Ulemavu Wote Utakapotoweka
WAKATI mmoja mwanamke aliyepooza miguu na mikono alisema kwamba watu wengi ni “wenye afya nzuri kwa muda mfupi tu.” Huo ni ukweli ulioje, kwa kuwa matatizo ya kimwili yanaweza kutupata sote hivi karibuni au baadaye! Hivyo, watu wengi wananunua miwani, lenzi zinazoambatanishwa na mboni ya jicho, meno bandia, vifaa vya kusaidia kusikia, vifaa vya elektroni vya kurekebisha mpigo wa moyo, na kupandikiziwa magoti. Hilo linapatana na Waroma 8:22 linalosema, “viumbe vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja hadi sasa.”
Kwa hiyo, sote tunaweza kufarijiwa na ahadi ya Mungu ya kuwarejeshea wanadamu watiifu afya kamili ya kimwili katika “dunia mpya” yenye uadilifu. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Andiko la Isaya 35:5, 6 husema hivi: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. . . . Mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”
Biblia hutabiri kwamba “umati mkubwa” utaokoka uharibifu wa mfumo huu mwovu wa mambo. (Ufunuo 7:9, 14; Zaburi 37:10, 11, 29) Hapana shaka kwamba mara baada ya uharibifu huo, wale wenye matatizo makubwa ya ulemavu na ya kiafya wataponywa mara moja udhaifu wao! (Isaya 33:24) Yesu alionyesha kimbele maponyo yatakayofanywa katika dunia mpya ya Mungu kwa kuponya magonjwa yayo hayo alipokuwa duniani. (Linganisha Marko 5:25-29; 7:33-35.) Mtu hawezi hata kueleza furaha ambayo watu watakuwa nayo na machozi ya shangwe watakayotoa wakati watu waliokatwa viungo vya mwili watakapotupilia mbali viungo vyao bandia, mikongojo, na viti vya magurudumu! Wakiwa na afya nzuri ya kimwili, ndipo watakapoweza kutimiza mgawo waliopewa na Mungu wa kugeuza dunia kuwa makao ya paradiso.—Luka 23:43.
Kwa wakati huu, watu walemavu leo bado wanahitaji kupambana na udhaifu wao. Nelson, mtu mlemavu aliye Kanada, asema hivi: “Ninapojisikitikia, mimi hufikiria maneno ya Yesu katika Mathayo 24:13: ‘Yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.’” Licha ya udhaifu wao, watu walemavu wanaweza kuwa kamili na timamu katika njia ya maana zaidi—kiroho—kwa kuvumilia katika imani ya Kikristo.—Yakobo 1:3, 4.
Mashahidi wa Yehova wamesaidia mamilioni ya watu kuikubali imani hii. Dell, mlemavu aliyenukuliwa katika makala iliyotangulia, asema hivi: “Hata sijui jinsi ninavyoweza kueleza nilivyohisi nilipojifunza kwamba matatizo ya kimwili kama yangu kwa kweli ni ya muda tu.” Naam, akiwa ametiwa nguvu na tumaini hilo, Dell—na wengine wengi ambao ni walemavu kama yeye—hawawezi kwa kweli kuitwa walemavu.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Watakaookoka uharibifu unaokuja watafurahia kuponywa kimwujiza udhaifu wao