Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • tp sura 9 kur. 94-107
  • Amani na Usalama Duniani Pote—Tumaini Lenye Kutegemeka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Amani na Usalama Duniani Pote—Tumaini Lenye Kutegemeka
  • Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Msingi Imara wa Kuwa na Uhakika
  • Dunia Kugeuka Kuwa Kao la Kibustani
  • Mwisho wa Ufukara na Utumwa Wenye Kuletwa na Uchumi
  • Afya na Uzima Wenye Kudumu
  • Uwezo wa Dunia Kuwa na Nafasi ya Kukaliwa na Idadi Hiyo ya Watu
  • Msingi Hakika kwa Furaha Yenye Kudumu
  • “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
    “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
  • Utawala wa Haki Wafanya Dunia kuwa Paradiso
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Baada ya Har-Magedoni, Dunia-Paradiso
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Je! Mungu Anajali?
    Je! Mungu Anajali?
Pata Habari Zaidi
Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
tp sura 9 kur. 94-107

Sura 9

Amani na Usalama Duniani Pote—Tumaini Lenye Kutegemeka

1, 2. Ni hali gani, zilizotabiriwa katika Biblia, ambazo zingeifanya dunia hii iwe mahali pazuri sana pa kuishi?

KAMA hali zenye amani, zenye usalama kweli kweli zingekuwapo kila mahali, dunia hii ingeweza kuwa mahali pa kufurahisha sana na penye kupendeza kuishi. Ijapokuwa haiko hivyo sasa, Biblia inatabiri kwamba bado dunia itakuwa kao zuri ajabu ambamo jamaa ya kibinadamu itafurahia uzima kwa ukamili.

2 Biblia inatoa ahadi gani? Twawezaje kuwa na hakika kwamba itatimizwa?

Msingi Imara wa Kuwa na Uhakika

3, 4. (a) Twajifunza nini kutokana na kutegemeka kwa sheria za msingi zinazouongoza ulimwengu wote mzima? (b) Ni nani Mfanyi wa sheria hizo, na kwa hiyo tuna sababu nzuri ya kuweka tumaini letu katika nini zaidi?

3 Sheria fulani za msingi zinauongoza ulimwengu wote mzima. Nyingi zazo hatuziweki maanani. Kucha, kuchwa, nyuso mbalimbali za mwezi, na majira yanakuja na kwenda katika namna inayosaidia kuleta imara ya maisha ya kibinadamu. Wanadamu wanaandika kalenda na kupanga utendaji mbalimbali miaka mingi mbele. Wanajua kwamba miendo ya jua, mwezi, na sayari ni yenye kutegemeka. Twaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

4 Mfanyi wa sheria hizo ni mwenye kutegemeka kabisa. Tunaweza kutegemea analosema na kutenda. Biblia inaahidi mfumo mpya wenye uadilifu katika jina lake, akiwa Muumba wa mbingu na dunia. (Isaya 45:18, 19) Katika kawaida yetu ya maisha ya kila siku, ni jambo la kawaida kuwategemea watu wengine kwa kipimo fulani—wale wanaoleta vyakula sokoni, wale wanaopeleka barua, na rafiki za karibu. Basi je! si jambo la akili, tuwe na uhakika zaidi sana katika Mungu na katika utimizo hakika wa ahadi zake?—Isaya 55:10, 11.

5. Ukosefu wa kusudio lo lote la ubinafsi katika yale ambayo Mungu ameahidi unatupaje imani?

5 Ingawa ahadi za wanadamu mara nyingi hazitegemeki, ahadi za Mungu zinategemeka kabisa na ni kwa faida yetu, si faida yake mwenyewe. Ingawa Mungu hahitaji cho chote kutoka kwetu, anapendezwa na wale wanaomwamini kwa sababu wanampenda yeye na njia zake za uadilifu.—Zaburi 50:10-12; 14.

6. Ni imani ya namna gani ambayo Biblia inatusaidia tujipatie?

6 Halafu, Biblia inazivutia nguvu zetu za kufikiri. Haitudai tuwe na imani yenye upofu au isiyo ya kiakili. Kwa kweli, inafasili imani ya kweli kuwa “taraja lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, wonyesho dhahiri wa mambo ya hakika ijapokuwa hayaonwi.” (Waebrania 11:1, NW) Katika Biblia, Mungu anatupa msingi unaofaa wa imani. Ufaaji wa msingi huo unakuwa wazi zaidi na zaidi wakati tunapokua katika maarifa ya Neno la Mungu na kuona ukweli walo ukifanya kazi katika maisha zetu wenyewe na katika utimizo wa mambo ya unabii walo.—Zaburi 34:8-10.

7. Tunapozichunguza ahadi za Biblia juu ya baraka za wakati ujao, haitupasi kutazamia kuziamini kututake tufanye nini?

7 Ahadi za Biblia juu ya baraka za wakati ujao zinapita sana yale ambayo wanadamu wanathubutu kutoa. Hata hivyo ahadi hizo hazitutaki tuamini mambo ambayo wanadamu hawajapata kuona yakitukia. Wala haziko tofauti na tamaa za kawaida za wanadamu. Fikiria chache za baraka hizo kubwa uone namna hii ilivyo kweli.

Dunia Kugeuka Kuwa Kao la Kibustani

8, 9. (a) Ni wazo gani linalopaswa kuletwa kwenye akili zetu na neno “paradiso”? (b) Je! kitu kama hicho kimepata kuwapo duniani? (c) Ni nini kinachoonyesha kwamba ni kusudi la Mungu kwa Paradiso ienee duniani pote?

8 Neno “paradiso” linatokana na maneno yanayofanana yaliyotumiwa katika nyakati za kale (Kiebrania, par·desʹ; Kiajemi, pairi·daeʹza; Kigiriki, pa·raʹdei·sos), maneno yaliyotumiwa kueleza vitu ambavyo kweli vilikuwako duniani wakati huo. Maneno hayo yote yana wazo la msingi la shamba zuri au bustani iliyo kama shamba zuri. Kama katika nyakati za kale, ndivyo na leo kuna mahali kama hapo pengi, pengine pakiwa ni bustani kubwa. Na mwanadamu ana tamaa ya asili ya kutaka sana uzuri wazo. Biblia inaahidi kwamba siku itakuja wakati sayari nzima hii itakapokuwa bustani ya namna hiyo iliyo kama shamba au paradiso!

9 Mungu alipowaumba binadamu wawili wa kwanza aliwapa iwe kao lao bustani ya Edeni, jina ambalo linamaanisha “Paradiso ya Furaha.” Lakini, paradiso haikukusudiwa iwe mahali hapo pamoja tu. Mungu aliwaambia: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze [dunia], na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28; 2:8, 9) Hii ingetia ndani kuieneza Paradiso kwenye miisho ya dunia, hilo likiwa ni kusudi lililotajwa na Mungu ambalo halikukomeshwa na mwendo wa kutokutii wa Adamu na Hawa. Yesu Kristo mwenyewe alionyesha tumaini hakika katika kusudi hilo alipoahidi mwanadamu aliyekufa kando yake kwamba angekuwa na nafasi ya kuishi katika Paradiso hiyo ya kidunia. (Luka 23:39-43) Hilo litatokeaje?

10. Kulingana na Ufunuo 11:18, ni vipingamizi gani vinavyozuia Paradiso ambavyo Mungu anaahidi kuviondoa?

10 Katika “dhiki kubwa” inayokuja Mungu ataondoa kabisa vizuizi vyote vinavyoizuia Paradiso yake ya kidunia inayokuja kwa ‘kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Hivyo Mungu atafanya jambo ambalo serikali za kibinadamu hazingeweza kufanya kamwe. Atawaondosha wote wale ambao kwa ubinafsi wanaichafua dunia ili watosheleze pupa ya kibiashara, wote wanaopiga vita vyenye hasara kubwa, na wote wanaoitumia dunia vibaya kwa sababu hawana heshima kwa zawadi za ukarimu ambazo Mungu ameandaa.

11. (a) Ni tukio gani la kihistoria linaloonyesha kwamba kurudishwa kwa Paradiso duniani si jambo linalotofautiana na maisha halisi ya kibinadamu? (b) Jambo hilo linatia imani yetu nguvu katika baraka gani iliyoahidiwa?

11 Ndipo dunia nzima itakapochanua uzuri. Ndipo hewa, maji na ardhi vitakuwa vizuri na safi. Kurudishwa huku kwa Paradiso si jambo lisiloaminika, wala si tofauti na matukio ya kweli ya maisha ya kibinadamu. Karne nyingi zilizopita, taifa la Israeli lilipotoka uhamishoni katika Babuloni, Yehova Mungu aliwarudisha kwenye nchi ya kwao, ambayo wakati huo ilikuwa mahame. Hata hivyo, kwa sababu ya baraka ya Mungu kuwa juu yao na kazi yao, upesi nchi ikawa nzuri sana hata jamii za watu waliokuwa jirani wakaweza kupaaza sauti hivi: ‘Imekuwa kama bustani ya Edeni!’ Nchi iligeuka ikawa yenye kuzaa sana, ikaondoa ogofyo lo lote la njaa ndogo na njaa kuu. (Ezekieli 36:29, 30, 35; Isaya 35:1, 2; 55:13) Aliyofanya Mungu kule nyuma yalionyesha kwa kiasi kidogo yale ambayo bado atafanya duniani pote ili kutimiza ahadi zake. Watu wote watakaohesabiwa wanastahili kuishi wakati huo watafurahia furaha za maisha zilizoandaliwa na Mungu katika Paradiso.—Zaburi 67:6, 7; Isaya 25:6.

Mwisho wa Ufukara na Utumwa Wenye Kuletwa na Uchumi

12. Ni hali gani za kiuchumi na za kikazi ambazo ni lazima zirekebishwe ikiwa tutakuwa na furaha ya kweli katika maisha?

12 Ufukara na utumwa kwa mifumo ya kitaifa ya uchumi ni mambo ya kawaida duniani pote. Ikiwa mamilioni ya watu wangeendelea kufanya kazi ya kujipatia riziki tu au kufanya kazi ngumu ili waweze kuishi tu au kufanya kazi isiyopendeza ya namna moja tu, yenye kufanya mtu awe kidude cha kazi tu, Paradiso haingeweza kufurahiwa kikweli.

13-15. (a) Tunapata wapi mfano wa kihistoria unaotuonyesha mapenzi ya Mungu kwa mwanadamu ni nini katika habari hii? (b) Mpango huo ulichangiaje usalama na kufurahia maisha kwa kila mtu na kila jamaa?

13 Mapenzi ya Mungu kwa mwanadamu katika habari hiyo yanaonwa kwa njia ambayo alielekeza mambo kama hayo kuhusiana na Israeli wa kale. Kule, kila jamaa ilipokea urithi wa shamba. (Waamuzi 2:6) Ingawa shamba hilo lingeweza kuuzwa, na watu mmoja mmoja wangeweza hata kujiuza wenyewe utumwani ikiwa waliingia katika deni, Yehova bado alifanya maandalizi ya kuzuia kuwa na mashamba mengi mno au kuwaweka watu katika utumwa wa muda mrefu. Jinsi gani?

14 Kwa njia ya maandalizi ya kiuchumi katika sheria aliyowapa watu wake. Mwaka wa saba wa utumwa ulikuwa “mwaka wa maachilio” ambapo ilikuwa lazima Mwisraeli ye yote aliyekuwa utumwani aachiliwe. Pia, kila mwaka wa 50 ulikuwa mwaka wa “Yubile” kwa taifa zima, mwaka wa “kupiga mbiu ya kuachwa mahuru” kwa wakaaji wote wa taifa hilo. (Kumbukumbu 15:1-9; Walawi 25:10) Ndipo mali yo yote ya urithi iliyokuwa imeuzwa iliporudishwa kwa mwenyewe wa kwanza. Wote waliokuwa utumwani waliachiliwa, hata ingawa haikuwa imepita miaka saba. Ulikuwa wakati wa shangwe ya kuungana tena kwa furaha kwa jamaa na mwanzo mpya wa kiuchumi katika maisha. Hivyo, hakuna shamba ambalo lingeweza kuuzwa kwa wakati wote. Kwa kweli kuuzwa kwalo kulikuwa ni kukodishwa tu ambako kungemalizika katika muda wa kufikia mwaka wa Yubile, si baada ya hapo.—Walawi 25:8-24.

15 Yote hayo yalisaidia sana kuleta uthabiti wa kiuchumi wa taifa na usalama na amani ya kila jamaa. Wakati sheria hizo zilipofuatwa, taifa lilizuiwa lisiwe katika hali yenye huzuni tunayoona leo katika nchi nyingi sana ambamo mna watu walio matajiri mno na wengine walio maskini mno. Manufaa zilizomjia mtu mmoja zililitia taifa nguvu, kwa maana hakuna aliyehitaji kuwa na mapendeleo machache na kugandamizwa na hali mbaya za kiuchumi. Kama ilivyoripotiwa wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani, “Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake.” (1 Wafalme 4:25) Leo watu wengi hawawezi kuutumia uwezo wa majaliwa yao yote na kuwa wepesi wa kutenda kwa sababu wananaswa katika mifumo ya kiuchumi inayowalazimisha watumikie tamaa za watu wachache au hata za mtu mmoja. Chini ya sheria za Mungu mtu mwenye bidii alisaidiwa achange uwezo wake ili kuongeza masilahi na ufurahifu wa wote. Jambo hilo linatupa kionyesho cha hisia ya kuwa na ustahili na fahari ya kibinafsi ambayo wale watakaopata uzima katika Mfumo Mpya wa Mungu watafurahia.

16. Kwa habari ya hali za maisha na hali ya mtu ya kiuchumi, Ufalme wa Mungu utaandalia nini raia wote wao?

16 Duniani pote unabii wa Mika 4:3, 4 utapata utimizo wa ajabu. Watu wanaopenda amani wenye kuishi chini ya utawala wa Mungu wenye uadilifu “wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha [Yehova, NW] wa majeshi kimesema hivi.” Hakuna ye yote wa raia za Ufalme wa Mungu atakayeishi katika vitongoji vichafu-vichafu au vijumba vya kupanga vilivyosongamana-songamana. Watakuwa na mashamba na makao yao wenyewe. (Isaya 65:21, 22) Zamani za kale Mfalme, Kristo Yesu, aliahidi kwamba ‘wenye upole watairithi dunia,’ naye anayo “mamlaka yote mbinguni na duniani” kuhakikisha kwamba hivi ndivyo itakavyokuwa.—Mathayo 5:5; 28:18, NW.

Afya na Uzima Wenye Kudumu

17-19. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba afya nzuri na maisha marefu ni tamaa za asili za wanadamu? (b) Ni mambo gani ya hakika juu ya maisha ya kibinadamu na juu ya mimea yanayofanya muda mfupi wa maisha ya mwanadamu uonekane kuwa wenye kushangaza? (c) Kuna habari gani juu ya ubongo wa kibinadamu inayoonyesha kwamba ni jambo la akili kuamini kwamba mwanadamu aliumbwa aishi milele?

17 Hata hivyo, ikiwa wakati ujao utakuwa wenye magonjwa, uzee na kifo, hakuna yo yote ya hali hizo nzuri sana ambayo ingeweza kuyafanya maisha yawe yenye amani na salama kikweli. Je! kutumainia ondoleo la mambo hayo yenye kutaabisha sana ni jambo lisilo la akili au lisilopatana na matukio ya kweli katika maisha ya kibinadamu? Hakika si tofauti na asili ya mwanadamu kutaka hilo, kwa maana wanadamu wametumia muda wote wa maisha zao na fedha nyingi sana wakijaribu kutimiza jambo hilo.

18 Kwa hiyo tumaini la afya na uzima wenye kudumu si jambo lisilo la akili hata kidogo. Kwa kweli, lisilo la akili ni hili: Kwamba wakati tu wanadamu wanapofikia umri wa kuanza kuwa na maarifa, ujuzi na uwezo wa kufanya mambo yanayofaa, ndipo wanapoanza kuzeeka na kufa hatimaye. Na bado kuna miti inayoishi maelfu ya miaka! Mbona mwanadamu, aliyeumbwa katika mfano wa Mungu, aishi kisehemu kidogo tu cha wakati ambao mimea fulani isiyo na akili inaishi? Ikifikiriwa kiakili, je! siye anayepaswa kuishi muda unaouzidi kwa mbali huo wa mimea?

19 Kwa wataalamu wanaochunguza kuzeeka, utaratibu wa kuzeeka ungali ni fumbo kwa sehemu kubwa. Jambo linaloleta fumbo pia, ni uhakika wa kwamba ubongo wa kibinadamu umeumbwa ukiwa na nafasi ya kuingiza habari ambazo ni kama hazina kikomo. Kama vile mwandikaji mmoja wa sayansi alivyosema, ubongo “unaweza kabisa kuchukua furushi lo lote la kujifunza na kumbukumbu ambalo mwanadamu ataelekea kuuwekelea—tena mara bilioni zaidi ya kadiri hiyo.”55 Maana yake ni kwamba ubongo wako unaweza kuchukua si furushi lo lote unaloweza kuuwekelea katika muda wa maisha ya miaka 70 au 80 tu, bali pia muda wa mara milioni elfu zaidi! Si ajabu mwanadamu ana kiu nyingi sana ya maarifa, tamaa nyingi ya kujifunza kufanya na kutimiza mambo. Hata hivyo anazuiwa na ufupi wa maisha yake. Je! ni jambo la akili kwamba ubongo wa kibinadamu uwe na nafasi kubwa ajabu ya kuingiwa na mambo na bado kiwe ni kijisehemu kidogo sana cha nafasi hiyo kinachotumiwa? Je! si jambo la akili zaidi kukata shauri, kama Biblia inavyofanya, kwamba Yehova aliumba mwanadamu aishi milele duniani na akampa ubongo uliofaa sana kusudi hilo?

20. Ni nini ambacho Biblia inasema kwamba Mungu ameahidi kufanyia wanadamu kwa habari ya matokeo ya dhambi, kutia na kifo chenyewe?

20 Biblia inaonyesha kwamba hapo kwanza mwanadamu alikuwa na nafasi ya kuishi milele, lakini akaipoteza kwa sababu ya uasi: “Kwa mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12) Lakini pia Biblia ina ahadi ya Mungu kwamba katika Paradiso itakayorudishwa, “mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:3, 4; linganisha 7:16, 17.) Inasema kwamba uzima wa milele, usio na matokeo ya dhambi, ndilo kusudi la Mungu kwa wanadamu. (Warumi 5:21; 6:23) Zaidi ya hilo, inaahidi kwamba baraka za Mfumo Mpya wa Mungu zitafunguliwa wazi kwa mabilioni ya watu ambao wamekufa zamani. Jinsi gani? Kwa ufufuo utakaoliacha likiwa tupu kaburi la ujumla la wanadamu wote. Yesu Kristo alitabiri hivi kwa uhakika: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wale wote walio katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake watoke.”—Yohana 5:28, 29, NW.

21, 22. Kwa sababu gani taraja la kurudishwa kwenye afya kamili si jambo la kutazamia mengi mno?

21 Sayansi ya kitiba leo inaweza kutengeneza “dawa zenye miujiza” na kufanya ajabu za upasuaji ambazo zingalionekana kama zisizoaminika hata makumi machache ya miaka iliyopita. Je! tutie shaka kwamba Yule aliyewaumba binadamu hawezi kufanya ajabu za maponyo ya kustaajabisha zaidi? Kwa uhakika Muumba ana uwezo wa kurudisha watu wenye mioyo ya uadilifu kwenye afya nyingi sana, hata kuugeuza utaratibu ule wa kuzeeka. Naye anaweza kufanya hivyo bila kutumia dawa, upasuaji, au viungo vya kuatikwa tu. Kwa huruma zake, Mungu ameandaa ushahidi wa kwamba kutumainia baraka hizo si kutazamia mengi mno.

22 Mungu alimpa Mwanaye alipokuwa duniani uwezo wa kufanya kazi zenye nguvu za kuponya. Kazi hizo zinatuhakikishia kwamba hakuna udhaifu, hitilafu au ugonjwa unaopita uwezo wa Mungu wa kuponya. Wakati mtu ambaye nyama yake ilijaa ukoma alipomsihi sana Yesu amponye, kwa huruma Yesu alimgusa mtu huyo na kusema: “Takasika.” Na, kama maandishi ya kweli yanavyosema, “na mara ukoma wake ukatakasika.” (Mathayo 8:2, 3) Yesu alifanya mambo kama hayo kwa kutazamwa na mashahidi wengi, kama vile mwanahistoria Mathayo anavyoripoti: “Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya; hata ule mkutano wakastaajabu . . . wakamtukuza Mungu wa Israeli.” (Mathayo 15:30, 31) Jisomee mwenyewe usimulizi kwenye Yohana 9:1-21 uone namna ilivyo ya uhakika na ya kweli habari ya kihistoria inayohusu maponyo hayo. Ukweli wa matukio hayo unashuhudiwa na mashahidi wengi, kutia na daktari, yule tabibu Luka.—Marko 7:32-37; Luka 5:12-14, 17-25; 6:6-11; Wakolosai 4:14.

23, 24. Kwa sababu gani si jambo lisilo la akili kuamini kwamba wafu watarudishwa kwenye uzima chini ya Ufalme wa Mungu?

23 Kwa sababu zinazofanana na hizo si lazima tuione ahadi ya Biblia “kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu” kama isiyosadikika. (Matendo 24:15) Sauti, sura, na vitendo vya mtu vinaweza kurudishwa kutokana na filamu au ukanda wa vidyo, hata miaka mingi baada ya kufa. Je! yule aliyemuumba mwanadamu, anayejua kabisa atomi na molekyuli zote zilizo katika umbo la mwanadamu, asiweze kufanya hata zaidi ya hivyo? Kompyuta zinazofanywa na mwanadamu zaweza kuweka na kusawazisha mabilioni ya vihabari mbalimbali. Lakini Mungu aliuumba ulimwengu wote mzima wenye kustaajabisha pamoja na mabilioni (maelfu ya mamilioni) ya magalaksi yaliyomo, kila galaksi likiwa na mabilioni ya nyota. Jumla inakuwa matrilioni, makwadrilioni, na hata zaidi! Hata hivyo, Zaburi 147:4 inasema: “Huihesabu idadi ya nyota, huzipa zote majina”! Kwa uhakika ingekuwa rahisi kwa Mungu, aliye na huo uwezo mkubwa ajabu wa kumbukumbu, kukumbuka utu wa watu mmoja mmoja ili aweze kuwarudisha kwenye uzima.—Ayubu 14:13.

24 Tena, Yehova aliandaa mifano ya kihistoria kuitia imani yetu nguvu katika tumaini hilo zuri ajabu. Alimpa Mwana wake uwezo wa kuonyesha kwa kiasi kidogo atakayoyafanya kwa kiasi kikubwa wakati wa utawala wake wenye uadilifu juu ya dunia. Yesu alifufua watu kadha waliokuwa wamekufa, mara nyingi akifanya hivyo hadharani ya watazamaji. Lazaro, ambaye Yesu alifufua karibu na Yerusalemu, alikuwa hata amekufa kwa muda wa kutosha mwili wake uanze kuoza. Hakika tumaini la ufufuo lina msingi unaofaa.—Luka 7:11-17; 8:40-42, 49-56; Yohana 11:38-44.

Uwezo wa Dunia Kuwa na Nafasi ya Kukaliwa na Idadi Hiyo ya Watu

25, 26. Wafu watakapofufuliwa, nafasi ya kuishi kila mtu itapatikana wapi?

25 Je! sayari hii yaweza kuandaa nafasi inayofaa kuishi idadi hiyo ya watu ambao wangetokana na ufufuo wa wafu? Ilichukua zaidi ya miaka 5,000 ili idadi ya watu ulimwenguni ifikie bilioni moja mapema katika miaka ya 1800. Leo, ni bilioni tano.

26 Basi, wale wanaoishi leo ni sehemu kubwa ya jumla ya watu ambao wamepata kuishi. Wengine wamekadiria kwamba jumla ya idadi ya watu katika historia yote ya kibinadamu ni karibu 15,000,000,000. Eneo la ardhi ya dunia ni zaidi ya hekta 15,000,000,000. Hiyo ingetoa kwa kila mtu nafasi ya zaidi ya hekta 1. Hii isingetoa nafasi ya kulima chakula tu, bali pia ingetoa nafasi ya misitu, milima, na maeneo mengine ya kutazamisha macho—bila ya msongamano usiofaa katika Paradiso. Halafu, pia, Biblia inaonyesha kwamba si wote wanaoishi sasa watakaookoka na kuishi katika Mfumo Mpya huo. Kwa kweli, Yesu alisema, “Iliyo pana na yenye nafasi ni barabara ile inayoongoza ndani ya uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kuipitia.” Yeye alisema pia kwamba wakati uharibifu wa ulimwengu utakapokuja, wale ambao hawafanyi mapenzi ya Yehova ‘wataondoka waingie ndani ya kukatiliwa mbali kwa milele.’—Mathayo 7:13; 25:46, NW.

27. Je! dunia ingeweza kutokeza chakula cha kuwatosha watu hao wote?

27 Lakini je! dunia ingeweza kutokeza chakula cha kuwatosha watu wengi hivyo? Wanasayansi wanadai leo kwamba ingeweza, hata chini ya hali za sasa. Ripoti ya The Toronto Star ilisema hivi: “Kulingana na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) tayari kuna mazao ya kutosha yanayokuzwa duniani pote kulisha kila mtu duniani kwa kalori 3,000 kwa siku, ambayo ni . . . karibu asilimia 50 juu ya kiwango kidogo zaidi kinachokubalika.”56 Kuhusu wakati ujao, ilieleza kwamba hata chini ya hali za leo, kungekuwa na chakula cha kutosha kushibisha mahitaji mara mbili ya idadi ya watu ya sasa ya ulimwengu. Pia, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova atawaongoza watu wake kuzitumia ifaavyo nguvu za dunia za kuwa na mazao ya kilimo, kwa maana Zaburi 72:16, NW inatuhakikishia sisi: “Kutakuja kuwa na nafaka tele dunaini; juu ya milima kutakuwa na mfuriko.”

28. Sababu gani hakuna hatari ya kwamba watu wakiwa wanaishi milele, mwishowe dunia ingesongamana watu mno?

28 Inatupasa tufahamu kusudi la Mungu ni nini, kama walivyoambiwa hapo kwanza binadamu wawili wa kwanza. Waliambiwa ‘waijaze dunia na kuitiisha,’ wakiieneza mipaka ya Edeni kwenye miisho ya dunia. (Mwanzo 1:28) Kwa wazi, hiyo inamaanisha, kuijaza dunia kwa kiasi cha kustarehesha, si kuijaza mno watu. Bado hiyo ingetoa nafasi ili dunia ‘iliyotiishwa’ iwe shamba zuri la duniani pote kwa kufuata kielelezo cha kao la kwanza la mwanadamu lililokuwa mfano wa shamba zuri. Kwa hiyo, amri hiyo ya kimungu inaonyesha kwamba katika wakati na njia ya Mungu, ongezeko la idadi ya watu lingeongozwa vizuri.

Msingi Hakika kwa Furaha Yenye Kudumu

29. Mahusiano pamoja na watu wengine yana matokeo gani juu ya furaha ya mtu?

29 Hata hivyo, hata mazingira mazuri, ufanisi wa vitu vya kimwili, kazi yenye kupendeza, na afya nzuri hayangekupa uhakikisho kamili wa kuwa na furaha yenye kudumu. Watu wengi leo wana mambo hayo lakini hawana furaha. Kwa sababu gani? Kwa sababu ya watu walio karibu nao ambao huenda wakawa ni wenye ubinafsi, wenye ugomvi, wanafiki, au wenye chuki. Furaha yenye kudumu katika Mfumo Mpya wa Mungu italetwa kwa kipimo kikubwa na badiliko la duniani pote katika mwelekeo wa watu. Upendo na heshima yao kwa Mungu na tamaa yao ya kutimiza makusudi yake kutaleta ufanisi wa kiroho. Bila huo, ufanisi wa vitu vya kimwili unakuwa usioridhisha na wa bure tu.

30. Twajuaje kwamba wale watakaoishi katika Mfumo Mpya wa Mungu watakuwa watu peke yao wanaosaidia kweli kweli kuleta amani na usalama wa wengine?

30 Ndiyo, ni furaha kweli kweli kuwa karibu na watu ambao ni wenye fadhili, wanyenyekevu, wenye urafiki—watu unaoweza kuwapenda kweli kweli na kuwatumaini, wanaohisi ivyo hivyo juu yako. (Zaburi 133:1; Mithali 15:17) Kumpenda Mungu ndiko kunakohakikisha upendo wa kweli kwa jirani, ambao utafanya maisha yawe yenye kupendeza sana katika Mfumo Mpya Wake. Wote wale ambao Mungu atapendelea kwa kuwapa uzima wa milele watakuwa watu ambao wamethibitisha upendo wao kwake na kwa mwanadamu mwenzao. Watu hao wakiwa jirani, rafiki, na wafanya kazi wenzi, utaweza kufurahia amani na usalama wa kweli na furaha yenye kudumu.—1 Yohana 4:7, 8, 20, 21.

31. Ikiwa twataka kweli kweli uzima katika Mfumo Mpya wa Mungu, inatupasa tufanye nini sasa?

31 Kwa kweli, taraja hilo la ajabu liko wazi kwako! Hivyo mwendo wa hekima unaofaa ni kuchunguza yanayotakwa ili kulipokea. Sasa ndio wakati wa kupatanisha maisha yako na matakwa ya Mungu kwa wale watakaoachiliwa waipite “dhiki kubwa” inayokuja.—2 Petro 3:11-13.

[Picha katika ukurasa wa 98]

Karibuni siku itafika wakati dunia nzima itakapogeuzwa iwe paradiso

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki