Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g02 9/8 kur. 26-27
  • Sala Ambazo Mungu Husikia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sala Ambazo Mungu Husikia
  • Amkeni!—2002
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ahadi za Mungu
  • Kushughulikia Matatizo ya Kibinafsi
  • Mkaribie Mungu Katika Sala
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Jinsi ya Kusali na Kusikiwa na Mungu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Je! Mungu Anasikiliza Sala Zako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Namna ya Kupata Msaada kwa Sala
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2002
g02 9/8 kur. 26-27

Maoni ya Biblia

Sala Ambazo Mungu Husikia

“Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa; fulizeni kutafuta sana, nanyi mtapata; fulizeni kubisha hodi, nanyi mtafunguliwa. Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta sana hupata, na kwa kila mtu anayebisha hodi hufunguliwa.”—LUKA 11:9, 10.

WAKIWA na tumaini hakika katika maneno ya Yesu Kristo yaliyoonyeshwa hapa juu, Wakristo wengi husali kwa Mungu kuhusu matatizo na mahangaiko yao, wakitumaini kwamba anawapenda na kuwajali. Hata hivyo, wengine huvunjika moyo wanapongoja majibu ya sala zao. Je, unaona kama sala zako hazijibiwi? Je, Mungu husikiliza unaposali?

Hata kama sala zako zinaonekana kama hazijibiwi, hiyo haimaanishi kwamba Mungu hakuzisikia. Biblia inatuhakikishia: “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yaelekea dua zao.” (1 Petro 3:12) Hivyo, Yehova husikia sala za waadilifu, ziwe zinatolewa kwa sauti au zinasemwa moyoni. (Yeremia 17:10) Yehova pia huchunguza mtazamo na hisia za kila mmoja anayesali, mambo ambayo huenda mtu anayesali asiyatambue au kuyaelewa kikamili.—Waroma 8:26, 27.

Hata hivyo, ni lazima sala zetu zitimize matakwa fulani ili Mungu azikubali. Kwanza, ni lazima zielekezwe kwa Mungu peke yake—si kwa Yesu, “mtakatifu fulani,” au kwa sanamu. (Kutoka 20:4, 5) Ni lazima pia sala zitolewe katika jina la Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. (Yohana 14:6) Je, hiyo inamaanisha kwamba Yesu husikia sala zetu halafu kuzituma kwa Mungu? La. Badala yake, tunaposali kwa Yehova katika jina la Yesu, tunajitambulisha kuwa wanafunzi wa Yesu. Pia, tunatambua kwamba ni kupitia fidia yake tu tunaweza kumfikia Mungu.—Waebrania 4:14-16.

Ni lazima sala zitolewe katika imani. Mtume Paulo alisema: “Bila imani haiwezekani kumpendeza [Mungu] vema, kwa maana amkaribiaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Mtu anawezaje kujua kama ana imani ya aina hiyo? Mwandishi wa Biblia Yakobo ajibu: “Nitakuonyesha imani yangu kwa kazi zangu.” (Yakobo 2:18) Ndiyo, imani hutokeza matendo, na matendo hayo huonyesha kwamba twampenda Mungu na tunajaribu kumpendeza.

Ni lazima pia waabudu wa Mungu wadumu katika sala. Yesu alionyesha jambo hilo wazi katika Luka 11:9, 10, andiko lililonukuliwa mwanzoni. Iwapo mtu anasali mara moja tu kuhusu jambo fulani, ni wazi kwamba jambo hilo si muhimu kwake.

Ahadi za Mungu

Haidhuru tunasali kwa bidii kadiri gani au tunaomba mara ngapi, bado tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Ingawa Yesu alisema wanafunzi wake wangekuwa na furaha, yeye hakusema kwamba hawangepata matatizo. (Mathayo 5:3-11) Hata hivyo, yeye alisema kwamba wanafunzi wake wangekuwa na furaha kujapokuwa maombolezo, njaa, kiu, au minyanyaso.

Furaha ambayo Yesu alizungumzia haingetokana na kukosa matatizo. Bali ingetokana na kuridhika kwa sababu tunamtumikia Mungu. Hivyo, tunaweza kupata furaha kiasi fulani yajapokuwa matatizo.—2 Wakorintho 12:7-10.

Kushughulikia Matatizo ya Kibinafsi

Basi je, ni kazi bure kusali kwa Mungu kuhusu matatizo ya kibinafsi kama vile kupata mwenzi wa ndoa au kushughulikia jamaa, afya, au matatizo ya kazi? Sivyo, kwa sababu ingawa Mungu haahidi kuyaondoa matatizo yetu kimuujiza, anaweza kutupatia hekima ya kuyashughulikia. Yakobo aliandika hivi kuhusu majaribu: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yakobo 1:5) Kwa hiyo, Yehova atatuongoza kupitia roho yake. Hiyo itatusaidia kuzielewa kanuni za Biblia na kuzitumia tunapofanya maamuzi.

Bila shaka, roho ya Mungu haitatuamulia mambo. Jitihada ya kibinafsi inahitajika. Kwa mfano, ikiwa tuna tatizo, je, tumefanya utafiti kulihusu na kuchunguza mambo yanayohusika? Tendo hilo lingeonyesha kwamba tuna imani. (Yakobo 2:18) Je, tumejaribu tena na tena kusuluhisha tatizo letu, tukiendelea kuomba mwongozo wa Mungu? (Mathayo 7:7, 8) Je, tumechunguza kwa makini kanuni za Biblia zinazohusika? Neno la Mungu litatufanya tuwe watu ‘hodari, walioandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Timotheo 3:16, 17)

Ingawa Mungu anaweza kuingilia mambo ya wanadamu na kutuondolea matatizo, yeye ameturuhusu tutumie hiari yetu. Kwa kusikitisha, wengi hutumia hiari hiyo kwa hasara ya wengine. Kwa hiyo, huenda matatizo mengine tunayosali yakomeshwe yataendelea hadi ulimwengu mpya wa Mungu uje. (Matendo 17:30, 31) Labda ni hali fulani mahali tunapoishi, kama vile uhalifu au vita; ama huenda ni kuvumilia magumu fulani yanayoletwa na wapinzani. (1 Petro 4:4) Ni lazima tukubali kwamba katika ulimwengu huu mwovu, hali fulani hazitakuwa bora.

Hata hivyo, Mungu anawapenda watumishi wake na anataka kuwasaidia. Wakati Ufalme wake pekee utakapoitawala dunia, yeye ataondoa kabisa matatizo mabaya ya ulimwengu huu. (Ufunuo 21:3, 4) Hadi wakati huo, tunapaswa kuomba msaada wake kwa bidii ili tuweze kukabiliana na matatizo maishani. Tukifanya hivyo, tutakuwa na uhakika kwamba Yehova atatimiza ahadi iliyorekodiwa katika kitabu cha Biblia cha Isaya 41:10: “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki