Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kuwapo kwa Mungu Siwezi kueleza jinsi ambavyo nilinufaika sana na mfululizo “Je, Kweli Mungu Yuko?” (Februari 8, 1999) Ulinifunza juu ya Mungu ambaye nimesikia sana habari zake japo sikuwa nimepata kumjua. Nawashukuru kwa dhati kwa kumulika kijia cha kweli kwa ajili ya watu kama mimi.
C. P., Brazili
Mwenye Kutumika Ijapokuwa Upofu Asanteni kwa ajili ya simulizi la maisha ya Polytimi Venetsianos, “Mwenye Furaha na Mwenye Kutumika Nijapokuwa Kipofu,” katika toleo la Februari 8, 1999. Moyo wangu umeguswa sana na ujasiri wake na imani yake katika Mungu. Kwa upande mmoja, mwanamke huyu wa pekee amepata hasara na shida nyingi maishani. Japo kwa upande mwingine, amenufaika sana kwa njia isiyo na kifani. Naamini kwamba simulizi lake litawasaidia sana na kuwatia moyo wote waliochoka katika mbio ngumu za uhai.
K. R., Urusi
Mavazi Nina umri wa miaka 11, sijui niseme nini katika kuwashukuru kwa ajili ya maagizo bora kabisa katika makala “Aina ya Mavazi Tunayovalia—Je, Yapasa Kufikiriwa?” (Februari 8, 1999) Hapo awali nilitaka kuvalia kama wanadarasa wenzangu. Lakini makala hii ilinisaidia kuelewa kwamba mavazi yangu yanapasa kuwa nadhifu—si yenye kufedhehesha au yenye kupita kiasi.
A. S., Estonia
Pindi kwa pindi mimi huhuzunika sana wengine wanaposema kwamba mavazi yangu ni ya kikale au ni rasmi. Makala yenu ilikuwa yenye kutia moyo sana kwa sababu ilithibitisha kwamba kufuata kanuni za Biblia kunafaa.
R. L., Brazili
Kwa miaka mingi niliwasikitikia na kuwachekelea Mashahidi wa Yehova. Ndipo nilipopewa na rafiki yangu nakala ya toleo la Amkeni! la Februari 8, 1999. Nilifurahia sana kusoma gazeti hilo na lilibadili maoni yangu juu ya Mashahidi. Makala iliyonivutia sana hasa ni ile iliyohusu mavazi, ilieleza zoea nililo nalo ninaponunua mavazi. Wakati ujao, sitakazia sana mavazi ya kimtindo. Nitamwomba rafiki yangu aniletee magazeti yenu zaidi ya kusoma!
U. B., Ujerumani
Viuavisumbufu Mke wangu nami tulipendezwa sana na makala “Viuavisumbufu Huua Zaidi ya Wadudu.” (Februari 22, 1999) Tukiwa wanamazingira, tumejaribu kukabiliana na kusumishwa kwa dunia hii. Inatia moyo kujua kwamba kuna watu huko Brazili, China, na nchi nyinginezo wanaohangaikia jambo hilo na ambao wanafanya kazi muhimu.
W. G., Kanada
Porojo Nawashukuru sana kwa ajili ya makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Porojo Ni Mbaya?” (Februari 22, 1999) Muda fulani uliopita, mimi binafsi niligundua jinsi porojo inavyoweza kuumiza, mtu fulani alipoeneza uvumi wa kwamba mimi ndiye ningefuata kutengwa kutanikoni. Uwongo huo uliniumiza sana! Mweneza-uvumi huyo aliomba msamaha, lakini utumainifu wangu kwake ulikwisha.
R. M., Uswisi
Porojo imeenea sana katika shule yetu, kwa hiyo makala hiyo ilinitia moyo sana na kuniimarisha. Ninaaibika kusema kwamba nimechafua sifa nzuri ya wengine kwa kupiga porojo. Hata nimechangia na kusikiliza maongezi ya marafiki ambao wamenena mabaya kuhusu wengine. Kwa hiyo niliposoma makala hiyo, nilishtuka na nikahisi kwamba kila sentensi ilikuwa ikinishauri juu ya mambo niliyokuwa nikifanya. Nimeaibikia porojo yote ambayo nimewahi kueneza. Najua kwamba porojo itaendelea shuleni mwetu, lakini nimeazimia kusimama imara na kutoshiriki porojo.
M. W., Japani