Maoni ya Biblia
Kuanzisha Urafiki Ukiwa na Lengo la Kufunga Ndoa
Julie na Lee walikuwa na urafiki wa kimapenzi na walikuwa wameazimia kubaki wakiwa safi kiadili.a Lakini jioni moja, walipokuwa peke yao, hisia zao za ngono zikaanza kupanda. Jambo la kupendeza ni kwamba walirudiwa na fahamu kabla hawajafanya kosa zito.
IBADA ya kweli inahusisha mengi zaidi ya kuhudhuria ibada ya kidini kila juma. Ni njia ya maisha inayoathiri mwenendo na viwango vya maadili vya mtu. Yesu Kristo alisema kuwa Mungu atawakubali tu wale ‘wanaofanya mapenzi’ Yake. (Mathayo 7:21) Ili kumpendeza Mungu, tunahitaji kuhakikisha kuwa uhusiano wetu na watu wa jinsia tofauti ni wenye kuheshimika na kwamba tunaanzisha urafiki wa kimapenzi tukiwa tu na lengo la kufunga ndoa.
Tunaweza kuhakikishaje kuwa uhusiano wenu ni safi machoni pa Mungu, hasa wakati huu ambapo watu wanashinikizwa kuvunja uaminifu wao wa maadili? Kwanza, tambua kwamba viwango vya Mungu viliwekwa ili kutufaidi. Pili, kubali ukweli wa kwamba sisi si wanadamu wakamilifu. Tatu, jiwekeeni mipaka mapema ya mwenendo ambao mtaepuka. Na nne, mhusisheni Mungu katika uhusiano wenu. Hebu tupitie hoja hizo moja baada ya nyingine.
Viwango Viliwekwa Ili Kutufaidi
Katika Isaya 48:17, 18, tunasoma hivi: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake. Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.”
Kwa kweli, amri na kanuni zilizo katika Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho, Biblia Takatifu, ziliandikwa ili kutufaidi. (2 Timotheo 3:16, 17) Ni uthibitisho wa wazi kwamba Muumba wetu anatujali sana na anataka tuwe na furaha na tufanikiwe katika kila sehemu ya maisha. (Zaburi 19:7-10) Je, hivyo ndivyo unavyohisi moyoni? Ikiwa ndivyo, unaonyesha hekima ya kweli.
Usijiamini Kupita Kiasi
Kama rafiki wa kweli, Yehova anatuambia ukweli kutuhusu. Kwa mfano, Neno lake linatuonya kuwa “moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” (Yeremia 17:9) Pia Biblia inasema: “Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mjinga, lakini yeye anayetembea katika hekima ndiye atakayeponyoka.”—Methali 28:26.
Watu wawili wa jinsia tofauti wanaweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanategemea mioyo yao wenyewe? Njia moja ni kujiingiza katika hali ambazo zinaweza kuwashawishi kutenda mambo yasiyofaa, kama mfano uliotajwa mapema. Njia nyingine ni kwa kupuuza mashauri yenye hekima ya wazazi wanaomwogopa Mungu. Wazazi hao wanajua kuwa hisia za ngono ni kama injini yenye nguvu ambayo inahitaji kudhibitiwa vizuri, hasa mtu anapokuwa kijana.
Kwa hiyo, vijana ‘wanaotembea katika hekima ya kimungu,’ huchukua kwa uzito mashauri ya wazazi wao. Kwa kweli, wanayachukua kwa uzito kwa kuwa wanajua wazazi wao wanawapenda sana hivi kwamba wanaweza kusema mambo ambayo huenda watoto wao hawataki kusikia. Bila shaka, Baba yako wa mbinguni, Yehova Mungu, anakupenda hata zaidi na anakushauri ‘uondoe masumbuko moyoni mwako, na uondolee mbali msiba kutoka katika mwili wako.’ (Mhubiri 11:9, 10) Utafanya hivyo jinsi gani? Kwa kukataa tamaa zisizofaa.
Wekeni Mipaka ya Mwenendo wa Kuepuka
“Wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” (Methali 13:10) Wenzi wenye busara wanapoanza uhusiano, wao hutii maneno ya andiko hilo kwa kukubaliana wataonyeshana upendo kwa kiasi gani na jinsi gani na kuazimia kutovuka mipaka hiyo. Kuonyeshana upendo kwa njia isiyofaa au kujiamini kupita kiasi ni kama kuendesha gari vibaya. Itakuwa kuchelewa mno kuamua kufuata sheria za barabarani unapotolewa kwenye gari lililopatwa na aksidenti!
Biblia inasema: “Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.” (Methali 22:3, Biblia Habari Njema) Wenzi wanaweza kuepuka matatizo haya yote kwa kukutana wakiwa katika kikundi cha watu au wakiwa na mtu wa tatu anayefaa. Madhara yanayoweza kutokea kwa sababu watu hawakuwa waangalifu yanatia ndani kusumbuliwa na dhamiri, kutojiheshimu, kukosa kumheshimu mwenzako, kujiaibisha, na kuwaaibisha wote wanaohusika kutia ndani watu wa familia. Hivyo, uwe mwangalifu; kubali kufuata kanuni za Maandiko na uazimie kutoziacha!
Mfanye Yehova Awe ‘Nyuzi ya Tatu’
Ndoa ni kama kamba yenye nyuzi tatu, Mungu akiwa ndiye uzi mkuu. Andiko la Mhubiri 4:12, linasema hivi: “Kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.” Kanuni hiyo inaweza pia kutumiwa na wenzi wanaochumbiana. Wale wanaotaka baraka za Mungu katika uhusiano wao, wanazipata wanapokuwa karibu naye kibinafsi. Zaburi 1:1-3 linasema hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu . . . Bali mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku . . . , na kila jambo analofanya litafanikiwa.”
Ndiyo, mtu anaweza kufanikiwa kikweli maishani, kutia ndani kufanikiwa wakati wa uchumba na katika ndoa, akifanya mambo kulingana na maoni ya Yehova. Kwa kweli, yeye ndiye Muumba wetu, na kuvutiwa na mtu kimahaba na ndoa ni zawadi zenye thamani kutoka kwake. Hivyo, tunahitaji kuheshimu sana zawadi hizo.—Yakobo 1:17.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
JE, UMEJIULIZA HIVI?
● Tunajua jinsi gani kuwa Mungu anatutakia mema wakati wote?—Isaya 48:17, 18.
● Ni jambo gani tunalopaswa kukubali kujihusu?—Yeremia 17:9.
● Ni nini siri ya kufaulu mnapochumbiana na pia baadaye katika ndoa?—Zaburi 1:1-3.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Wenzi wenye busara wanapoanza uhusiano, wao hukubaliana wataonyeshana upendo kwa kiasi gani na jinsi gani na kuazimia kutovuka mipaka hiyo inayopatana na Maandiko