Jina la Mungu Katika Vizazi Vingi
YEHOVA Mungu anataka mwanadamu ajue na kulitumia jina lake. Hilo linaonekana wazi kwa uhakika wa kwamba Yeye aliwafunulia jina Lake watu wawili wa kwanza kabisa duniani. Sisi twajua kwamba Adamu na Hawa walilijua sana jina la Mungu kwa sababu Hawa alipokwisha kumzaa Kaini, alisema hivi kulingana na maandishi ya awali ya Kiebrania: “Nimepata mtu mume kwa msaada wa Jehova.”—Mwanzo 4:1, OTSWMSA.
Baadaye tunasoma kwamba watu waaminifu kama Henoki na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu.’ (Mwanzo 5:24; 6:9, ZSB) Basi, wakati huo bila shaka walilijua jina la Mungu. Jina hilo liliokoka ile Gharika kuu pamoja na mtu mwadilifu Noa na jamaa yake. Ujapokuwa uasi mkubwa uliotokea wakati fulani baadaye katika Babeli, watumishi wa kweli wa Mungu waliendelea kulitumia jina lake. Linaonekana mamia ya mara katika sheria ambazo Mungu aliwapa Waisraeli. Katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati pekee linaonekana mara 551.
Siku za waamuzi, kwa wazi Waisraeli hawakuepa kutumia jina la Mungu. Hata walilitumia katika kusalimiana. Tunasoma (katika Kiebrania cha awali) juu ya Boazi akisalimu wavunaji wake, akisema: “Jehova nawe pamoja nanywi.” Wakajibu salamu yake kwa kusema: “Jehova nakubarikie.”—Ruthu 2:4, OTSWMSA.
Katika historia yote ya Waisraeli mpaka wakati waliporudi Yuda baada ya utumwa wao katika Babuloni, jina la Yehova liliendelea kutumiwa na watu wote. Mfalme Daudi, mwanamume mwenye kukubalika kwa moyo wa Mungu mwenyewe, alilitumia jina la Mungu sana—laonekana mamia ya mara katika zaburi alizoandika. (Matendo 13:22) Pia jina la Mungu lilitiwa katika majina binafsi mengi ya Waisraeli. Hivyo tunasoma juu ya Adoniya (“Bwana Wangu ni Yah”—“Yah” ni kifupi cha Yehova), Yonathani (“Yehova Ametoa”), Mika (“Ni Nani aliye kama Yah?”) na Yoshua (“Yehova Ni Wokovu”).
Nje ya Biblia
Pia kuna ushahidi kutoka vyanzo vilivyo nje ya Biblia unaoonyesha matumizi makubwa sana ya jina la Mungu katika nyakati za kale. Mwaka wa 1961 pango la kale la kuzikia wafu lilivumbuliwa mwendo mfupi upande wa magharibi-kusini ya Yerusalemu, kulingana na ripoti iliyo katika kichapo kinachoitwa Israel Exploration Journal (Buku la 13, Na. 2). Juu ya kuta zake palikuwa na maandishi ya Kiebrania yanayoonekana kuwa ya tarehe ya tangu nusu ya pili ya karne ya nane K.W.K. Maandishi hayo yana maneno kama haya “Yehova ndiye Mungu wa dunia nzima.”
Mwaka wa 1966 ripoti ilichapishwa katika Israel Exploration Journal (Buku la 16, Na. 1) juu ya vipande vya udongo wa mfinyanzi vikiwa na mwandiko wa Kiebrania juu yavyo. Vipande hivyo vilipatikana katika Aradi, kusini mwa Israeli. Vipande hivyo viliandikwa katika nusu ya pili ya karne ya saba K.W.K. Kimojapo kilikuwa barua ya kibinafsi aliyoandikiwa mtu anayeitwa jina Eliashibu. Barua hiyo inaanza hivi: “Kwa bwana wangu Eliashibu: Yehova na akutakie amani.” Na inaisha kwa kusema: “Anakaa katika nyumba ya Yehova.”
Mwaka wa 1975 na wa 1976, wachimbuzi wa mambo ya kale waliokuwa wakifanya kazi katika Negebu walivumbua mkusanyo wa maandishi ya Kiebrania na ya Kifoinike juu ya kuta zilizopigwa lipu, vyungu vikubwa vya kuwekea vitu na vyombo vya mawe. Maandishi hayo yalitia ndani neno la Kiebrania la Mungu, pia jina la Mungu, YHWH, katika herufi za Kiebrania. Majuzi katika Yerusalemu wenyewe, ulipatikana ukanda mdogo wa fedha uliokunjwa, unaelekea kuwa wenye tarehe ya tangu wakati wa kabla ya uhamisho wa Kibabuloni. Wachunguzi-habari wanasema kwamba ukanda huo ulipokunjuliwa, jina la Yehova katika Kiebrania lilipatikana limeandikwa juu yake.—Biblical Archaeology Review, Machi/Aprili 1983, ukurasa wa 18.
Mfano mwingine wa matumizi ya jina la Mungu unapatikana katika zile zinazoitwa Barua za Lakishi. Barua hizo, zikiwa zimeandikwa juu ya vigae, zilipatikana kati ya miaka 1935 na 1938 katika magofu ya Lakishi, mji wenye boma uliokuwa wenye kutokeza sana katika historia ya Israeli. Zinaonekana kuwa ziliandikwa na afisa fulani katika kituo cha kijeshi cha Yudea, akimwandikia mkubwa wake, jina lake Yaoshi, katika Lakishi, inaelekea kuwa ni wakati wa vita vilivyokuwa kati ya Israeli na Babuloni kuelekea mwisho wa karne ya saba K.W.K.
Kati ya vigae vinane vyenye kusomeka vizuri, saba vinaanza ujumbe wavyo kwa salamu kama hii: “Yehova na amfanye bwana wangu aone majira haya akiwa na afya njema!” Kwa jumla, jina la Mungu linaonekana mara 11 katika taarifa saba hizo, zikionyesha waziwazi kwamba jina la Yehova lilikuwa likitumiwa kila siku kuelekea mwisho wa karne ya saba K.W.K.
Hata watawala wapagani walijua hata wakatumia jina la Mungu walipokuwa wakimtaja Mungu wa Waisraeli. Hivyo, juu ya Jiwe la Moabu, Mfalme Mesha wa Moabu anajivunia matendo yake ya uhodari ya kivita juu ya Israeli na, kati ya mambo mengine, anaeleza hivi: “Kemoshi aliniambia, ‘Nenda, kachukue Nebo kutoka Israeli!’ Basi nikaenda usiku nikaupiga tangu kupambauka mpaka adhuhuri, nikautwaa na kuua wote . . . Nami nikachukua humo [vyombo] vya Yehova, nikiviburuta mbele ya Kemoshi.”
Katika kuyataja matumizi hayo yasiyo ya Kibiblia ya jina la Mungu, kichapo Theologisches Wörterbuch zum Alten Testament (Kamusi ya Kitheolojia ya Agano la Kale), katika Buku la 3, safu ya 538, kinasema hivi: “Hivyo, vithibitisho vya kimaandishi 19 vya Tetragramatoni kwa namna ya jhwh vinashuhudia katika habari hii kutegemeka kwa maandishi ya awali ya Masoreti; zaidi ya yote, vingi zaidi vyaweza kutazamiwa kutoka Nyaraka za Kale za Aradi.”—Kilichotafsiriwa kutoka Kijeremani.
Jina la Mungu Halikusahauliwa
Uzoelevu wa jina la Mungu na matumizi yalo uliendelea mpaka kwenye siku za Malaki, aliyeishi karibu miaka 400 iliyopita kabla ya wakati wa Yesu. Katika kitabu cha Biblia chenye jina lake, Malaki analipa jina la Mungu cheo kikuu, akilitumia kwa jumla ya mara 48.
Wakati uliposonga mbele, Wayahudi wengi wakaja kuishi mbali na nchi ya Israeli, na baadhi yao hawangeweza tena kuisoma Biblia katika lugha ya Kiebrania. Kwa sababu hiyo, katika karne ya tatu K.W.K., kukawa na mwanzo wa kutafsiri sehemu ya Biblia iliyokuwako wakati huo (“Agano la Kale”) katika Kigiriki, iliyokuwa lugha mpya ya mataifa yote. Lakini jina la Mungu halikupuuzwa. Watafsiri walilitunza, wakiliandika kwa namna ya Kiebrania. Nakala za kale za Septuagint ya Kigiriki ambazo zimetunzwa kufikia wakati wetu zinashuhudia hilo.
Lakini, hali ilikuwaje wakati Yesu alipotembea juu ya dunia hii? Twaweza kujuaje kama yeye na mitume wake walitumia jina la Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Katika barua hii, iliyoandikwa juu ya kigae katika nusu ya pili ya karne ya saba K.W.K., jina la Mungu linaonekana mara mbili.
[Hisani]
(Picha hii imetolewa kwa ruhusa ya Department of Antiquities and Museums ya Israeli)
[Picha katika ukurasa wa 13]
Jina la Mungu linapatikana pia katika Barua za Lakishi na juu ya Jiwe la Moabu