Wameazimia Kutokata Tamaa
TOLEO la Amkeni! la Oktoba 22, 1998 lilikuwa na makala fupi juu ya Matt Tapio mwenye umri wa miaka 17 ambaye alipambana na kansa kwa muda mrefu. Ilikuwa yenye kichwa “Hakukata Tamaa.” Hatimaye Matt akafa Aprili 19, 1998, makala hiyo ilipokuwa ikitayarishwa.
Makala hiyo ilinukuu mahoji ya Matt yaliyorekodiwa na kusikilizwa katika mkutano mmoja wa Mashahidi wa Yehova, mahoji hayo yaliwagusa moyo hasa wasomaji vijana. Haya ni baadhi ya maelezo yao.
Deseree, mwenye umri wa miaka 20 kutoka Kanada, aliandika jinsi habari hiyo ilivyomwathiri yeye na mwenzi wake katika huduma ya wakati wote waliposoma jinsi Matt alivyompenda Yehova: “Tulilia machozi. Na tukaendelea kulia kwa muda fulani. . . . Jinsi ambavyo sisi sote, hasa vijana, tuwezavyo kujifunza kutoka kwa Matt ‘kufanya yote tuwezayo sasa! . . . Hata jambo jipi litokee, usikome kamwe kutoa ushahidi juu ya Yehova’!”
Erin, kutoka Kentucky, Marekani, aliandika hivi: “Singeweza kujizuia kulia nilipokuwa nikisoma simulizi lake. Nikiwa msichana mwenye umri wa miaka 16 mwenye afya njema, ninataka kufanya yote niwezayo kwa ajili ya Yehova nikiwa na uwezo, ili kwamba siku moja, atakapofufuliwa, nitaweza binafsi kumwambia Matt jinsi simulizi lake la maisha lilivyonitia moyo.” Vivyo hivyo, Maria, kijana mwenye umri wa miaka 15 kutoka Texas, Marekani, alieleza hivi: “Nimeazimia kufanya yote niwezayo kwa ajili ya Yehova maadamu nina afya njema. Shauri la Matt limenisaidia sana.”
Jessica, kijana kutoka South Carolina, Marekani, aliandika: “Nina umri wa miaka 13, na mimi binafsi nilitiwa moyo sana kuona kijana mwingine mwenye bidii nyingi sana na upendo kwa ajili ya Yehova. Kwa kusoma juu ya hali ya Matt Tapio niling’amua jinsi nilivyobarikiwa kuwa na afya njema. Nimeongeza jina la Matt kwenye orodha yangu ya ndugu na dada ambao ninapanga kusalimu katika mfumo mpya!”
Sara, kutoka San Severino Marche, Italia, aliandika hivi: “Makala hiyo ilinifanya nilie. Nina umri wa miaka 17, sawa na Matt. Kwa kuwa nina afya njema, tamaa yangu ni kwamba nisiache kamwe kusema juu ya Yehova kama Matt asivyoacha, hata katika nyakati ngumu zaidi za maisha yake. Asanteni kwa kuchapisha masimulizi ya maisha kama hili, ambayo hutuchochea tutumie wakati bora zaidi maishani mwetu, wakati wetu, na nguvu zetu kwa ajili ya Yehova.—Mhubiri 12:1.”
Wategemezwa na Tumaini la Ufufuo
Mtu awe mchanga au mzee, ni jambo la kawaida leo kupatwa na kifo. Kijana aitwaye Heidi mwenye umri wa miaka 19 alisema hivi: “Katika majuma mawili yaliyopita, nimepoteza watu wawili niliowapenda sana katika kifo, jambo pekee linalonitegemeza ni tumaini la kuwaona katika ufufuo.
“Nimefurahishwa sana na Matt na azimio lake thabiti la kuendelea kutolea wengine ushahidi japo alikuwa mgonjwa sana. Yeye ni kielelezo bora kwa wote, na ninatazamia kumkumbatia wakati wa ufufuo.”
Mama mmoja aitwaye Nancy aliandika: “Nilisoma makala hiyo nikilia. Binti yetu Rachelle alikufa kutokana na uvimbe kwenye shina la ubongo Januari 11, 1996, siku mbili tu kabla ya Matt kutimiza mradi wake wa kubatizwa. Rachelle alikuwa na umri wa miaka sita tu alipokufa kutokana na uvimbe huo, lakini kama Matt, hakukata tamaa, na alijaribu kufanya yote aliyoweza kumpendeza Yehova.
“Itakuwa siku tukufu Yehova atakapotupa baraka ya kumwona binti yetu akiwa na afya bora na uwezo wa kufurahia kikamili maisha yake ya utotoni. Kama Yairo na mkewe, tutapigwa na ‘bumbuazi ya upeo wa shangwe kubwa.’”—Marko 5:42.
Shannon, kutoka Georgia, Marekani, aliandika: “Simulizi hili lilinionyesha kwamba unaweza kushikamana na Yehova hata ukiwa mgonjwa. Hata ingawa sina ugonjwa mbaya sasa na sikuzote nimekuwa na afya nzuri, nitahifadhi habari hii ili niisome baadaye.
“Ninatumaini kwamba wazazi wa Matt watafarijiwa na tumaini la ufufuo. Mimi pia nilimpoteza rafiki wa karibu katika kifo—nyanya yangu, mwaka wa 1995. Ninashukuru sana kwa sababu ninamjua Yehova na kwa kuwa ninatumaini kuwaona wapendwa wangu tena.”
Tineja Mhispania aliandika hivi: “Wazazi wangu walinifundisha mimi na dada zangu wanne faida ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Lakini baada ya kusoma simulizi hili, nimegundua kwamba tunaweza kuanza kuona mikutano hii kuwa ya kawaida tu. Ningependa kuwapongeza wazazi wa Matt kwa kumwelimisha vema kiroho. Wao ni kielelezo kwetu sote. Ningependa kuwajulisha kuwa ijapokuwa ni vigumu kukabiliana na utupu wa kumpoteza mpendwa katika kifo, Yehova yuko nasi daima.
“Ninatumaini kukutana na Matt katika ulimwengu mpya. Ningependa kumwambia kwamba yeye ni kielelezo bora na kwamba sote tunamkumbuka mioyoni mwetu. Yehova ni Mungu wa walio hai, na sasa Matt yuko mahali sawa na dada yangu aliyekufa miaka minne iliyopita—katika kumbukumbu la Yehova. (Luka 20:38) Matt, dada yangu Eva, na watumishi wengine waaminifu wa Mungu wako humo. Yehova ni mwema ajabu, naye hatatuacha kamwe.”
Kwa kweli, tumaini la ufufuo ni lenye kustaajabisha sana. Na tulithamini, na tuonyeshe uthamini wetu kwa ahadi hii tukufu kwa kumkumbuka Muumba wetu kila siku, kama alivyofanya Mwanaye mpendwa, Yesu Kristo.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Deseree
[Picha katika ukurasa wa 24]
Erin
[Picha katika ukurasa wa 24]
Maria
[Picha katika ukurasa wa 24]
Jessica
[Picha katika ukurasa wa 25]
Sara
[Picha katika ukurasa wa 25]
Heidi
[Picha katika ukurasa wa 25]
Nancy, akiwa na mumewe na bintiye Rachelle
[Picha katika ukurasa wa 25]
Shannon