa ni kwa kiwango kidogo. (1 Timotheo 4:8) Lakini kamwe usihangaikie kupita kiasi uzito wako. “Labda mwendo wa hekima zaidi,” uchunguzi kuhusu umbo la mwili wafikia mkataa, “ni kufanya mazoezi mengi—na kukubali jinsi ulivyo badala ya kujaribu kujifinyanga ufikie kiwango cha urembo chenye vizuizi visivyo na msingi.” Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 33 nchini Marekani aliona mfikio huu kuwa wenye kusaidia. “Nimekuwa na sheria moja sahili,” yeye asema. “Fanyia kazi jambo unaloweza kubadili kihalisi, na usitumie muda kwa jambo usiloweza kubadili.”
Ukiwa na mtazamo wa maisha unaofaa na kuongezea mwiko unaofaa wa mlo na mazoezi ya kutosha, yaelekea kilogramu zozote unazohitaji kupunguza zitapungua.
Kutafuta “Mwandamani wa Kweli”
Baada ya kufanyia uchunguzi idadi ya watu kadhaa wenye hamu ya chakula isiyo ya kawaida, Profesa James Pennebaker alifikia mkataa kwamba kwa kiwango kikubwa, utaratibu wao wa kula na kutapika ulikuwa ukiwalazimisha wanawake hao waishi maisha maradufu. Asema: “Karibu kila mtu aliyehojiwa kwa hiari alisema kuhusu wakati na jitihada nyingi mno iliyohitajiwa kuficha marafiki wake wa karibu na familia mazoea yake ya kula. Wote waliishi kwa kudanganya na walichukia jambo hilo.”
Kwa hiyo, hatua itakayotokeza nafuu, ni kuacha kunyamaza. Watu wanaojinyima chakula na wenye hamu ya chakula isiyo ya kawaida wanahitaji kuzungumza kuhusu tatizo hilo. Lakini kwa nani? Mithali moja ya Biblia husema: “Rafiki [“mwandamani wa kweli,” NW] hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” (Mithali 17:17) Huyo ‘mwandamani wa kweli’ aweza kuwa mzazi au mtu mzima mwingine aliyekomaa. Wengine wameona uhitaji wa kumfunulia siri mtu fulani aliye na uzoefu wa kutibu matatizo ya kula.
Mashahidi wa Yehova wana msaada wa ziada—wazee wa kutaniko. Wanaume hawa wanaweza kuwa “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:2) Bila shaka, wazee si madaktari, kwa hiyo kwa kuongezea shauri lao huenda bado ukahitaji matibabu. Hata hivyo, wanaume hawa wenye sifa za kiroho wanaweza kuwa msaada mkubwa sana katika kupona kwako.b—Yakobo 5:14, 15.
Hata hivyo, mtu unayeweza kumtumaini zaidi aweza kuwa Muumba wako. Mtunga-zaburi aliandika: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Naam, Yehova Mungu anapendezwa na watoto wake wa kidunia. Kwa hiyo usipuuze kamwe kusali kwake kuhusu mahangaiko yako ya ndani. Petro atuonya kwa upole: “Huku mkitupa hangaiko lenu lote juu yake, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.”—1 Petro 5:7.
Inapokuwa Lazima Kulazwa Hospitalini
Kulazwa hospitalini kwenyewe si ponyo. Hata hivyo, ikiwa msichana amekosa lishe ya kutosha kwa kukosa sana hamu ya chakula, huenda ikawa lazima apewe utunzaji wa pekee. Kwa kukiri wazi, si rahisi mzazi kuchukua hatua hii. Mfikirie Emily, ambaye binti yake alihitaji kulazwa hospitalini baada ya maisha kuwa, kama asemavyo Emily, “yasiyovumilika kwake na kwetu.” Aongezea hivi: “Kumpeleka hospitalini, akilia, ni jambo lililokuwa gumu zaidi kunipata, ni siku mbaya zaidi ambayo nimepata kuwa nayo.” Hali ya Elaine ilifanana na yake, ambaye pia alilazimika kumlaza hospitalini binti yake. “Nafikiri pindi iliyokuwa mbaya zaidi ninayoweza kukumbuka,” asema, “ni wakati alipokuwa hospitalini na akakataa kula na ikawa lazima wamlishe kwa mipira. Nilihisi kana kwamba wamevunja mapenzi yake.”
Huenda kulazwa hospitalini kusipendeze, lakini katika visa fulani huenda kukahitajika. Kwa idadi kubwa ya watu walio na matatizo ya kula, inasaidia kupona. Emily asema hivi kuhusu binti yake: “Alihitaji kulazwa hospitalini. Alianza kupata nafuu alipolazwa hospitalini.”
Kuishi Bila Matatizo ya Kula
Hatua za kupona zatia ndani kujifunza kuishi bila tatizo la kula kwa mtu asiyekuwa na hamu ya chakula au mwenye hamu ya chakula isiyo ya kawaida. Hili laweza kuwa jambo gumu. Kwa kielelezo, Kim, akadiria kwamba katika awamu yake ya kujinyima chakula, alipoteza kilogramu 18 katika miezi kumi. Lakini, ili apate tena kilogramu 16, ilimchukua muda wa miaka tisa! “Kwa magumu makubwa,” asema Kim, “pole kwa pole nilijifunza kula kwa njia ya kawaida tena, bila kuhesabu kila kalori, kupima chakula, kula vyakula vyenye kalori chache tu, kuwa na wasiwasi ikiwa sikujua kilichomo ndani ya chakula au kitindamlo, au kula chakula cha mchana kwenye mikahawa yenye kuuza saladi mbalimbali.”
Lakini ili Kim apate kupona, mengi zaidi yalihusika. “Nilijifunza kutambua na kuonyesha hisia zangu kwa maneno badala ya matendo au tabia za chakula,” yeye asema. “Kufahamu njia mpya za kukabili na kutatua mahitilafiano pamoja na wengine kulitokeza fursa za uhusiano wa karibu pamoja na marafiki na familia.”
Kwa wazi, ni vigumu kupata nafuu kutokana na tatizo la kula, lakini jitihada zilizofanywa mwishowe zinafaidi. Ndivyo Jean, aliyenukuliwa katika makala ya kwanza ya mfululizo huu, aaminivyo. “Kurudia kula kusiko na utaratibu,” asema, “kungekuwa sawa na kurudi kwenye chumba cha wagonjwa wa akili baada ya kuishi ukiwa huru kwa muda fulani.”
[Maelezo ya Chini]
a Amkeni! haliungi mkono matibabu yoyote hususa. Wakristo wanapaswa kufanya uamuzi wao wenyewe wakihakikisha kwamba matibabu yoyote wanayopata hayahitilafiani na kanuni za Biblia. Wengine hawapaswi kuchambua au kuhukumu maamuzi hayo.
b Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kusaidia watu wasiokuwa na hamu ya chakula na wenye hamu ya chakula isiyo ya kawaida, ona makala “Kusaidia Wenye Matatizo ya Kula,” katika toleo la Amkeni! la Februari 22, 1992, la Kiingereza, na mfululizo “Matatizo ya Kula—Ni Nini Kinachoweza Kufanywa?,” katika toleo la Desemba 22, 1990, la Kiingereza.
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Kuweka Msingi wa Kupona
UNAPASWA kufanya nini unaposhuku kwamba binti yako ana tatizo la kula? Bila shaka, huwezi kupuuza hali hiyo. Lakini utaanzishaje mazungumzo hayo? “Nyakati nyingine kumwuliza moja kwa moja hufanya kazi, lakini mara nyingi hutokeza hisia za mfadhaiko kwa sababu ya yeye kukosa kujibu,” asema mwandishi Michael Riera.
Kwa sababu hii, mfikio wenye upole waweza kuwa wenye matokeo zaidi. “Unapozungumza na binti yako,” apendekeza Riera, “anahitaji kuelewa na kuhisi kwamba haumshtaki kwa kosa lolote. Ikiwa unaweza kutokeza hali ya namna hii, vijana wengi watakuwa wanyofu kuzungumza nawe, hata watahisi wametulizwa kwa njia fulani. Wazazi fulani wamefanikiwa kuwaandikia barua vijana wao wakiwaeleza hangaiko na utegemezo wao. Kisha, wanapokuwa na maongezi, tayari msingi unakuwa umewekwa.”
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
Ugumu kwa Wazazi
KUWA na mtoto mwenye tatizo la kula hutokeza magumu mengi kwa wazazi. “Lazima mzazi awe thabiti na mwenye kudhamiria ikiwa mtoto atasaidiwa,” asema baba mmoja. “Unamwona mtoto wako akiharibiwa machoni pako.”
Ikiwa una mtoto mwenye tatizo la kula, inatazamiwa tu kwamba nyakati nyingine utafadhaishwa na tabia yake ya ukaidi. Lakini uwe mwenye saburi. Usiache kuonyesha upendo. Emily, ambaye binti yake alikuwa na tatizo la kujinyima chakula, akiri kwamba sikuzote jambo hili halikuwa rahisi. Hata hivyo, asema: “Sikuzote nilijaribu kuendelea kumgusa; nilijaribu kumkumbatia; nilijaribu kumbusu. . . . Nilifikiri ikiwa nitaacha kumwonyesha shauku na kuacha kumwonyesha upendo, hatutakuwa na uhusiano mzuri wa familia tena.”
Mojawapo njia bora ya kusaidia mtoto wako apone kutokana na tatizo la kula ni kuwasiliana naye. Katika kufanya hivyo, huenda ukahitaji kumsikiliza zaidi kuliko kuongea. Na ujizuie usimkatishe kwa kumwambia “Hiyo si kweli” au, “Hupaswi kuhisi namna hiyo.” Kwa kweli, ‘usizibe masikio yako usisikie kilio cha maskini.’ (Mithali 21:13) Kunapokuwa na mazungumzo yaliyo wazi, kijana atakuwa na mahali pa kupata msaada nyakati za taabu na huenda asielekee kuishia kwa mazoea ya kula yasiyofaa.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Inahitaji saburi, uelewevu, na upendo mwingi sana kusaidia wenye matatizo ya kula