Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Mavazi Nawaandikia kuhusu makala “Aina ya Mavazi Tunayovalia—Je, Yapasa Kufikiriwa?” (Februari 8, 1999) Nathamini jitihada zenu katika kutuandalia “chakula kwa wakati ufaao.” (Mathayo 24:45) Ijapokuwa baadhi ya maelezo katika makala hiyo yalionekana kuwa maoni ya kibinafsi. Kusema kwamba “T-shati zinazotangaza bingwa umpendaye wa sinema au wa michezo . . . zaweza kukuchochea uabudu mashujaa—ibada ya sanamu” ni jambo lisilofaa. Inawezekana kumpenda, au hata kuvutiwa na mwanariadha bila kuvunja sheria za Biblia.
M. D., Ufaransa
Tunathamini maelezo haya manyofu, lakini hatukunuia kuweka sheria au kuanzisha kanuni ya mavazi. Makala yetu iliwatia moyo wasomaji watumie “utimamu wa akili” wanapofanya uchaguzi wao juu ya mavazi. (1 Timotheo 2:9, 10) Maelezo juu ya T-shati hayakulazimisha kauli bali yalikiri uwezekano wa kwamba kuvaa mitindo fulani kwaweza kumwathiri mvaaji mwenyewe. Ingawa huenda kusiwe na kosa lolote katika kuvutiwa na ustadi au kipaji cha mtu fulani, je, lingekuwa jambo la hekima kwa Mkristo kuvaa kitu ambacho wengine wanapokiona wangefikiri kwamba unavutiwa na mtindo-maisha na maadili ya mtu asiyeishi kupatana na viwango vya Biblia?—Mhariri.
Mhamishwa Katika Siberia Niliguswa sana na simulizi lenye kustaajabisha la Lembit Toom, “Nusu Karne Chini ya Utawala wa Kiimla” (Februari 22, 1999), hivi kwamba singeweza kujizuia kuonyesha uthamini wangu. Imani yenye nguvu kwa Yehova Mungu ndiyo iliyomsaidia kuokoka nyakati hizo ngumu. Kwa kweli ndugu zetu katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti wanastahili uhuru walio nao sasa.
J. D., Marekani
Mti Ambao Huimba Shukrani za kuhisiwa moyoni kwa ajili ya makala mnazochapisha kuhusu vitu vya asili. Nilithamini hasa makala “Mti Ambao Huimba.” (Machi 8, 1999) Sikujua lolote juu ya whistling thorn. Baada ya kusoma juu ya wimbo unaotokezwa wakati miiba yake mirefu na vinundu vyenye mashimo vinapotikisika kwenye upepo, nilifikiria Zaburi 96:12, 13: “Miti yote ya mwituni iimbe kwa furaha mbele za BWANA.” Mti huo usio wa kawaida humsifu Yehova kwa njia ya pekee.
M. D., Italia
Rio de Janeiro Nikiwa Mcarioca, mkazi wa Rio, makala yenu “Rio de Janeiro—Maridadi na Lenye Kuvutia” (Machi 8, 1999) ilinipendeza sana na kunielimisha. Waandishi wa habari wenye kuchochea hisia wameharibu sana sifa ya Rio.
O. D. C., Brazili
Habari yenu ilikuwa imetayarishwa kwa uangalifu kama kawaida. Mliepuka kueleza maoni hasi juu ya watu maskini, ambao hulaumiwa mara nyingi kwa ajili ya matatizo ya kijamii ya Rio.
V. R. L., Brazili
Barua kwa Wazazi Nilitiwa moyo sana na makala “Barua ya Pekee kwa Wazazi Wao.” (Machi 8, 1999) Nilipaswa kuwaandikia wazazi wangu barua kama hiyo. Waliweka kielelezo kizuri katika kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ukawaida katika huduma, na ukaribishaji-wageni. Baba yangu alikuwa mtumishi wa huduma; lazima awe alikuwa na shughuli nyingi za kutaniko. Na bado, alitupangia tafrija, na hatukuwaonea wivu kamwe wanashule wenzetu. Alikufa katika aksidenti ya gari alipokuwa akirejea nyumbani kutoka katika mkusanyiko wa Kikristo, na maisha yetu yakabadilika ghafula. Mimi hutiwa moyo kuendelea kumtumikia Yehova nikumbukapo mtindo-maisha wake wa kuweka Ufalme kwanza na imani ya mama yangu.
S. K., Japani