Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 10/8 kur. 18-19
  • Jinsi ya Kuchagua Mwenzi wa Ndoa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kuchagua Mwenzi wa Ndoa
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Angalia Zaidi ya Sura ya Nje Tu
  • ‘Oa au Olewa Katika Bwana Tu’
  • Ndoa za Kupangwa
  • Kuwekea Nyumba Yako Msingi Mzuri
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Mwongozo wa Mungu Katika Kuchagua Mwenzi wa Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Ndoa—Zawadi Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Ndoa​—Zawadi Kutoka kwa Mungu
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 10/8 kur. 18-19

Maoni ya Biblia

Jinsi ya Kuchagua Mwenzi wa Ndoa

MWANAMKE MSEJA ALIULIZWA, “JE, UMEPATA KUFIKIRIA JUU YA KUOLEWA?” “KUFIKIRIA?” AKAJIBU MARA MOJA. “NAHANGAIKA.”

MAELEZO hayo mafupi ya mwanamke huyo yaeleza mengi kuhusu jinsi ambavyo watu fulani hutamani kupendwa na kuwa na mwenzi. Wengi huona kupata mwenzi wa ndoa kuwa mojawapo ya mambo ya maana zaidi maishani. Hivyo, ulimwenguni pote, kumekuwa na huduma chungu nzima zinazokusudiwa kusaidia watu wapate mwenzi wa ndoa. Hata hivyo, katika sehemu nyingi za ulimwengu, idadi ya ndoa zinazovunjika yapita idadi ya ndoa zenye mafanikio.

Katika nchi za Magharibi ni jambo la kawaida watu kuchagua mwenzi wao wa ndoa. Kwa upande mwingine, katika sehemu fulani za Afrika na Asia, kungali na ndoa za kupangwa kidesturi. Kwa vyovyote vile, utaratibu huo haupaswi kuchukuliwa kivivi hivi. Maamuzi mengine machache ambayo mtu hufanya maishani yanaweza kuleta furaha au huzuni kwa kadiri ileile. Ndoa yenye upendo yaweza kupendeza zaidi na kutosheleza. Kinyume na hilo, kifungo chenye ugomvi chaweza sikuzote kuwa chanzo cha maumivu na mkazo wa akili.—Mithali 21:19; 26:21.

Wakristo wa kweli, kama watu wengine, wanataka kifungo chao cha ndoa kiwaletee shangwe na uradhi. Lakini pia wanatamani kumpendeza Mungu na kumheshimu. (Wakolosai 3:23) Mungu akiwa Muumba na Mwanzilishi wa ndoa, anajua kindani yaliyo mahitaji yetu halisi na yaliyo bora kwetu. (Mwanzo 2:22-24; Isaya 48:17-19) Mbali na hilo, amejionea mamilioni mengi zaidi ya ndoa, zilizo nzuri na zilizo mbaya, kwa maelfu ya miaka ya kuwapo kwa binadamu. Anajua linalosaidia na lisilosaidia. (Zaburi 32:8) Kupitia Neno lake Biblia, yeye huweka waziwazi, kanuni hususa zinazoweza kusaidia Wakristo wafanye uchaguzi unaotegemea ujuzi. Ni zipi baadhi ya kanuni hizo?

Angalia Zaidi ya Sura ya Nje Tu

Kule ambako watu wako huru kuchagua mwenzi wa ndoa, huenda wakakutana kijuu-juu na watakaokuwa wenzi wao au wakajulishwa na rafiki zao au familia zao. Mara nyingi, kupendezwa kimahaba huchochewa na uvutio wa kimwili mara ya kwanza. Ingawa hicho kwa hakika ni kichocheo cha asili na chenye nguvu, Biblia hututia moyo tuangalie zaidi ya sura ya nje tunapofikiria kufunga ndoa.

“Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; bali mwanamke amchaye BWANA, ndiye atakayesifiwa,” yasema Mithali 31:30. Mtume Petro alisema juu ya “vao lisilofisidika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.” (1 Petro 3:4) Naam, sifa za kiroho za atakayekuwa mwenzi—ujitoaji wa mtu huyo kwa Mungu na upendo kwa Mungu na vilevile utu wake wa Kikristo—ni za maana zaidi ya urembo wa kimwili. Ni jambo la muhimu kutumia wakati katika kufanya uchaguzi ufaao, ukichagua mtu anayeshiriki miradi ileile ya kiroho na ambaye anajitahidi kuonyesha matunda ya roho ya Mungu. Hilo litachangia zaidi kuwa na kifungo cha ndoa chenye furaha.—Mithali 19:2; Wagalatia 5:22, 23.

‘Oa au Olewa Katika Bwana Tu’

Kuwa na miradi na itikadi zinazofanana na mtu unayetaka kufunga ndoa naye ni jambo la maana sana. Ndoa ni jambo gumu, likitaka wenzi wote wafanye marekebisho mengi katika tabia na mtazamo. Kwa wazi, kadiri unavyokuwa na mambo mengi yanayofanana na atakayekuwa mwenzi wako, ndivyo itakavyokuwa rahisi kufanya marekebisho hayo.

Hilo hutusaidia kuona kwa nini mtume Paulo alisihi Wakristo waepuke “[kufungiwa] nira pamoja na wasioamini.” (2 Wakorintho 6:14) Paulo alijua kwamba kuoa mtu ambaye hana imani ileile na uelewevu uleule wa kanuni za Biblia kwaweza kutokeza mabishano na kutoelewana. Sihi yenye upole ya ‘kuoa au kuolewa katika Bwana tu’ inafaa. (1 Wakorintho 7:39) Hiyo huonyesha kufikiri kwa Mungu. Wale wanaoifuata kwa hekima huepuka magumu na matatizo mengi mabaya sana.—Mithali 2:1, 9.

Ndoa za Kupangwa

Vipi maeneo ambayo ndoa za kupangwa zingali desturi? Kwa kielelezo, kusini mwa India, wengine wamekadiria kwamba asilimia 80 ya ndoa zote zimepangwa na wazazi. Iwe wazazi Wakristo hufuata au hawafuati desturi hiyo ni uamuzi wa kibinafsi. Kwa vyovyote, ndoa hizo zilizopangwa hufaulu zaidi, maadili ya kiroho yanapotangulizwa.

Wale wanaopendelea ndoa za kupangwa huhisi kwamba hilo huweka utaratibu wa kufanya uamuzi mikononi mwa watu wenye uzoefu na wakomavu. “Wazazi wengine hufikiri kwamba kwa sababu ya umri wa watoto wao na ukosefu wa uzoefu, hawawezi kutegemewa kufanya uamuzi ufaao kuhusu ukomavu wa kiroho wa atakayekuwa mwenzi wao,” asema mzee mmoja Mkristo katika Afrika. “Vijana hawana uzoefu maishani nao huenda wakaamua mambo kulingana na hisia-moyo,” aongezea kusema mhudumu mwenye kusafiri kutoka India. Kwa kuwa wazazi wanajua tabia ya watoto wao vizuri kuliko mtu mwingine yeyote, wanahisi kwamba wako katika hali ya pekee ya kuwachagulia kwa hekima watoto wao. Pia watakuwa na hekima kufikiria maoni ya mwanamume na mwanamke huyo kijana.

Hata hivyo, wazazi wanapopuuza kanuni za Biblia, wanaweza kupatwa na matokeo yasiyofaa ndoa hiyo inapokuwa na magumu baadaye. Kwa sababu mara nyingi hakuna nafasi ya kutosha mapema ili wanaotazamia kuoana kujuana vizuri, huenda matatizo yakatokea. Na yatokeapo, aeleza baba Mkristo katika India, “mwelekeo huwa kulaumu wazazi.”

Kwa wazazi Wakristo wanaopanga ndoa, lazima wafikirie kwa uangalifu nia. Miradi ya kimwili au tamaa ya kupata sifa inapoongoza uchaguzi wa mwenzi wa ndoa, matatizo hutokea. (1 Timotheo 6:9) Kwa hiyo, wale wanaopanga ndoa wanapaswa kujiuliza hivi, ‘Je, uchaguzi huu utahakikisha furaha na hali nzuri ya kiroho kwa wenzi wote wawili? Au badala yake ni kuboresha hali ya familia au utajiri au kupata faida za kifedha?’—Mithali 20:21.

Shauri la Biblia liko wazi na ni lenye mafaa. Mtu anapofikiria kupata mwenzi wa ndoa, wema-adili na hali ya kiroho ya atakayekuwa mwenzi wake sikuzote yapasa kuwa mambo ya kuhangaikia, bila kujali jinsi uchaguzi huo utakavyofanywa. Jambo hilo lifanywapo, Yehova Mungu, yule Mwanzilishi wa mpango wa ndoa, anaheshimiwa na wale wanaofunga ndoa wanaweza kuanza ndoa yao kwenye hali imara ya kiroho. (Mathayo 7:24, 25) Hilo litachangia kifungo chenye furaha, chenye kupendeza.y

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki