Sura 9
Ni Nani Anayeongoza Njia Kuelekea Wokovu?
1. (a) Ni lazima tutii nini ili tuje tusalimishwe katika “dhiki kubwa”? (b) Hilo lilionyeshwaje kwa jinsi Mungu alivyomtumia Musa?
TUNAWEZA kuokolewa katika ulimwengu mbovu huu na kuhifadhiwa hai katika “dhiki kubwa” ikiwa tunaukubali tu uongozi wa Yesu Kristo na kutoa ushahidi wenye kusadikisha kwamba tunamsikiliza kweli kweli na kutembea katika hatua zake. (Matendo 4:12) Hilo lilitolewa mfano vizuri na matukio yaliyozunguka kuokolewa kwa Waisraeli wa asili katika Misri mwaka wa 1513 K.W.K. Kwa njia ya muujiza Yehova alisalimisha Waisraeli katika Bahari Nyekundu na kuharibu jeshi la Wamisri lililofuatia. Katika yote hayo, Mungu alimtumia Musa aongoze watu wake.—Yoshua 24:5-7; Kutoka 3:10.
2. (a) Ni nani waliokuwa “kundi kubwa la watu waliochangamana” walioondoka Misri pamoja na Waisraeli? (b) Ni jambo gani ambalo bila shaka lilivutia wengi wao? (c) Bila kukawia walijaribiwa juu ya jambo gani?
2 Waisraeli waliposafiri kutoka Misri wakiwa na tazamio la kuingia Nchi ya Ahadi, wengine walijiunga nao. Kama Musa alivyoandika baadaye: “Kundi kubwa la watu waliochangamana nao wakakwea pamoja nao.” (Kutoka 12:38) Hao walikuwa nani? Ni Wamisri au wageni wengine waliojiunga na Israeli. Walikuwa wameona mapigo yenye kutia woga ambayo Yehova alikuwa ameleta juu ya taifa la Misri lenye uonevu ili aonyeshe kwamba yeye alikuwa ndiye Mungu wa kweli mmoja tu na kwamba miungu ya Misri ilikuwa ya uwongo na haingeweza kuokoa wale walioiabudu. Bila shaka, pia, waliyosikia kutoka kwa Waisraeli juu ya tazamio la uzima katika “nchi ijaayo maziwa na asali” yaliwapendeza. (Kutoka 3:7, 8; 12:12) Lakini, je! pia walimkubali Musa kuwa ndiye aliyesimamishwa na Mungu awe mtawala na mkombozi wa watu Wake? Bila kukawia walijaribiwa.—Matendo 7:34, 35.
3. (a) Kwa nini ilikuwa lazima wafuate maelekezo ya Musa? (b) Ni nini iliyokuwa maana ya ‘kubatizwa katika Musa’? (c) Kwa nini hilo ni la maana kwa Waisraeli wa kiroho?
3 Israeli, pamoja na “kundi kubwa la watu waliochangamana,” walipokaribia fuo za Bahari Nyekundu, mfalme wa Misri na majeshi yake ya kivita aliwafuatia nyuma ili awarudishe katika utumwa. Ili waokolewe, ilikuwa lazima wakae pamoja na kufuata maelekezo ya Musa, kwa sababu Yehova alikuwa akitumia Musa awaongoze. Kwa kutumia wingu lisilo la kiasili Yehova akalizuia jeshi hilo wakati alipokuwa akiyatenga maji ya bahari na kukausha bonde la bahari. Tofauti kabisa na yaliyowapata Wamisri baadaye, Israeli wote na “kundi kubwa la watu waliochangamana” waliokoka pamoja na Musa kwa kuvuka bonde kavu hilo la bahari. (Kutoka 14:9, 19-31) Walipokuwa wakipita humo, kuta za maji zikiwa kulia na kushoto kwao na wingu la kuwapo kwa Mungu juu yao, jambo lenye maana lilitukia. Biblia inalisema jambo hilo kuwa ni ubatizo—si ubatizo halisi katika maji, bali ule wa mfano katika Musa akiwa nabii wa Yehova, yeye aliyetumwa na Mungu awe Mkombozi wao. (1 Wakorintho 10:1, 2) Hali kadhalika, Waisraeli wote wa kiroho watakaouokoka uharibifu wa ulimwengu huu mbovu lazima wapate ubatizo ulio kama huo katika Kristo akiwa mkombozi na kutoa ushahidi wenye kusadikisha kwamba wanafuata sana uongozi wake. ‘Kundi la watu wenye kuchangamana’ la kisasa lazima liandamane nao.
4. Mamlaka ambayo Yehova amempa Kristo ni kubwa kadiri gani?
4 Yehova amempa Mwanaye, Yesu Kristo, mamlaka kubwa. Kupitia yeye Mungu amefanya iwezekane kwetu ‘tuokolewe kutoka mfumo wa mambo wa sasa ulio mbovu,’ hata hatuna haja ya kushiriki msiba mbaya utakaoupata. (Wagalatia 1:3-5, New World Translation; 1 Wathesalonike 1:9, 10) Kupitia Musa, Yehova aliwapa Waisraeli sheria zilizohusu matazamio ya maisha ya papo hapo ya watu. Walipotii sheria hizo walifaidika sana. Lakini pia sheria fulani zilikuwa na adhabu ya kifo ikiwa kungekuwa ukosefu wa kutii. Baadaye, Yesu akawa nabii mkubwa kuliko Musa. Yale aliyofundisha yalikuwa “maneno ya uzima wa milele,” na kutotii maneno hayo kwa makusudi kunaongoza kwenye kifo ambacho katika hicho hakuna ukombozi. Kwa hiyo, ni jambo la maana kama nini tuzingatie moyoni yale anayosema!—Yohana 6:66-69; 3:36; Matendo 3:19-23.
5. Ni jambo gani linalofanya kutii Yesu kuwe kwenye kuvutia sana?
5 Wazo hilo la kutii kiongozi halionekani kuwa lenye kutamanika kwa watu fulani. Wameona mamlaka ikitumiwa vibaya sana. Lakini maneno ya Yesu mwenyewe yanaonyesha roho ambayo ni yenye kutumainisha. Anatualika kwa uchangamshi hivi: “Njoni kwangu, ninyi nyote mnaomenyeka na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Bebeni nira yangu na kujifunza kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia pole na hali ya kujishusha katika moyo, na ninyi mtapata burudisho la nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:28-30, New World Translation) Lo! hilo ni tazamio lenye kuvutia kama nini! Wale wanaokubali mwaliko huo mchangamfu, wakimtumainia yeye kabisa, hawatakata tumaini. (Warumi 10:11) Wataona usalama kama ule wanaoona kondoo walio katika kundi la mchungaji mwenye upendo.
MCHUNGAJI MWEMA ALIYE WA KWELI KWELI
6. (a) Taifa la Israeli lilikuwaje kama kondoo katika zizi la kondoo? (b) Ni ahadi gani ambayo Yehova alifanya kuhusu mchungaji wa “kondoo” hao, na ilitimizwaje?
6 Taifa la Israeli lilikuwa kama kundi la kondoo la Yehova. Yeye alitoa agano la Torati, lililotumika kuwa kama kuta za zizi la kondoo lenye ulinzi, likiwalinda na njia ya maisha ya mataifa yasiyomwogopa Mungu. Pia lilielekeza wenye kuitikia kwenye Masihi. (Waefeso 2:14-16; Wagalatia 3:24) Kwa habari ya huyo Mchungaji-Mfalme wa Kimasihi, Yehova alitabiri hivi: “Nitaweka mchungaji mmoja juu [ya kondoo zangu], naye atawalisha, naam, mtumishi wangu, Daudi.” (Ezekieli 34:23, 31) Hiyo haikuwa na maana kwamba Daudi, ambaye wakati huo alikuwa amekufa, yeye binafsi angetawala tena akiwa mfalme juu ya watu wa Mungu. Badala yake, Yehova angeinua kutoka ukoo wa kifalme wa Daudi mchungaji-mfalme ambaye kupitia yeye Mungu angetoa usalama. (Yeremia 23:5, 6) Katika nyakati mbalimbali wanadamu walijidai kwa uwongo kuwa wakombozi wa Kimasihi, lakini mwaka wa 29 W.K., Yehova alimtumia Yohana Mbatizaji amjulishe Yesu Kristo kwa “kondoo” wa Israeli kuwa ndiye aliyetumwa kweli kweli na Mungu, yule Masihi aliye na sifa za kweli za kumtambulisha. Huyo alikuwa Mwana wa kimbingu wa Mungu, ambaye asili ya uhai wake ilikuwa imehamishwa ikapelekwa kwenye tumbo la uzazi la bikira wa Kiyahudi ili apate kuzaliwa katika ukoo wa kifalme wa Daudi. Jina Daudi maana yake ni “mpendwa,” hivyo, kwa kufaa, baada ya ubatizo wa Yesu katika maji, Yehova alitangaza kwa sauti yenye kusikika kutoka mbinguni: “Wewe ni Mwana wangu, yule mpendwa; nimekukubali wewe.”—Marko 1:11, New World Translation.
7. (a) Akiwa “mchungaji mwema,” Yesu alionyeshaje kina cha hangaiko lake la upendo kwa “kondoo”? (b) Hiyo ilitofautianaje na mwenendo wa akina masihi wa uwongo waliotangulia?
7 Punde kuliko miezi minne kabla ya kufa kwake, Yesu alisema: “Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.” (Yohana 10:11) Alitofautisha daraka lake na lile la akina masihi wa uwongo waliokuwa wametangulia kuja, akisema: “Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang’anyi. Aingiaye mlangoni ni mchungaji wa kondoo. Bawabu humfungulia huyo, na kondoo humsikia sauti yake; naye huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje. Naye awatoapo nje kondoo wake wote, huwatangulia; na wale kondoo humfuata, kwa maana waijua sauti yake. Mgeni hawatamfuata kabisa, bali watamkimbia; kwa maana hawazijui sauti za wageni.”—Yohana 10:1-5, 8.
8. (a) Ni katika ‘zizi gani la kondoo’ ambamo Yesu aliongoza Wayahudi waliomfuata? (b) Ni wangapi ambao ameingiza katika zizi hilo?
8 Wale walio katika zizi la kondoo la Kiyahudi walioitikia uongozi wa lile agano la Torati walimkubali Yesu kuwa ndiye Masihi wakati Yohana Mbatizaji akiwa “bawabu” alipomjulisha kwao. Wakajithibitisha kuwa “kondoo” za Yesu mwenyewe, naye akawaongoza kwenye zizi jipya la kondoo la mfano, ambalo ni la Yehova. Zizi hilo lilifananisha uhusiano wenye kibali pamoja na Yehova kwa kutegemea agano jipya, lililofanywa pamoja na Israeli wa kiroho na likafanywa imara kwa damu ya Yesu mwenyewe. Kupitia agano hilo ikawa inawezekana kwao kupata uzima wa kimbingu pamoja na Kristo, “mbegu” ya Abrahamu ambaye kupitia kwake baraka zingekuja kwa watu wa mataifa yote. (Waebrania 8:6; 9:24; 10:19-22; Mwanzo 22:18) Yesu Kristo, ambaye Mungu alifufua kutoka kwa wafu na kumrudisha kwenye uzima wa kimbingu, ndiye “mlango” wa zizi hilo la kondoo la agano jipya. Kupatana na kusudi la Babaye, ameingiza katika zizi hilo hesabu ya kiasi tu—144,000 tu—wa kwanza kutoka kati ya Wayahudi, na baadaye kutoka kati ya Wasamaria na Mataifa. Akiwa ndiye Mchungaji Mwema, Yesu anajua kila mmoja wa kondoo zake kwa jina na anawatunza na kuwaangalia kwa upendo, kila mmoja binafsi.—Yohana 10:7, 9; Ufunuo 14:1-3.
9. Ni nani “kondoo wengine” ambao Yesu anataja, na wanakusanywa lini?
9 Ingawa hivyo, Yesu hachungi “kundi dogo” tu la wale wanaopata Ufalme wa kimbingu. (Luka 12:32) Alisema hivi pia: “Kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Hao ni akina nani? Ni watu wasio katika agano jipya; si Waisraeli wa kiroho. Lakini wanaingizwa katika ushirika pamoja na washiriki wa Israeli wa kiroho wakati hao wangali wapo duniani na wakiwa wanahitaji aina ya uchungaji ambao Yesu anasimulia. “Kondoo wengine” hao ni watu ambao, wakati wa hizi siku za mwisho, wanakusanywa ndani ya mwandalio wa Yehova wa kupata uzima wa milele duniani kwa kutegemea imani yao katika ubora wa dhabihu ya damu ya Yesu. Ni wale wale wanaotajwa kuwa “mkutano mkubwa” katika Ufunuo 7:9, 10, 14, na hivyo wana tazamio la kuokoka dhiki kubwa inayokuja.
10. Ni jambo gani linalotakwa ili mtu awe mmoja wa hao “kondoo wengine”?
10 Ili mtu atajwe kwa kufaa kuwa mmoja wa hao “kondoo wengine” wanaolindwa na kuhifadhiwa na Mchungaji Mwema, ni lazima ‘asikilize’ sauti Yake na kutoa ushahidi wa kuwa kweli kweli sehemu ya “kundi moja” ambalo ni pamoja na warithi wa kweli kweli wa Ufalme wa kimbingu. Je! wewe unafanya hivyo? Unasikiliza sauti yake kwa uangalifu wa kadiri gani?
11. Ni nini kitakachotoa ushahidi kwamba ‘tunasikiliza’ kweli kweli aliyosema Yesu katika Yohana 15:12?
11 Bila shaka unajua kwamba Yesu alisema: “Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi.” (Yohana 15:12) Amri hiyo ina matokeo gani maishani mwako? Je! upendo unaoonyesha ndio aina ile ambayo Yesu aliwekea mfano? Je! ni upendo wa kujinyima kweli kweli? Je! matendo yako na hisia zako zinatoa ushahidi wa upendo huo kuelekea wote katika kundi la Kikristo na kuelekea washiriki wa jamaa yako mwenyewe?
12. (a) Ikiwa ‘tunafundishwa katika Yesu’ kweli kweli, hilo litafanya mabadiliko ya kadiri gani ndani yetu? (b) Hivyo, imetupasa tuwe tukifanya nini na mambo tunayojifunza kutoka Biblia?
12 Mtume Paulo anaeleza kwamba ‘tukimsikia’ Yesu kweli kweli na ‘kufundishwa katika yeye,’ utu mzima wetu utabadilika. Tutaweka mbali utu unaolingana na njia yetu ya zamani ya maisha na tutavaa “utu mpya,” unaoonyesha sifa bora za Yehova. (Waefeso 4:17-24; Wakolosai 3:8-14) Unapojifunza Biblia, je! unafikiria kwa uzito sehemu ambazo wewe binafsi unahitaji uzirekebishe ili umpendeze Mungu? Je! unadhamiria kufanya mabadiliko hayo? Je! unaijali kazi ya lazima ambayo Yesu aliamuru ifanywe wakati wetu—kazi ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu uliosimamishwa—na unatafuta njia za kuishiriki? Je! kuthamini fadhili zisizostahilika za Mungu kuelekea wewe kunachochea ndani yako tamaa ya moyo wote ya kufanya hivyo?—Mathayo 24:14.
13. (a) Ikiwa sisi si waangalifu, huenda mioyo yetu ikatupotezaje? (b) Basi, ni lazima tuzifuate hatua za Kristo kwa kadiri gani?
13 Yatupasa tuwe waangalifu tusiruhusu mioyo yetu itupoteze. Mamilioni ya watu wanajidai kuwa wanamwamini Yesu Kristo, na labda wanaweza kutaja baadhi ya mambo aliyofundisha, lakini wanafuata yale tu wanayoona yanawafaa. Huenda wengine wanaepuka kujitia katika mwenendo wanaodhani ni mbaya sana. Huenda tazamio la kuishi katika dunia-Paradiso chini ya Ufalme wa Mungu likaonekana zuri kwao, na huenda wanafurahia kushirikiana sasa pamoja na wale wanaojitahidi kwa moyo mnyofu kufuata kanuni za Kikristo maishani mwao. Lakini ikiwa tunataka tuwe kati ya wale watakaookoka waingie katika “dunia mpya,” ni lazima tusikilize kwa makini kila jambo analosema Yesu. Ni lazima tufahamu kwamba hatuwezi kufaulu kuelekeza hatua zetu wenyewe. Ni lazima tumsikilize Mwana wa Mungu, yeye aliyeagizwa na Yehova awe Mkombozi wa watu Wake, tutembee kwa uangalifu katika hatua zake.—Yeremia 10:23; Mathayo 7:21-27; 1 Petro 2:21.