Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 8/22 kur. 18-23
  • Kumtumikia Mungu Licha ya Kukabiliwa na Kifo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumtumikia Mungu Licha ya Kukabiliwa na Kifo
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nabarikiwa kwa Elimu Nzuri
  • Harakati Mpya ya Kidini
  • Kutiwa Kwangu Gerezani Mara za Kwanza-Kwanza
  • Kukutana Kulikongojewa Sana
  • Matukio Yaliyoongoza Kwenye Ubatizo
  • Mnyanyaso Mpya Tena
  • Miaka Tisa ya Mateso
  • Kuwekwa Huru na Kufungwa Tena
  • Nafunguliwa, Lakini Bado Nanyanyaswa
  • Uhuru wa Kuhubiri Hatimaye!
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Nilikuwa Mwanasiasa Lakini Sasa Mimi Ni Mkristo
    Amkeni!—2002
  • Mungu Amekuwa Msaidiaji Wetu
    Amkeni!—1999
  • Toka Ufukara Hadi Utajiri Mkubwa Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 8/22 kur. 18-23

Kumtumikia Mungu Licha ya Kukabiliwa na Kifo

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JOÃO MANCOCA

Juni 25, 1961, askari walitawanya mkutano wetu wa Kikristo katika Luanda, Angola. Watu 30 kati yetu walipelekwa gerezani na kupigwa vibaya sana hivi kwamba askari wakawa wakirudi baada ya kila nusu saa kuona kama kulikuwa na mtu yeyote aliyekufa. Wengine wao walisikika wakisema kwamba lazima Mungu wetu awe ni wa kweli, kwa kuwa sote tulinusurika.

BAADA ya kupigwa huko, nilibaki katika gereza la São Paulo kwa miezi mitano. Kisha miaka tisa iliyofuata, nilihamishwa kutoka katika gereza moja hadi jingine na kupigwa zaidi, kunyimwa vitu, na kuhojiwa-hojiwa. Muda mfupi baada ya kuachiliwa kwangu kutoka kifungoni mwaka wa 1970, nilikamatwa tena, na wakati huu nilipelekwa kwenye kambi ya kifo yenye sifa mbaya ya São Nicolau, sasa iitwayo Bentiaba. Nilizuiwa huko kwa miaka miwili na nusu.

Huenda ukajiuliza kwa nini raia mwenye kutii sheria kama mimi nitiwe gerezani kwa kusema na wengine juu ya itikadi zangu zinazotegemea Biblia na pale nilipojifunzia habari njema za Ufalme wa Mungu kwa mara ya kwanza.

Nabarikiwa kwa Elimu Nzuri

Nilizaliwa Oktoba 1925 karibu na mji wa Maquela do Zombo, kaskazini ya Angola. Baba alipokufa mwaka wa 1932, Mama alinipeleka kwa ndugu yake huko Kongo ya Ubelgiji (sasa ijulikanayo kuwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo). Hakutaka kufanya hivyo, lakini hakuweza kuniandalia kitu.

Mjomba wangu alikuwa wa dini ya Baptisti, naye alinitia moyo kusoma Biblia. Ijapokuwa nilikuwa mshiriki wa kanisa lake, njaa yangu ya kiroho haikutoshelezwa na yale niliyojifunza, wala sikuchochewa kumtumikia Mungu. Hata hivyo, mjomba wangu alinipeleka shuleni na kunisaidia kupata elimu nzuri. Pamoja na mambo mengine, nilijifunza kuongea Kifaransa. Baada ya muda, nilijifunza kuongea Kireno pia. Baada ya kumaliza shule, nilipata kazi nikawa mtaalamu wa telegrafia ya redio (njia ya upelekaji na upokeaji wa simu za upepo) katika kituo cha redio cha kati katika Léopoldville (ambayo sasa ni Kinshasa). Kisha, nilipokuwa na umri wa miaka 20, nikamwoa Maria Pova.

Harakati Mpya ya Kidini

Mwaka huohuo, 1946, nikawa chini ya uvutano wa kiongozi wa kwaya ya Angola wa Kanisa la Baptisti aliyeelimika. Alikuwa na hamu ya kuelimisha na kuboresha hali ya watu wasemao lugha ya Kikongo wanaoishi kaskazini ya Angola. Alikuwa amepata tafsiri ya Kireno ya kijitabu cha Kiingereza The Kingdom, the Hope of the World, kilichochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society na kugawanywa na Mashahidi wa Yehova.

Kiongozi huyo wa kwaya alitafsiri kijitabu hiki katika Kikongo na kukitumia kuongoza mazungumzo ya Biblia ya kila juma na kikundi chetu cha Waangola ambao tulikuwa tukifanya kazi katika Kongo ya Ubelgiji. Baada ya muda, kiongozi huyo wa kwaya aliandikia makao makuu ya Watch Tower Society katika Marekani akitaka fasihi nyingine zaidi. Hata hivyo, habari aliyotupatia ilichanganyika na mafundisho ya makanisa. Hivyo, sikuweza kutofautisha waziwazi kati ya Ukristo wa kweli na mafundisho yasiyo ya Kimaandiko ya Jumuiya ya Wakristo.

Hata hivyo, niligundua kwamba ujumbe wa Biblia ulio katika fasihi za Watch Tower Society ulikuwa tofauti na chochote kile nilichopata kusikia katika Kanisa Baptisti. Kwa mfano, nilijifunza kwamba Biblia huona jina la Mungu la kibinafsi, Yehova, kuwa la maana zaidi na kwamba Wakristo wa kweli hujiita ifaavyo Mashahidi wa Yehova. (Zaburi 83:18; Isaya 43:10-12) Zaidi ya hilo, moyo wangu ulichangamshwa na ahadi ya Biblia ya uhai wa milele katika paradiso duniani kwa wale watakaomtumikia Yehova kwa uaminifu.—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3-5.

Ijapokuwa ujuzi wangu juu ya kweli ya Biblia ulikuwa mdogo, nilihisi kama nabii Yeremia, ambaye hakuweza kuzuia tamaa yake ya kusema juu ya Mungu wake, Yehova. (Yeremia 20:9) Washiriki wa funzo letu la Biblia walijiunga nami katika kuhubiri nyumba hadi nyumba. Pia nilifanya mikutano ya watu wote katika uwanja wa mjomba wangu, nikitumia mialiko niliyochapa ya kualika watu. Wakati mmoja watu 78 walihudhuria. Hivyo, harakati mpya ya kidini ikaanzishwa chini ya uongozi wa kiongozi wa kwaya ya Angola.

Kutiwa Kwangu Gerezani Mara za Kwanza-Kwanza

Bila kujua, harakati yoyote iliyohusiana na Watch Tower Society ilikatazwa katika Kongo ya Ubelgiji. Hivyo, Oktoba 22, 1949, wachache kati yetu tulikamatwa. Kabla ya kesi yetu, hakimu aliongea nami faraghani na kujaribu kufanya mipango ya kuniweka huru, kwa kuwa alijua kwamba nilikuwa mfanyakazi wa serikali. Lakini ili nipate uhuru wangu, ningelazimika kukana harakati hiyo iliyokuwa imeundwa kwa sababu ya kuhubiri kwetu, nami nikakataa kufanya hivyo.

Baada ya miezi miwili na nusu gerezani, wenye mamlaka waliamua kuturudisha baadhi yetu ambao tulikuwa Waangola nchini kwetu. Hata hivyo, tuliporudi Angola, wenye mamlaka wa ukoloni waliokuwa Wareno walitilia shaka utendaji wetu na kukatiza uhuru wetu. Washiriki zaidi wa harakati yetu walifika kutoka Kongo ya Ubelgiji, na hatimaye tukawa watu zaidi ya 1,000 waliotawanyika kotekote Angola.

Baada ya muda, wafuasi wa kiongozi mashuhuri wa kidini Simon Kimbangu walitiwa ndani ya harakati yetu. Watu hao hawakupendezwa kujifunza fasihi za Watch Tower Society, kwa kuwa waliamini kwamba Biblia ingeweza kufafanuliwa tu na mwasiliani-roho. Wengi katika harakati yetu waliunga mkono maoni hayo, kutia ndani kiongozi wa kwaya, ambaye bado alionwa kuwa kiongozi wetu. Nilisali kwa bidii ili Yehova atukutanishe na mwakilishi wa kweli wa Watch Tower Society. Nilitumaini kwamba hilo lingesadikisha harakati yote ikubali kweli ya Biblia na kukataa mazoea yasiyo ya Kimaandiko.

Washiriki fulani wa harakati hiyo walichukia kuhubiri ambako wachache kati yetu tulikuwa tukifanya. Kwa hiyo walitusaliti kwa wenye mamlaka na kutushtaki kuwa viongozi wa harakati ya kisiasa. Tokeo likawa kwamba, katika Februari 1952 wengine wetu tulikamatwa, kutia ndani Carlos Agostinho Cadi na Sala Ramos Filemon. Tulifungiwa ndani ya seli isiyo na madirisha. Hata hivyo, mlinzi mwenye urafiki alileta chakula kilicholetwa na wake zetu pamoja na taipureta ili tuweze kutengeneza nakala zaidi za vijitabu vya Watch Tower Society.

Baada ya majuma matatu tulihamishwa hadi Baia dos Tigres, eneo la jangwa lililo kusini ya Angola. Tulikwenda pamoja na wake zetu huko. Tulihukumiwa miaka minne yenye kazi ngumu, tukifanyia kazi kampuni ya kuvua samaki. Baia dos Tigres haikuwa na bandari ya mashua za uvuvi, kwa hiyo wake zetu walipita kwa shida wakienda na kurudi kuanzia asubuhi hadi usiku wakibeba samaki wengi wazito kutoka kwenye mashua.

Katika kambi hii ya gereza, tulikuta washiriki wengine wa harakati yetu na tukajaribu kuwashawishi waendelee kujifunza Biblia. Lakini walichagua kumfuata Toco, yule kiongozi wa kwaya. Baada ya muda, wakaitwa Watoco.

Kukutana Kulikongojewa Sana

Tulipokuwa Baia dos Tigres, tuligundua anwani ya ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ya Northern Rhodesia (ambayo sasa ni Zambia) na kuandika tukiomba msaada. Barua yetu ilipitishwa hadi kwenye ofisi ya tawi ya Afrika Kusini, ambayo ilituandikia, ikituuliza jinsi tulivyopata kupendezwa na kweli ya Biblia. Makao makuu ya Watch Tower Society, kule Marekani, yalijulishwa juu yetu, na mipango ikafanywa ya kutuma mwakilishi wa pekee atuone. Huyo alikuwa John Cooke, mishonari mwenye miaka mingi ya uzoefu katika nchi za kigeni.

Baada ya Ndugu Cooke kufika Angola, yalitimia majuma kadhaa kabla ya kuruhusiwa kututembelea na wenye mamlaka Wareno. Alifika Baia dos Tigres Machi 21, 1955, naye akaruhusiwa kukaa nasi kwa siku tano. Maelezo yake ya Biblia yalikuwa yenye kuridhisha sana, nami nilisadikishwa kwamba aliwakilisha tengenezo la pekee la kweli la Yehova Mungu. Siku ya mwisho ya ziara yake, Ndugu Cooke alitoa hotuba ya watu wote yenye kichwa “Habari Njema Hizi za Ufalme.” Jumla ya watu 82 walikuwepo, kutia na msimamizi mkuu wa Baia dos Tigres. Kila mtu aliyehudhuria alipokea nakala iliyochapishwa ya hotuba hiyo.

Katika miezi mitano aliyokaa Angola, Ndugu Cooke alikutana na Watoco kadhaa, kutia na kiongozi wao. Hata hivyo, wengi wao hawakupendezwa kuwa Mashahidi wa Yehova. Hivyo, mimi na washiriki wangu tuliwajibika kujulisha msimamo wetu waziwazi kwa wenye mamlaka. Tulifanya hivyo kwa kuandika barua rasmi, ya Juni 6, 1956, na kuiandikia “Mtukuzwa wa Wilaya ya Moçâmedes.” Tuliandika kwamba hatukuwa na uhusiano tena kamwe na wafuasi wa Toco na kwamba twapaswa kuonwa kuwa “washiriki wa Sosaiti ya Mashahidi wa Yehova.” Pia tuliomba kwamba tupewe uhuru wa ibada. Lakini, badala ya hukumu yetu kupunguzwa, iliongezwa hadi miaka miwili.

Matukio Yaliyoongoza Kwenye Ubatizo

Hatimaye tuliachiliwa mnamo Agosti 1958, na tulipokuwa tukirudi Luanda, tulikuta kikundi kidogo cha Mashahidi wa Yehova. Kilikuwa kimepangwa mwaka uliotangulia na Mervyn Passlow, mishonari aliyetumwa Angola kuchukua mahali pa John Cooke ambaye tayari alikuwa amehamishwa nchini kufikia wakati ambao tulikuwa tumefika. Kisha, mwaka wa 1959, Harry Arnott, mishonari mwingine wa Mashahidi wa Yehova, alikuja. Hata hivyo, alikamatwa aliposhuka kwenye uwanja wa ndege, pia sisi watatu ambao tulikuwa tukimngoja.

Wale wengine wawili, Manuel Gonçalves na Berta Teixeira, Mashahidi Wareno waliobatizwa hivi majuzi, walifunguliwa baada ya kuonywa wasifanye mikutano mingine yoyote. Ndugu Arnott alihamishwa, nami nilionywa kwamba nisipotia sahihi hati nikitangaza kwamba sikuwa Shahidi tena, ningerudishwa Baia dos Tigres. Baada ya kuhojiwa kwa muda wa saa saba, nikaachiliwa bila kutia sahihi yoyote. Baada ya juma moja, mwishowe niliweza kubatizwa, pia rafiki zangu Carlos Cadi na Sala Filemon. Tulikodi nyumba huko Muceque Sambizanga, kiunga cha Luanda, kikawa sehemu ya kutaniko la kwanza la Mashahidi wa Yehova katika Angola.

Mnyanyaso Mpya Tena

Idadi yenye kuongezeka ya watu wenye kupendezwa walianza kuhudhuria mikutano. Baadhi yao walikuja kutupeleleza, lakini walifurahia mikutano na baadaye wakawa Mashahidi wa Yehova! Hali ya siasa ilikuwa inabadilika, na hali ikawa ngumu zaidi kwetu baada ya machafuko ya utaifa ya Februari 4, 1961. Ujapokuwa uwongo ulioenezwa juu yetu, tulifanikiwa kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo Machi 30, kukiwa na wahudhuriaji 130.

Katika Juni, nilipokuwa nikiongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi, mkutano wetu ulitawanywa na polisi wa jeshi. Wanawake na watoto waliachiliwa, lakini wanaume 30 waliokuwapo walichukuliwa, kama ilivyoonyeshwa kwenye utangulizi. Tulipigwa mfululizo kwa muda wa saa mbili kwa rungu. Nilitapika damu kwa miezi mitatu baada ya hapo. Nilikuwa na hakika kwamba ningekufa, hata yule aliyenipiga aliniambia hivyo. Wengi ambao walipigwa walikuwa wapya, wanafunzi wa Biblia wasiobatizwa, kwa hiyo nilisali kwa bidii kwa ajili yao: “Yehova, linda kondoo zako.”

Twamshukuru Yehova kwa kuwa, hakuna mmoja wao aliyekufa, jambo ambalo lilishangaza askari hao. Baadhi ya askari hao walichochewa kumsifu Mungu wetu, ambaye walisema, alituwezesha kuokoka! Wanafunzi wengi wa Biblia hatimaye wakawa Mashahidi waliobatizwa, na sasa baadhi yao wanatumikia wakiwa wazee Wakristo. Mmoja wao, Silvestre Simão, ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Angola.

Miaka Tisa ya Mateso

Kama nilivyotaja mwanzoni, niliteseka katika njia nyingi kwa muda wa miaka tisa iliyofuata na nikahamishwa kutoka gereza moja au kambi moja ya kazi ngumu hadi nyingine. Katika sehemu hizi zote, niliweza kutolea ushahidi wafungwa wa kisiasa, ambao wengi wao ni Mashahidi waliobatizwa leo. Mke wangu Maria, aliruhusiwa kuandamana nami.

Tulipokuwa kwenye kambi ya kazi ngumu ya Serpa Pinto, wafungwa wanne wa kisiasa walikamatwa walipokuwa wakijaribu kutoroka. Waliteswa kikatili sana hadi kifo mbele ya wafungwa wote ili kuwaogopesha hata wasifikirie kutoroka. Baadaye kamanda wa kambi alinitisha mbele ya Maria na watoto hivi: “Nikikushika ukihubiri tena, utauawa kama wale wengine waliojaribu kutoroka.”

Mwishowe, katika Novemba 1966, tulijikuta katika ile iliyokuwa kambi ya kifo mbaya zaidi ya São Nicolau. Tulipofika huko, nilishtuka kukuta kwamba kamanda wa kambi alikuwa Bw. Cid, mtu aliyenipiga hata karibu nife kwenye gereza la São Paulo! Watu wengi zaidi walikuwa wakiuawa kila mwezi, na familia yangu ililazimishwa kutazama mapigo hayo ya kinyama. Hilo lilimsababisha Maria achanganyikiwe akili na hajapona vizuri tangu wakati huo. Hatimaye, niliweza kupata ruhusa ya kumwondosha yeye na watoto waende Luanda, ambako binti zangu wawili wakubwa, Teresa na Joana, waliwatunza.

Kuwekwa Huru na Kufungwa Tena

Niliachiliwa mwaka uliofuata, Septemba 1970, na kuungana na familia yangu na ndugu wote katika Luanda. Nilitoa machozi nilipoona jinsi kazi ya kuhubiri ilivyokuwa imeendelea kwa muda wa miaka tisa ambayo sikuwapo. Nilipopelekwa gerezani katika 1961, kutaniko katika Luanda lilikuwa na vikundi vinne vidogo-vidogo. Sasa kulikuwa na makutaniko manne makubwa, yaliyopangwa vizuri na kusaidiwa baada ya kila miezi sita na mwakilishi anayesafiri wa tengenezo la Yehova. Nilishangilia sana kuwa huru, lakini uhuru wangu ulikuwa wa muda mfupi.

Siku moja mwelekezi wa Kikosi cha Polisi wa Upelelezi cha PIDE ambacho sasa kimetoweka kabisa, aliniita. Baada ya kunirairai mbele ya binti yangu Joana, alinipa hati moja niitie sahihi. Hati hiyo iliorodhesha kazi ambazo ningefanya nikiwa mpelelezi wa PIDE na kama ningekubali ningepata vitu vingi vya kimwili kwa sababu ya kazi yangu. Nilipokataa kutia sahihi, nilitishwa kurudishwa São Nicolau, ambapo niliambiwa, sitawekwa huru tena.

Katika Januari 1971, baada ya miezi minne tu ya kuwekwa huru, vitisho hivyo vilitekelezwa. Kwa ujumla, wazee Wakristo 37 kutoka Luanda walikamatwa na kupelekwa São Nicolau. Tulifungwa jela huko hadi Agosti 1973.

Nafunguliwa, Lakini Bado Nanyanyaswa

Mwaka wa 1974 uhuru wa kidini ulitangazwa katika Ureno, na baada ya hapo uhuru huo ulienezwa kwenye mikoa ya wasimamizi Wareno. Katika Novemba 11, 1975, Angola ilijipatia uhuru kutoka kwa Ureno. Ilisisimua kama nini mwezi wa Machi mwaka huohuo, kuwa na makusanyiko yetu ya mzunguko kwa uhuru! Nilikuwa na pendeleo la kutoa hotuba ya watu wote kwenye mikusanyiko hiyo yenye shangwe katika uwanja wa michezo wa Sports Citadel huko Luanda.

Hata hivyo, serikali mpya, ilipinga msimamo wetu wa kutokuwamo, na vita vya wenyewe kwa wenyewe vilichacha kotekote Angola. Hali ikawa mbaya sana hivi kwamba Mashahidi wazungu walilazimishwa kukimbia kutoka nchini. Tukiwa ndugu watatu, tuliwekwa tusimamie kazi ya kuhubiri katika Angola chini ya mwelekezo wa ofisi ya tawi ya Ureno ya Mashahidi wa Yehova.

Upesi jina langu lilianza kuonekana katika magazeti na kutangazwa redioni. Nilishtakiwa kuwa mwakilishi wa ubeberu wa kimataifa na kuwajibika kwa sababu ya Mashahidi Waangola kukataa kujiunga na vita. Tokeo ni kwamba, niliitwa mbele ya liwali wa kwanza wa wilaya ya Luanda. Kwa heshima, nilimweleza msimamo wa kutokuwemo wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, msimamo ambao wafuasi wa mapema wa Yesu Kristo walikuwa nao. (Isaya 2:4; Mathayo 26:52) Niliposema kwamba nilikuwa nimekaa gerezani zaidi ya miaka 17 na katika kambi za kazi ngumu wakati wa utawala wa ukoloni, aliamua kutonikamata.

Siku hizo, ilihitaji moyo mkuu ili mtu atumikie akiwa Shahidi wa Yehova katika Angola. Kwa kuwa nyumba yangu ilikuwa ikipelelezwa, ilitubidi tuache kuitumia kwa ajili ya mikutano. Lakini kama alivyosema mtume Paulo, ‘tulisongwa katika kila njia, lakini hatukufinywa kupita tuwezavyo kusonga.’ (2 Wakorintho 4:8) Hatukuwa wasiotenda katika huduma yetu kamwe. Niliendelea katika kazi ya kuhubiri, nikitumikia nikiwa mhudumu asafiriye na kuimarisha makutaniko katika wilaya za Benguela, Huíla, na Huambo. Wakati huo nilitumia jina jingine, Ndugu Filemon.

Katika Machi 1978 kazi yetu ya kuhubiri ilipigwa marufuku tena, nami nikajulishwa na vyanzo vyenye kutegemeka kwamba wanamapinduzi washupavu walikuwa wamepanga kuniua. Kwa hiyo nilikimbilia nyumbani mwa Shahidi mmoja wa Nigeria ambaye alikuwa mwajiriwa wa ubalozi wa Nigeria nchini Angola. Mwezi mmoja baadaye, hali ilipokuwa imetulia, niliendelea kutumikia akina ndugu nikiwa mwangalizi wa mzunguko.

Yajapokuwa marufuku na vita vya wenyewe kwa wenyewe, maelfu ya Waangola waliitikia mahubiri yetu. Kwa sababu ya ukuzi mzuri katika idadi ya watu waliokuwa wakiwa Mashahidi, halmashauri ya nchi iliwekwa ili ishughulikie kazi ya kuhubiri katika Angola, chini ya mwelekezo wa ofisi ya tawi ya Ureno. Wakati huo, nilisafiri mara kadhaa hadi Ureno, nilikopokea mazoezi mazuri kutoka kwa wahudumu wenye sifa za ustahili, na vilevile utunzaji wa kitiba niliohitaji.

Uhuru wa Kuhubiri Hatimaye!

Nilipokuwa katika kambi za kazi ngumu, wafungwa wa kisiasa mara nyingi walinidhihaki na kusema kwamba singewekwa huru kamwe kama ningeendelea kuhubiri. Lakini nilijibu: “Huu bado si wakati wa Yehova kufungua mlango, lakini akiufungua, hakuna mtu atakayeweza kuufunga.” (1 Wakorintho 16:9; Ufunuo 3:8) Mlango wa fursa ya kuhubiri bila vizuizi ulifunguliwa wazi baada ya kuporomoka kwa Muungano wa Sovieti katika 1991. Wakati huo tulianza kupata uhuru zaidi wa ibada katika Angola. Mwaka wa 1992 kazi ya Mashahidi wa Yehova ilihalalishwa kirasmi. Mwishowe, mwaka wa 1996 ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliwekwa katika Angola, nami niliwekwa kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi.

Katika miaka mingi nilipokuwa gerezani, kwa njia fulani, familia yangu ilitunzwa sikuzote. Tulikuwa na watoto sita, na watano kati yao wangali hai. Mpendwa wetu Joana alikufa mwaka jana kwa sababu ya kansa. Wanne kati ya watoto wetu waliobaki ni Mashahidi waliobatizwa, lakini mtoto wetu mwingine bado hajachukua hatua ya ubatizo.

Ndugu Cooke alipotutembelea mwaka wa 1955, tulikuwa na jumla ya Waangola wanne waliokuwa wakitangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Leo kuna wapiga-mbiu wa Ufalme zaidi ya 38,000 nchini, nao wanaongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya 67,000 kila mwezi. Miongoni mwa wale wanaohubiri habari njema wengi wao ni wale waliotunyanyasa zamani. Hiyo inathawabisha kama nini, nami namshukuru Yehova kwa kunihifadhi hai na kuniruhusu nitimize tamaa yangu yenye bidii ya kutangaza neno lake!—Isaya 43:12; Mathayo 24:14.

[Ramani katika ukurasa wa 20, 21]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo

Kinshasa

Angola

Maquela do Zombo

Luanda

São Nicolau (sasa ni Bentiaba)

Moçâmedes (sasa ni Namibe)

Baia dos Tigres

Serpa Pinto (sasa ni Menongue)

[Hisani]

Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Chini: Nikiwa na John Cooke mwaka wa 1955. Sala Filemon yuko kushoto

Kulia: Naungana tena na John Cooke baada ya miaka 42

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na mke wangu, Maria

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki