Wakristo na Jina Hilo
HAKUNA mtu anayeweza kusema kwa uhakika kabisa ni wakati gani Wayahudi wa kidini walipoacha kutamka jina la Mungu kwa sauti na badala yake wakatumia maneno mengine ya Kiebrania ya kusema Mungu na Bwana Mwenye Enzi Kuu. Watu fulani wanaamini kwamba jina la Mungu liliacha kutumiwa kila siku kabla ya wakati wa Yesu. Lakini kuna ushahidi wenye nguvu unaoonyesha kwamba kuhani mkuu aliendelea kulitamka kwenye ibada katika hekalu—hasa siku ya Upatanisho—mpaka wakati hekalu lilipoharibiwa mwaka wa 70 W.K. Kwa sababu hiyo, Yesu alipokuwa duniani, matamshi ya jina hilo yalijulikana, ingawa labda halikutumiwa kote kote.
Kwa nini Wayahudi waliacha kulitamka jina la Mungu? Labda, angalau kidogo, ni kwa sababu ya kutumia isivyofaa maneno haya ya amri ya tatu: “Usitaje jina la Jehova Mngu wako kwa upuuzi.” (Kutoka 20:7, OTSWMSA) Bila shaka, amri hiyo haikukataza matumizi ya jina la Mungu. Kama ilikataza, kwa nini watumishi wa kale wa Mungu kama Daudi walilitumia pasipo wasiwasi na bado wakafurahia baraka ya Yehova? Na ni kwa nini Mungu alilitamka kwa Musa na kumwambia Musa akawaeleze Waisraeli aliyekuwa amemtuma?—Zaburi 18:1-3, 6, 13; Kutoka 6:2-8.
Ingawa hivyo, kufikia wakati wa Yesu kulikuwako na elekeo lenye nguvu la kuchukua amri za kiasi za Mungu na kuzifasiri kwa njia yenye kupita kiasi sana. Kwa mfano, ile amri ya nne ya Amri Kumi iliwapa Wayahudi wajibu wa kuishika siku ya saba ya kila juma kuwa siku ya kupumzika, Sabato. (Kutoka 20:8-11) Wayahudi wa kidini waliitumia amri hiyo kupita kiasi sana, wakitunga sheria nyingi-nyingi za kuongoza hata kitendo kilicho ki-do-go sana ambacho kingeweza-au-kisingeweza kufanywa siku ya Sabato. Bila shaka ni katika roho iyo hiyo walitumia kupita kiasi sana amri ya kiasi inayosema jina la Mungu halipasi kamwe kudharauliwa, wao wakasema halipasi hata kutamkwa.a
Yesu na Jina Hilo
Je! Yesu angalifuata pokeo hilo lisilopatana na maandiko? Hasha! Kwa hakika yeye hakusita kufanya kazi za kuponesha wagonjwa siku ya Sabato, hata ijapo kufanya hivyo kulimaanisha kuzivunja sheria za Wayahudi zilizotungwa na wanadamu, hata kuhatirisha uhai wake. (Mathayo 12:9-14) Kwa kweli, Yesu alilaani vikali Wafarisayo akiwaambia kuwa ni wanafiki kwa sababu mapokeo yao yalipita cheo cha Neno la Mungu aliloongoza kwa roho yake. (Mathayo 15:1-9) Kwa sababu hiyo, haielekei kwamba angalisita kulitamka jina la Mungu, hasa kwa sababu jina lake mwenyewe, Yesu, lilimaanisha “Yehova ni Wokovu.”
Pindi moja, Yesu alisimama katika sinagogi akasoma kisehemu cha kitabu cha kukunjwa cha Isaya. Sehemu aliyosoma ilikuwa ile tunayoita leo Isaya 61:1, 2, ambapo jina la Mungu linaonekana zaidi ya mara moja. (Luka 4:16-21) Je! angalikataa kulitamka jina la Mungu mahali hapo, badala yake aseme “Bwana” au “Mungu”? Hasha. Hiyo ingalimaanisha alikuwa akifuata pokeo lisilopatana na maandiko la viongozi wa kidini Wayahudi. Lakini, tunasoma hivi: “Alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao.”—Mathayo 7:29.
Kwa kweli, kama tulivyojifunza hapo mapema, yeye alifundisha wafuasi wake kusali hivi kwa Mungu: “Jina lako litukuzwe.” (Mathayo 6:9) Na katika sala usiku ule kabla ya kuuawa, alisema hivi kwa Baba yake: “Nilionyesha jina lako kwa watu wale ulionipa katika dunia . . . Baba Mutakatifu, uwalinde kwa jina lako [ulilonipa, UV].”—Yoane 17:6, 11, ZSB.
Kwa habari ya mitajo hiyo iliyotolewa na Yesu juu ya jina la Mungu, kitabu kinachoitwa Der Name Gottes (Jina la Mungu) kinaeleza hivi, kwenye ukurasa wa 76: “Ni lazima tuufahamu uhakika wenye kustaajabisha kwamba ufahamu wa kimapokeo wa Agano la Kale juu ya Mungu ni wa kwamba ni ufunuo wa jina lake na kwamba huo unaendelezwa mpaka kwenye zile sehemu za kumalizia za Agano la Kale, ndiyo, unaendelea hata kuingia katika zile sehemu za mwisho za Agano Jipya, ambamo, kwa mfano katika Yohana 17:6, tunasoma: ‘Nilionyesha jina lako.’”
Ndiyo, lingekuwa jambo la kipumbavu kufikiri kwamba Yesu alisita kutumia jina la Mungu, hasa aliponakili zile sehemu za Maandiko ya Kiebrania zilizokuwa na jina hilo.
Wakristo wa Kwanza
Je! wafuasi wa Yesu katika karne ya kwanza walitumia jina la Mungu? Walikuwa wameamriwa na Yesu wafanye wanafunzi kutoka mataifa yote. (Mathayo 28:19, 20) Wengi kati ya watu ambao wangehubiriwa hawakuwa na wazo juu ya Mungu aliyekuwa amejifunua mwenyewe kwa Wayahudi kwa jina Yehova. Wakristo hao wangewezaje kuwajulisha aliye Mungu wa kweli? Je! ingetosha kumwita Mungu au Bwana? Hapana. Mataifa hayo yalikuwa na miungu yao wenyewe na mabwana wao wenyewe. (1 Wakorintho 8:5) Wakristo hao wangaliwezaje kutofautisha wazi kati ya aliye Mungu wa kweli na miungu ya uongo? Ni kwa kulitumia tu jina la Mungu wa kweli.
Hivyo, wakati wa mkutano wa wazee katika Yerusalemu, mwanafunzi Yakobo alisema hivi: “Simeoni ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya unabii yapatana na hayo.” (Matendo 15:14, 15) Katika hotuba yake yenye kujulikana sana siku ya Pentekoste, mtume Petro alieleza sehemu yenye maana ya ujumbe wa Kikristo aliponakili maneno ya unabii wa Yoeli, yanayosema: “Awae yote atakaelilingana jina la Jehova ataponywa.”—Joeli 2:32, OTSWMSA; Matendo 2:21.
Mtume Paulo haachi shaka juu ya jinsi jina la Mungu lilivyo na umaana kwake. Katika barua yake kwa Waroma, ananakili maneno ayo hayo ya nabii Yoeli na anaendelea kuwatia moyo Wakristo wenzake waonyeshe imani yao katika maneno hayo kwa kutoka kwenda kuhubiria wengine jina la Mungu ili hao, pia, wapate kuokolewa. (Warumi 10:13-15) Baadaye aliandika katika barua yake kwa Timotheo, akisema: “Acheni kila mmoja anayetaja jina la Yehova aache kabisa mambo yasiyo ya uadilifu.” (2 Timotheo 2:19, New World Translation) Mwishoni mwa karne ya kwanza, mtume Yohana alitumia jina la Mungu katika maandishi yake. Usemi huu “Haleluya,” unaomaanisha “Msifuni Yah,” unaonekana mara nyingi katika kitabu cha Ufunuo 19:1, 3, 4, 6.
Ingawa hivyo, Yesu na wafuasi wake walitabiri kwamba uasi-imani ungetokea katika kundi la Kikristo. Mtume Petro alikuwa ameandika hivi: ‘Kwenu kutakuwako waalimu wa uongo.’ (2 Petro 2:1; ona pia Mathayo 13:36-43; Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:3; 1 Yohana 2:18, 19.) Maonyo hayo yalitimizwa. Tokeo moja ni la kwamba jina la Mungu lilisukumiwa nyuma. Hata likaondolewa katika nakala na tafsiri za Biblia! Na tuone hilo lilivyotukia.
[Maelezo ya Chini]
a Watu fulani wanatoa sababu nyingine: Labda Wayahudi walivutwa na falsafa ya Kigiriki. Kwa mfano, Filo, mwanafalsafa wa Kiyahudi wa Aleksandria ambaye karibu aliishi wakati mmoja na Yesu, alivutwa sana na Plato, mwanafalsafa Mgiriki, aliyefikiriwa na yeye kuwa aliongozwa na roho ya Mungu. Kichapo Lexicon des Judentums (Kamusi ya Mambo ya Wayahudi), kinaeleza chini ya “Philo,” kwamba Filo ‘aliunganisha lugha na mawazo ya falsafa ya Kigiriki (Plato) pamoja na imani ya Wayahudi iliyofunuliwa’ na ya kwamba jambo la kwanza yeye ‘alikuwa na uvutano wa waziwazi juu ya mababa wa kanisa la Kikristo.’ Filo alifundisha kwamba Mungu alikuwa asiyeelezeka na, kwa sababu hiyo, asiye na jina.
[Picha katika ukurasa wa 14]
Picha hii ya kuhani mkuu wa Kiyahudi, mwenye ishara katika Kiebrania juu ya kilemba chake ambayo maana yake “Utakatifu ni wa Yehova,” inapatikana katika Vatikani
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kama inavyoonyesha tafsiri hii ya Biblia katika Kijeremani ya mwaka wa 1805, Yesu aliposoma katika sinagogi kitabu cha kukunjwa cha Isaya, alitamka jina la Mungu kwa sauti kuu.—Luka 4:18, 19
[Picha katika ukurasa wa 16]
Petro na Paulo walilitumia jina la Mungu waliponakili maneno ya unabii wa Yoeli.—Matendo 2:21; Warumi 10:13