Sura 12
Agano Jipya la Mungu Lakaribia Kutimizwa
1. (a) Ni jambo gani lingeipata dunia yetu ikiwa Mungu hangeshikamana na agano lake kuhusu mchana na lile linalohusu usiku? (b) Kwa kuwa Mungu anashikamana kishikamanifu na maagano yake, tunaweza kuwa na uhakika gani?
SISI tungefanya nini ikiwa Mungu hangeshikamana sana na agano lake kuhusu mchana na lile linalohusu usiku? Badala ya kuwa mchana na usiku zikibadilishana, dunia yetu ingeangaziwa nuru yenye kuendelea sikuzote au ifunikwe na giza lenye kuendelea sikuzote. (Mwanzo 1:1, 2, 14-19) Lakini Mungu anashikamana kwa ushikamanifu na maagano yake. Kwa hiyo tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba mwezi, jua, na magalaksi ya mbinguni havitaharibiwa kamwe; wala sayari yetu Dunia.
2. Yehova aliwaambia Wayahudi nini kuhusiana na agano lake la mchana na lile la usiku?
2 Akisema juu ya agano lake la mchana na lile la usiku, Mungu aliwaambia Wayahudi waliokuwa chini ya ufalme wa nyumba ya kifalme ya Daudi hivi: “Kama mkiweza kulivunja agano langu la mchana, na agano langu la usiku, hata usiwepo tena mchana na usiku kwa wakati wake; ndipo agano langu nililolifanya na Daudi, mtumishi wangu, laweza kuvunjika, hata asiwe na mwana wa kumiliki katika kiti chake cha enzi.”—Yeremia 33:20, 21.
3. Maneno hayo yanaonyesha nini kwa habari ya agano lake pamoja na Daudi kwa ajili ya Ufalme wa milele?
3 Katika maneno hayo tuna ushuhuda usio wa moja kwa moja kwamba dunia yetu, pamoja na jua na mwezi vitadumu. (Mhubiri 1:4) Dunia yetu sikuzote itakaliwa na wanadamu, ili wao wafurahie uzuri wa mchana na wa usiku chini ya Mungu mshika-agano, Muumba wanadamu. Na kama vile Yehova ameshikamana kwa uthabiti na agano lake la mchana na lile la usiku, ndivyo yeye ameshikamana kishikamanifu na agano lake na Mfalme Daudi wa kale kwa ajili ya Ufalme wa milele katika mstari wa jamaa ya Daudi. Ndivyo ilivyo ijapokuwa imekuwa lazima kiti cha Ufalme kihamishwe kutoka duniani kwenda kwenye mbingu zisizoonekana.—Zaburi 110:1-3.
4. (a) Agano la Mungu pamoja na Daudi kuhusu Ufalme wa milele linashirikishwa na agano jipi jingine? (b) Yesu Kristo alisema nini juu yalo, na chini ya hali gani?
4 Agano la Mungu kuhusu Ufalme wa milele katika ukoo wa Daudi linashirikishwa na agano jingine, lile “agano jipya.” Agano hilo ambalo lingechukua mahali pa agano la kale lilitajwa na Yesu. Hiyo ilikuwa baada ya kwisha kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa ya Kiyahudi pamoja na wanafunzi wake waaminifu katika usiku wa Nisani 14, 33 W.K. Alianzisha kile kilichokuja kuitwa “chakula cha Bwana.” Yeye alijua kwamba, katika siku iyo hiyo ya Kupitwa, angemwaga damu yake kwa kujidhabihu. Kwa sababu hiyo, alichukua kikombe cha divai nyekundu, lakini kabla ya kukipitisha kwa mitume wake waaminifu, alisema hivi: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa uwezo wa damu yangu.”—Luka 22:20, NW; 1 Wakorintho 11:20, 23-26.
5. Ahadi ya Mungu ya agano jipya ilifanywa kwa nani, na je! ile Jamhuri ya Israeli inajidai kuwa katika agano hilo?
5 Kama vile lile agano la kale, agano jipya linafanywa pamoja na taifa lakini si taifa lo lote la yale ya Jumuiya ya Wakristo. Ijapokuwa ahadi ya hilo agano jipya ilifanywa kupitia nabii Yeremia kwa taifa la Israeli zaidi ya miaka 2,500, ile Jamhuri ya Israeli ya leo haijidai kuwa katika agano hilo jipya. Badala yake, Jamhuri ya Israeli ikawa mwanachama wa UM.
6. Kulingana na Yeremia sura ya 31, kwa sababu gani Mungu aliona uhitaji wa kufanya agano jipya, na lingeleta matokeo gani?
6 Ni kwa sababu gani Mungu alitaka agano jipya? Unabii wa Yeremia 31:31-34 unaeleza: “Angalia, siku zinakuja, asema [Yehova], nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. Si kwa mfano wa agano lile nililolifanya na baba zao, katika siku ile nilipowashika mkono, ili kuwatoa katika nchi ya Misri; ambalo agano langu hilo walilivunja, ingawa nalikuwa mume kwao, asema [Yehova]. Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema [Yehova]; Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue [Yehova]; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema [Yehova]; maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.”
Agano Bora Lenye Mpatanishi Bora
7. Je! Hilo agano jipya ni kufanywa upya tu kwa lile agano walilovunja Waisraeli, na kwa sababu gani ni bora zaidi ya lile agano la Torati?
7 Agano jipya si kufanywa upya tu kwa agano lile la mapema ambalo Waisraeli walivunja. Sivyo kabisa! Kwa kuwa mtume Paulo anawaandikia Wakristo katika Roma, akisema: “Ninyi hamko chini ya sheria bali chini ya fadhili zisizostahilika.” (Warumi 6:14, NW) Kweli kweli ni agano jipya, na lilitazamiwa liwe bora, kwa kuwa Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote anaweza kufanya mambo yawe bora zaidi kwa habari ya wale anaokubalia waingie katika hilo agano jipya. Jambo moja ni kwamba, yeye alimwinua mpatanishi aliye bora zaidi, au mtu wa katikati, katika kulianzisha hilo agano jipya. Mpatanishi huyo hakuwa mwanadamu asiyekamilika, mwenye kuambukizwa dhambi kama alivyokuwa nabii Musa.
8. (a) Hilo agano jipya lina nini inayolifanya kuwa bora zaidi ya agano la Torati? (b) Ni nani Mpatanishi wa hilo agano jipya lililo bora zaidi? (c) Waebrania 8:6, 13 husema nini juu ya hilo agano jipya na hali ya juu zaidi ya Mpatanishi walo, na kukiwa na matokeo gani juu ya hilo agano la zamani?
8 Lile agano la Torati lililopatanishwa kupitia nabii Musa lilikuwa zuri lenyewe. Walakini, agano hilo lilitoa nafasi kwa dhabihu za wanyama ambao damu yao haingeweza kusafisha dhambi za kibinadamu. Kwa hiyo ili Yehova Mungu aanzishe agano lililo bora zaidi, ni lazima kuwe na mpatanishi aliye bora zaidi akiwa na dhabihu bora zaidi. Mpatanishi huyu anayehitajiwa sana alithibitika kuwa Yesu Kristo. Ikionyesha namna mpatanishi huyo alivyo wa hali ya juu zaidi akilinganishwa na nabii Musa, Biblia inatoa maelezo yanayofuata: “Lakini sasa [Yesu] amepata huduma iliyo bora zaidi, kwa kadiri alivyo [mpatanishi] wa agano lililo bora, lililoamriwa juu ya ahadi zilizo bora. . . . Kwa kule kusema, Agano jipya, amelifanya lile la kwanza kuwa kuukuu.”—Waebrania 8:6, 13.
Mahali pa Agano la Kale “Kuukuu” Pachukuliwa
9. (a) Lile agano la kale lilitoweka siku gani? (b) Ni jambo gani lililotukia asubuhi hiyo, na ni katika uhakikisho wa nini?
9 Agano hili “kuukuu” au lisilofanya kazi, lilitoweka siku 50 baada ya kufufuliwa kwa Mpatanishi wa agano jipya. Hilo lilitukia siku ya Pentekoste. Asubuhi ya siku hiyo, ile iliyofananishwa na Sikukuu ya Kukusanya ya Kiyahudi ilianza. Jinsi gani? Basi, wanafunzi 120 waaminifu wa Mpatanishi wa lile agano jipya walikusanyika pamoja katika chumba cha orofa katika Yerusalemu wakapokea roho takatifu iliyoahidiwa, katika kutimiza unabii wa Yoeli 2:28-32. Ilionyesha uhakika wa kuanza kwa agano hilo jipya kwa kutoa ushuhuda unaosikika na kuonekana kwa watazamaji wote.
10. Siku hiyo ya Pentekoste, ilidhihirishwaje kwamba wanafunzi wa Yesu walikuwa wamepakwa mafuta kwa roho takatifu?
10 Wakati Yesu alipopanda kutoka maji ya ubatizo na roho takatifu ikamwagwa juu yake, kwa mwujiza roho hiyo ilifananishwa na mfano wa njiwa akining’inia juu ya kichwa chake. Lakini kwa habari ya wanafunzi hao Waebrania 120 siku hiyo ya Pentekoste, kupakwa mafuta kwao kwa roho takatifu kulidhihirishwaje? Ni kwa kuonekana kwa ndimi kama zile za moto juu ya vichwa vyao na kwa kukirimiwa uwezo wa kutangaza Neno la Mungu kwa lugha za kigeni ambazo hawakuwa wamejifunza kamwe.—Mathayo 3:16; Matendo 2:1-36.
11. (a) Ni jambo gani linalopasa kuwa wazi kwa Wayahudi, na kwa sababu gani? (b) Tunajuaje kwamba Wayahudi hawaambiani, “Mjue [Yehova]”! Na ni furaha gani ambayo hawana?
11 Inapasa kuwa dhahiri kwa Wayahudi na marabi wao kwamba agano la Torati ya Musa halitendi kazi tena. Tangu kuharibiwa kwa Yerusalemu na majeshi ya Warumi mwaka wa 70 W.K., hawajapata kuwa na hekalu. Wakati huo, maandishi yao ya kiukoo yalipotea au yakaharibiwa. Hivyo leo hawajui ni nani aliye wa kabila la Lawi na ni nani aliye mzao wa Haruni ili kutumikia katika cheo cha kuhani mkuu kwa ajili ya taifa la Kiyahudi. Badala ya kuambiana, “Mjue [Yehova]”! wanaona kule kutamka jina hilo la kimungu ni kukufuru. Kwa hiyo wao hawashiriki furaha ya Mashahidi wa Yehova juu ya uhakika wa kwamba mahali pa agano lile la kale “kuukuu” pamechukuliwa na agano jipya.
“Agano la Milele”
12. (a) Ni sala gani ambayo Mashahidi wa Yehova wanaweza kutoa kutoka moyoni? (b) Yesu alifufuliwa akiwa na nini kutoka kwa wafu?
12 Tofauti kabisa na hali ya Wayahudi leo, Mashahidi wa Yehova wanaye Kuhani Mkuu anayetenda kwenye mkono wa kuume wa Mungu katika mbingu. Yeye ndiye Mpatanishi wa lile agano jipya, mpatanishi aliye mkuu zaidi kuliko Musa. Kutoka moyoni, hao Mashahidi wa Yehova wanaweza kujiunga na mwandikaji wa sala kwenye Waebrania 13:20, 21: “Basi, Mungu wa amani aliyemleta tena kutoka kwa wafu Mchungaji Mkuu wa kondoo, kwa damu ya agano la milele, yeye Bwana wetu Yesu, awafanye ninyi kuwa wakamilifu katika kila tendo jema, mpate kuyafanya mapenzi yake.” Kwa kuwa “Mchungaji Mkuu” huyo alitoa uhai wake wa kibinadamu kwa ajili ya “kondoo,” yeye angeweza kufufuliwa kutoka kwa wafu katika mwili wa roho usioweza kufa, usio na damu lakini akiwa na ubora wa damu ya lile agano jipya ambalo kwa uaminifu limehifadhiwa na ambalo ni la milele katika matokeo yalo mema.
13. (a) Kifo cha yule Mpatanishi wa agano jipya kinakumbukwaje kila mwaka na Mashahidi wa Yehova? (b) Mifano hiyo inafananisha nini?
13 Kile kifo chenye dhabihu cha Mpatanishi wa lile agano jipya, Yesu Kristo, kinakumbukwa kila mwaka na Mashahidi wa Yehova katika tarehe ya kila mwaka ya “chakula cha Bwana” cha jioni. Ule mkate usio na chachu wanaoshiriki wale walio katika hilo agano jipya wakati wa ‘chakula cha jioni’ unafananisha mwili mkamilifu wa Mpatanishi, nayo divai inafananisha ile damu safi, isiyochafuliwa ambayo, kulingana na Maandiko, ilikuwa na ubora wenyewe wa uhai wa Mpatanishi huyo.—1 Wakorintho 11:20-26; Mambo ya Walawi 17:11.
14. Wakati wale walio katika agano hilo jipya wanaposhiriki mifano ya Ukumbusho, wanafanya nini, kusema kwa njia ya mfano?
14 Wakati wale walio katika hilo agano jipya wanaposhiriki kikombe cha divai ya Ukumbusho kwenye “chakula cha Bwana” cha jioni ni kwa njia ya mfano tu kwamba wanakunywa damu, ile ya Mpatanishi wa lile agano jipya. Pia ni kwa njia ya mfano kwamba wanakula mwili wake wakati wanaposhiriki mkate usiotiwa chachu wa Ukumbusho. Kwa kufanya hivyo, kusema kwa njia ya mfano, wanaonyesha imani yao katika dhabihu ya ukombozi ya Mwana wa Mungu, yule Mkombozi wa wanadamu wote.
15. (a) Tayari hilo agano jipya limeishi muda gani, na kweli kweli limethibitikaje kuwa agano bora zaidi? (b) Kwa sababu gani agano jipya hilo linaweza kuitwa “agano la milele”?
15 Lile agano jipya, ambalo sasa lina umri wa zaidi ya miaka 1,950, linakaribia kutimiza kusudi lalo. Tayari limeishi karne nyingi zaidi ya lile agano la Torati ya Musa. Likiwa na msingi wa ahadi bora zaidi na dhabihu bora zaidi Mpatanishi bora zaidi, kweli kweli limethibitika kuwa agano bora zaidi. Kwa sababu haliwezi kupitwa wala mahali palo hapahitaji kuchukuliwa na agano jipya lililo bora kulipita, hilo agano jipya ambalo limefaulu linatajwa kuwa “agano la milele.”—Waebrania 13:20.
16. Inatupasa tumshukuru Yehova Mungu kwa ajili ya nini?
16 Shukrani zimwendee Mungu Mwenye Nguvu Zote, Yehova, kwa kuwa amemwinua Mpatanishi aliye bora zaidi ya Musa, ambaye kupitia kwake Yeye angeweza kuliondolea mbali kisheria lile agano la Torati la Musa kwa kulipigilia misumari kwenye mti wa mateso na kuandaa damu ya agano jipya la milele.
[Picha katika ukurasa wa 105]
Lile agano jipya ambalo Yesu alipatanisha ni bora zaidi ya lile agano la kale ambalo Musa alipatanisha