Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 6/22 kur. 20-25
  • Mungu Amekuwa Msaidiaji Wetu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mungu Amekuwa Msaidiaji Wetu
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Malezi ya Kidini
  • Kujifunza na Kutumia Kweli
  • Kuhubiri kwa Njia za Werevu
  • Wakati wa Mtihani Mkali
  • Maisha Katika Kambi
  • Namna Tulivyohubiri
  • Kuachiliwa, na Kurudi Maputo
  • Kusawazisha Madaraka
  • Twaendelea Kupokea Baraka Kutoka kwa Mungu
  • Wakosa Kuvumiliwa Kwa Mara Nyingine
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Kumtumikia Yehova Katika Majira Yenye Kupendeleka na Katika Yenye Matata
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Uhuru wa Ibada Msumbiji Wamalizwa Kikatili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Yehova Hutujali Sikuzote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 6/22 kur. 20-25

Mungu Amekuwa Msaidiaji Wetu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA FRANCISCO COANA

“Ukikataa kutii wenye mamlaka, utafishwa!” ndugu yangu akatoa onyo.

“Hiyo ingekuwa bora kuliko kuishi chini ya hali hizi za kutisha,” nikateta.

HAYO yalikuwa mazungumzo kati yangu na kaka yangu katika Septemba 1975. Alikuwa amekuja kuniletea chakula wakati wa kifungo changu katika Maputo (wakati huo iliitwa Lourenço Marques), kusini mwa Msumbiji. Zaidi ya 180 kati yetu, wengi wao wakiwa Mashahidi wa Yehova, walifinyana ndani ya seli moja. Ndugu yangu aliudhika sana nami hivi kwamba hakuniachia chakula alicholeta!

Ili kukusaidia uelewe kukutana huku kulikojaa hisia, acha nirudi nyuma na kueleza jinsi nilivyojikuta gerezani.

Malezi ya Kidini

Nilizaliwa mwaka wa 1955 katika familia ya Kipresibiteri katika kijiji cha Calanga Wilayani Manica. Si mbali sana na jiji kubwa la Maputo. Ijapokuwa Baba hakuwa akienda kanisani, Mama alikuwa akienda, na angeandamana na watoto wake watano kanisani siku za Jumapili. Mapema maishani mwetu, alitufundisha Sala ya Bwana, na ningeikariri mara nyingi. (Mathayo 6:9-12) Nikiwa mvulana mchanga, nilimwuliza Mama maswali kama vile “Kwa nini sisi hufa?” na, “Je, watu watalazimika kufa sikuzote?”

Mama alisema kwamba kifo kilikuwa sehemu ya kusudi la Mungu—kwamba wale wanaotenda mabaya wataenda helo na wale wanaotenda mema wataenda mbinguni. Ijapokuwa sikumjibu lolote, jibu lake lilinihuzunisha. Ukweli mchungu kuhusu kifo ulinisumbua, hasa baada ya baba yetu mpendwa kufa nilipokuwa na umri wa miaka kumi tu. Baadaye nilitamani sana kujua hali ya wafu na kama wana tumaini lolote.

Kujifunza na Kutumia Kweli

Muda mfupi baada ya kifo cha Baba yangu, mmoja wa walimu shuleni alitumia kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Hadi Paradiso Iliyopatikana kufundisha darasa letu. Kitabu hicho, kilichochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society, kilikuwa cha lugha ya Kizulu, ya Afrika Kusini. Mwalimu alikubali nikiazime, na ijapokuwa sikujua vizuri lugha ya Kizulu, nilifurahishwa na niliyojifunza kutoka kwa maandiko ya Biblia yaliyotajwa.

Nilipokuwa na umri wa miaka 16, ndugu yangu ambaye alikuwa mleta-riziki katika familia aliitwa kwenye utumishi wa kijeshi. Huo ndio wakati ambao nilianza kufanya kazi kwenye kampuni ya marashi katika Maputo na kuhudhuria shule ya kiufundi usiku. Wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana kazini, nilimwona Teófilo Chiulele, mmoja wa Mashahidi wa Yehova—sikuzote alikuwa akisoma Biblia. Teófilo alipoona ninapendezwa, alianza kuzungumza nami.

Baadaye, Shahidi mwingine, Luis Bila, alianza kuongoza funzo la Biblia pamoja nami. Nilitulizwa kujua kwamba wafu hawajui jambo lolote na kwamba wana tumaini la kurudishwa tena kwenye uhai kupitia ufufuo. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 5:28, 29) Nilimwandikia Mama barua mara moja na kumweleza majibu ya Biblia ya maswali niliyokuwa nimemwuliza. Alifurahi kujua kwamba hatimaye nilipata majibu yenye kutegemeka.

Nikiwa nimechochewa na shauku ya yale niliyokuwa nikijifunza, nilijitayarisha kushiriki mambo hayo na wengine. Niliruhusiwa kutoa hotuba za Biblia shuleni lakini si kanisani. Punde si punde sikukaribishwa tena kanisani. Hata washiriki wa familia yangu walianza kuninyanyasa, licha ya kwamba Mama alipendezwa na itikadi zangu mpya. Kaka yangu alinipiga vibaya sana. Upinzani huo ulipokosa kufua dafu, washiriki wa familia yangu walianza kunidhihaki, hasa waliponiona nikitoa sala wakati wa chakula. Hivyo ningetoa sala nikiwa ndani ya bafu kabla sijaja mezani kula. Nilihisi kwamba ‘Mungu alikuwa msaidiaji wangu.’—Zaburi 54:4, NW.

Kisha Luis alizuiwa kuja nyumbani kwetu kujifunza Biblia pamoja nami. Baada ya hapo, tulijifunzia nyumbani kwake. Nilipoanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki kazi ya kuhubiri, ningejikuta nimefungiwa nje baada ya kurudi nyumbani. Kama tokeo, niliishia kulala katika nyumba za Mashahidi mbalimbali.

Hatimaye, katika Mei 13, 1973, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kupitia ubatizo wa maji. Wakati huo, Msumbiji ilikuwa chini ya utawala wa kikoloni wa serikali ya Ureno, iliyokuwa imewapiga marufuku Mashahidi wa Yehova katika Ureno na kwenye koloni zake zote. Katika Oktoba 1, 1974, nikawa painia, kama waeneza-evanjeli wa wakati wote waitwavyo na Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa nilikuwa na mradi wa kuwa mishonari, nilianza kujifunza Kiingereza kusudi niweze kustahili kuhudhuria Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, Marekani, ili kuzoezwa kazi ya umishonari.

Kuhubiri kwa Njia za Werevu

Katika miaka hiyo ya marufuku, polisi wa wakoloni Wareno, PIDE, waliwatia gerezani Mashahidi wengi kwa ajili ya kuhubiri. Hivyo ili tusigunduliwe tulitumia njia za werevu. Kwa mfano, tungehubiri katika nyumba moja na kisha kwenda kwa nyingine katika eneo tofauti. Pia, wawili kati yetu wangeenda kwenye bustani ya jiji wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana au jioni. Mmoja angeketi karibu na mtu fulani na kuanza kusoma gazeti la habari. Upesi, yule mwingine angeketi chini, angetazama gazeti la habari, na kusema jambo kama hili: “Lo, ebu ona jinsi watu wengi walivyokufa! Lakini je, ulijua kwamba chini ya serikali ya Mungu mambo haya hayatatokea tena?”

Mazungumzo yangefuatia ambapo yule aliyekuwa akisoma gazeti la habari angeomba athibitishiwe katika Biblia mambo ambayo yule mwingine alikuwa amesema. Kisha tungepanga kukutana siku itakayofuata ili kuendeleza mazungumzo. Kwa njia hii mara nyingi tuliweza kuhusisha mtu aliyeketi karibu nasi katika mazungumzo yetu kuhusu unabii wa Biblia, na mafunzo mengi ya Biblia yalianzishwa. Tungemshukuru Mungu kwa kutusaidia.

Wakati wa Mtihani Mkali

Katika Aprili 25, 1974, udikteta katika Ureno ulikoma, na kukatokea mabadiliko mengi sana ya kisiasa katika koloni za Wareno. Katika Msumbiji, wafungwa wa kisiasa, vilevile Mashahidi waliokuwa wamefungwa kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo katika mambo ya kisiasa, walisamehewa. Lakini, katika Juni 25, 1975, miezi 14 tu baadaye, Msumbiji ilipata uhuru kutoka kwa Ureno. Siku chache baadaye, kukatokea wimbi jipya la mnyanyaso dhidi ya Mashahidi. Vikundi vya ujirani vilitumwa kuwakamata Mashahidi wote ambao wangeweza kupatikana. Tulionwa kuwa “wawakilishi waliobakia wa Ukoloni wa Wareno.”

Katika Septemba, nililazimishwa kuhudhuria mkutano wa kikundi jirani. Nilipowasili, niliona kwamba wote waliokuwa katika kikundi changu cha kujifunza Biblia walikuwako. Tuliamrishwa tuseme kwa sauti kubwa shime za kisiasa zilizotukuza chama kinachotawala. Tulipokataa kwa heshima, tulipelekwa gerezani na kuwekwa ndani ya seli iliyojaa watu wengi niliyoitaja mwanzoni.

Seli hiyo ilikuwa na watu wengi sana hivi kwamba hatungeweza kusonga kwa urahisi. Ili wachache wapate nafasi ya kulala sakafuni, wengine walihitaji kuketi au kusimama. Kulikuwa na choo kimoja tu, na mara nyingi kilikuwa kimeziba, hivi kwamba uchafu ungeelea juu, na kutokeza uvundo mbaya sana. Chakula chetu kilikuwa spageti zenye mafuta mengi zilizojaa mifupa ya samaki na nzi wakubwa, na ambazo tulilazimika kuzila bila kunawa mikono. Kwa siku 19, tukiwa zaidi ya 180 tulivumilia hali hizi zilizokuwa mbaya sana. Kisha tulihamishwa hadi mahali ambapo ni Mashahidi pekee waliokuwa wamefungiwa, kutia ndani wanaume, wanawake, na watoto. Katika miezi michache iliyofuata, watoto wengi walikufa kwa sababu ya hali mbaya gerezani.

Hatimaye, serikali iliamua kuwafukuza Mashahidi hadi Carico, eneo lililo mbali upande wa kaskazini. Lengo lilikuwa kututenga na wengine. Wakati huo kulikuwa na Mashahidi takriban 7,000 katika Msumbiji, asilimia kubwa walikuwa wamebatizwa katika 1974 na 1975. Nikitambua kwamba tungehitaji fasihi za Biblia katika kipindi cha kutenganishwa, nilipata idhini ya kurudi nyumbani kuchukua chakula na vitu kadhaa kwa ajili ya safari. Pasipo kuonwa na ofisa aliyeandamana nami, nilitoa biskuti kiasi fulani katika masanduku na kupakia fasihi za Biblia kwenye sehemu ya chini ya masanduku hayo. Katika nyakati hizo, hatukuogopa. Tulimtumaini Mungu atusaidie.—Waebrania 13:6.

Maisha Katika Kambi

Tuliwasili Carico katika Januari 1976 na kupata Mashahidi wengi kutoka nchi jirani ya Malawi wakiishi katika kambi walizokuwa wamejenga. Kutoka mwaka wa 1972 hadi 1975, watu zaidi ya 30,000, kutia ndani watoto, walikuwa wametoroka mnyanyaso wa kidini uliokuwa wa kinyama katika Malawi. Waliruhusiwa kuingia kaskazini mwa Msumbiji kama wakimbizi, na tulipowasili, walitualika kuishi nao katika nyumba zao na kushiriki vitu vichache walivyokuwa navyo.

Kwa kuwa wengi wetu hatukuwa na ujuzi wa kujenga, ndugu zetu wa Malawi walituonyesha jinsi ya kujenga nyumba kwa kutengeneza matofali na kuyatumia pamoja na mimea kutoka kichakani. Pia walitufundisha jinsi ya kukuza chakula na kufanya mambo mengine ya kujiendeleza wenyewe. Hivyo nikajifunza useremala, kilimo, na kushona nguo. Ufundi huo tuliopata ulikuja kufaidi wengi wetu tuliporudi kwenye majiji yetu ya asili.

Hangaiko letu kuu lilikuwa kudumisha hali ya kiroho, na ni kweli kwamba hatukukosa chakula cha kiroho. Jambo hilo liliwezekanaje? Naam, kama ilivyotajwa mwanzoni, tulipopelekwa uhamishoni, wengi wetu tulitumia ubunifu wetu kuleta fasihi za Biblia pamoja na vitu vinginevyo. Pia, nakala ndogo sana za Mnara wa Mlinzi zilichapishwa na Mashahidi wa Yehova katika Afrika Kusini. Hii ilifanya iwe rahisi kuziingiza kwenye kambi.

Baada ya maombi mengi, katika Desemba 1, 1978, ndoa ya kwanza iliruhusiwa ndani ya kambi. Siku hiyo nilimwoa Alita Chilaule, ambaye baba yake alikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kubatizwa katika Maputo huko nyuma mwaka wa 1958. Watoto wetu wawili walipozaliwa, Dorcas na Samuel, tuliwafundisha kumpenda Yehova, na tulienda nao kwa ukawaida kwenye mikutano ya Kikristo. Baadaye, tulipata mtoto mwingine, anayeitwa Jaimito.

Namna Tulivyohubiri

Mashahidi walipewa ruhusa ya kuondoka kwenye kambi ili kuuza vitu, kutia ndani chakula walichokuwa wamekuza. Wengi wetu tulitumia fursa hii kuhubiri. Kwa hakika, niliweka bei ya chumvi kuwa ya juu sana kimakusudi ili mtu yeyote asiweze kuinunua. Hata hivyo, watu wengi niliokutana nao waliitikia ujumbe wa Ufalme, na nikaanza mafunzo ya Biblia kadhaa.

Mmoja wa wanafunzi wangu wa Biblia alizungumza na mkurugenzi wa kampuni fulani iliyo karibu na Milange aliyeonyesha upendezi katika Biblia. Nilipoarifiwa kuhusu jambo hilo, niliwasiliana na mkurugenzi huyo. Aliitikia kwa kunialika nimzuru. Hivyo nilificha fasihi za Biblia na kuanza safari, ikionekana kana kwamba ninaenda kumuuzia fanicha fulani nilizokuwa nimetengeneza.

Nilipowasili, nilipata nyumba inalindwa na askari-jeshi; nikaingiwa na hofu. Hata hivyo, mtu huyo alitoka na kuwaambia askari-jeshi kwamba hakutaka kusumbuliwa. Tulianza funzo letu la Biblia saa 11 jioni, na alipendezwa sana hivi kwamba hatukumaliza mpaka saa 11 asubuhi iliyofuata! Baadaye, alikubali kupokea fasihi zetu kutoka Ureno, kwa kuwa barua zake hazikuwa zimewekewa kizuizi chochote. Kisha angenipa fasihi hizo, na ningezipeleka kwenye kambi.

Kweli, baadhi yetu tulitiwa mbaroni na kukamatwa mara kadhaa kwa sababu ya utendaji wetu wa kuhubiri. Lakini, wengi walipoitikia ujumbe wa Ufalme, tulikuwa na hakika kwamba Mungu alikuwa anatusaidia, kama alivyowasaidia Wakristo wa karne ya kwanza.—Matendo, sura ya 3 hadi 5.

Kuachiliwa, na Kurudi Maputo

Katika Septemba 1985, baada ya kufikiria hali kwa sala iliamuliwa kwamba tungepanga kuondoka kwenye kambi katika kikundi kikubwa. Ijapokuwa wengine walibaki katika kambi za Carico na kujitenga na Mashahidi wa Yehova wengineo kwa miaka saba iliyofuata, wengine walitorokea Malawi na Zambia. Mimi na mke wangu tuliamua kwenda pamoja na watoto wetu kwenye mji ulio karibu wa Milange. Niliajiriwa kazi huko na kupata mahali pa kuishi, na tukaendelea na huduma yetu. Mwaka uliofuata tulirudi Maputo hatimaye.

Hapo kwanza tuliishi pamoja na watu wa jamaa. Ilikuwa vigumu kupata kazi ya kuajiriwa, lakini baada ya muda nilifaulu kupata kazi. Alita aliuza njugu karanga zilizochomwa ili kuongezea mapato yetu ya chini. Kwa kuwa nilikuwa nimeboresha Kiingereza changu, nilitoa ombi la kazi kwa Ubalozi wa Uingereza. Nilifuzu mitihani hiyo na kuajiriwa kazi iliyonipa mshahara mara 20 zaidi ya nilivyokuwa nikipokea awali! Nilihisi kwamba Yehova alikuwa amenisaidia kwelikweli, na nikamshukuru kwa sala.

Kusawazisha Madaraka

Hatimaye, katika Februari 11, 1991, serikali ya Msumbiji iliwapa Mashahidi wa Yehova utambuzi wa kisheria. Ilikuwa tarehe tuliyoikumbuka kama nini! Mwaka uliofuata nilialikwa nitumikie nikiwa mshiriki wa halmashauri ya kusimamia kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova katika Msumbiji. Wakati huo, watoto wetu walikuwa na umri wa miaka 12, 9, na 6 tu. Nilisali usiku kucha nikimwomba Yehova anipe hekima ya kufanya maamuzi yaliyosawazika katika kushughulikia madaraka ya familia na ya kitengenezo.

Tuliweza kujipatia trela ndogo, tuliyoitumia kufanyia biashara. Tuliajiri mapainia kadhaa kupika na kuuza sandwichi, na biashara ikafana. Hivyo, nilikuwa na wakati wa kutunza mapendeleo mapya ya kitengenezo. Pia tulihitaji nyumba, kwa kuwa haikuwezekana kuendelea kukodi nyumba tuliyokuwa tukiishi. Hivyo nilitoa ombi kwa wenye mamlaka nikiwaeleza hali ya familia yangu. Punde si punde tukapata kibali cha kununua nyumba. Jambo hilo lilitangazwa sana na vyombo vya habari kwa kuwa nilikuwa mkazi wa kwanza wa Msumbiji kununua nyumba kutoka kwa serikali.

Mimi na Alita tumebarikiwa kuwa na watoto waliokubali kufuata programu ya maagizo ya kiroho. (Kumbukumbu la Torati 6:6-9) Tumekuwa na zoea la kuzungumzia andiko la Biblia la siku saa 11:40 asubuhi, kisha kusoma Biblia pamoja baada ya hapo. Kwa kuwa watoto wetu wanahitaji kwenda shuleni mapema, wamezoea ratiba hii ya mapema. Ijumaa saa 12:00 jioni, tunafanya funzo la familia, ambapo watoto huzungumza pamoja nasi juu ya habari kadhaa za Biblia ambazo wamefanyia utafiti katika juma. Wakati huo pia sisi hujizoeza utoaji kwa ajili ya huduma.

Watoto wetu wote wamebatizwa. Kwa hakika, Dorcas na Samuel wamekuwa wakitumikia wakiwa mapainia tangu 1994, na tangu Jaimito abatizwe, amekuwa akifanya upainia msaidizi. Watoto hawa wangali shuleni, na kila mmoja wao ana mradi wa kupanua utumishi wake baadaye. Alita ana usawaziko kwa kutumia wakati wake kufanya upainia na kushughulikia kazi za nyumbani. Nilitumikia nikiwa painia kwa miaka mingi kutia ndani miaka nilipokuwa kwenye kambi za vizuizi. Hata hivyo, tangu mwaka wa 1993, nimekuwa nikifanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova wakati wa mchana.

Twaendelea Kupokea Baraka Kutoka kwa Mungu

Mnamo 1997, nilipokea baraka kubwa sana ya kuhudhuria mtaala wa miezi miwili wa washiriki wa Halmashauri ya Tawi. Mtaala huo ulifanyiwa Marekani kwenye Kitovu cha Kielimu cha Watchtower, Patterson, New York. Hivyo, jitihada zangu za kujifunza Kiingereza zilithawabishwa kwa mara nyingine tena. Nikiwa njiani kuelekea nyumbani, niliweza kuzuru watumishi wa Yehova katika nchi nyinginezo, na jambo hili lilifanya moyo wangu ujawe na uthamini kwa udugu wetu wa ulimwenguni pote kama nini!

Upendo huu miongoni mwa Wakristo wa kweli umekuwa jambo linalochangia kuvutia maelfu zaidi ya watu wenye moyo mweupe kushirikiana na Mashahidi wa Yehova katika Msumbiji. (Yohana 13:35) Kutoka watu wapatao 7,000 waliokuwa wakihubiri tulipokuwa tumefukuzwa hadi kwenye kambi za vizuizi, sasa tuna zaidi ya 29,000 wanaohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu Msumbiji kote. Hawa wanashirikiana na makutaniko zaidi ya 665; ni 4 tu yaliyokuwako mwaka wa 1958.

Mnamo 1993, plani zilikubaliwa za ofisi ya tawi katika Maputo ambayo ingekuwa na wafanyakazi wa tawi zaidi ya 75 na kushughulikia mpanuko huo wa ajabu wa ibada safi katika Msumbiji. Baada ya ujenzi uliochukua muda wa miaka minne hivi, mradi huo ulikamilika. Kisha, katika Desemba 19, 1998, tulikuwa na shangwe isiyo na kikomo kuwa na watu 1,098 kutoka nchi nyingi kwa ajili ya kuwekwa wakfu kwa majengo haya mazuri. Katika programu hiyo, nilikuwa na pendeleo la kuhoji watu walioishi miaka kadhaa uhamishoni katika Carico. Niliomba wale waliopelekwa uhamishoni wainue mikono yao, wahudhuriaji wakachochewa hisia kwelikweli walipoona mamia ya mikono ikiinuliwa.

Siku iliyofuata, umati wa watu 8,525 walikuwako kwenye Jumba la Mkusanyiko la Matola kusikiliza kurudiwa kwa programu ya wakfu, ripoti zenye kutia moyo kutoka nchi nyinginezo, na hotuba za Biblia zilizotolewa na wageni kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, Brooklyn, New York.

Kweli, tangu nilipojua kweli ya Biblia nikiwa kijana, nimepata upinzani kutoka kwa familia, vitisho vya kufishwa, na mnyanyaso mbaya sana ambao wakati fulani ulinifanya nifikiri kwamba ni afadhali kufa kuliko kuendelea kuishi. Lakini, ninashangilia kwa sababu uhusiano wangu na Yehova umekamilishwa na mambo yaliyonipata. Kwa kweli, kama alivyosema mtunga-zaburi wa Biblia, “Mungu ndiye anayenisaidia; Bwana ndiye anayenitegemeza nafsi yangu.” (Zaburi 54:4) Limekuwa pendeleo lisilo na kifani kwangu na kwa familia yangu kutumikia Yehova pamoja na familia ya ulimwenguni pote ya waabudu wake.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mashahidi wakiwa mbele ya Jumba la Ufalme lililojengwa walipokuwa wametengwa na wengine

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kufurahia funzo la Biblia la familia yetu

[Picha katika ukurasa wa 25]

Wale waliokuwa kwenye kambi za Carico waliinua mikono yao

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki