Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 7/15 kur. 8-13
  • Mchungaji Mwema na “Zizi Hili” Lake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mchungaji Mwema na “Zizi Hili” Lake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Zizi la Kondoo la Mapema, Chini ya Torati
  • Zizi Jipya Chini ya Mchungaji Mwema
  • Yale Mazizi ya Kondoo na Yule Mchungaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Mazizi ya Kondoo na Mchungaji
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • “Mchungaji Mwema” na Lile “Kundi Dogo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Mchungaji Mwema na Mazizi ya Kondoo
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 7/15 kur. 8-13

Mchungaji Mwema na “Zizi Hili” Lake

1, 2. (a) Mfalme Daudi alimweleza Yehova jinsi gani katika Zaburi 23:1? (b) Kwa sababu gani ilifaa kumfananisha Yehova na mchungaji na Israeli kama kondoo wake?

“[YEHOVA] ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu. Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, kando ya maji ya utulivu huniongoza.” Mvulana mmoja aliyekuwa mchungaji wakati mmoja na pia mpiga-kinubi, na baadaye akawa mfalme wa taifa la Israeli, alitumia maneno hayo kuanza mmoja wa nyimbo zake zenye kupendwa sana.​—Zaburi 23:1, 2.

2 Ni taifa la kale la Israeli tu ambalo mtunga zaburi mwingine angeweza kuandikia maneno ya Zaburi 95:6, 7: “Njoni, tuabudu, tusujudu, tupige magoti mbele za [Yehova] aliyetuumba. Kwa maana ndiye Mungu wetu, na sisi tu watu wa malisho yake, na kondoo za mkono wake.” Ingawa mfalme wa kibinadamu wa taifa la Israeli angeweza kufananishwa na mchungaji, taifa hilo lilikuwa na mchungaji aliye juu zaidi, yaani Yehova Mungu. Ndiye Mchungaji aliye mzuri kabisa ambaye anaweza kuigwa na wanaume wanaotumikia wakiwa wachungaji kwa usemi wa mfano katika kundi la watu walio wakf wa Yehova.

3. Kumtaja Yehova kuwa Mchungaji kulifaaje hata kuhusiana na Yesu?

3 Mfalme Daudi alitangulia kuwa kivuli cha Yesu Kristo, isipokuwa Yesu Kristo ni mkubwa kuliko Daudi wa zamani, ambaye alikuwa babu yake wa kifalme. Kwa kufaa sana, basi, angeweza kutumia na kutaja maneno ya Daudi: ‘Yehova ndiye mchungaji wangu.’ Je! mtangulizi wake, Yohana Mbatizaji, hakuelekeza kidole kwa Yesu Kristo aliyekuwa akikaribia kwa kuwaambia wasikilizaji waliokuwa karibu naye hivi: “Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu”? (Yohana 1:29, 36) Kwa kumsema Yesu kuwa Mwana-kondoo, wa jamaa ya kondoo, huenda ikawa Yohana alikuwa akiyafikiria maneno ya Isaya 53:7: ‘Alipelekwa kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni.’ Na katika kitabu kile cha mwisho kabisa cha Biblia, kuanzia Ufunuo 5:6 na kuendelea, Yesu aliyetukuzwa anatajwa mara 28 kuwa Mwana-Kondoo wa mfano.

4. Ni kwa jinsi gani Yesu alikuwa kama kondoo katika zizi la kondoo na hilo zizi la kondoo lilikuwa nini?

4 Kwa kuzaliwa kimwujiza duniani alikuwa amezaliwa ndani ya taifa la Israeli, mwaka wa 2 K.W.K. Hivyo akaja chini ya agano la Torati ambalo Yehova, yule Mchungaji wa Israeli, alikuwa amefanya pamoja na watu wake wachaguliwa. Hilo agano la Torati, pamoja na Amri Kumi zalo, lilikuwa limepatanishwa kwa ajili ya taifa la Israeli na nabii Musa. (Wagalatia 4:4, 5) Na Yesu, akiwa mshiriki wa hao watu wachaguliwa, alikuwa mmoja wa kondoo wa mfano ambao Yehova ndiye alikuwa Mchungaji Mkubwa Kabisa wao. Hivyo Yesu alikuwa katika zizi la kondoo la mfano, yaani, kuwa na uhusiano wenye upendeleo pamoja na Mchungaji wa Kimungu akiwa amelindwa na agano la Torati ya Musa lililokuwa kama ukuta wa ulinzi.

5. Ni nini sababu ya kuwa na maoni tofauti juu ya zizi la kondoo la Yohana 10:1?

5 Je! hapa tunamaanisha kwamba lile “zizi” la kondoo linalotajwa katika Yohana sura ya 10, mstari wa 1, ni mpango wa agano la Torati ya Musa? Hasa-a! Yaliyokuwa maelezo ya hapo mbele ya zizi la kondoo kuwa ni agano la Kiabrahamu msingi wake ulikuwa ni yale maoni ya kwamba Yohana sura ya 10 ilitaja moja kwa moja zizi moja tu, na kama ingekuwa hivyo, basi kwa kufaa agano la Kiabrahamu ndilo lingekuwa maana yake. Hata hivyo, kujifunza zaidi sura hiyo kulionyesha kwamba kwa kweli Yesu alizungumza juu ya zizi zaidi ya moja. Kwa hiyo, kama tutakavyoona, ikafaa rekebisho la ufahamu lifanywe.

6. Unaonaje juu ya marekebisho hayo ya ufahamu wa mambo ya Kibiblia?

6 Mara kwa mara marekebisho hayo yanakuwa ya lazima, kwa maana Mithali 4:18 inatuambia kwamba “njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” Oh, ndiyo, wapinzani wa ile kweli wenye kuasi imani ‘wanasagia meno’ mafunuo hayo yanayokuja hatua kwa hatua, lakini sisi hatuhangaishwi nao. (Matendo 7:54) Bali, sisi tunamshukuru Yehova kwamba “nuru imemzukia mwenye haki, na furaha wanyofu wa moyo.” (Zaburi 97:11) Sisi tuna uhakika kwamba mtafurahi sana kujua maana yenyewe hasa ambayo mfano wa Yesu wa yale mazizi ya kondoo unayo kwenu na kwa Mashahidi wa Yehova wengine wote leo.

Zizi la Kondoo la Mapema, Chini ya Torati

7. Kuhusiana na zizi la kondoo la Kiisraeli, Yesu alichukuaje daraka jipya mwaka 29 W.K.?

7 Namna gani, basi, juu ya hilo zizi la kondoo la agano la Torati ya Musa? Baada ya Yesu kuwa amebatizwa na Yohana Mbatizaji, na akawa amepakwa mafuta kwa roho takatifu ya Yehova na akawa amemaliza siku 40 za kujaribiwa katika jangwa la Yudea, Yesu Kristo alikuja kwenye zizi la kondoo la Kiisraeli akiwa Mchungaji wa kiroho katika mwaka wa 29 W.K. Yesu Kristo alisema kwamba yeye alikuwa ametumwa hasa kwenye “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mathayo 10:6; 15:24) Kufikia wakati huo yeye alikuwa amekuwa mmoja tu wa Waisraeli wa kimwili wenye kuishi ndani ya mpango wa zizi la kondoo wa agano la Torati ya Musa. Lakini sasa, baada ya kupakwa mafuta na kuzaliwa kwa roho ya Yehova, Yesu Kristo angeweza kuja kwenye hilo zizi la kondoo akiwa katika daraka lake mpya la kuwa “mchungaji mwema.”​—Yohana 10:11.

8. Ni nani aliyekuwa bawabu wa mfano wa Yohana 10:3, na jinsi gani hivyo?

8 Yohana Mbatizaji ndiye aliyekuwa wa kwanza kumtambua Yesu kuwa yule Mchungaji wa Kweli aliyewekwa na Mchungaji Mkubwa wa Wote, Yehova Mungu. Yesu hakuja kufanya unyang’anyi katika zizi la kondoo bali alikuja kufanya shughuli halali. Kwa njia yenye kuheshimika angeweza kujitokeza akubaliwe aingie katika zizi la kondoo la taifa la Israeli. Kwa kupatana na unabii wa Malaki 4:5 (linganisha Mathayo 11:12-14; Luka 1:13-17), Yohana alikuwa amepewa na yule Mchungaji Mkubwa wa Wote mgawo wa kuwa “bawabu” wa lile zizi la kondoo la Kiisraeli. (Yohana 1:15, 17, 19-28; 10:3) Yohana alitambua vithibitisho vya Yesu Kristo vya kuwa Mchungaji mdogo wa Yehova Mungu na pasipo kukawia akawa tayari kumwacha aingie, kumtambulisha kuwa Mchungaji wa Kimasihi ambaye angeita kondoo zake kwa majina na kuwaongoza malishoni.

9, 10. Yesu alifaaje maelezo yake mwenyewe juu ya mchungaji, na wachungaji Waisraeli walishughulikaje na kondoo zao?

9 Yesu alitimiza maelezo yake mwenyewe juu ya Mchungaji wa Kweli na Mwema, kama yanavyotajwa katika maneno haya kwenye Yohana 10:1-5: “Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang’anyi. Aingiaye mlangoni ni mchungaji wa kondoo. Bawabu humfungulia huyo, na kondoo humsikia sauti yake; naye huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje. Naye awatoapo nje kondoo wake wote, huwatangulia; na wale kondoo humfuata, kwa maana waijua sauti yake. Mgeni hawatamfuata kabisa, bali watamkimbia; kwa maana hawazijui sauti za wageni.”

10 Mchungaji wa kale wa Kiisraeli alizoeana sana na kondoo zake. Alikuwa akitoa mwito wa sauti isiyoweza kupatana na ya mwingine, naye aliitumia kuita kondoo zake wakusanyike pamoja wapokee uangalizi wake binafsi. Zaidi ya hilo, yeye alimpa kila mmoja wa kondoo zake jina lake mwenyewe. Kila kondoo angetii na kuitikia wakati jina lake mwenyewe liliitwa. Kondoo walijua uzito na mvumo wa sauti ya mchungaji wao mwenyewe na kwa hiyo hawangeitikia sauti ya mgeni asiyekuwa mwangalizi wao.

11. Sisi binafsi twapaswa tuoneje juu ya daraka la Yesu akiwa Mchungaji?

11 Kulingana na hilo, ni faraja kama nini kwetu kuwa tumehakikishiwa kwamba Mchungaji wetu wa kiroho anajua kila mmoja wetu kwa jina na anaweza kumpa kila mmoja wetu uangalizi na utunzaji wa kibinafsi! Sisi tusiwe kama wengi wa wasikilizaji wa siku za Yesu ambao hawakuuelewa ufananishi wenye maana sana aliowaeleza. Kwenye Yohana 10:6 imeandikwa hivi ili maneno haya yawe mfano wa kutuonya: “Mithali hiyo Yesu aliwaambia; lakini wao hawakuelewa na mambo hayo aliyowaambia.”

12. “Wageni” ambao Yesu alizungumza juu yao ni nani, na walikuwaje hivyo?

12 Waisraeli wale wengine waliokuja wakadai kuwa wao ndio Masihi, au Kristo aliyeahidiwa, ndio ambao Yesu aliwabandika jina la kuwa wageni. Hawakutambulishwa kuwa wao ni Mchungaji wa Kimasihi wa Yehova na yule “bawabu” wake aliyewekwa, ambaye alikuwa Yohana, yule ambaye Yesu mwenyewe alimjia ili abatizwe. Kwa kufanya hivyo Yesu hakukosea. (Mathayo 3:1-7; Marko 1:1-7; Luka 3:1-9) Ilikuwa ni kwa kusudi la kuwalinda watu kwamba Yesu akaona ni vizuri ajijulishe kwa watu kuwa Ndiye Yehova alikuwa akiwapelekea awe mchungaji wa kiroho wao. Pia kusudi lilikuwa kuwafunua wazi wachungaji wadanganyifu.

Zizi Jipya Chini ya Mchungaji Mwema

13. Mungu alifanya badiliko gani kwa habari ya zizi la kondoo lake?

13 Jambo la maana ni mtu aingie katika zizi la kondoo linalofaa, siku za huko nyuma na hata leo. Je! hilo linadokeza kwamba kungekuwako badiliko la mazizi ya kondoo yenye kukubaliwa na Yehova Mungu? Ndiyo. Yale ambayo Yesu aliendelea kusema katika Yohana sura ya 10 na yale yanayoonyeshwa na mambo ya uhakika ya historia​—hayo yote mawili yanaonyesha kwamba Mungu angeweka zizi jipya mahali pa zizi la kondoo la Kiisraeli chini ya Torati. Angalia hilo tunapoendelea na maneno ya Yesu.

14, 15. Kwa sababu gani ni wazi kwamba katika Yohana 10:7-10 Yesu alisema juu ya zizi la kondoo jipya?

14 “Basi Yesu aliwaambia tena,” kwenye Yohana 10:7-10, “Amin, amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. Wote walionitangulia ni wevi na wanyang’anyi; lakini kondoo hawakuwasikia. Mimi ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho. Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.”

15 Angalia katika kifungu hicho Yesu anajisema yeye mwenyewe kuwa mlango wa zizi la kondoo analolitaja sasa, mlango wa kuingia katika hili zizi la kondoo la Mchungaji Mkubwa wa Wote, Yehova Mungu. Yesu siye aliyekuwa mlango wa mfano wa kuingia ndani ya zizi la kondoo la Israeli wa kimwili, kwa maana yeye mwenyewe alikuwa amezaliwa katika taifa hilo kwa uzazi wa kibikira kutokana na Mariamu bikira Myahudi. Yesu siye aliyekuwa mpatanishi aliye kama mlango wa agano la Torati ambalo kupitia hilo taifa la Israeli lilikuwa limeingizwa ndani ya uhusiano wa pekee kabisa pamoja na Yehova Mungu. Ilikuwa zamani sana kabla ya Yesu kuzaliwa duniani Yehova Mungu alipoliambia taifa la Israeli hivi: “Ni ninyi tu niliowajua katika jamaa zote zilizo duniani.” (Amosi 3:2) Mchungaji mdogo wa kweli wa Yehova Mungu angewaita kondoo wa kwanza wa kundi lake watoke katika zizi la kondoo la Kiyahudi lililo la mfano kisha awaongoze waingie ndani ya malisho ya pekee ya kiroho. Kwa hiyo lazima iwe sasa Yesu alikuwa ameanza kuzungumza juu ya zizi la kondoo jipya ambalo yeye, Mchungaji Mwema, alikuwa mlango walo katika maana nyingine.

16. (a) Kulikuwa kumekuwa kidokezi gani cha mapema kwamba Yehova angekuwa na zizi la kondoo jipya? (b) Yesu alionyeshaje kwamba hilo zizi la kondoo jipya lilikuwa karibu kutokea?

16 Wayahudi waliokataa kuwa wanafunzi wake wenye mfano wa kondoo walijisikia kwamba lao tu ndilo lililokuwa zizi la kondoo ambalo Yehova Mungu alilifikiria na kwamba lingeendelea kuwako mpaka wakati ujao usiojulikana. Wao hawakulifikiria lile “agano jipya” ambalo Yehova Mungu alikuwa ameahidi kuanzisha kulingana na unabii wa Yeremia 31:31-34. Hiyo ilimaanisha kungekuwa na uhusiano mpya pamoja na Yehova Mungu na, kwa hiyo, kungekuwa na zizi la kondoo la mfano lililo jipya. Yesu Kristo siye aliyekuwa mlango wa kuingia ndani ya zizi la kondoo ambalo lingefutiliwa mbali, liwe halina tena ukuta wa ulinzi wa Yehova. (Waebrania 8:7-13) Katika usiku alioadhimisha sikukuu yake ya mwisho ya Kupitwa akiwa pamoja na wanafunzi wake Wayahudi, Yesu alisema maneno yenye maana kubwa alipokuwa akiwapa divai ya Kupitwa. Aliipa divai hiyo maana ya mfano, akisema: “Kikombe hiki kinamaanisha lile agano jipya kwa uwezo wa damu yangu, ambayo itamwagwa chini kwa ajili yenu.”​—Luka 22:20, NW; Mathayo 26:27-29.

17, 18. (a) Hilo zizi la kondoo jipya ambalo Yesu ni Mchungaji Mwema walo lilikuwa nini? (b) Yeye pia angeweza kufananishwaje na mlango wa zizi hilo jipya?

17 Yesu Kristo angekuwa ndiye mlango wa kuingia kwenye zizi la kondoo lenye kudumu, zizi ambalo lingechukua mahali pa lile zizi la kwanza la kondoo la Wayahudi waliotahiriwa waliokuwa chini ya agano la Torati ya Musa. Wakati Yesu alipowaacha nyuma duniani wanafunzi wake kisha akapaa mbinguni siku 40 baada ya kufufuliwa kwake kati ya wafu, alipaa akiwa bado ana haki yake ya kuwa na uzima mkamilifu wa kibinadamu. Yeye hakuwa ameipoteza haki hiyo kwa kutenda dhambi yo yote katika mwili. (Isaya 53:3-12; Matendo 8:30-35) Kwa hiyo, alikuwa na utayari wa kutumikia kuwa mpatanishi na kutumia haki ya uzima hiyo, iliyofananishwa na damu yake, ili atie muhuri agano jipya lililo zuri zaidi kwa ajili ya wanafunzi wake duniani. Alifanya hivyo si baada ya siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. wakati ambao roho takatifu ilimiminwa juu ya wanafunzi watiifu wa Kiyahudi waliokuwa wakingoja Yerusalemu.

18 Hivyo wanafunzi hao wakaingizwa ndani ya lile agano jipya, kukawa na zizi jipya la kondoo, zizi la kuwa na uhusiano pamoja na Yehova Mungu kwa kulitegemea agano jipya lililotiwa muhuri na damu ya Yesu Kristo. Kondoo wa mfano wa hili zizi jipya walizaliwa kwa roho ya Yehova na wakapakwa mafuta kwa roho hiyo. Yesu Kristo ndiye aliyekuwa mlango wa kuingia kwenye zizi hilo na pia ndiye aliyekuwa Mchungaji Mwema aliyewekwa na Yehova atunze kondoo walio ndani ya zizi.

19. Unabii katika Zekaria 13:7 ulitimizwa kwa njia gani?

19 Wakati wa zile sehemu za siku tatu ambazo Yesu alikuwa amekamatwa na akawa mfu katika kaburi, alikuwa amelazimika kumpokeza kabisa yule Mchungaji Mkubwa wa Wote, Yehova Mungu, uangalizi na utunzaji wa wanafunzi wake waliokuwa mfano wa kondoo. Hapo ndipo uneni wa Yehova kwenye Zekaria 13:7 ulipotimizwa, yaani: “Mpige mchungaji, nao kondoo watatawanyika; nami nitaugeuza mkono wangu juu ya wadogo.” Mkono wa yule Mchungaji Mweza Yote, Yehova, uligeuzwa ukawa juu ya wanafunzi hao wadogo, mpaka wakaja kurudishwa tena kwa Mchungaji mdogo wake aliyefufuliwa, Yesu Kristo.​—Mathayo 26:31, 32.

20. Ni kwa njia gani andiko la Yohana 10:16 linaelekeza kwenye tazamio la zizi jingine bado litokee, na kwa sababu gani hilo lapasa kuwa jambo la kushughulikiwa nasi?

20 Lakini akiwa anafikiria hili zizi la kondoo jipya chini ya Mchungaji Mwema, angalia kwamba katika Yohana 10:16 Yesu alisema: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao imenipasa kuwaleta.” Je! hilo halionyeshi kwamba yeye angekuwa na zizi jingine, la pili, ambalo angekuwa Mchungaji Mwema walo? Ikiwa ndivyo, lingetokea wakati gani na ni nani wangekuwa kondoo ndani yalo? Hayo ni maswali yenye kufaa sana wakati huu, na majibu yayo yanaweza kuhusu moja kwa moja tumaini lako na mataraja ya milele. Basi na tuchunguze jambo hilo.

Wewe Utajibuje?

◻ Yesu alizaliwaje ndani ya zizi la kondoo, na Mchungaji wa zizi hilo alikuwa nani?

◻ Yesu alikuja akiwa katika daraka jipya gani katika mwaka 29 W.K.?

◻ Yohana Mbatizaji alitumikia katika daraka gani kuhusiana na zizi la kondoo la Kiisraeli?

◻ Zizi la kondoo jipya ambalo Yesu alikuwa Mchungaji Mwema walo lilikuwa nini?

◻ Ni nini kinachoonyesha kwamba bado kungalikuja zizi la kondoo jingine?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Akiwa bawabu wa mfano, Yohana Mbatizaji alimkaribisha Mchungaji Mwema, Yesu

[Picha katika ukurasa wa 11]

Yesu aliwaingiza kondoo wake ndani ya zizi ia kondoo jipya. Zizi hilo lilikuwa nini?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki