Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 10/22 kur. 8-11
  • Ushirikina—Kwa Nini Ni Hatari Sana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ushirikina—Kwa Nini Ni Hatari Sana?
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Simulizi Lenye Kuelimisha
  • Chanzo Hatari
  • Hirizi za “Bahati Njema” na Ibada ya Sanamu
  • Jinsi Tunavyoweza Kujua juu ya Wakati Ujao
  • Wakati Ujao Mtukufu Unaoahidiwa na Mungu
  • Je, Kuna Upatano Kati ya Ushirikina na Mafundisho ya Biblia?
    Amkeni!—2008
  • Ushirikina—Mbona Umedumu Sana?
    Amkeni!—1999
  • Je, Ushirikina Unaongoza Maisha Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Dini ya Kweli Inafukuzia Mbali Woga Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 10/22 kur. 8-11

Ushirikina—Kwa Nini Ni Hatari Sana?

JE, USHIRIKINA unaweza kukudhuru? Huenda baadhi ya watu wakapuuza kabisa wazo hilo au wakapunguza hatari hiyo. Hata hivyo, katika kitabu chake Believing in Magic—The Psychology of Superstition, Profesa Stuart A. Vyse aonya: “Ushirikina waweza kuongoza kwenye hali mbaya ya maisha iwapo mtu atatumia fedha nyingi kwa watabiri wanaotumia tufe la kioo, wapiga-ramli, wanaotabiri kwa kutumia tarakimu au Kadi za Ubashiri, au ikiwa mazoea ya mtu ya kishirikina yanamfanya awe mchezaji sugu wa kamari.” Kuruhusu ushirikina uongoze maisha yetu kwaweza kuwa na matokeo mabaya sana.

Kama tulivyoona, itikadi nyingi za kishirikina hufuatwa ili zipunguze hofu ya wakati ujao. Hata hivyo ni muhimu kutofautisha baina ya ushirikina na ujuzi wenye kutegemeka juu ya wakati ujao. Fikiria kielelezo kimoja.

Simulizi Lenye Kuelimisha

Mnamo 1503, baada ya kuvinjari pwani ya Amerika ya Kati, Christopher Columbus alifaulu kufikisha vyombo vyake viwili vya mwisho katika ufuo wa kisiwa kinachoitwa sasa kisiwa cha Jamaika. Hapo mwanzoni, wakazi wa kisiwa hicho waliwapa chakula kwa ukarimu wavumbuzi waliokwama. Hata hivyo, punde si punde, matendo maovu ya mabaharia yaliwafanya wakazi hao wakome kuwapa chakula. Hali ilizidi kuwa mbaya, kwa kuwa muda mrefu ungepita kabla ya meli nyingine kuwasili ili kuwaokoa.

Kulingana na simulizi hilo, Columbus alichunguza kitabu chake cha matukio ya mwaka na akapata kwamba kupatwa kamili kwa mwezi kungetukia Februari 29, 1504. Kwa kutegemea ushirikina wa wakazi wa kisiwa hicho, aliwaonya kwamba endapo wangekataa kuwapa mabaharia wake chakula basi giza lingefunika mwezi. Wakazi hao walipuuza onyo hilo—mpaka kupatwa kwa mwezi kulipoanza! Ndipo, “kwa kilio kikubwa na maombolezo,” wakaja “mbio kutoka kila upande kuelekea zile meli wakiwa wamebeba vyakula vingi.” Wavumbuzi hao waliandaliwa vyakula kwa muda wote waliokaa hapo.

Wakazi wa kisiwa hicho waliona kwamba Columbus alikuwa amefanya mzungu wa ajabu. Lakini mkataa wao ulikuwa wa kishirikina tu. Kwa kweli, “utabiri” huo ulitegemea mizunguko ya kawaida ya dunia, mwezi, na jua. Waastronomia wanaweza kutabiri kwa usahihi kupatwa kwa mwezi au jua muda mrefu kabla hakujatukia, na habari hizo huandikwa katika vitabu vya matukio ya mwaka. Zaidi ya hayo, mizunguko dhahiri ya magimba ya kimbingu huwawezesha waastronomia kujua mahali barabara yatakapokuwa wakati wowote ule. Kwa hiyo, gazeti la habari litangazapo wakati wa macheo au wa machweo, unaliona kuwa jambo hakika.

Kwa kweli, Muumba Mtukufu wa magimba ya kimbingu ndiye chanzo cha habari inayochapishwa juu ya wakati wa kupatwa, wa macheo, na machweo. Lakini utabiri wa wapiga-ramli, wataalamu wa maono, watabiri wanaotumia tufe la kioo, na watabiri wanaotumia kadi za ubashiri hutoka katika chanzo tofauti, kinachompinga Mungu Mweza Yote. Fikiria tunachomaanisha.

Chanzo Hatari

Katika Matendo 16:16-19, rekodi takatifu huripoti kwamba “msichana-mtumishi fulani” katika jiji la kale la Filipi aliwapa mabwana-wakubwa wake faida nyingi kwa “ufundi [wake] wa kutabiri.” Hata hivyo, simulizi hilo linasema waziwazi kwamba, chanzo cha utabiri wake hakikuwa Muumba mweza yote, bali “roho mwovu wa uaguzi.” Kwa hiyo, huyo msichana-mtumishi alipoteza uwezo wake wa kutabiri mtume Paulo alipomfukuza roho huyo mwovu.

Tunapoelewa kwamba utabiri wa aina hiyo hutoka kwa roho waovu, tunafahamu kwa nini Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilitaarifu hivi: “Asionekane kwako . . . mtu atazamaye nyakati mbaya [mwaguzi], wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo [mwasiliani-roho], wala mchawi . . . Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Kwa hakika, adhabu iliyotolewa na Sheria kwa ajili ya mazoea hayo ilikuwa kifo.—Mambo ya Walawi 19:31; 20:6.

Huenda ukashangaa kujua kwamba mazoea mengi ya kishirikina yanayoonekana kuwa yasiyodhuru yanaongozwa na roho waovu. Na bado, Biblia husema kwamba Shetani ‘hujigeuza umbo mwenyewe kuwa malaika wa nuru.’ (2 Wakorintho 11:14) Shetani na roho wake waovu wanaweza kufanya mazoea hatari yaonekane kuwa yasiyodhuru, hata yenye manufaa. Nyakati nyingine, huenda wakatunga mambo ya ajabu na kuyafanya yatukie kihalisi, huku wakidanganya watazamaji katika kufikiri kwamba ndege hizo zatoka kwa Mungu. (Linganisha Mathayo 7:21-23; 2 Wathesalonike 2:9-12.) Hilo hueleza kwa nini mambo fulani yanayotabiriwa na watu wanaodai kuwa na uwezo wa pekee hutukia nyakati nyingine.

Bila shaka, watu wengi wanaodai kuwa na uwezo wa pekee ni wajanja, walaghai tu, wanaowapora fedha watu wasiojihadhari. Lakini wawe ni walaghai au la, wote hutumiwa sana na Shetani ili kuwapotosha watu wasimfuate Yehova, na kuwapofusha kwa “habari njema yenye utukufu.”—2 Wakorintho 4:3, 4.

Hirizi za “Bahati Njema” na Ibada ya Sanamu

Namna gani hirizi za “bahati njema” na mazoea ya kishirikina yanayofuatwa na watu ili wapate hisi ya usalama na kudhibiti matukio yasiyotazamiwa maishani? Mambo hayo hutokeza kwa hila hatari kadhaa. Kwanza, huenda mtu mshirikina akaruhusu maisha yake yaongozwe na kani zisizoonekana. Anapuuza kabisa mantiki na sababu, badala yake anafuata hofu isiyo na msingi.

Mwandikaji mmoja ataja hatari nyingine ya kiasili. Yeye asema: “Mtu fulani anapotegemea kulindwa na hirizi ya bahati njema halafu inakosa kumlinda, huenda mtu huyo akaelekea kulaumu wengine kwa sababu ya msiba [unaompata], badala ya kukubali daraka hilo mwenyewe.” (Linganisha Wagalatia 6:7.) Kwa kupendeza, mwandishi wa insha Ralph Waldo Emerson alisema hivi wakati mmoja: “Watu hafifu huamini bahati . . . Watu wenye nguvu kiadili huamini sababu na matokeo.”

Mara nyingi “sababu na matokeo” katika maisha yetu hutokeza matukio ya ghafula—‘wakati na tukio lisilotazamiwa’ ambalo hutupata sote. (Mhubiri 9:11) Matukio yasiyotazamiwa hayatokani na mawazo tu ya kigeugeu ya “bahati njema.” Wakristo wanajua kwamba mazoea ya kishirikina na hirizi za kimizungu haziathiri hata kidogo matokeo ya matukio yasiyotazamiwa. Mambo hayo yanapotukia, sisi hukumbuka ukweli huu wa Biblia: “Hamjui uhai wenu utakuwa nini kesho. Kwa maana nyinyi ni ukungu unaotokea kwa muda kidogo na kisha kutoweka.”—Yakobo 4:14.

Zaidi ya hayo, Wakristo wa kweli wanajua kwamba kwa kawaida staha ya kiibada hutolewa kwa hirizi za bahati njema vilevile kwa desturi au mazoea ya kishirikina. Kwa hiyo, Wakristo huona mambo hayo yote kuwa ibada ya sanamu, inayopingwa waziwazi katika Neno la Mungu.—Kutoka 20:4, 5; 1 Yohana 5:21.

Jinsi Tunavyoweza Kujua juu ya Wakati Ujao

Hili halimaanishi kwamba Wakristo hawajali juu ya wakati ujao. Kinyume cha hilo, kusababu kuzuri kunaonyesha waziwazi kwamba kuna faida kubwa ya kujua mambo ya wakati ujao. Kujua kwetu kimbele mambo yatakayotukia kutatuwezesha kuchukua hatua inayofaa itakayotunufaisha sisi na wapendwa wetu.

Ingawa hivyo, kuna uhitaji mkubwa wa kutafuta habari hii kutoka kwa chanzo kinachofaa. Nabii Isaya alionya: “Watu watakuambia, tafuta jumbe kwa wapiga-ramli na kwa wawasiliani . . . Nawe utawajibu, ‘Sikilizeni yale ambayo Bwana anawafundisha! Msisikilize wawasiliani—wanayowaambia hayatawafaidi kitu.’”—Isaya 8:19, 20, Today’s English Version.

Mtungaji wa Biblia ndiye chanzo kinachofaa cha habari yenye kutegemeka juu ya wakati ujao. (2 Petro 1:19-21) Kitabu hiki kilichopuliziwa kina uthibitisho chungu nzima wa kwamba unabii uliotabiriwa na Mungu mweza yote Yehova, ni wenye kutegemeka—kwa kweli, ni wenye kutegemeka kama mizunguko ya magimba ya kimbingu “inayotabiriwa” katika vitabu vya matukio visivyohesabika. Ili kutoa mfano wa usahihi kamili wa unabii wa Biblia, fikiria kielelezo hiki. Acha tuwazie kwamba mtu fulani mashuhuri leo anajitokeza na kutabiri matukio yatakayotukia miaka 200 iliyo mbele, katika mwaka wa 2199. Utabiri wake una mambo yafuatayo:

◻ Pigano kali la kijeshi litazuka kati ya mataifa ambayo kwa sasa si mataifa ya ulimwengu yenye nguvu yanayopingana, na matokeo yake yatabadili historia.

◻ Mbinu itakayotumiwa itahusisha kazi kubwa ya uhandisi ya kugeuza mkondo wa mto mkubwa.

◻ Jina la mshindi linatajwa—miaka mingi hata kabla hajazaliwa.

◻ Mwisho wa taifa litakaloshindwa unaelezwa, na kuongeza muda wa utabiri huo hadi karne nyingi baadaye.

Endapo utabiri huu wote ungetimizwa, je, usingeliwafanya watu wazingatie mambo mengine yaliyotabiriwa juu ya wakati ujao na mtu huyo?

Mambo ambayo tumeyaeleza yalitukia kihalisi. Miaka ipatayo 200 kabla ya Wamedi na Waajemi kuipindua Babiloni, Yehova alitabiri yafuatayo kupitia nabii Isaya:

◻ Pigano kali la kijeshi lingezuka kati ya Babiloni na Muungano wa Umedi na Uajemi.—Isaya 13:17, 19.

◻ Mbinu itakayotumiwa itahusisha kukaushwa kwa handaki la mto unaolinda. Kwa kuongezea, malango ya jiji hilo lenye kuta imara yangeachwa wazi.—Isaya 44:27–45:2.

◻ Mshindi angeitwa Koreshi—aliyetabiriwa miaka ipatayo 150 kabla hajazaliwa.—Isaya 45:1.

◻ Halafu, Babiloni ungeangamizwa kabisa.—Isaya 13:17-22.

Utabiri huo wote ulitukia barabara. Basi je, haistahili utumie wakati na jitihada zako katika kuzingatia unabii mwingine uliotabiriwa na Yehova katika Neno lake lililoandikwa?

Wakati Ujao Mtukufu Unaoahidiwa na Mungu

Biblia hutabiri nini? Biblia huahidi kwamba katika ulimwengu mpya utakaoletwa na Mungu, hakuna mtu atakayeteseka kwa sababu ya ukosefu wa usalama kuhusu wakati ujao. Angalia uhakikisho wa Mungu kwa wale watakaoishi wakati ule: “Hapana mtu atakayewatia [watu wangu] hofu.”—Mika 4:4.

Biblia yaendelea kuahidi kwamba Mungu ‘ataufumbua mkono wake, na kukishibisha kila kilicho hai matakwa yake.’ (Zaburi 145:16) Je, utimizo wa unabii huo uko mbali sana? La hasha! Miaka mingi mapema Biblia iliahidi kwamba hali tunazoziona duniani leo huthibitisha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo mwovu wa mambo uliopo.—2 Timotheo 3:1-5.

Karibuni Muumba mwenye upendo atakomesha hali mbovu zilizopo. Atakomesha vita vyote, visababishi vya ukosefu wa usalama ulimwenguni pote na kuteseka. Zaidi ya hayo, chuki, ubinafsi, uhalifu, na jeuri hayatakuwapo tena milele. Biblia inaahidi: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.

Miongoni mwa baraka nyingi ambazo watu watafurahia katika ulimwengu huo mpya ni afya bora. Hata kifo na majonzi yanayoletwa nacho hayatakuwapo tena. Mungu mwenyewe asema: “Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.”—Ufunuo 21:4, 5.

Wakati huo hakuna mwanadamu atakayehatarishwa na matukio yasiyotazamiwa yanayobadili maisha na kusababisha vifo leo. Hakutakuwapo pia roho waovu na Shetani, wanaosababisha hofu ya kishirikina na uwongo mbaya. Kweli hizi zenye kusisimua ziko katika Biblia.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kuna uhusiano mkubwa kati ya ushirikina na mazoea ya uwasiliani-roho

[Hisani]

Isipokuwa mwanamke aliye katika tufe la kioo: Les Wies/Tony Stone Images

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ushirikina hautakuwako katika ulimwengu mpya wa Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki