Kutafuta Mambo Yaliyokusudiwa Kimbele ya Mwanadamu
KWA nini itikadi ya kwamba maisha yameamuliwa kimbele imeenea sana? Katika enzi zote, mwanadamu amejaribu kutatua fumbo la maisha na kutafuta kusudi la matukio yanayotukia. “Ni katika jitihada hizo kwamba wazo la ‘mungu’, ‘tukio lililopangwa lisiloepukika’, na ‘nasibu’ huibuka, ikitegemea iwapo matukio hayo yamesababishwa na mtu fulani, na asili, au bila asili,” aeleza mwanahistoria Helmer Ringgren. Historia imejaa itikadi, hekaya, na ngano chungu nzima zinazohusu kuamuliwa kimbele kwa maisha na tukio lililopangwa lisiloepukika.
Mtaalamu wa historia ya Ashuru Jean Bottéro asema: “Kwa ujumla hali yetu ya maisha huathiriwa sana na ustaarabu wa Mesopotamia,” aongezea kwamba ni katika Mesopotamia ya kale au Babilonia tunakopata “maitikio na mawazo ya kale zaidi yaliyo wazi ya mwanadamu juu ya nguvu zinazozidi zile za kibinadamu, na mfumo wa kidini wa kale zaidi unaoweza kutambuliwa.” Ni hapa pia tunapopata vyanzo vya itikadi ya kwamba maisha yameamuliwa kimbele.
Vyanzo vya Kale vya Itikadi ya Kwamba Maisha Yameamuliwa Kimbele
Katika magofu ya kale ya Mesopotamia, katika Iraki ya sasa, waakiolojia wamegundua baadhi ya maandishi ya kale zaidi kuwahi kupatikana. Maelfu ya mabamba ya kikabari hutuonyesha waziwazi jinsi maisha yalivyokuwa katika ustaarabu wa kale wa Sumer na Akkad katika jiji mashuhuri la Babiloni. Kulingana na mwakiolojia Samuel N. Kramer, wakazi wa Sumer “walihangaishwa na tatizo la kuteseka kwa binadamu, hasa visababishi vyake vya kifumbo.” Jitihada zao za kutafuta majibu ziliwaongoza kwa wazo la kuamuliwa kimbele kwa maisha.
Katika kitabu chake Babylon, mwakiolojia Joan Oates asema kwamba “kila Mbabiloni alikuwa na mungu au mungu-mke wake binafsi.” Wababiloni waliamini kwamba miungu “iliamua kimbele wakati ujao wa kila mwanadamu, akiwa mtu mmoja-mmoja na wa watu wote kwa ujumla.” Kulingana na Kramer, wakazi wa Sumer waliamini kwamba “miungu inayodhibiti ulimwengu ilipanga na kutekeleza uovu, uwongo, na jeuri ikiwa sehemu muhimu ya ustaarabu.” Itikadi juu ya kuamuliwa kimbele kwa maisha ilienea sana na kuthaminiwa sana.
Wababiloni walidhani kwamba iliwezekana kujua mipango ya miungu kupitia uaguzi—“njia ya kuwasiliana na miungu.” Uaguzi ulihusisha kujaribu kutabiri mambo ya wakati ujao kwa kuchunguza, kufumbua, na kufasiri habari na matukio. Kwa kawaida, ndoto, tabia ya wanyama, na matumbo yalichunguzwa. (Linganisha Ezekieli 21:21; Danieli 2:1-4.) Matukio yasiyotazamiwa au yasiyo ya kawaida yaliyoonwa kuwa yalifunua mambo ya wakati ujao yalirekodiwa kwenye mabamba ya udongo.
Kulingana na msomi Mfaransa wa staarabu za kale Édouard Dhorme, “tunapochunguza historia ya kale ya Mesopotamia, tunapata mtabiri na wazo la uaguzi.” Uaguzi ulikuwa sehemu muhimu ya maisha. Kwa kweli, Profesa Bottéro asema kwamba “ilionekana kuwa kila kitu kingechunguzwa ili kupata habari za uaguzi . . . Ulimwengu wote mzima ulionwa kuwa chombo ambacho kingefunua habari za wakati ujao baada ya kuchunguzwa kwa uangalifu.” Hivyo Wamesopotamia walizoea sana unajimu ili kutabiri mambo ya wakati ujao.—Linganisha Isaya 47:13.
Kwa kuongezea, Wababiloni walitumia dadu au kupiga kura katika uaguzi. Katika kitabu chake Randomness, Deborah Bennett aeleza kwamba vitu hivi “viliondoa uwezekano wa kuelekezwa na mwanadamu na hivyo kuiruhusu miungu iamue mambo bila kuvurugwa.” Hata hivyo, uamuzi wa miungu haukuonwa kuwa usioweza kubadilika. Msaada wa kuepuka mabaya uliweza kupatikana kwa kusihi miungu.
Kuamuliwa Kimbele kwa Maisha Katika Misri ya Kale
Katika karne ya 15 K.W.K., jiji la Babilonia lilishirikiana sana na Misri. Mazoea ya kidini yaliyohusiana na kuamuliwa kimbele kwa maisha pia kulipitishwa pamoja na tamaduni nyingine. Kwa nini Wamisri wakakubali kuitikadi kuamuliwa kimbele kwa maisha? Kulingana na John R. Baines, profesa wa Elimu ya Historia ya Misri katika Chuo Kikuu cha Oxford, “dini nyingi za [Kimisri] zilijishughulisha na jitihada za kujaribu kufahamu na kuitikia mambo na matukio yasiyojulikana.”
Kati ya miungu mingi ya Misri, Isis alielezwa kuwa “mwanamke anayedhibiti uhai, kiongozi wa kuamulia watu maisha kimbele na mambo yatakayopata watu.” Wamisri walizoea pia uaguzi na unajimu. (Linganisha Isaya 19:3.) Mwanahistoria mmoja asema: “Mbinu zao za kuifikia miungu hazikuwa na mpaka.” Ingawa hivyo, Misri haikuwa ustaarabu wa pekee ulioiga wazo la kuamuliwa kimbele kwa maisha kutoka kwa Babiloni.
Ugiriki na Roma
Inapohusu mambo ya kidini, “Ugiriki ya kale haikukosa kuathiriwa na uvutano mkubwa wa Babilonia,” asema Jean Bottéro. Profesa Peter Green aeleza kwa nini itikadi ya tukio lililopangwa lisiloepukika ilipendwa na wengi katika Ugiriki: “Katika ulimwengu usiotumainika, ambamo watu walihofia sana matokeo ya maamuzi yao wenyewe, na mara nyingi wakajihisi wakiwa watumwa tu, wakielekezwa huku na huku na uhitaji wa kufuata yaliyoamuliwa maishani mwao ambayo yalikuwa ya kifumbo na yasiyobadilika, amri ya miungu ilikuwa njia mojawapo ambayo wakati ujao wa mtu uliweza kupangwa. Mambo yaliyoamuliwa kimbele yangeweza kutabiriwa kwa kutumia ujuzi wa pekee au maono. Huenda ikawa habari asiyopenda kusikia; lakini angalau akiwa ameonywa kimbele angeweza kujitayarisha.”
Mbali na kuwahakikishia watu juu ya wakati ujao, kuitikadi kwamba maisha yameamuliwa kimbele kulitumiwa pia kwa makusudi mengine mabaya. Wazo la kuamuliwa kimbele kwa maisha lilisaidia kutiisha umma, na kwa sababu hiyo, kulingana na mwanahistoria F. H. Sandbach, “itikadi ya kwamba ulimwengu mzima ulitawalwa na Uongozi wa Kimungu ungewavutia jamii ya watawala.”
Kwa nini? Profesa Green aeleza kwamba itikadi hii “ilitetea haki ya—kiadili, kitheolojia, na umaana—wa mfumo wa kijamii na wa kisiasa: ilikuwa mbinu yenye uwezo na hila ya kujifaidi iliyowahi kubuniwa na watawala wa Ugiriki. Uhakika wa kwamba jambo lolote laweza kutukia ulimaanisha kwamba ilikuwa imeamuliwa litukie; na kwa kuwa maumbile yalikuwa na mwelekeo unaofaa kwa wanadamu, jambo lililoamuliwa ni lazima liwe lilifaa.” Kwa kweli, lilitokeza “uteteaji wa haki za kibinafsi zenye ukatili.”
Jambo la kwamba wengi waliamini maisha yameamuliwa kimbele linadhihirishwa na fasihi za Kigiriki. Baadhi ya mitindo ya fasihi za kale iliyokuwapo ni mashairi marefu, hekaya, na tanzia—iliyokazia sana kuamuliwa kimbele kwa maisha. Kulingana na ngano za Kigiriki, mwisho wa mwanadamu uliwakilishwa na miungu ya kike mitatu iliyoitwa Moirai. Klotho alisokota uzi wa uhai, Lakesisi aliamua urefu wa maisha, na Atropo aliukata muda wa uhai ulipokwisha. Waroma walikuwa pia na miungu mitatu kama hiyo waliyoiita Parcae.
Waroma na Wagiriki walikuwa na hamu ya kujua tukio lisiloepukika ambalo lilidhaniwa kuwa lingewapata mwishowe. Hivyo, waliiga na kuendeleza zaidi unajimu na uaguzi wa Babiloni. Waroma waliyaita matukio yaliyotumiwa kutabiri wakati ujao portenta, au ishara. Jumbe ambazo zilitolewa na ishara hizi ziliitwa omina. Kufikia karne ya tatu K.W.K., unajimu ulipendwa sana katika Ugiriki, na katika mwaka wa 62 K.W.K., buruji ya kale zaidi ya mambo ya nyota ya Wagiriki ikabuniwa. Wagiriki walipendezwa sana na unajimu hivi kwamba kulingana Profesa Gilbert Murray, unajimu “uliathiri sana fikira za Wagiriki jinsi ambavyo ugonjwa mpya unavyozukia watu wanaoishi katika kisiwa cha mbali.”
Katika kujaribu kujua matukio ya wakati ujao, Wagiriki na Waroma walienda sana kwa waaguzi au wawasiliani-roho. Ilidhaniwa kwamba miungu iliwasiliana na wanadamu kupitia watu. (Linganisha Matendo 16:16-19.) Matokeo ya itikadi hizi yalikuwa nini? Mwanafalsafa Bertrand Russell alisema hivi: “Hofu ikazuka badala ya tumaini; kusudi la maisha lilikuwa kuepuka misiba badala ya kutumia maisha kwa njia inayofaa.” Mambo kama hayo yakawa ubishi katika Jumuiya ya Wakristo.
Mijadala ya “Wakristo” Juu ya Kuamuliwa Kimbele kwa Maisha
Wakristo wa mapema waliishi katika utamaduni ulioathiriwa sana na mawazo ya Wagiriki na Waroma juu ya matukio yasiyoepukika na kuamuliwa kimbele kwa maisha. Kwa mfano, wale wanaoitwa eti Baba wa Kanisa, walitegemea sana nadharia za wanafalsafa Wagiriki kama vile Aristotle na Plato. Tatizo moja walilojaribu kutatua lilikuwa, Mungu mjua-yote, mweza-yote, ‘atangazaye mwisho tangu mwanzo,’ atakuwaje Mungu mwenye upendo? (Isaya 46:10; 1 Yohana 4:8) Ikiwa Mungu alijua mwisho tangu mwanzo, wakasababu, basi bila shaka alijua kimbele kwamba mwanadamu angetumbukia katika dhambi na alijua matokeo yake yenye msiba.
Origen, mmojawapo wa waandishi Wakristo wa mapema waliokuwa mahiri, alisababu kwamba jambo moja muhimu la kukumbuka ni wazo la hiari. “Kwa kweli, kuna vifungu vingi katika Maandiko vinavyothibitisha waziwazi kuwapo kwa uhuru wa hiari,” akaandika.
Origen alisema kwamba kusema kuwa kani fulani isiyojulikana ndiyo inayoelekeza matendo yetu “si kweli wala hakupatani na kusababu kuzuri, lakini ni usemi wa mtu anayetaka kupotoa wazo la hiari.” Origen alisababu kwamba japo Mungu ana uwezo wa kujua matukio kimbele kulingana na wakati, hili halimaanishi kwamba ndiye anayesababisha tukio au kwamba ni sharti litukie. Hata hivyo, si wote waliokubaliana naye.
Baba wa Kanisa aliyekuwa maarufu, Augustine (354-430 W.K.), aliufanya mjadala huo kuwa mgumu alipopinga athari za hiari katika matukio. Augustine aliweka msingi wa dhana ya Jumuiya ya Wakristo ya kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu. Vichapo vyake, hasa De libero arbitrio, vilitumiwa sana katika mijadala katika Enzi za Kati. Hatimaye mjadala huo ulifikia upeo wakati wa Marekebisho Makubwa ya Kidini, huku Jumuiya ya Wakristo ikiwa imesambaratika kwa sababu ya wazo la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu.a
Itikadi Iliyoenea Kote
Ingawa hivyo, mawazo juu ya kuamuliwa kimbele kwa maisha hayapatikani tu katika nchi za Magharibi. Waislamu wengi hudhihirisha itikadi yao juu ya tukio lililopangwa lisiloepukika kwa kusema “mektoub”—imeandikwa—wanapokumbwa na msiba. Ingawa ni kweli kwamba dini nyingi za Mashariki hukazia fungu la mtu katika wakati wake ujao, hata hivyo kuna mambo yanayodokeza nadharia ya kuamuliwa kimbele kwa maisha katika mafundisho yao.
Kwa mfano, karma katika Uhindu na Ubudha, ni tukio lisiloepukika linalotokana na matendo ya mtu katika maisha ya awali. Katika China maandishi ya kale zaidi kugunduliwa yako kwenye magamba ya kobe yaliyotumiwa katika uaguzi. Kuamuliwa kimbele kwa maisha pia kulikuwa sehemu ya itikadi za wenyeji wa Amerika. Kwa mfano, Waazteki walibuni kalenda za kuagua zilizotumiwa kufunua mambo yatakayompata kimbele. Itikadi zinazohusu kuamuliwa kimbele kwa maisha zimeenea sana katika Afrika.
Kuenea kote kwa dhana ya kuamuliwa kimbele kwa maisha kunaonyesha kwa hakika kwamba mwanadamu ana uhitaji muhimu wa kuitikadi mweza-yote. John B. Noss, akiri hivi katika kitabu chake Man’s Religions: “Dini zote zaonyesha kwa njia moja au nyingine kwamba mwanadamu hawezi kujielekeza. Yeye huhusika sana na hata hutegemea nguvu za Asili na za Kijamii za nje. Iwe ni kwa njia isiyo dhahiri au waziwazi, yeye anajua kwamba yeye si kani muhimu iliyo peke yake ambayo inaweza kudumu kwa kujitenga.”
Kwa kuongezea uhitaji wa kuitikadi Mungu, tuna uhitaji muhimu wa kufahamu mambo yanayotukia. Japo hivyo, kuna tofauti baina ya kutambua Muumba mweza-yote na kuitikadi kwamba yeye hukusudia kimbele mambo yatakayotupata bila kubadilika. Tuna fungu gani katika kuamua yatakayotupata wakati ujao? Mungu ana fungu gani?
[Maelezo ya Chini]
a Ona gazeti-jenzi letu, Mnara wa Mlinzi, la Februari 15, 1995, ukurasa 3-4.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kalenda ya unajimu ya Babiloni, mwaka wa 1,000 K.W.K.
[Hisani]
Musée du Louvre, Paris
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wagiriki na Waroma waliitikadi kwamba mwisho wa mwanadamu unaamuliwa na miungu ya kike mitatu
[Hisani]
Musée du Louvre, Paris
[Picha katika ukurasa wa 7]
Isis wa Misri, “mwamuzi wa mambo yatakayompata mwanadamu na wa matukio ya wakati ujao”
[Hisani]
Musée du Louvre, Paris
[Picha katika ukurasa wa 8]
Maandishi ya kale zaidi ya Kichina kwenye magamba ya kobe yalitumiwa katika uaguzi
[Hisani]
Institute of History and Philology, Academia Sinica, Taipei
[Picha katika ukurasa wa 8]
Nyota za unajimu huonekana kwenye sanduku hili la Uajemi
[Hisani]
Photograph taken by courtesy of the British Museum