Sura ya 23
Wataka Nini Maishani?
1-6. (a) Ili upate faida zote maishani, inakupasa uwe na nia ya kufanya nini? (b) Ili uwe na maisha yenye furaha, ni jambo gani lililo la maana hata zaidi ya kazi fulani bora? (c) Bababu gani Biblia yaweza kukusaidia jambo hilo?
UNAPOKUWA kijana, unakuwa na tumaini la maisha mengi mbele. Labda yanaonekana kuwa yanaendelea kufika mbali kama barabara isiyo na upeo. Yatakufikisha wapi?
2 Bila shaka barabara ya uzima itakutolea mambo fulani yenye kushangaza, pamoja na mambo yenye kukatisha tumaini. Lakini, kama tulivyokwisha kuona katika kitabu hiki, kuna mambo mengi unayoweza kufanya sasa ili uhakikishe kwamba unapata faida zote za maisha. Ulizo ni hili, Je! una nia ya kujaribu sana kama inavyotakiwa?
3 Vijana wengi wanafikiria kazi watakayofanya wakiisha kumaliza masomo ya shule. Labda wewe vilevile umefikiria hivyo. Lakini hata ikiwa unafanya kazi gani, ukiifanya vibaya, haitakufurahisha sana. Kuna jambo moja la maana kuliko hilo.
4 Tuseme umekuwa fundi bora sana wa kuandika ramani za ujenzi au fundi wa kuchora picha na kuchonga sanamu, fundi wa mashine, fundi wa kupiga muziki, mkulima, mwalimu wa shule, au vyo vyote. Je! huo ni uhakikisho wa kwamba maisha yako yatakuwa yenye furaha? Sivyo kabisa. Jambo la maana zaidi ni hili: Wewe utakuwa mtu wa namna gani? Watu wengi wamekuwa na kazi bora walizosomea lakini wamefanya maisha yao kuwa ya bure; wakawa watu wasio na furaha.
5 Ndiyo sababu Biblia ni ya maana sana. Biblia ni kama mkusanyo wa barua zilizotoka kwa Muumba wetu. Akiwa Baba yetu wa mbinguni, anataka tuwe na furaha, nasi imetupasa tupendezwe na yale anayotaka kutuambia. Tumekwisha kuona maongozi anayotupa kwa kujibu maulizo yetu yaliyo mengi sana. Bila shaka yote yanafaa, sivyo? Bila maongozi hayo kutoka kwake, tungewezaje kuwa na hakika ya jambo la kufanya, au kujua jambo ambalo lingekuwa la faida yetu.
6 Hilo latukumbusha maneno ambayo mtume Paulo alimwandikia Timotheo, kijana mfanya kazi mwenzake. Paulo alimsihi aendelee katika mambo aliyokuwa amejifunza tangu utoto juu ya Biblia na kusema: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” (2 Timotheo 3:14-17) Lo lote linalofaa sana maishani—hata iwe kazi gani—utakuwa tayari vya kufaa kulitenda vizuri ukikubali uongozwe na Neno la Mungu. Laweza kukufanya uwe mwana au binti bora, mume au mke bora, baba au mama bora, mfanya kazi bora, rafiki bora na, zaidi ya yote, mtumishi bora wa Muumba wako.
KUCHUKUA DARAKA
7-11. Kama inavyoonyeshwa katika Biblia, ni nini iliyo njia ya kupata faida zote maishani?
7 Ukiisha muda kidogo, utakuwa na mambo fulani mazito ya kuamua. Utafika wakati itakapokupasa ujichukulie daraka. Kwa sasa uko kama kinda (mtoto wa ndege) la tai. Labda unajua kwamba mara nyingi tai wanajenga vioto vyao juu sana katika pembe ya genge (mwamba mrefu) refu sana kwenda juu. Makinda yanapoanza kupigapiga mabawa na kuwa tayari kuruka, tai wazazi wanayasukuma kwenye pembe ya kioto, kisha yanaruka! Mtazamaji mmoja anasema kwamba alimwona tai mzazi akimwangusha mtoto mmoja chini kadiri ya futi kama 90 (27 metres) kabla ya yeye mwenyewe kuruka chini, na alipotandaza mabawa yake, akamwacha mtoto aangukie mgongo wake. Kisha akaruka kurudi kwenye kioto na kufanywa vivyo hivyo mara nyingi mpaka tai mdogo alipokwisha kujua kuruka.—Bulletin of the Smithsonian Institution, Vol. CLXVII, Ukurasa 302.
8 Kwa habari yako, wazazi wako wamejaribu sana kujenga nyumba na kufanya mipango mingi. Lakini huwezi kuwategemea milele wakutumikie wala kukufanyia maamuzi makubwa. Na hivi ndivyo ilivyo utakapofikia umri wa kuamua kuondoka nyumbani. Wazazi wako wanaweza kukusaidia uwe tayari kuchukua daraka kama mwanamume au mwanamke mzima ili iwe vyepesi kwako mpaka utakapoweza kujitegemea mwenyewe, kama vile tai mzazi anavyofanyia mtoto wake. Lakini itakupasa wewe vilevile utimize sehemu yako.
9 Umbo la mabawa yenye nguvu ya tai na uwezo wake wa asili wa kuruka ulitokana na Muumba mwenye hekima yote. Basi yatupasa sote tufahamu kwamba njia ya kupata faida zote za maisha ni kumtegemea Yeye. Hata kama wazazi wako wameweza kukupa mwanzo mzuri (au mbaya) namna gani, hata kama una akili na mwili mzuri namna gani, itakupasa ufahamu sikuzote uhitaji wa kuongozwa na Yehova Mungu na kumwomba nguvu ufuate maongozi yake. Yeye aliongoza maneno haya yaandikwe kwa ajili ya vijana kama wewe:
10 “Sikiliza maneno yangu; tega sikio lako, uzisikie kauli zangu. Zisiondoke machoni pako; uzihifadhi ndani ya moyo wako. Maana ni uhai kwa wale wazipatao, na afya ya mwili wao wote. Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima. . . . Macho yako yatazame mbele, na kope zako zitazame mbele yako sawasawa. Ulisawazishe pito la mguu wako, na njia zako zithibitike.”—Mithali 4:20-26.
11 Kadiri utakavyomtegemea Yehova Mungu na Neno lake upate uongozi, ndivyo barabara yako ya uzima itakavyosawazika zaidi.
KUMFANYA MUNGU AWE RAFIKI YAKO
12, 13. (a) Zaidi ya kuepuka mambo ambayo Biblia inasema ni mabaya, tunahitaji jambo gani jingine ikiwa Mungu atakuwa rafiki yetu? (b) Njia ya kuwa na urafiki huo ilitayarishwaje kwa ajili yetu? (Yohana 14:6)
12 Unawezaje kufanya hivyo? Si kwa kuepuka tu mambo ambayo Neno la Mungu linaonyesha kuwa mabaya. Inakupasa ufanye urafiki wa kipekee na Yehova kama Baba yako wa mbinguni. Labda wazazi wako wanaweza kukuelekeza huko, lakini hawawezi kukufanyia urafiki huo. Inakupasa ufanye hivyo mwenyewe, ufanye urafiki na Yehova. Ikiwa wataka Muumba wa ulimwengu huu ulio mkubwa mno awe rafiki yako, anataka nini kwako?
13 Ili atayarishe jambo hilo, Yehova Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa wa kwanza kwenye Dunia hii atimize mgawo, akamfanya azaliwe kama mwanadamu. Alipokua akawa mtu mzima, Mwana wa Mungu alitoa uhai wake kwa ajili yetu. Kama Biblia inavyosema: “Twamwona yeye aliyefanywa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu aionje mauti kwa ajili ya kila mtu.”—Waebrania 2:9.
14, 15. (a) Sote twaweza kuona nini maishani mwetu kinachoonyesha kwamba sisi si wakamilifu? (Warumi 5:12; 7:21-23) (b) Dhambi zinafananishwa na nini katika Mathayo 6:12? “Deni” hiyo yaweza kulipwa namna gani?
14 Biblia yaonyesha kwamba ilitakiwa hivyo kwa sababu sote ni watu wasiokamilika na wenye dhambi. Si vigumu kwako kuona jambo hilo kuwa kweli, kwa sababu labda nyakati nyingine umeona ni vigumu sana kuepuka kufanya mambo uliyojua kuwa mabaya. Bila shaka nyakati nyingine umekosa nguvu ukashindwa na tamaa fulani isiyo nzuri. Sisi sote tulirithi maelekeo ya kufanya mabaya kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, na ndiyo maana jamii nzima ya wanadamu inakufa.
15 Lakini Mwana wa Mungu alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu iwe njia ya kufutia makosa yetu yote. Biblia inatusaidia tufahamu jambo hilo kwa kufananisha dhambi na “deni.” (Mathayo 6:12) Kwa mfano, ukieneza uvumi fulani usio wa kweli juu ya mtu mwingine, bila shaka ungesema kwamba ‘una deni’ ya kumwomba msamaha, sivyo? Maana yake una “deni” kwake kwa sababu ya kosa hilo ulilofanya. Lakini deni tuliyo nayo kwa Mungu ni kubwa mno hata hatuwezi sisi wenyewe kuilipa hata kidogo. Walakini, uhai mkamilifu wa kibinadamu wa Kristo Yesu ni wenye bei kubwa sana hata unaweza kufuta deni zote tulizo nazo kwa Mungu kwa sababu ya dhambi tuliyorithi, na ndiyo maana Mwana wa Mungu alitoa uhai wake kwa ajili yetu.
16-18. (a) Ni kwa sababu gani unaona kwamba Mungu anastahili tumshukuru kwa mambo yaliyofanywa kupitia kwa Mwana wake? (Warumi 5:6-10) (b) Ni mambo gani tunayoweza kufanya ili tuonyeshe shukrani hizo?
16 Basi njia ya kufanya urafiki na Mungu iko tayari. Lakini yatupasa tuonyeshe kwamba tunaona ubora wa mpango aliofanya kwa kumtoa Mwana wake mwenyewe awe dhabihu, na vilevile ubora wa mambo aliyofanya Mwana wake kwa kutufia sisi. Inatupasa tuonyeshe kwamba tunauamini mpango huo wa Mungu. Yesu alisema hivi: “Baba ampenda Mwana, naye amempa vyote mkononi mwake. Amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele; asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inamkalia.”—Yohana 3:35, 36.
17 Ebu wazia, tuseme ikiwa ungeokoa mtu anayezama katika maji au anayeelekea kufa katika nyumba inayoteketea—na kwa kufanya hivyo wewe mwenyewe ufe. Namna gani ikiwa mtu huyo ambaye uliokoa hangeshukuru hata kidogo, hata bila kuona maana ya kwenda kwa wazazi wako akawashukuru kwa sababu ya vile ulivyomfanyia kwa upendo? Unadhani baba yako mwenyewe angeonaje? Basi, unaweza kufahamu ni kwa sababu gani Yehova ana haki ya kuudhika na kuvunja urafiki na wale wanaojua mambo ambayo Mwana wake alitendea wanadamu lakini hawashukuru.
18 Unaweza kushukuru kwa maisha yako. Unaweza kuonyesha kwamba unasikitika sana kwa makosa ambayo umefanya kisha umwombe Mungu ‘amalize deni zako’ kupitia kwa dhabihu ya Mwana wake. Unaweza kujiweka mwenyewe wakf kwa Mungu umtumikie muda unaobaki wa maisha yako, (ufanye) yanayompendeza. Biblia inaonyesha kwamba tunaweza kuonyesha mfano wa kujiweka wakf hivyo kwa kubatizwa katika maji. Lakini, hilo si jambo la kufanya haraka-haraka. Huwezi kumwambia Mungu kwamba utamtumikia kisha ugeuze nia yako. Hivyo ndivyo watoto wadogo walivyo; hawana hakika na jambo wanalotaka kufanya. Lakini unapofikia hali ya kuwa mwanamume au mwanamke, unafikia hali ya maisha unapoweza kuamua. Basi hilo ni jambo unalotakiwa ufikirie sana.
KULIWEZA JARIBU
19-21. (a) Lile jaribu unalopata linafananaje na lile alilopata Daudi alipokwenda kupigana na Goliathi? (1 Samweli 17:4-11, 26-51; Yohana 15:17-20; Yakobo 4:4) (b) Twawezaje kuwa na hakika kwamba inawezekana kushinda jaribu hilo? (Yohana 16:33; Wafilipi 4:13; Mithali 3:5, 6)
19 Haitakuwa vyepesi sikuzote kuendelea kujionyesha kwamba wewe ni rafiki ya Mungu. Biblia inaonyesha kwamba itakuwa vigumu sana kwako kwa sababu ulimwengu mzima si rafiki ya Mungu bali ni adui yake. Lakini usiogope. Unaweza kuonyesha roho ile ile aliyoonyesha Daudi mtumishi wa Mungu alipokuwa kivulana tu. Alikuwa amekwenda kwenye kambi ya Waisraeli wakati walipofikiwa na majeshi ya Wafilisti, waliokuwa waabudu wa miungu ya uongo. Mtu mwenye kupigania Wafilisti—jitu lililoitwa Goliathi—lilidhihaki Waisraeli, likiwachokoza ili wapigane nalo. Daudi alisikia. Ijapokuwa alikuwa kijana tu, alimwamini sana Yehova. Akaitikia mwito huo wa kupigana, akaliendea jitu hilo lenye silaha nyingi, akaliangusha chini kwa jiwe moja katika kombeo la mchungaji.
20 Leo unakutana na ulimwengu wenye uadui, lakini usiogope. Yehova ni Mungu yule yule Mwenye Nguvu Zote aliyekuwako wakati wa Daudi, nawe waweza kushinda ukionyesha uhodari na, zaidi ya yote, kuamini kwamba Yeye hatakuacha hata kidogo bali atakutegemeza na kukupa nguvu unayohitaji.
21 Wanaume na wanawake wengine, kutia na vijana wengi, wamevumilia magumu, wakaweka maisha zao katika hatari au hata wakafa ili watumikie serikali fulani ya kisiasa ya duniani. Walakini, ni heshima inayopita heshima zote kumtumikia Muumba wa ulimwengu mzima! Ebu fikiria sasa namna jambo hilo linavyoweza kukupa uzima unaopita ule anaofurahia mtu ye yote duniani leo.