Kundi Lililotiwa Mafuta Kuutangaza Ufalme
1. Ni nini yaliyokuwa maulizo juu ya wokovu wa ulimwengu miaka elfu mbili iliyopita?
MAULIZO yanayohusu ulimwengu wote yanatukabili leo. Yanahusiana na maulizo ambayo tungeyakabili ikiwa tungalikuwa tukiishi Mashariki ya Kati yapata miaka elfu mbili iliyopita. Wakati huo maulizo haya yalihusu ulimwengu wote kwa sababu yalihusu mwokozi wa ulimwengu wote, Masihi! Wakati wa kujitokeza kwake kwa mara ya kwanza ulikuwa umefika. Hivyo watu wenye kupendezwa walikuwa wakimtazamia. Je! angeshangiliwa kwa furaha na ulimwengu wote wa wanadamu ajitokezapo? Au je! angewakatisha tamaa kwa kufanya yale aliyokuwa ameagizwa afanye wakati huo? Ni nani ambao wangesadikishwa kwamba yeye alikuwa Masihi ambaye alifanya yale yale ambayo Maandiko Matakatifu yalitabiri juu yake, hivyo wamfuate kama Kiongozi wao? Ni nani ambao hawangechukizwa naye bali wangevutwa waje kwake? Ni nani leo wanaovutwa kwa Masihi mwenye kuokoa ulimwengu, na namna gani?
2. (a) Yule Mkuu wa “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu angetimiza wajibu gani? (b) Wale wengine wa “uzao” huo wa mwanamke wangekuwa nani, na wangefundishwa na nani?
2 Kwa ajili ya uongozi wetu salama leo, na tukumbuke kwamba Masihi wa kweli angekuwa Yule Mkuu wa “uzao” uliotabiriwa wa “mwanamke” wa Mungu, na ya kwamba ‘angeumizwa kisigino’ na Nyoka Mkuu, Shetani Ibilisi. “Mwanamke” huo au mama wa “uzao” huo ni tengenezo la Mungu la kimbinguni lililo kama mke ambalo washiriki wake ni viumbe vitakatifu vya kiroho, ‘wana wa Mungu wa kweli’ wa kimalaika. Washiriki wa “uzao” wa mwanamke huyo ulioahidiwa ni wana wake, Yule Mkuu akiwa ndiye Masihi na wengine wakiwa wafuasi wake wa kiroho. Kuhusu washiriki hawa wadogo wa “uzao” wa mwanamke tunayo maneno ya Isaya 54:13 kama vile yalivyoelekezwa kwa “mwanamke” wa mfano: “Na watoto wako wote watafundishwa na [Yehova]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” Kwa kufaa, ‘wana’ hawa wangefundishwa na Yehova, Mume wa kimbinguni wa mwanamke huyo, aliye Baba wa “uzao” huo.—Isa. 54:5.
3. Yesu aliyatumia maneno “watoto” juu ya nani katika Isaya 54:13, na hawa sasa wanafundishwaje pasipo kuwapo kwa kuonekana kwa Mwalimu?
3 Yule Mkuu wa “uzao” wa mwanamke, Yesu Kristo, alitumia maneno yanayoelekezwa kwa mwanamke huyo katika Isaya 54:13, Kuhusiana na jambo gani? Alipokuwa akizungumza na Wayahudi ambao hawakuvutwa kwake kama Masihi na kwa hiyo walikuwa wakinung’unika juu yake, Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho. Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na [Yehova]. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu.” (Yohana 6:44, 45) Bila shaka, Yehova si Mwalimu anayeonekana wa ye yote wetu, bali ametoa kwetu kitabu cha mafundisho kilichoongozwa kwa roho yake. Kwa hiyo kupitia kwacho na kwa utendaji wa roho yake takatifu, yeye anatufundisha mambo ya hakika juu ya “uzao” wa Kimasihi wa “mwanamke” wake. Kwa njia hiyo yeye aliwavuta kwake Masihi, Yule Mkuu wa “uzao” huu, wale washiriki wadogo, ambao ndio washiriki wa kundi.
4. Kufikia mwaka wa tatu wa utendaji wa Yesu wa hadharani, maoni ya mitume wa Yesu yalitofautianaje na yale ya watu juu ya alichokuwa?
4 Kufikia wakati huo, katika mwaka wa tatu wa utendaji wa Yesu wa hadharani, Wayahudi walipaswa kuwa wamefikia uamuzi fulani juu ya kwamba huyu mfanya miujiza alikuwa nani katika kusudi la Mungu. Ni wangapi kati yao walioonyesha kwamba walikuwa ‘wamefundishwa na Yehova’ kuhusu Masihi wake? Ulikuwa wakati wenye kufaa kwa Yesu kuuliza mitume wake juu ya jambo hili:
“Akawauliza, Je! makutano hao wanasema ya kuwa mimi ni nani? Wakamjibu wakisema, Yohana Mbatizaji; lakini wengine, Eliya; na wengine, kwamba mmoja wa manabii wa kale amefufuka. Akawaambia, Nanyi mwasema ya kwamba mimi ni nani? Petro akamjibu akasema, Ndiwe Kristo wa Mungu. Akawaonya, akawakataza wasimwambie mtu neno hilo; akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka.”—Luka 9:18-22; linganisha Marko 8:27-30.
5. Kulingana na Mathayo 16:16-19, Yesu alisema nini kwa Petro katika kujibu ulizo hilo?
5 Masimulizi ya mtume Mathayo yatoa maelezo zaidi juu ya jambo hili, yakisema: “Simoni Petro akajibu na kusema: Wewe ni Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai. Yesu akajibu, akamwambia: Heri wewe, Simoni wa Yona; kwa kuwa mwili na damu hazikukufunulia neno hili, lakini Baba yangu aliye mbinguni. Nami ninakuambia, Wewe ni Petro, na juu ya mwamba huu nitajenga kanisa langu; wala milango ya Hadeze haitalishinda. Nitakupa funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani [litakuwa limefungwa] mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, [litakuwa limefunguliwa] mbinguni.”—Mt. 16:16-19, ZSB.
6. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Petro hakuyafasiri vibaya maneno ya Yesu juu ya “mwamba,” naye Paulo alisema ni nani aliyekuwa “mwamba”?
6 Kutokana na pongezi hili alilopewa Petro ni wazi kwamba alikuwa amefunzwa na Yehova naye alikuwa amejifunza kutoka Kwake. Kwa hiyo alivutwa kwa Yesu naye akaja kwake akiwa Masihi au Kristo. Jina la Petro lamaanisha “jiwe,” au “kisehemu cha mwamba.” Walakini hili halikumaanisha kwamba ndiye aliyekuwa “mwamba” ambao juu yake Yesu angejenga kundi lake. Wala “mwamba” haukuwa ungamo ambalo Petro alikuwa amelifanya: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” “Mwamba” ulikuwa Yesu mwenyewe. Petro hakuyafahamu vibaya maneno ya Yesu. Wala hakudai kuwa “mwamba” (Kigiriki, petra) huo hata kidogo kulingana na 1 Petro 2:4-10. Na zaidi ya hayo, mtume Paulo, ambaye maandishi yake Petro alitambua kuwa sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa na Mungu, aliandika hivi: “Kwa maana waliunywea [Waisraeli jangwani] mwamba wa [ki]roho uliowafuata; na mwamba ule ni Kristo.”—1 Kor. 10:4; 2 Pet. 3:15, 16.
7, 8. (a) Mitume walidhani kwa makosa ufalme wa Masihi ungekuwa nini? (b) “Funguo” za ufalme wa mbinguni zingepewa nani, walakini kundi lingejengwa juu ya nani?
7 Wakati Yesu alipozungumza na mitume wake juu ya ufalme, walifikiria ufalme wenye msingi wake juu ya serikali ambayo ingekuwa na makao yake makuu huko Yerusalemu, ambapo Mfalme Daudi alipata kutawala. Walimtazamia Yesu kama Masihi kusimamisha serikali yake huko Yerusalemu, kama mrithi wa Mfalme Daudi. Ushuhuda wa kuonyesha kwamba hilo ndilo lililokuwa wazo lao ni kwamba walimwambia Yesu hivi baada ya kufufuliwa kwake kutoka kwa wafu: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?” (Matendo 1:6) Wakati huo, kabla ya kuadhimisha Sikukuu ya Pentekoste ya mwaka 33 C.E., hawakufahamu kwamba ufalme wa Kristo aliyefufuliwa ungekuwa wenye nguvu zipitazo za kibinadamu ambao ungetawala zaidi ya taifa la kidunia la Israeli. Ikiwa hivyo, ilifaa kwamba baada ya Petro kukubali kwamba yeye ndiye Kristo, Yesu alizungumza juu ya “ufalme wa mbinguni.”
8 Angempa Petro “funguo” hizo. (Mt. 16:19) Hata hivyo, kundi lingejengwa na Yesu juu ya “mwamba” wa kifalme, mfalme wa Kimasihi. Na kama vile “milango ya Hadeze” isingezuia msingi wa “mwamba” bali Yesu Kristo angefufuliwa kutoka kaburini katika siku ya tatu, vivyo hivyo, hiyo “milango ya Hadeze” isingeshinda kundi la Masihi. Nalo pia lazima lifufuliwe kutoka kwa wafu.
9. Wafuasi wa Kristo wangeletwa pamoja wawe nini, na hivyo wao vilevile wangekuwa, kama Israeli wa kale?
9 Tofauti na mitume Wakristo, taifa la Israeli liliachwa limevurugika juu ya Yesu alikuwa nani katika kusudi la Yehova. Kwa hiyo Waisraeli mmoja mmoja ambao walimkubali kuwa Masihi au Kristo wangekusanywa pamoja wafanywe taifa jipya. Taifa hili lingekuwa kundi kama vile tu Israeli wa kale lilivyokuwa. Wangekuwa kundi la watangazaji wa mfalme wa Kimasihi na ufalme wake!
10. Katika 1 Petro 2:8-10, Petro aliutajaje ukweli huo wenye kutokeza, na ni nini kinachotiwa ndani katika “fadhili” zinazopaswa kutangazwa kote kote?
10 Uhakika wenye kutokeza ulipata kufahamika na mtume Petro akiwa mmoja wa wale ‘waliofunzwa na Yehova.’ Mojawapo ya mambo ya mwisho aliyoandikia waamini wenzake lilikuwa na maneno haya: “Waliwekwa [Waisraeli wasioamini] kusudi wapate hayo. Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewatoa mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:8-10) “Fadhili” za Yule wa ajabu zingetia ndani uwezo wake wa kutimiza kusudi lake kuhusu Masihi wake ujapokuwapo upinzani wa wale ambao walimkataa Mwanawe kuwa Masihi. “Watu wa milki ya Mungu” wana wajibu wa kusifu Yehova kwa ajili ya ufalme wake wa Kimasihi.—Isa. 43:21.
11, 12. Kwa sababu gani Yesu aliahidi kuletea wanafunzi wake “msaidizi,” na Yesu alisema nini juu ya msaidizi huyu?
11 “Taifa takatifu” jipya halingeweza kuchukua wajibu huo kwa nguvu zake lenyewe katikati ya ulimwengu wenye uadui. Yesu, akifahamu hili, alisema hivi kwa mitume wake waaminifu kabla ya kutwaliwa kutoka kwao kwa kukamatwa na adui zake: ‘Sitawaacha ninyi yatima . . . Lakini msaidizi roho takatifu, ambayo Baba ataipeleka kwa jina langu, itawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaamuru.’ Vilevile: “Ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia. Nanyi pia mnashuhudia kwa kuwa tangu mwanzo mmekuwapo pamoja nami.”—Yohana 14:18, 26; 15:26, 27.
12 Vilevile Yesu aliongeza hivi: “Mimi nisipoondoka, Msaidizi hatakuja kwenu; . . . Yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake. Yeye atanitukuza mimi; kwa kuwa atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasha habari. Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, kuwapo pamoja nami.”—Yohana 14:18, 26; 15:26, 27.
—Kutoka Holy Spirit—The Force Behind the Coming New Order, sura ya 6.