“Mchungaji Mwema” na Lile “Kundi Dogo”
“Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.”—Luka 12:32.
1. Yehova akiwa mwangalizi anafananishwa na nani na Mfalme Daudi na nabii Isaya?
MFALME DAUDI wa Bethlehemu, ambaye wakati mmoja alikuwa kijana mchungaji, alianza mojayapo ya zaburi zake zilizoongozwa na Mungu kwa maneno haya: “[Yehova] ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu.” (Zab. 23:1) Naye nabii Isaya, mwandikaji wa Biblia mwenzake, vilevile alimfananisha Yehova na mchungaji, akisema: “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake.” (Isa. 40:11) Lakini Yehova ana mchungaji mdogo wake. Kwa kufaa sana yeye anamwita, “mtumishi wangu, Daudi.”
2. (a) Ni Daudi yupi ambaye maneno ya Ezekieli 37:24, 25 yanahusu? (b) Yesu aliutumiaje unabii wa Zekaria 13:7, na kwa sababu gani hivyo?
2 Mamia mengi ya miaka baada ya Mfalme Daudi kufa, Yehova alimwongoza Ezekieli, mwandikaji mwingine wa Biblia, atabiri hivi: “Na mtumishi wangu, Daudi, atakuwa mfalme juu yao, nao wote watakuwa na mchungaji mmoja; . . . na Daudi, mtumishi wangu, atakuwa mkuu wao milele.” (Eze. 37:24, 25) Lazima unabii huu uwe unahusu mchungaji mdogo wa Yehova, Yesu Kristo, Daudi Mkuu Zaidi. Katika usiku wa Nisani 14, 33 W.K., wakati Yesu Kristo aliposalitiwa, akapelekwa kizuizini na kuletwa ajaribiwe mbele ya adui zake, unabii wa Zekaria 13:7 ulipata kutimizwa: “Amka, Ee upanga, juu ya mchungaji wangu, na juu ya mtu aliye mwenzangu, asema [Yehova] wa majeshi; mpige mchungaji, nao kondoo watatawanyika.” Yesu Kristo mwenyewe aliutumia unabii huo katika njia hiyo.—Mt. 26:31; Marko 14:27.
3, 4. (a) Kwa sababu gani Wayahudi waliompinga Yesu kuhusiana na ponyo la mwanamume aliyezaliwa akiwa kipofu waliendelea na dhambi yao? (b) Baadaye, wakati wa sikukuu ya kuzinduliwa kwa hekalu majira ya baridi, ni kwa sababu gani Yesu hakuwahesabu Wayahudi hao wenye kupinga kati ya “kondoo” wake?
3 Kwa hiyo Yesu Kristo hakuwa akijitanguliza, bali alikuwa na haki ya kujilinganisha na mchungaji akajiita “mchungaji mwema.” (Yohana 10:6, 11, 14) Jambo hilo lilitukia kuhusiana na mwujiza wake aliofanya wa kumponya mwanamume aliyekuwa amezaliwa akiwa kipofu. Watu wasioamini miongoni mwa watu wake mwenyewe walipinga jambo hilo, wakamwuliza: “Je! sisi nasi tu vipofu?” Ni jambo gani lililofuata ulizo hilo lenye kukaidi? “Yesu akawaambia, Kama mngekuwa vipofu, msingekuwa na dhambi; lakini sasa mwasema, Twaona; basi dhambi yenu inakaa.” (Yohana 9:40, 41) Wakati fulani baadaye, wakati wa sikukuu ya kuzinduliwa hekalu la Yerusalemu, katika majira ya baridi (Desemba) ya mwaka 32 W.K., Yesu aliwaambia hivi Wayahudi fulani wasioamini waliokuwa wanamzunguka:
4 “Kazi hizi ninazozifanya kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia. Lakini ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu. Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami [nitawapa] uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu. Mimi na Baba tu umoja.”—Yohana 10:19-30.
5. Katika Yohana 10:1-5, Yesu alimfananisha na nani mtangulizi wake ambaye angemjulisha kwa Israeli?
5 Watu hao wasioamini si kwamba tu waliukataa ushuhuda uliotolewa na kazi za Yesu juu ya yeye alikuwa nani, bali vilevile waliukataa ushuhuda wa mtangulizi wa Yesu, yule mwanamume aliyemjulisha Yesu kwa Waisraeli akiwa Masihi, Kristo. Yesu alitaja namna mchungaji wa kweli alivyohitaji kuwa na kitambulisho kama hicho, aliposema hivi: “Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang’anyi. Aingiaye mlangoni ni mchungaji wa kondoo. Bawabu humfungulia huyo, na kondoo humsikia sauti yake; naye huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje. Naye awatoapo nje kondoo wake wote, huwatangulia; na wale kondoo humfuata, kwa maana waijua sauti yake. Mgeni hawatamfuata kabisa, bali watamkimbia; kwa maana hawazijui sauti za wageni.”—Yohana 10:1-5.
“ZIZI LA KONDOO” NA “BAWABU”
6. Ni kwa sababu gani lile “zizi la kondoo” la mfano ambamo “bawabu” alimwingiza halikuwa ule mpango wa Agano la Torati?
6 Hivyo, sasa, “zizi la kondoo” na “Bawabu” humaanisha nini, kwa kuwa Yesu alipata kuwa seremala huko Nazareti wala yeye hakupata kamwe kuwa mchungaji wa kondoo halisi? Kwanza, hilo “zizi la kondoo” halikumaanisha ule mpango wa Agano la Torati ambao Yehova Mungu alianzisha pamoja na taifa la Israeli kupitia kwa Musa akiwa mpatanishi. Bila shaka Yesu hakuhitaji kuingizwa katika huo mpango wa Agano la Torati na “bawabu” Myahudi ye yote. Yesu alikuwa amezaliwa katika mpango huo. Wagalatia 4:4, 5 husema hivi: “Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria.” Ili awakomboe, Yesu alikufa.
7. (a) Ni siku gani ya mwaka 33 W.K. ambayo katika hiyo Yehova aliumaliza ule mpango wa Agano la Torati alioufanya pamoja na Israeli, na kwa sababu gani? (b) Ni kwa sababu gani, kuanzia na Pentekoste ya mwaka 33 W.K. na kuendelea, hakukuwa na mpango wa Agano la Torati ambao kutoka huo Yesu angewaongoza Wayahudi?
7 Ili aweze kumpelekea Mungu bei ya ukombozi, Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu katika siku ya tatu ya kifo chake katika mwaka 33 W.K. Katika siku ya 40 kuhesabu tangu siku ya ufufuo wake, Yesu alipaa kurudi mbinguni. Siku kumi baada ya hapo ikafika ile sikukuu ya Pentekoste ya Wayahudi ya majira ya Masika, Siwani 6, 33 W.K. Katika siku hiyo Mungu alimtumia aimimine roho takatifu juu ya wanafunzi wake waliokuwa wakingojea huko Yerusalemu. Hiyo ilimaanisha kwamba yeye alikuwa ameonekana mbele za Mungu ili kumtolea bei ya dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu ili kuwakomboa wanadamu wote waliokuwa wameuzwa katika dhambi, kutia na Wayahudi. Kwa hiyo, katika siku hiyo, Yehova Mungu alilimaliza lile agano la Torati na mahali pake pakachukuliwa na agano jipya lililoahidiwa, akilifanya pamoja na wanafunzi waliozaliwa kwa roho wa Mpatanishi, Yesu Kristo, wala hakulifanya na Wayahudi. (Kol. 2:13, 14) Kwa hiyo, hakukuwa tena na agano la Torati la Kiyahudi ambalo kutoka hilo Mchungaji Yesu angeweza kuwaongoza Wayahudi walioamini.
8. (a) Kwa hiyo, basi, hilo “zizi la kondoo” lilifananisha nini? (b) Kwa hiyo, Wazao wa asili wa Ibrahimu walikuwa wakitazamia nini?
8 Kwa msaada wa hayo yaliyosemwa hapo juu, ulizo linajitokeza hata zaidi, “zizi la kondoo” alilolitaja Yesu katika Yohana 10:1 lafananisha nini kweli kweli? Pasipo shaka lazima liwe lilifananisha jambo lililotangulia na lililotia mengi zaidi na kuendelea kwa muda mrefu zaidi kuliko agano la Torati la mwaka 1513 K.W.K. Jambo hilo ni lile agano la Ibrahimu. Wakati mzee huyo wa ukoo alipovuka Mto Frati katika mwaka 1943 K.W.K. na kuingia katika Nchi ya Ahadi, ahadi ya Mungu kwake ilianza kutenda kazi kwake na kwa wazao wake wa wakati ujao: “Nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.” (Mwa. 12:3) Miaka mingi baadaye, wakati Ibrahimu alipoonyesha nia yake ya kumtoa mwanawe Isaka awe dhabihu, Mungu aliongezea ahadi yake: “Na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwa. 22:17, 18) Tangu wakati huo na kuendelea, wazao wa Ibrahimu walianza kuutazamia huo “uzao” uliokuwa ukija. Kwa hiyo, lile “zizi la kondoo” lilifananisha mpango wa Agano la Ibrahimu. Wale wenye mfano wa kondoo waliotiwa ndani yake wangefananisha wale waliokuwa wakiungojea ule “uzao” ulioahidiwa uliokuwa ukija.
9. Ni nani ambaye hangeruhusiwa na. “bawabu” kupita na kuingia kwenye “zizi la kondoo”?
9 Iwapo hao wenye mfano wa kondoo walitangulia kujua juu ya huo “uzao” au hapana, wangeukaribisha ulipojulishwa kwao na unapoletwa kwao. Ye yote ambaye angejaribu kujipatia “kondoo” hao kwa njia ya udanganyifu ili awatumie kwa faida yake mwenyewe angekuwa “mwivi na mnyang’anyi.” “Bawabu” wa zizi la kondoo hangemjulisha kwa kondoo Masihi au Kristo wa uongo wa namna hiyo. Ye yote ambaye angepitia kwa “mlango” na kufunguliwa na “bawabu” angekuwa ndiye “mchungaji” wa kweli, ule “uzao” wa Ibrahimu.
10. “Bawabu” huyo alionekana kuwa nani, na ni kulingana na unabii gani?
10 Walakini, je! huyo “bawabu” alikuwa nani? Ilionekana kwamba alikuwa Yohana Mbatizaji, mwanamume wa jamaa ya kikuhani wa kabila la Lawi. Mungu alikuwa ameahidi kumtuma mtangulizi wa “uzao” wa Ibrahimu. Katika Malaki 3:1 ilikuwa imetabiriwa hivi: “Angalieni, namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu; naye Bwana mnayemtafuta, atalijilia hekalu lake ghafula; naam, yule mjumbe wa agano mnayemfurahia, angalieni, anakuja, asema [Yehova] wa majeshi.” (Marko 1:1-11) Kwa hiyo Yohana alikuwa akiutafuta ‘uzao wa Ibrahimu’ uliokuwa ukija na, kwa hiyo, yeye alikuwa mtu mwenye mfano wa kondoo sawasawa na wale waliokuwa katika zizi la kondoo la mpango wa Agano la Ibrahimu. Hata hivyo, Yohana aliuawa baada ya kufanya utumishi wake wa pekee kwa muda wa mwaka mmoja au zaidi. Kwa hiyo yeye hakuendelea kuwa hai mpaka Pentekoste ya mwaka 33 W.K. ili apate kuwa mmoja wa lile “kundi dogo” la warithi watiwa mafuta washirika katika ufalme wa mbinguni.—Mt. 11:11-14; 14:1-12; Luka 12:32; Gal. 3:16.
11. (a) Yesu alimthibitishaje Yohana Mbatizaji kuwa mtangulizi wake? (b) Yesu alikuwa “mjumbe” wa agano jipi alipokuwa akifuatana na Bwana Yehova kuingia kwenye hekalu?
11 Alipokuwa akizungumza sehemu aliyotimiza Yohana Mbatizaji katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova, Yesu aliwaambia Wayahudi hivi: “Huyo ndiye aliyeandikiwa haya, Tazama, mimi namtuma mjumbe wangu mbele ya uso wako, atakayeitengeneza njia yako mbele yako.” (Mt. 11:10) Hivyo, Yesu aliutumia unabii wa Malaki 3:1 kuhusu Yohana Mbatizaji, akiwa yeye aliyetumwa mbele ya Yehova na ya “mjumbe wa agano” wake. Yesu Kristo, anayekuja pamoja na Bwana Yehova katika hekalu ili kulikagua, ndiye yule mjumbe, si wa lile agano la Torati, wa lile agano la Ibrahimu. Wale waliouamini unabii wa Yehova na waliotiwa ndani ya mpango wa Agano la Ibrahimu walikuwa wakikutazamia kuja kwake huyo “mjumbe” wa Kimasihi.
12. Yohana Mbatizaji alisema nini juu ya namna alivyokuja ‘kumjua’ aliye mkuu wa “uzao wa Ibrahimu’?
12 Kwa habari ya yule mkuu wa huo ‘uzao wa Ibrahimu,’ Yohana Mbatizaji alisema hivi: ‘Niliiona roho ikishuka kama hua kutoka mbinguni; nayo ikakaa juu yake. Wala mimi sikumjua; lakini yeye aliyenipeleka kubatiza kwa maji, huyo aliniambia, Yeye ambaye utaiona roho ikishuka na kukaa juu yake, huyo ndiye abatizaye kwa roho takatifu. Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu.’—Yohana 1:31-34.
13. (a) Yohana Mbatizaji alimfungulia “mlango” yule Mchungaji wa kweli wakati gani? (b) Wakati huo Yohana alikuwa akielekeza kwenye ‘uzao wa Ibrahimu’ wa namna gani?
13 Yesu hakuepuka kupitia kwenye “mlango” ili kuingia katika zizi la kondoo. Alipokuwa na umri wa miaka 30 yeye alimwendea Yohana Mbatizaji ili apate kuzamishwa katika maji. Baada ya kutumia siku 40 jangwani akiwa chini ya majaribu, alirudi akiwa na uhakika alipokuwa Yohana Mbatizaji pamoja na hesabu fulani ya wanafunzi wake. Alipokuwa akimkaribia “bawabu” wa mfano wa lile zizi la Agano la Ibrahimu, Yohana alimwona akija akapaza sauti hivi: “Tazama, Mwana-Kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu!” (Yohana 1:29, 36) Si Mwana-Kondoo aichukuaye dhambi ya taifa la Israeli, bali “Mwana-Kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu!” Kwa njia hiyo, Yohana Mbatizaji akamfungulia “mlango” wa mfano yule Mchungaji wa kweli aliyekuwa na vitambulisho vilivyohitajiwa kutoka kwa Mchungaji wa Ulimwengu Wote, Yehova Mungu. Alipokuwa akivuta fikira za wanafunzi wake kwa Yesu aliyekuwa akikaribia, Yohana hakuwa akiwaelekeza kwa Myahudi wa vivi hivi tu aliyetahiriwa na ambaye ni mzao wa asili wa Ibrahimu wa kidunia. Hapana, yeye alikuwa akiwaelekeza kwa Mtiwa Mafuta, mzao aliyezaliwa kwa roho wa Yehova Mungu, Ibrahimu Mkuu Zaidi. Yeye ndiye aliyekuwa mkuu wa ule “uzao” wa Ibrahimu wa Kimbinguni ambaye kupitia kwake jamaa zote za dunia zingejibarikia.
14. (a) Alipokuwa akilikaribia lile “zizi la kondoo,” je! Yesu alikuwa akiwatafuta Wayahudi wa asili na wanadamu wengine wote kwa ujumla? (b) Mchungaji wa Mashariki ya Kati alikuwa akimwitaje kondoo mmoja mmoja aje kwake?
14 Kwa hiyo yeye alistahili kukubaliwa na “bawabu” aingie kwenye lile “zizi la kondoo” la mfano, ule mpango wa Agano la Ibrahimu. Yeye ndiye aliyekuwa mchungaji wa kweli, naye alikuja kutafuta, si Wayahudi wala wanadamu wengine wo wote kwa ujumla, bali wale ambao wangeitikia na kukubali nafasi ya kuwa pamoja naye sehemu ya ule ‘uzao wa Ibrahimu’ wenye sehemu nyingi ambao kupitia kwa huo baraka zingewajia mataifa yote. Wengi wa Wayahudi wa asili walimkataa walakini baki la Wayahudi wa asili lilimkubali. Hao ndio waliokuwa “kondoo” waliosikia sauti yake. Kwa hiyo, wakati alipowaita “kondoo wake kwa majina yao,” wao waliitikia, naye akawapeleka nje kwenye malisho. Huko Mashariki ya Kati mchungaji alikuwa akimpa kila kondoo jina lake mwenyewe.
15. (a) Mchungaji atatoaje sauti ya kuwaita kondoo wote kwa wakati mmoja, na ni kwa sababu gani hawatadanganyika na kuwafuata “wageni”? (b) Huo ni mfano wenye ulinzi kwa nani waufuate leo?
15 Walakini, wakati mchungaji alipotaka kuwaita kondoo wake wote pamoja, alikuwa akitoa sauti iliyoelekezwa kwa kondoo wote, tuseme, sauti ya kutatarika kama vile Sh-ri-ri-ri-ri-ri kwa namna ya sauti isiyoweza kutokezwa na wachungaji wengine. Ndivyo ilivyo kwamba, “naye awatoapo nje kondoo wake wote, huwatangulia; na wale kondoo humfuata,” kwa sababu wanaitambua sauti yake isiyoweza kuigwa na mwingine. Masikio yao ni yenye kusikia sana nayo yanawatambua “wageni” na waigaji. Wao hawatadanganywa na kufuata “wageni” hao wenye kushukiwa, na pengine wenye makusudi mabaya. Huo ni mfano mzuri wa kufuatwa kwa uangalifu na wale wenye mfano wa kondoo walio washiriki wa lile “kundi dogo,” ambao inampendeza Ibrahimu Mkuu Zaidi mwenye kuwakubali kuwapa Ufalme.
16. Ni kwa sababu gani Wayahudi hawakufahamu mfano ambao Yesu aliwaambia kuhusu mchungaji na kondoo wake?
16 Je! sisi leo tunafahamu maana ya yale Yesu alikuwa akisema juu yake hapo? Kwa habari ya Wayahudi wasioamini waliokuwa katika mpango wa Agano la Torati, hawakufahamu namna mfano alioutoa Yesu ulivyohusu. Ni kama vile yasemavyo masimulizi: “Mithali hiyo Yesu aliwaambia; lakini wao hawakuelewa na mambo hayo aliyowaambia.” (Yohana 10:6) Wao hawakuijua sauti ya Mchungaji wa Kimasihi, naye hakuwajua na kuwaita kwa majina yao wenyewe. Hali ya upofu ya kujifanya wao wenyewe iliwazuia wasimtambue. Sisi leo tusiwe kama wao.
“MLANGO WA KONDOO”
17. Kulingana na Yohana 10:7-10, Yesu alijifananisha na sehemu gani nyingine ya zizi la kondoo?
17 Kufikia hapo Yesu alibadili usemi wake wa mfano ili atoe mfano wa sehemu nyingine ya maana kuhusu jambo hilo. “Basi, Yesu aliwaambia tena, Amin, amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. Wote walionitangulia ni wevi na wanyang’anyi; lakini kondoo hawakusikia. Mimi ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho. Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili awe na uzima, kisha wawe nao tele.”—Yohana 10:7-10.
18. (a) Ni nani duniani ambaye hujaribu kutenda kama bawabu wa “mlango” wa mfano kwa Yesu? (b) Yesu alisema juu ya jamii gani ikiwa sehemu ya ishara ya “mwisho wa taratibu ya mambo,” na je! jamii hiyo inatumika kama bawabu kwa Yesu aliye “mlango”?
18 Ebu na tuangalie kwamba Yesu hasemi juu ya “bawabu” kuhusiana na yeye akiwa “mlango.” Yeye hasemi juu ya aitwaye “wakili wa Kristo,” kiongozi fulani wa madhehebu ya kidini ajidaiye kuwa hawezi kufanya kosa. Yesu alisema hivi: “Mimi ndimi mlango wa kondoo.” Na miezi fulani baadaye alisema hivi juu yake mwenyewe: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6) Maneno yake hayo hayakosi kuangalia kwamba, wakati Yesu alipokuwa akitoa unabii wake mrefu juu ya “ishara ya kuwapo [kwake] na ya mwisho wa taratibu ya mambo,” yeye alitabiri juu ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” ambaye bwana wake “atamweka . . . juu ya vitu vyake vyote.” (Mt. 24:3, 45-47) Lakini hiyo inahusu jamii ya “mtumwa” ya wafuasi wake waaminifu, wenye akili, ambayo angeiweka iangalie vitu vyake vyenye kuonekana duniani, na zaidi katika wakati huu wa “mwisho wa taratibu ya mambo.” Walakini, kuwekwa huko hakuifanyi jamii hiyo ya “mtumwa” kuwa “bawabu” wa Yesu.
19. Wale walio katika zizi la kondoo la mpango wa Agano la Ibrahimu wanafanyiza “kundi” kubwa kadiri gani, nao wokovu wao unapatikana kupitia kwa njia gani?
19 Yesu ni “mlango” wa mfano kwa hao wafuasi wake wenye mfano wa kondoo wanaofanywa pamoja naye kuwa sehemu ya ule ‘uzao wa Ibrahimu.’ Kwa hiyo wao wamo ndani ya lile “zizi la kondoo” la mpango wa Agano la Ibrahimu. Wote pamoja wanakuwa washiriki wa “kundi dogo” tu, kusema kwa kulinganisha, 144,000 tu wakiwa chini yake Mchungaji wao. Kwa kweli, wanafanyiza yale makabila 12 ya Israeli wa kiroho, nao wanasimama juu ya Mlima Sayuni wa kiroho pamoja na “Mwana-Kondoo wa Mungu,” Yesu Kristo. (Luka 12:32; Ufu. 7:1-8; 14:1-5) Wao wanauhesabia wokovu wao urithi wa kimbinguni, wala si wakili fulani wa Kristo, bali yeye aliye “mlango wa kondoo.” Kwa kuwa Yesu alisema hivi: “Mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho.” (Yohana 10:9) Akisema kwa niaba ya hilo “kundi dogo” liliko na tumaini la kimbinguni, mtume Paulo anamtaja “Bwana wetu Yesu Kristo. Ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya imani kuifikia neema hii ambayo tunasimama ndani yake; na kufurahi katika tumaini la utukufu wa Mungu.”—Rum. 5:1, 2; Efe. 2:18; 3:12.
20. Mchungaji mdogo wa Yehova amekuwa tofauti namna gani na wale “makristo wa uongo, na manabii wa uongo” waliokuja badala yake?
20 Katika unabii wake kuhusu “mwisho wa taratibu ya mambo,” Yesu alitabiri kwamba “makristo wa uongo, na manabii wa uongo” wangetokea wakiwa na udanganyifu mkuu. Hao wamekuja badala ya Kristo wa kweli, nao watu waliodanganywa waliowafuata wadanganyaji hao, wameibwa kidini wakauawa na kuharibiwa kiroho, ikiwa si kwa halisi. (Mt. 24:3, NW, 24, 25; Yohana 10:8, 10) Kwa upande mwingine, Yesu alikuja kama mwokoaji wa uhai, na kuvitolea viumbe vya kibinadamu nafasi ya kufurahia uzima mwingi zaidi ya ule walio nao sasa. Huo ni uzima wa milele mkamilifu na ulio katika mipango ya usalama ambayo imefanywa na Yehova Mungu, Mchungaji Mkuu Zaidi kupita wote. Kwa hiyo, Yesu Kristo, mchungaji mdogo wake mwenye kujinyima, ndiye tunayepaswa kufuata sisi, ikiwa tunatamani kupata uzima wa milele tukiwa “kondoo” wa Mungu.